Juu ya Mambo ya Lazima (PD 3)

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,991
On Necessary Things (Public Discourse 3)

Na. M. M. Mwanakijiji

Kuna vitu visivyo vya lazima na vitu vya lazima. Kuna vitu ambavyo mwanadamu anaweza kuishi bila kuwa navyo na vipo vile ambavyo ni lazima awe navyo. Hata vile ambavyo ni lazima awe navyo kuna vilivyo vya msingi na vile vya upili na hata utatu. Lakini vyovyote vile siyo tu kwa mwanadamu lakini pia katika jamii ya watu kuna vitu ambavyo ni vya msingi kwa jamii yoyote ili iweze kufanikiwa na kujihakikishia uwepo wake na vipo vile ambavyo vinakuja baada ya vile vya msingi, yaani vile vya lazima kutimizwa kwanza.

Mmoja wapo wa wataalamu wa mambo ya tabia za binadamu Bw. Abraham Maslow aliandika kitu kile ambacho alikiita "Mpangilio wa Mahitaji" (Hierarchy of Needs) ambapo alielezea vile ambavyo katika maisha ya mwanadamu ni muhimu kufikia kile ambacho amekiita ni "fulfillment" (kuridhika) na kufikia kilele cha Kujitambua (self-actualization). Katika Mpangilio huo wa mahitaji Maslow anasema kuwa kabla ya mahitaji ya utatu kufikiwa ambayo yanafikia kwenye "self-actualization" basi kuna mahitaji ya msingi (basic needs) ambayo yanahitajika kutimizwa kwanza.

Katika Jedwali lake la kuelezea mahitaji hayo Maslow anasema kabla mwanadamu hajapata kuridhika basi mahitaji ya msingi ambayo ni yale ya maumbile kwanza ambayo ni mahitaji ya kijima (physiological and fundamentally primitive) kama kula, kulala, kujisaidia, kujihifadhi n.k. Na kwa mfuatano huo mahitaji yaliyo juu yake yapo yale Usalama (security) hasa mahitaji ya usalama wa mali, ajira, maadili, familia n.k. Juu ya haya yapo mahitaji ya Upendo na kufungamana (love and belonging) hapa ndipo mahitaji ya mapenzi, urafiki, familia, udugu n.k. Na Juu ya haya ndipo unakutana na mahitaji ya kujiona (esteem) ambapo mtu anakuwa na kujiamini, kujiheshimu, kuheshimu wengine, kufanikiwa, n.k Juu yake ndipo unakutana na mahitaji ya Kujitambua (self-actualization).

Sasa ukiangalia mpangilio wa mahitaji hayo Maslow anachosema ni kuwa kabla mtu hajaanza kutafuta mahitaji ya usalama wa ajira yake, mali yake n.k ni lazima kwanza atimize mahitaji yake ya msingi ambayo ni kula, kulala, makazi bora n.k

Hii inatupeleka wapi?

Lengo langu siyo kuzungumzia mahitaji ya mtu mmoja mmoja bali kuangalia kama jamii na kama taifa hatuna budi kujiuliza kama tunazingatia vitu vya "lazima" ili tuwe na taifa tunalolitaka (self-actualization). Yaani, ukiangalia mataifa yaliyoendelea utaona kuwa yamejaribu kwa kiwango kikubwa kutimiza mahitaji yale ya msingi ya watu na hata yale ya usalama, na kwa kiasi kikubwa yamejenga vizuri mahitaji ya 'kujiona" kiasi kwamba utaona watu wanaotoka kwenye mataifa hayo wao kama wananchi wanajiona vizuri zaidi kulinganisha na mataifa yanayohangaika kuendelea.

Hapa ndipo inanirudisha wakati wa Uhuru. Je sisi kama nchi ni vitu gani tulitakiwa tuvifanye kwanza? Hofu yangu ni kuwa tulianza vizuri sana (ingawa kuna watu hawataki kuamini hivyo). Jukumu la serikali ya Mwalimu ilikuwa siyo kutufikisha kwenye "self-actualization" bali kuliandaa taifa kutimiza mahitaji ya msingi (basic needs).

Nakumbuka Mwalimu alikuja na hilo wazo la "Mahitaji ya Msingi" ambayo naamini yalitokana na elimu hii ya Maslow kwamba Watanzania kabla hawajafikia kiwango fulani hawana budi kutimiza mahitaji fulani ya msingi ambayo yalikuwa ni yale mahitaji ya msingi ya mwanadamu ambayo ni Chakula (bora na chenye lishe), Mavazi (hifadhi ya mwili wake), Malazi (usalama wa nafsi yake), na elimu.

Lakini kwa kuangalia Taifa changa jukumu la kwanza kabisa ambalo naamini lilikuwa sahihi ni kuhakikisha kuwa Taifa hilo linakuwepo (to ensure that the nation survives). Leo hii sisi tunaweza kupiga kelele na kuikosoa serikali na kurusha kila madongo kwa serikali ya kwanza lakini ukweli ni kuwa serikali ile ilitimiza jukumu lake kwa kiwango cha juu kabisa (with flying colors) kwa kuhakikisha kuwa Tanzania kama Taifa linakuwepo, katika usalama, mipaka yake intact na watu wake wamoja.

Na katika kutimiza hilo Taifa likajaribu kufanya mambo kadhaa ya msingi kama elimu, kampeni ya UPE, kampeni ya Mtu ni Afya (nakumbuka "mtu ni afya mwananchi elewa"), kampeni ya Chakula bora (nilikuwa namsikiiliza Mbaraka na wimbo wake wa "vyakula vya aine nne") na pia nakumbuka vizuri kampeni ya "Nyumba bora" (tuliambiwa ni lazima iwe na choo)! Katika haya yote ukirudi nyuma utaona kuwa serikali ile ilikuwa inajaribu kuliongoza taifa kutimiza mahitaji ya msingi. Hivi vilikuwa ni vitu vya lazima.

Ndipo hatuna budi kujiuliza kwa Taifa changa kama la Tanzania ni vitu gani vya msingi ambavyo vingestahili kufanywa na vingine kusubiriwa kidogo? Ni vitu gani vya lazima ambavyo tulitakiwa kuvifanya ili kuliandaa taifa kwa mafanikio?

Leo hii tunapoangalia mwelekeo wa Taifa letu inaonekana kana kwamba tuko kwenye level ya juu kabisa ya mahitaji ya Taifa (self actualization) na ya kuwa tumeshatimiza mahitaji yetu ya msingi kama demokrasia.

Mahitaji hayo ya msingi ambayo tulitakiwa kuanza kuyatengeneza (siyo kama nchi tu) katika nchi ya kidemokrasia (hasa baada ya utawala wa Rais Mwinyi) naamini hatujafanya hivyo. Vile vitu vya lazima ambavyo vinahitajika kuwemo katika demokrasia hatukivifanyia kazi ipasavyo.

Leo hii naelewa kwanini baadhi ya sheria zilianza kufanyiwa mabadiliko mwanzoni mwa miaka ya 80 (wakati Mwalimu alipokuwa kweli amedhamiria kustaafu). Baadhi ya sheria kali nyingi zilianza kufutwa wakati huo na matarajio ya sisi wengi ni kuwa wakati ule ndio ulikuwa wakati muafaka wa kuanza kweli kujenga demokrasia.

Naamini ni lazima turudi kufanya vitu vya msingi sambamba na vile tunavyoendelea navyo. Vitu hivyo vya msingi (vya lazima) katika utawala wa kidemokrasia ni hivi vifuatavyo:

a. Mgawanyo wa Madaraka na Mfumo wa Kusimamiana (separation of power and the system of checks and balances). Kwa muda mrefu Tanzania tumekuwa tukizungumzia kile tunachokiita kama "balance of power" ambapo tunasema kuwa tuna mihimili mitatu ya dola. Lakini kwa kiwango kikubwa hatujaweka mfumo mzuri wa kusimamiana kati ya pande hizi tatu.

b. Utawala wa Sheria (the rule of law). Mojawapo ya vitu ambavyo vinatofautisha utawala wa kidemokrasia na ule wa kiimla au wa kifalme ni kuwa sheria ndiyo Mbabe (the tyranny of the law). Kwamba katika nchi hiyo Sheria ni kitu kinachotukuzwa kuliko kitu kingine chochote. Hili nitafafanua katika makala yangu ya Tanzania Daima wiki hii kuelezea kwanini Ofisi ya Mwendesha Mashtaka siyo huru!

c. Uwazi wa vyombo vya Umma: Mojawapo ya vitu vya msingi katika demokrasia ni kuhakikisha kuwa chombo chochote cha umma kinachotumia kodi za wananchi hata senti moja tu ni lazima kiwe wazi kwa wananchi hao. Katika utawala wa demokrasia hakuna chombo/mtu/ofisi/taasisi/idara au chumba chochote ambacho kinatumia fedha za walipa kodi ambacho ni "siri". Leo hii nikitaka kujua Rais analipwa mshahara wa kiasi gani itakuwa mbinde. Leo mtu akisimama na kuuliza hivi wale waandishi wa vyombo binafsi wanalipiwa na serikali wakati Rais au Waziri Mkuu anaposafiri wanalipwa hivyo kwa misingi gani, jibu lake itakuwa ni vurugu! Hivyo ni lazima kufungua taasisi za serikali kwa wananchi na hapa inanileta kwenye jambo la nne.

d. Uhuru wa vyombo vya habari. Uwepo na kuendelea kuwepo kwa sheriia ya Magazeti ya mwaka 1976, sheria ya Usalama wa Taifa ya 1970 (na mabadiliko yake) na sheria ya Madaraka ya Rais wakati wa Dharura ni uwazi kuwa hakuna uhuru wa vyombo vya habari nchini. HIvi sasa vyombo vingi vya habari vinafanya kazi si kwa sababu viko huru bali kwa sababu vimeachiliwa kufanya kazi kwa hisani ya Waziri.

Vyombo vya habari vya TAnzania havifanyi kazi yake kwa sababu vinauhuru ndani yake la hasha! vinafanya kazi kwa sababu Waziri anayehusika ameamua kutoviingilia kati lakini akiamu wakati wowote ule anaweza kuvizima na kuvifungia.

Leo hii uhuru wetu wa vyombo vya habari bado haujajalibiwa kabisa. Uhuru huo utajaribiwa pale ambapo itatokea vurugu nchini, au uchafuzi fulani na vyombo vya habari vikaruhusiwa kuripoti kama ilivyo.

e. Ushirikishwaji wananchi katika maamuzi ya Taifa lao. Katika utawala wa demokrasia, watu ndio wanaipa serikali nguvu yake na ni wao ndio waamuzi wa mwisho wa hatima ya maisha yao. Leo hii kazi hii imeachiwa kikundi cha watu wachache ambao wanaamini kuwa wao ndio zawadi ya mungu kwa raia. Kundi la watu hawa ndio waamuzi wa nini kifanyike, nani asemwe na nani asisweme; ni wao wanaamua bila kujali matwaka ya watu (sijasema wanachama wao) na wanafanya wapendalo.

Katika demokrasia ya kweli wananchi wana sauti ambayo inazidi sauti ya majeshi. Sauti hiyo ya watu imekusanywa mahali pamoja tu hapo ni Bungeni. Hata hivyo Bunge ni wawakilishi tu wa wananchi na siyo kwamba wanakuwa mbadala wa wananchi wenyewe. WAbugne wasiowakilisha matakwa ya wananchi wanapoteza sifa yao ya kuwa wawakilishi. Siku wabunge wakianza kuwakilisha vyama vyao, itikadi zao, marafiki zao au familia zao wanapoteza sifa na tunu ya kuwa wabunge.

Ni kwa sababu hiyo basi wananchi wanabakia na uwezo wa kumuondoa Mbunge yeyote kwa kura. Binafsi ningependa kuona pia tuongeze uwezo leo hii wa kumrecall Mbunge yeyote wakati wowote baada ya mwaka mmoja tangu achaguliwe au wakati wowote kabla ya mwaka wa mwisho wa ubunge wake. Wananchi wawe na uwezo wa kumtimua mbunge wao wakati wowote ule endapo wataona kuwa hawakilishi maslahi yao.

Nguvu hii ya wananchi ni lazima ilindwe kwenye demokrasia.

Katika maelezo hayo marefu nimeelezea sana kuhusu vitu vya lazima na vya msingi. Vipo vile vya mtu mmoja mmoja na vipo vile vya jamii nzima na hasa vile vya nchi ya kidemokrasia. Ili tuweze kufikia mafanikio kama Taifa nakuweza kuona maisha ya afueni kwa wananchi wetu ni lazima tufanye vitu vya msingi kwanza.

Tulipoacha kufanya yale ya msingi na kuanza kushughulikia yale ya mwisho tunajaribu kujenga nyumba bila kuchimba msingi kama walivyofanya Kenya, Zaire, Uganda, Rwanda n.k Nchi hizi zote zilifikiria kuwa kupata uhuru peke yake inatosha kuanza kulijenga Taifa. Leo hii nchi hizi zimegundua (ingawa zimechelewa) kuwa kuna vitu vya msingi vinahitajika kufanywa kwanza kabla hujaanza kujenga jumba la mafanikio. Vinginevyo mafanikio yake utayajenga kwenye msingi dhaifu na siku ukitokea msuko suko kidogo tu jengo lako linaporomoka kama biskuti zilichovywa kwenye chai ya rangi!

Nasema, ni lazima tufanye vitu vya msingi kwanza kabla hatujaanza kufanya vile vingine. Tusipofanya hivyo, tutajikuta tunajenga mafanikio yetu kwenye msingi wa mchangani ambao haujachimbwa chini sana. HIvyo mafanikio yetu ni mafanikio ya kupotosha kwani yanatukuza kilichojuu tu na hivyo yanakuwa ni mafanikio tete. Nasema turudi kwenye vitu vya msingi kwanza.
 
c. Uwazi wa vyombo vya Umma: Mojawapo ya vitu vya msingi katika demokrasia ni kuhakikisha kuwa chombo chochote cha umma kinachotumia kodi za wananchi hata senti moja tu ni lazima kiwe wazi kwa wananchi hao. Katika utawala wa demokrasia hakuna chombo/mtu/ofisi/taasisi/idara au chumba chochote ambacho kinatumia fedha za walipa kodi ambacho ni "siri". Leo hii nikitaka kujua Rais analipwa mshahara wa kiasi gani itakuwa mbinde. Leo mtu akisimama na kuuliza hivi wale waandishi wa vyombo binafsi wanalipiwa na serikali wakati Rais au Waziri Mkuu anaposafiri wanalipwa hivyo kwa misingi gani, jibu lake itakuwa ni vurugu! Hivyo ni lazima kufungua taasisi za serikali kwa wananchi na hapa inanileta kwenye jambo la nne.

Hii mimi ndiyo inayonitibua! Siri hata pasipo ulazima wa siri!
 
On Necessary Things (Public Discourse 3)
Na. M. M. Mwanakijiji ........................................................................ ...............................................................................................
Hapa ndipo inanirudisha wakati wa Uhuru. Je sisi kama nchi ni vitu gani tulitakiwa tuvifanye kwanza? Hofu yangu ni kuwa tulianza vizuri sana (ingawa kuna watu hawataki kuamini hivyo). Jukumu la serikali ya Mwalimu ilikuwa siyo kutufikisha kwenye "self-actualization" bali kuliandaa taifa kutimiza mahitaji ya msingi (basic needs).

Nakumbuka Mwalimu alikuja na hilo wazo la "Mahitaji ya Msingi" ambayo naamini yalitokana na elimu hii ya Maslow kwamba Watanzania kabla hawajafikia kiwango fulani hawana budi kutimiza mahitaji fulani ya msingi ambayo yalikuwa ni yale mahitaji ya msingi ya mwanadamu ambayo ni Chakula (bora na chenye lishe), Mavazi (hifadhi ya mwili wake), Malazi (usalama wa nafsi yake), na elimu.

Kwangu sehemu moja iliyosahaulika na kutopewa umuhimu wake kamili ni mawasiliano na hasa katika nyanja ya usafiri. "Self-actualization" kama taifa bila msingi wenye njia thabiti ya ndani inayowawezesha wananchi wake kuwasiliana kwa urahisi ni vigumu kufanikiwa haraka. Mawasiliano kama ya barabara yanarahisisha utolewaji wa huduma kama elimu na afya na ni muhimu katika kuhakikisha ulinzi na usalama. Uduni wa mawasiliano huzorotesha mwingiliano katika jamii na hivyo kurutubisha makundi na utengano. Naamini mawasiliano imara yangeondoa umuhimu wa kuanzisha vijiji vya ujamaa kwani ingekuwa rahisi kusambaza huduma inakohitajiwa. Kwamba hadi leo hii kuna sehemu haziwezi kufikiwa kwa urahisi ni ishara tosha kuwa kuna sehemu tulilipua.
 
mag, wenzio wanasema wamekupatia cell phones siku hizi; mawasiliano gani unayoyataka. Leo mtu anaweza kuzungumza toka kijijini hadi mjini..
 
mag, wenzio wanasema wamekupatia cell phones siku hizi; mawasiliano gani unayoyataka. Leo mtu anaweza kuzungumza toka kijijini hadi mjini..

Ninaposema mawasiliano naongelea "transportation" kwa ujumla wake (labda kiswahili kinanipa taabu). Cell phone haifikishi chakula wala dawa bila barabara, reli n.k.
 
Mwanakajiji,
Mkuu maneno mazito sana na mazuri kuyazungumzia. Huyu Maslov anajaribu kutukumbusha tu kwani haya maswala hayana elimu..nikiwa na maana kuwa hayana uvumbuzi..Hata hivyo kasahau KUNYWA kwani kunywa na KULA ni vitu viwili tofauti.

Tatizo la viongozi wetu ni wapuuzi, wameshindwa kabisa kuweza maazimio toka Nyerere alipoondoka. Sasa hivi kila kitu tunapangiwa na IMF, hayo ya Millenium sijui Kupunguza Umaskini na kadhalika..lakini wapi bado tunavurunda kishenzi..
Hata ukitazama mpango wa Saccos nchi kama Uganda na Kenya wameweza kufanikiwa vizuri sana na kiasi kwamba wakulima wa nchi hizo wameweza kuongeza pato la kilimo mwaka hadi mwaka..Sisi ndio kwanza Kikwete alizigawa ovyo ovyo, sijui kwa watengeneza vyungu na shanga za Kimasai.
Yaani basi tu hakuna haja ya kuendelea!
 
e. Ushirikishwaji wananchi katika maamuzi ya Taifa lao. Katika utawala wa demokrasia, watu ndio wanaipa serikali nguvu yake na ni wao ndio waamuzi wa mwisho wa hatima ya maisha yao. Leo hii kazi hii imeachiwa kikundi cha watu wachache ambao wanaamini kuwa wao ndio zawadi ya mungu kwa raia. Kundi la watu hawa ndio waamuzi wa nini kifanyike, nani asemwe na nani asisweme; ni wao wanaamua bila kujali matwaka ya watu (sijasema wanachama wao) na wanafanya wapendalo.

Katika demokrasia ya kweli wananchi wana sauti ambayo inazidi sauti ya majeshi. Sauti hiyo ya watu imekusanywa mahali pamoja tu hapo ni Bungeni. Hata hivyo Bunge ni wawakilishi tu wa wananchi na siyo kwamba wanakuwa mbadala wa wananchi wenyewe. WAbugne wasiowakilisha matakwa ya wananchi wanapoteza sifa yao ya kuwa wawakilishi. Siku wabunge wakianza kuwakilisha vyama vyao, itikadi zao, marafiki zao au familia zao wanapoteza sifa na tunu ya kuwa wabunge.

Ni kwa sababu hiyo basi wananchi wanabakia na uwezo wa kumuondoa Mbunge yeyote kwa kura. Binafsi ningependa kuona pia tuongeze uwezo leo hii wa kumrecall Mbunge yeyote wakati wowote baada ya mwaka mmoja tangu achaguliwe au wakati wowote kabla ya mwaka wa mwisho wa ubunge wake. Wananchi wawe na uwezo wa kumtimua mbunge wao wakati wowote ule endapo wataona kuwa hawakilishi maslahi yao.

Nguvu hii ya wananchi ni lazima ilindwe kwenye demokrasia.

Mkuu Mwanakijiji,

Hapa tupo ukurasa mmoja, maana yake ni moja tu nayo ni mabadiliko ya katiba.
 
Back
Top Bottom