Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,810
- 15,395
Mtoto JonBenet Ramsey
John na Patsy Ramsey
Patsy Ramsey
JonBenet, Melinda, Burke na John Andrew Ramsey
John na Patsy Ramsey wakitangaza zawadi
John Mark Karr mtu aliyejipachika tuhuma za mauaji ya mtoto JonBenet Ramsey
Mnamo Desemba 26, 1996 mwili wa mtoto JonBenet Patricia Ramsey aliyekuwa na umri wa miaka sita wakati huo ulikutwa ghorofa ya chini (Basement) ya nyumba yao, ikiwa ni karibu saa nane tangu aliporipotiwa kutekwa nyara na watu wasiojulikana. Tukio hilo liliibua hisia tofauti miongoni mwa jamii ya Wamarekani kwa sababu, JonBenet pamoja na kuwa na umri mdogo, lakini alikuwa anashikilia mataji takriban 50 ya urembo kwa watoto aliyoshiriki katika maeneo tofauti nchini humo.
Jina la JonBenet ni muunganiko wa majina ya baba yake John Bennet Ramsey 53, bilionea na mmiliki wa viwanda nchini Marekani na mama yake Patricia (Patsy) Ramsey ambaye naye aliwahi kushikilia taji la West Virginia mwaka 1977 nchini Marekani. Kutokana na mama yake kushiriki mashindano ya urembo enzi ya usichana wake, vivyo hivyo alitaka na mwanaye pia afuate nyayo zake.
Awali John alifunga ndoa na mwanamke aliyetajwa kw ajina la Lucinda Pasch Ramsey Cindy mnamo July 1966 na walibahatika kupata watoto watatu ambao ni Elizabeth Ramsey ambaye alizaliwa mwaka 1969, lakini alikuja kufariki mnamo agosti 1, 1992 kwa ajali ya gari huko Illinois, Melinda Ramsey alizaliwa mwaka 1972 na John Andrew Ramsey aliyezaliwa mwaka 1976. Kati ya mwaka 1977 na 1978 John Bennet Ramsey na mkewe Lucinda Pasch Ramsey Cindy waliaachana kisheria.
Mnamo Novemba 5, 1980 John Ramsey alifunga ndoa na Patricia Paugh Ramsey (Patsy) huko Atlanta Georgia na mtoto wa kwanza Burke Hamilton Ramsey alizaliwa mwaka 1987 na mtoto wao wa pili na wa mwisho JonBenet Ramsey alizaliwa mnamo Agosti 6, 1990 huko Atlanta Georgia.
Alikuwa ni Patsy Ramsey mama wa mtoto JonBenet aliyeamka asubuhi na mapema na siku ya Desemba 26, 1996 na kukutana na barua ndefu sebuleni yenye kurasa tatu iliyoandikwa kwa mkono ikiwafahamisha kwamba mtoto wao JonBenet ametekwa nyara na watekaji hao walikuwa wanahitaji kiasi cha dola za marekani zipatazo 118,000 ili wamrejeshe akiwa salama. Pia barua hiyo ilikuwa na tishio la kutahadharisha familia ya JonBenet kwamba iwapo watawajulisha Polisi au FBI, Binti yao hatakuwa salama.
Kwa mujibu wa Patsy Ramsey, haraka sana alianza kuchunguza hapo nyumbani kwao akianzia chumbani alipolala JonBenet na kwingineko, lakini hakuweza kumwona mwanaye zaidi ya kumkuta mwanaye mwingine wa kiume aitwae Burke aliyekuwa na umri wa miaka 9, akiwa amelala. Aliamua kwenda kumuamsha mumewe na kumpa ile barua ya watekaji. Pamoja na kwamba barua ile ilikuwa na tishio la kuitaka familia ile kutowajulisha Polisi juu ya suala lile, John Bennet Ramsey aliwajulisha Polisi na wakat huo huo aliwasiliana na meneja wa Bank anakoweka fedha zake ili akamilishe mipango ya kumpatia hizo fedha zinazotakiwa na watekaji haraka iwezekanavyo.
Polisi walifika katika eneo la tukio muda mfupi baada ya kujulishwa. Utekaji nyara na mauaji siyo jambo la kutarajiwa sana katika mji wa Boulder, Colorado. Ukweli ni kwamba, hadi kufikia tarehe hiyo ya 26, Desemba, kulikuwa hakuna hata mtu mmoja aliyewahi kuuawa kwa zaidi ya mwaka. Polisi wa Boulder walilazimika kuomba msaada kutoka kwa Polisi wa Denver na FBI. Muda si mrefu Polisi wale walifika na kwa kushirikiana na FBI walikagua nyumba yote iliyokuwa na vyumba 15, huku ikiwa imezungukwa na eneo la bustani la eka mbili, lakini hawakumpata mtoto JonBenet.
Walipomaliza kukagua nyumba hiyo waliihoji familia ya JonBenet kwa saa kadhaa na pia walikaa na familia hiyo kwa muda kiasi wakisubiri simu kutoka kwa watekaji, ambapo hata hivyo hakuna simu iliyopigwa na ilipofika saa saba mchana maafisa wa Polisi na FBI waliondoka katika eneo la tukio wakiacha maagizo kwa familia ya John Ramsey kuendelea kumtafuta mtoto wao JonBenet, pale pale kwenye eneo la nyumbani kwao.
Kwa mujibu wa maelezo ya John Ramsey ni kwamba aliendesha msako mkali katika nyumba yao kwa dakika 15 baada ya Polisi kuondoka. Msako huo ulijumuisha kila kona ya nyumba ile na hatimaye waliukuta mwili wa mtoto wao JonBenet akiwa amekwishauawa. Mwili huo waliukuta ukiwa kwenye chumba ambacho kilikuwa hakitumiki na ambacho vioo vyake vya madirisha vilikuwa vimevunjika. Ramsey aliuchukuwa mwili wa mwanae na kukimbia nao hadi sebuleni ambapo aliulaza karibu na mti wa Mkirismas ambapo mkewe alijaribu kutoa huduma ya kwanza ya kumpulizia hewa mdomoni akidhani labda mtoto amepoteza fahamu tu, lakini kumbe likwishafariki. Wakati huo huo majirani waliokuwa pale nyumbani kuwafariji walipiga simu ya dharura na kuwajulisha Polisi juu ya kupatikana kwa mtoto JonBenet akiwa amekwisha kufa.
Kitendo cha Ramsey kuuondoa mwili wa mwanae kutoka katika eneo la tukio kwa sababu ya kutaka kuokoa maisha yake, kinaweza kueleweka kwamba alikuwa na nia nzuri juu ya maisha ya mwanae, lakini kwa upande mwingine kitendo kile kilikuwa kimetibua kabisa uchunguzi ambao ulitakiwa ufanyike pale pale kwenye eneo la tukio kabla ya kuondoa mwili huo. Hivyo kitendo cha kuondoa mwili huo kilisababisha kikosi cha uchunguzi kushindwa kufanya uchunguzi wa mwili huo ukiwa kwenye eneo la tukio. Hata hivyo Polisi waliuchukuwa mwili wa mtoto na kuondoka nao na baadae usiku huo mwili huo ulifanyiwa uchunguzi katika ofisa ya uchunguzi wa vifo ya wilaya.
Siku iliyofuata asubuhi Daktari bingwa anayeshughuka na uhalifu dhidi ya watoto Dk. Charles Wecht alisema kwamba JonBenet alifariki saa nne usiku. Alieleza kwamba kifo chake kilisababishwa na kuzibwa pumzi na kupigwa kichwani na pia alikuwa amenajisiwa. Katika majumuisho yake kuhusiana na kifo cha mtoto JonBenet, Dk. Wecht alisema kwamba mtu aliyemuuwa mtoto huyo anaonekana ni mtu ambaye JonBenet alimfahamu na kumuamini. Dk. Wecht aliendelea kusema kwamba, JonBenet alikamatwa kama mateka na kuteswa lakini nia ya mtesaji ilikuwa ni kumnajisi kitu ambacho mtoto huyo hakukikubali, hivyo wakati anaendelea kumtesa ndipo akapoteza maisha. Kitu ambacho mhusika hakukitarajia. Kwa kifupi ni kwamba, ulikuwa ni mchezo ambao ulitoa matokea mabaya. Alimalizia kusema Dk. Wecht.
Kwa kawaida kesi yoyote ya mauaji Polisi huanza kuitupia macho familia husika au mtu wa karibu na rafiki wa familia hiyo. Familia ya Ramsey haikuweza kuepuka hilo. Siku iliyofuata baada ya taarifa za kitaalamu kutolewa kuhusiana na kifo cha mtoto huyo, John na Patsy Ramsey walihojiwa kwa muda mrefu katika kituo cha Polisi cha Boulder na pia walitoa vielelezo vya nywele, damu kwa ajili ya vipimo vya DNA na pia muandiko wao kwa ajili ya kufananisha na muandiko wa kwenye barua ya muuaji. John Ramsey na mkewe waliwaambia polisi kwamba siku hiyo ya Krismas familia nzima ilikwenda kulala mapema kwa sababu siku inayofuata asubuhi walikuwa na mpango wa kusafiri kwenda katika mji wa Minneapolis kwa ajili ya mapumziko ya Krismas. Walimlaza JonBenet saa mbili kamili usiku na usiku huo hawakusikia purukushani yoyote. Kitu kilichowashtua asubuhi ni pale mkewe alipoona barua iliyoachwa na watekaji nyara ya madai ya fedha. Hata hivyo kutokana na Polisi kutokuwa na ushahidi wa kutosha wa kuwafungulia mashitaka ilibidi wawaachie.
Siku iliyofuata asubuhi ya Desemba 29, baada ya misa ya kifamilia iliyofanyika katika kanisa la St. Johns Episcopal lililoko katika mji huo wa Boulder wanafamilia hao walisafiri kwa ndege na mwili wa JonBenet hadi katika mji wao wa zamani Atlanta Georgia ambapo walifanya mazishi ya mtoto wao ambayo yalihudhuriwa na waombolezaji zaidi ya 200. JonBenet alizikwa na moja kati ya magauni yake aliyowahi kushiriki nalo kwenye mashindano ya urembo.
Wakati huo huo Polisi walikuwa wakindelea kuipeleleza familia ya Ramsey kuhusiana na mauaji hayo na baada ya siku kadhaa walikuja na taarifa zenye viashiria ambavyo vilikuwa vinaonesha kwamba kati y John Ramsey au mkewe Patsy Ramsey au wote kuna uwezekano walihusika na mauaji ya JonBenet. Polisi walipata vielelezo kadhaa katika nyumba yao ya Boulder. Mojawapo kilikuwa ni kijidaftari kidogo kilichotumiwa na mtekaji nyara kuandika barua ya ujumbe kwa familia ya Ramsey lakini kukiwa na karatasi kadhaa zlizotumiwa kuandika ujumbe huo lakini zikaachwa kutokana na kukosewa.
Polisi walishangaa kwa sababu waliamini kwamba mtekaji nyara yeyote angeandaa barua ya ya kudai malipo ya utekaji nyara (Ramsom Letter) muda mrefu kabla ya kutekeleza utekaji nyara. Hivi inawezekana kweli mtekaji nyara huyo akae muda wote huo kwenye nyumba ya mtu aliyemteka nyara na apate muda wa kukaa na kuandika barua yenye kurasa tatu kwa mkono kisha aondoke, tena akiwa amefanya jaribio la kuandika barua hiyo mara mbili baada ya kukosea? Hili ni swali ambalo liliwaumiza Polisi vichwa.
Polisi pia kupitia picha zilizopigwa kwenye mwili JonBenet ukiwa umevuliwa nguo na kamera maalum inayoweza kusafisha picha hapo hapo muda mfupi baada ya kupigwa (Polaroid Camera) waliona makovu ya michubuko kwenye mikono yake kwa juu karibu na kwapa. Polisi walikuwa walijiuliza kwamba, je JonBenet alikuwa ni mhanga wa unyanyaswaji wa kijinsia na aidha wazazi wake au mtu aliye karibu na familia hiyo?
Katika nyumba ya Ramsey iliyoko Minneapolis anayoitumia kwa likizo, maofisa wa Polisi walikuta kamba ambayo inafanana kabisa na kamba ambayo ilitumika kumnyongea JonBenet. Swali ni je ilifikaje pale? Utata mwingine uliowapa Polisi wakati mgumu kupata majibu ya kuridhisha ni kiasi cha fedha kilichotajwa na mtekaji nyara. Polisi ilikuwa haiwaingii akilini kwamba mtu bilionea kama John Ramsey aamriwe atoe kiasi cha dola sipatazo 118,000 tu. Kwa nini isiwe milioni moja, au mbili au hata zaidi?
Ilibainika kwamba kiasi cha hizo dola 118,000 kilichohitajiwa na mtekaji nyara ndicho ambacho John Ramsey alilipwa kama Bonus yake ya mwaka kutokana na faida iliyozalishwa na kampuni yake. Je inawezekana jambo hili likawa ni nasibu (Coincidence) tu? Wapelelezi katika kesi hii iliyojaa utata walikuwa wakijiuliza maswali mengi ambayo hayakuwa na majibu. Wapelelezi wa Polisi waliamini kwamba, kama familia ya Ramsey haikuhusika na kumuuwa mtoto wao, basi inawezekana muuwaji wa mtoto wao ni mtu wao wa karibu ambaye anafahamu kwa usahihi taarifa zao za kifedha.
Kulikuwa hakuna mahali popote katika nyumba yao kulionyesha kwamba mtekaji nyara alitumia nguvu ili kuingia katika nyumba yao, hapakuwepo na dalili yoyote ya nyumba hiyo kuvunjwa. Lakini hata hivyo Polisi walikuwa wanajiuliza, iweje mtambo maalum wa ulinzi (Security system) ulizimwa?
Lakini swali ambalo lilikuwa linawatatiza Polisi hao wa upelelezi lilikuwa, ni kwa nini JonBenet Ramsey aliuwawa? Ni jambo lililowazi kwamba aliuwawa muda mrefu tu kabla ya mke wa Ramsey hajaona barua iliyoachwa na mtekaji nyara ya kudai malipo, na mwili wake uliachwa mle mle ndani mahali ulipokutwa. Je ni kitu gani ambacho familia ya Ramsey ingenufaika nacho kwa kuwalipa watekaji wakati wanajua mtoto JonBenet amekwishakufa?
Wakati kukiwa hakuna mtuhumiwa yeyote ambaye ameshatiwa mbaroni kuhusiana na mauaji ya binti yao, familia ya Ramsey ilikuwa inajua dhahiri kwamba wanatiliwa mashaka kuhusika na mauaji ya binti yao. Mnamo Januari 1, 1997, ikiwa imepita wiki moja tangu binti yao auawe, John na Patsy Ramsey walisafiri kwa ndege wakiwa pamoja na timu ya washauri wao kuelekea Atlanta. Walipokuwa kule, waliaonekana kwenye TV ya CNN, lengo likiwa sio kuomba msaada katika kufanikisha kukamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa mhusika wa mauaji ya binti yao, bali pia kukanusha tuhuma za kuhusishwa na mauaji ya mtoto wao. Akizungumza kupitia TV ya CNN John Ramsey alisema, tuhuma hizi zimetutia kichefuchefu alikuwa akizungumzia habari zilizosambaa kwenye vyombo vya habari zikimtuhumu yeye na mkewe kuhusika na mauaji ya binti yao.
Sisi ni familia iliyobobea kwenye ukristo. Alisema, kisha akaongeza, na kuhusishwa kwetu katika jambo hilo, ni kitu kisichowezekana
Ramsey alisema kwamba, ametoa zawadi ya kiasi cha doal 50,000 kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa zitakazopelekea kukamatwa kwa muuwaji wa JonBenet. Aliendelea kusema kwamba amekubaliana na mpelelezi wa zamani wa FBI aliyestaafu John Douglas arudi kazini kushughulikia kesi ya mwanae. John Douglas ni mpelelezi mahiri aliyejijengea heshima katika shirika hilo la upelelezi la nchini Marekani la FBI. Wakati wa mahojiano yao na CNN Patsy hakuwa mzungumzaji lakini baadae alisema kwa kifupi kwamba anaamini muuwaji wa binti yao yupo na hajakamatwa tu.
Polisi wa mji wa Boulder hawakufurahishwa na maelezo ya familia ya Ramsey wakati wanaongea na CNN, na siku iliyofuata Meya wa mji huo na maofisa wa Polisi waliitisha mkutano na vyombo vua habari ambapo walikanusha kauli iliyotolewa na mke wa Ramsey aliposema kwamba muuwaji wa binti yao yupo na hajakamatwa. Maofisa hao walisisitiza kwamba mauaji ya JonBenet siyo endelevu, hivyo waliwataka wakazi wa mji huo kulala kwa amani bila hofu kwa sababu hakutatokea mauaji kama hayo tena. Maofisa hao walidai kwamba wanamjua aliyemuuwa mtoto JonBenet Ramsey na bado kitambo kidogo watathibitisha madai yao.
Kwa muda mfupi Polisi walihamisha hisia zao kuwatuhumu John na Patsy Ramsey na mauaji ya binti yao na kulekeza hisia zao kwa watoto wake aliowazaa katika ndoa yake ya awali waitwao Melinda na John Andrew Ramsey.
Pamoja na minongono iliyoenea kwamba walionekana katika mji huo wa Bouliver siku ya Krismas, lakini wote walidai kwamba walikuwa Atlanta siku hiyo ya tarehe 25 Decemba na siku iliyofuata yaani tarehe 26 Desemba waliondoka katika mji huo kuelekea katika mji wa Minneapolis ambapo walipanga kukutana na baba yao pamoja na mama yao wa kambo na wanae katika nyumba yao wanayoitumia wakati wa likizo hapo Minneapolis, hata hivyo rafiki mmoja wa familia aliwapigia simu na kuwajulisha kwamba mtoto JohnBenet ametekwa nyara na hajulikani alipo. Walipanda ndege hadi katika mji wa Denver na hapo walichukuwa taxi hadi Boulder.
Polisi waliyachukuwa maelezo yao na kutokana na kutokuwa na muunganiko na tukio hilo, walibadilisha hisia zao kutoka kwa watoto hao na kuwageukia John na Patsy Ramsey wazazi wa mtoto JonBenet.
Mnamo Februari 8. 1997 Kitengo cha kuzuia uhalifu cha Boulder kilitangaza kwamba familia ya Ramsey itatoa awadi ya dola 100,000 kwa mtu yeyote atakayejitokeza kutoa taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwa muuaji na kuhukumiwa. Rais wa kitengo cha kuzuia uhalifu cha kimataifa Larry Wieda alifafanua juu ya hatua hiyo. Tunachofanya ni kuhakikisha hakuna taarifa zinazotupita juu ya tukio hili. Aliendelea kusema kwamba kwa kawaida taasisi anayoiongoza huwa inatoa zawadi inayofikia dola 10,000, lakini akaongeza, Siwezi kukumbuka kesi yoyote ambayo ilipatiwa ufumbuzi kutokana na kiasi kikubwa cha zawadi kilichoahidiwa.
Hata hivyo kiwango hicho kilichotangazwa na familia ya Ramsey kiliamsha mwamko kutoka kwa jamii ya Wamarekani kutoa taarifa kwenye taasisi hiyo ya kuzuia uhalifu. Kwa muda mfupi taasisi hiyo ilipokea simu zaidi ya 1,500 kutoka kwa raia wema ambao walidai kwamba wana taarifa ambazo zitasaidia kupatikana kwa muuaji. Mpaka kufikia katikati ya Februari Polisi walikuwa wamepokea barua zipatazo 1,000 na simu zapatazo 3,000. Polisi walisema kwamba kati ya hizo taarifa ni asilimia 5 to ambazo zinaonekana huenda zikazaa matunda, lakini pia waliwatahadharisha wananchi kutowapotezea Polisi muda. Kauli hiyo ilitokana na baadhi ya taarifa kuonekana zisizo na mashiko. Akitolea mfano baadhi ya taaarifa hizo ni pamoja na zile ambazo wapo waliodai kwamba wana uwezo wa kufanya miujiza na kumbaini muuaji.
Kuanzia hapo, Polisi wakawa hawatoi taarifa zozote kwenye vyombo vya habari kuhusiana na kesi hiyo, na upelelezi wa kesi hiyo ulionekana kufanywa kwa siri sana. Wakati John Meyer wa kitengo cha uchunguzi wa maiti katika wilaya ya Boulder alipomaliza uchunguzi wa mwili wa JonBenet Ramsey hapo mnamo Februari 11, 1997, alikataa kutoa taarifa kwa undani kuhusiana na matokeo ya uchunguzi wake akidai kwamba askari wa upelelezi wa mji huo wa Boulder na waendesha mashitaka wanaohusika na kesi hiyo walimuonya kwamba, iwapo atatoa matokeo ya uchunguzi wake itaathiri kwa kiasi kikubwa mwenendo wa upelelezi wao katika kumtafuta muuaji.
Msemaji wa kitengo hicho cha uchunguzi wa maiti alisema kwamba, miongoni mwa taarifa za uchunguzi wa mwili wa binti huyo ambazo Polisi na ofisi ya mwanasheria wa wilaya ambazo wasingependa ziwekwe hadharani ni kuhusu majeraha mangapi yamekutwa kwenye mwili wa marehemu, idadi ya vielelezo vilivyokusanywa baada ya uchunguzi, na mbinu iliyotumiwa na muuaji kutekeleza mauaji hayo (details of the Modus operand of the killer)
Hata hivyo kuna taarifa iliyovuja kufuatia uchunguzi wa mwili wa binti huyo ni kwamba, mwili wa binti huyo ulikutwa ukiwa na michubuko ya muda mrefu katika uke ambapo ripoti hiyo ilieleza kwamba michubuko hiyo inawezekana ilitokana na binti huyo kunajisiwa mara kwa mara.
Haraka sana msemaji wa familia ya Ramsey Pat Korten alizungumzia tuhuma hizo na alimshirikisha aliyekuwa daktari wa binti huyo ambaye alikanusha kwamba hajawahi kuona ushahidi wowote kwa binti huyo unaoonyesha kwamba alikuwa akinyanyaswa kijinsia. Mwezi huo wa Februari haukuwa mzuri sana kwa familia ya Ramsey, kutokana na jinsi Polisi walivyokuwa wakiizungumzia kesi ya binti yao na hiyo ilisababisha mahusiano ya familia ya Ramsey na Polisi kutokuwa mazuri.
Ilipofika Februari 12, 1997, Polisi waliwataka John na Patsy Ramsey kuripoti makao makuu ya Polisi kwa ajili ya kutoa sampuli nyingine ya muandiko wao kwa mkono. Msemaji wa familia hiyo Pat Korten akizungumza na vyombo ya habari aliwaambia waandishi wabari kwamba wateja wake wamekataa kukubaliana na matakwa hayo ya Polisi kwa sababu walishatoa sampuli zao za muandiko wao, pamoja na damu na sampuli ya nywele zao. Ofisi ya mwanasheria wa wilaya ilijibu hoja hiyo na kutishia kutumia mamlaka ya mahakama kumshurutisha John na Patsy Ramsey kutekeleza matakwa ya Polisi.
Kutokana na tishio hilo Ramsey na mkewe walikubali kutoa ushirikiano kwa Polisi, hivyo walikwenda kutoa sampuli ya mwandiko wao. Hata hivyo siku chache baadae Polisi waliwasiliana na Ramsey na mkewe wakihitaji tena sampuli ya miandiko yao. Kitendo hicho kilisababisha msemaji wa familia ya Ramsey Pat Korten kuzungumzia jambo hilo kwenye vyombo vya habari. Akiongea na vyombo vya habari msemaji huyo alisema, walileta maombi yao yasiyo na maandishi kwamba wanahitaji sampuli nyingine ya muandiko, na tulitoa ushirikiano, hivi sana wanahitaji tena sampuli nyingine, sisi tunawaambia watupe sababu ambayo itatuingia akilini ya kuhitaji sampuli hiyo mara kwa mara. Tumekuwa na ushirikiano na Polisi tangu awali, lakini sasa sidhani kama tunaweza kuendelea . Nadhani, lakini sina uhakika.
Kutokana na John na Patsy Ramsey kuonekana makao makuu ya Polisi mara kwa mara, waandishi wa habari walijenga nadharia kwamba wao ndio washukiwa wakuu wa mauaji hayo. Kuanzia hapo wakawa wanawindwa na vyombo vya habari kila waendapo ambapo nao wakawa wanawakwepa kwa kuhama kutoka eneo moja la siri walipokuwa wamejificha hadi jingine ili kuwakwepa waandishi wa habari.
Mnamo Februari 24, 1997, mwanasheria wa wilaya ya Boulder Alex Hunter aliiwasilisha maelezo mafupi kuhusu kesi hiyo katika mahakama ya wilaya kuhusiana na shauri hili ambalo bado lilikuwa likiwaumiza vichwa wapelelezi wa Marekani. Kwa kifupi mwanasheria huyo alisema, John na Patsy Ramsey bado hawajaondolewa kwenye tuhuma za mauaji ya binti yao.
Msemaji wa familia ya Ramsey hakuikalia kimya taarifa ile. Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari hapo mnamo Februari 25, Pat Korten alisema, kinachotakiwa ni kusikiliza kile Polisi na ofisi ya mwanasheria wa wilaya walichokisema kwamba wanaichukulia familia ya Ramsey kama watuhumiwa namba moja katika orodha yao. Hata hivyo Polisi waliwataka tena John na Patsy Ramsey kwenda kutoa sampuli nyingine ya muandiko wao kwa mkono, lakini hata hivyo walionekana kukosa ushahidi makini wa kuwafikisha mahakamani.
Mnamo June 24, 2006 Patricia Ramsey (Patsy) alifariki akiwa na umri wa miaka 49 huku akiacha kitendawili cha kukamtwa kwa muuaji wa mwanae hakijateguliwa. Mama huyu alifariki kwa ugonjwa wa kansa ya kizazi, ambayo aligundulika kuwa nayo mwaka 1993. Alizikwa pembeni ya kaburi la mwanaye JonBenet Ramsey huko Georgia.
[h=3]Mnamo Agosti 16, 2006 mtu mmoja aliyetajwa kwa jina la John Mark Karr raia wa Marekani aliyekuwa akifundisha Kiingereza nchini Thailand alikamtwa baada ya kukiri kwamba ni yeye aliyemuuwa mtoto JonBenet Ramsey. John Mark Karr alikuwa akiwasiliana kwa njia ya barua pepe (email) na mwandishi mmoja wa habari na profesa wa chuo kiku cha Colorado aitwae Michael Tracey. John Karr Alikuwa akitumia anuani ya barua pepe ya December261996@yahoo.com . tarehe hiyo ndiyo ambayo mtoto Jonbenet aliuawa.[/h][h=3]Alirudishwa nchini Marekani lakini baada ya uchunguzi wa vipimo vya DNA vikaonyesha kwamba havifanani na vile vilivyokutwa kwenye mwili wa mtoto JonBenet.[/h]Mnamo Agosti 28, 2006 ofisi ya mwanasheria ya wilaya ya Boulder ilisema kwamba John Mark Karr hatashitakiwa kwa kusababisha usumbufu na alitaja gharama za upelelezi wa tuhuma zake alizojipachika kuwa zilifikia kiasi cha dola 13,000 na kiasi kingine kinachookadiriwa kufikia dola 30,000.
Rafiki wa karibu wa familia ya Karr aitwae McCrary alisema kwamba Karr hakuhusika na mauaji hayo, huyu ni mtu mwenye tabia ya kubaka watoto wadogo (Pedophile) na sio muuaji alisema McCrary. McCrary alimuelezea John Karr kama mtu mwenye akili za ziada (Genuis) ambaye alitumia mbinu hiyo ya kukiri Kumuua mtoto JonBenet ili kukwepa kifungo nchini Thailand ambapo alikuwa kikabiliwa na tuhuma mbalimbali za ubakaji wa watoto. Na alijua kwamba kwa kukiri kwake kuhusika na mauaji hayo atarudishwa nchini Marekani ambapo alijua wazi hatakutwa na hatia ya kosa hilo.
Mnamo mwaka 2010 Johna Mark Karr alitangaza rasmi kutaka atambuliwe kama mwanamke (Trans Woman) ingawa hakufanya upasuaji wa kubadili jinsia. Alitaka atambuliwe kwa jina la Alexis Valoran Reich na alipata kitambulisho rasmi chenye utambulisho huo mpya na alibadilisha muonekano wake na mavazi kwa kuvaa kama mwanamke
Alexis Valoran Reich
John Bennet Ramsay na familia yake walihamia katika jimbo la Michigan na kuanza maisha mapya baada ya misukosuko ya kesi hii.
Hata hivyo bado Polisi wanaendelea na upelelezi wa kesi hii.