Junius
JF-Expert Member
- Mar 11, 2009
- 3,181
- 139
Kagame na Kabila wakikenua
Viongozi wa Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo walifanya mkutano wa kipekee hapo Alhamis ambapo waliafikiana kudumisha ushirikiano wa kiuchumi na katika maswala ya usalama.
Mazungumzo kati ya Rais Paul Kagame na mwenzake, Joseph Kabila yalifanyika katika mji wa Goma.
"Ni hatua kubwa ya kwanza," Rais Kabila aliwaambia waandishi wa habari baada ya mkutano huo.
Kwa upande wake, Rais Kagame alimhakikishia mwenzake kwamba Rwanda haitokubali kutumiwa kama ngome ya waasi dhidi ya serikali ya DRC.
Rasilmali na usalama
Viongozi hao walikubaliana kwamba nchi zao zitashirikiana katika kubuni miradi ya kuchimba rasilmali ya gesi kwenye ziwa Kivu na pia kufufua tume za pamoja.
Rwanda bado inamshikilia Nkunda
Mwezi mmoja umepita tangu Rais Kagame na Rais Kabila kuteua mabalozi kwa nchi hizo mbili, ishara kwamba uhusiano kati ya nchi hizo mbili unaimarika.
Mnamo mwezi wa Januari, nchi hizo mbili zilikubaliana kuendesha harakati za pamoja za kuwaangamisa waasi wa Hutu FDLR ambao wamejenga ngome yao nchini DRD.
Baadhi ya wapiganaji wa FDLR wanashutumiwa kwa kuhusika katika mauaji ya kimbari ya mwaka wa 1994 kabla ya kutorokea DRC.
Laurent Nkunda
Hali kadhalika, Rwanda imemkamata kiongozi wa kundi la waasi wa kabila la Watutsi nchini DRC, Laurent Nkunda.
Nkunda bado anashikiliwa na Rwanda licha ya ombi la DRC la kumtaka arudishwe nchini humo ili kufunguliwa mashtaka.
Hata hivyo, Rais Kagame alimhakikishia mwenzake, "ninaahidi kwamba Laurent Nkunda na kundi la CNDP hawatoruhusiwa kuendesha harakati zao za kuitatiza DRC wakiwa nchini Rwanda."
Viongozi hao wawili wanatazamiwa kukutana tena mnamo mwezi wa Oktoba au Novemba jijini Kinshasa.
SOURCE:BBC SWAHILI SERVICE