Elections 2010 Joto la Uchaguzi Mkuu Zanzibar 2010:

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,297
33,082
Wakati zoezi la uchukuaji fomu za urais Zanzibar utaanza Juni 21, mwaka huu, joto la mtu atakayemrithi Rais Amani Abeid Karume, limezidi kupanda.
Kampeni za chinichini zinafanyika kwa kasi, huku baadhi ya vigogo wakihofia kuwepo dalili za kuchezewa `mchezo mchafu.’
Uchunguzi uliofanywa na Nipashe mjini hapa, ulibaini kuwa wanaotajwa kutaka kugombea urais wa Zanzibar, wamekuwa na wakati mgumu kuzunguka Pemba, Unguja na Tanzania Bara, wakitafuta kuungwa mkono.
“Mara nyingine wanapishana angani wakiwa kwenye ndege,” alisema mmoja wa vyanzo vyetu ndani ya CCM kisiwani hapa.
Inaelezwa kuwa ziara za wagombea watarajiwa hao, zinalenga kukutana na wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) ya CCM, yenye mamlaka ya kumtangaza mgombea urais wa Zanzibar.
Kampeni hizo tayari zimesababisha CCM Zanzibar kutoa maonyo mara kadhaa kwa wagombea hao, huku kukiwepo vitisho vya kuwafuta katika uteuzi, watakaobainika kuendesha kampeni kabla ya wakati uliopangwa na chama hicho.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Saleh Ramadhan Ferouz, alisema chama hicho kimeamua kubadilisha ratiba ya uchukuaji fomu za urais wa Zanzibar.
Alisema kamati maalum ya Nec, Zanzibar, itakutana Julai 9 mwaka huu, kuweka alama kwa wanachama watakaojitokeza kuwania nafasi urais.
Orodha hiyo itawasilishwa katika vikao vya Kamati Kuu (CC) na Nec kwa uamuzi wa mwisho.
"Suala la mgombea urais ni zito na ndio maana tumeamua lishughulikiwe mwanzo, kabla ya wagombea wengine", alisema Ferouz.
Hata hivyo, uchunguzi wa Nipashe unaonesha kwamba wakati ratiba hiyo mpya ikitolewa, wana-CCM wenye nia ya kugombea urais Zanzibar, wapo katika hatua za mwisho, kukamilisha kampeni kwa wajumbe wa Nec waliopo Zanzibar na Tanzania Bara.
Hata hivyo, suala la serikali ya mseto Zanzibar linaonekana kuwavuruga vigogo wa CCM, ambapo baadhi yao wameamua kwenda kinyume na msimamo wa chama hicho na kuanza kuwashawishi wananchi kupiga kura ya hapana kwa serikali ya umoja wa kitaifa.
Habari zilizopatikana ndani ya CCM kisiwani hapa, zinasema kuwa jina la mwanasiasa mwandamizi, aliyewahi kushika moja ya nafasi za juu katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), linatajwa kupewa nafasi kubwa ya kupitishwa.
Mwanasiasa huyo (jina tunalihifadhi) anadaiwa kupata mafanikio baada ya kuwashawishi wajumbe wengi wa Nec upande wa Tanzania Bara.
Anatajwa kuwa ni mzoefu wa kampeni za kuwania kuteuliwa nafasi ya urais kupitia CCM.
Wanachama kadhaa akiwemo aliyewahi kuwa Waziri Kiongozi wa SMZ, Dk Ghalib, Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Shein, wanatajwa kuwa na nia ya kugombea nafasi hiyo.
Pia wamo Waziri Kiongozi wa Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha, Naibu Waziri Kiongozi, Ali Juma Shamuhuna, Waziri wa Nchi Afisi ya Makamu wa Rais (Muungano) Mohammed Seif Khatib.
Wengine ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Haroun Ali Suleiman, Naibu Waziri wa Masuala ya Afrika Mashariki, Mohammed Aboud.
Mwingine ni Balozi Ali Karume, ambaye alikuwa wa kwanza kutangaza hadharani nia yake ya kutaka kumrithi Rais Karume ambaye ni kaka yake.
Inaelezwa kuwa kutajwa kwa Dk. Shein kutaka kuwania nafasi hiyo, kumesababisha baadhi ya wenye nia ya kugombea, kuondokana na azma hiyo kwa madai ya kulinda itifaki, kwa vile miongoni mwao ni wasaidizi wake wa karibu katika nafasi ya Umakamu wa Rais.
CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom