Kiwi
JF-Expert Member
- Sep 30, 2009
- 1,054
- 990
Mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, ameonya kuwa kama wagombea ubunge na udiwani kupitia chama chake watabweteka, kuna uwezekano kwa wapinzani kuibuka na ushindi katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, mwaka huu.
Alitoa angalizo hilo jana alipokuwa akizungumza na viongozi wa chama hicho ngazi ya mashina, matawi, kata zilizopo katika jimbo la Kawe jijini Dar es Salaam.
Alisema wagombea ubunge na udiwani kupitia CCM, wanapaswa kutambua kuwa uchaguzi ni kama vita, ambayo chama na wagombea wanawajibika kutumia nafasi zilizopo kwa umakini ili kupata ushindi.
Rais Kikwete alisema viongozi na wagombea ubunge na udiwani wa chama hicho wanapaswa kuzungumzia kero za wananchi badala ya kusoma Ilani ya Uchaguzi katika kampeni zao.
Alisema ilani hiyo itakayotekelezwa kati ya 2010 na 2015, inazungumzia zaidi mambo ya kitaifa yasiyogusa moja kwa moja mahitaji ya watu katika baadhi ya maeneo hapa nchini.
Alisema wagombea ubunge na udiwani wa CCM, wana wajibu wa kuwafahamisha wananchi jinsi serikali ilivyotatua na jinsi inavyoendelea kushughulikia kero za kijamii.
Viongozi wenzangu, shida za wananchi tunazijua kwa kuwa tuko madarakani katika serikali ya awamu ya nne tuliposhinda mwaka 2005, tulikuta matatizo na tukaahidi kuyashughulikia. Tumeshughulikia mengi, yapo ambayo tunaendelea kuyashughulikia na mengine bado, ni wajibu wetu kuwafahamisha wananchi ili watuelewe, alisema.
Alisema viongozi na wagombea wanapaswa kurejea katika mashina, matawi, kata, majimbo na ngazi nyingine za kichama, ili kuangalia matatizo husika na kutoa taarifa sahihi kwa wananchi.
Rais Kikwete alisema kila eneo katika nchi lina matatizo yake, ambayo si lazima yafanane na eneo jingine na kwamba kushinda au kushindwa kwa wagombea wa CCM, kutatokana na namna walivyoshughulikia kero zilizopo. Usitegemee ujenzi wa daraja la Mkapa kule Rufiji, likampa ushindi mtu aliye Bukoba, si rahisi na huwezi kuzungumzia changamoto zinazolikabili jiji la Dar es Salaam katika upande wa msongamano wa magari wakati unagombea Bukoba... ni vitu ambavyo haviendani, alisema.
Rais Kikwete alisema wagombea ubunge na udiwani wa CCM watasaidiwa na jinsi walivyoshughulikia matatizo ya jamii na kusoma ilani ya chama hicho katika kampeni zao.
Aliwataka wagombea wanapokuwa kwa wananchi, wawaeleze ni kwa nini wanapaswa kuichagua CCM na kwa nini wawachague wao (wagombea wa CCM). Na sio kuchagua tu, bali muwaeleze wananchi kwa nini wanapaswa kuichagua CCM kwa kura nyingi, kwani hilo nalo ni la msingi kwa uimara wa chama, alisema.
Alisema CCM inahitaji kura nyingi zitakazokiwezesha kupata nafasi 100 za wabunge wa viti maalum. Wabunge hao wanatokana na jinsi chama kilivyopata kura nyingi, hivyo wafahamisheni wananchi wawaelewe kuhusu jambo hili, alisema.
Pia, Rais Kikwete aliwataka wagombea walioshinda kura za maoni kuwafuata makada walioshindwa ili kupanga mbinu za ushindi kwa pamoja. Alisema suala la kuondoa tofauti kati ya walioshinda na walioshindwa, linawagusa wagombea ubunge na udiwani na si viongozi pekee. Najua binadamu tunatofautiana kupona majereha, wapo ambao inawachukua muda mfupi na wengine inawachukua muda mrefu, lakini mwisho wa siku sisi wote ni wana CCM, alisema.
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara) Pius Msekwa, Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha na viongozi mbalimbali wa chama na serikali.
Wakati huo huo, Rais Kikwete amesema hakuna mkazi wa Kigamboni atakayepoteza haki zake katika mradi wa ujenzi wa mji wa kisasa katika eneo hilo. Alisema hayo wakati akizungumza katika mkutano wa kuzindua kampeni za ubunge na udiwani katika jimbo la Kigamboni jana.
Alisema watendaji wanaohusika katika mradi huo, wanatakiwa kuhakikisha kuwa kila mtu analipwa kwa mujibu wa thamani ya nyumba anayomiliki na bila kuzungushwa. Rais Kikwete, alisema viongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, wanapaswa kutoa maelezo sahihi kwa wananchi kuhusu ujenzi huo, ili waondokane na dhana kwamba lengo ni kulimikilisha eneo hilo kwa wawekezaji.
Alisema kauli nyingi za uzushi zilishatolewa kuhusu mradi huo, ikiwemo ya kumhusisha (Kikwete), kwamba alitarajia kuiuza ardhi ya Kigamboni kwa Rais mstaafu wa Marekani, George Bush. Niliyasikia maneno hayo, lakini nikayapuuzia kwa sababu nilijua yalikuwa ni uzushi mtupu, alisema. Rais Kikwete alisema anaunga mkono wazo la ujenzi huo kwa vile litapunguza msongamano wa wakazi wa Kigamboni kwenda maeneo ya katikati ya jiji kwa ajili ya kutafuta mahitaji yao.
Pia, Rais Kikwete alisema mipango inafanyika kuifanya hospitali ya Taifa ya Muhimbili kuwa na hadhi ya kimataifa, ili itoe huduma wagonjwa wanatoka nje ya nchi. Alisema Taifa limemudu kutibu magonjwa kama moyo, na kwamba jitihada sasa zinaelekezwa katika kufanikisha tiba ya ubongo na mishipa ya fahamu.
Rais Kikwete alisema ujenzi wa daraja la Kigamboni utafanyika hivi karibuni na kwamba hivi sasa jumla ya wakandarasi sita wamejitokeza kuomba zabuni. Alisema mkandarasi atakayeshinda atashirikiana na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa ajili ya ujenzi.
Kuhusu tatizo la maji jijini Dar es Salaam, Rais Kikwete alisema serikali itahakikisha linashughulikiwa na kuwa historia katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
CHANZO: NIPASHE
Naona JK anatapatapa hajui ashike lipi aache lipi. Kweli maji yamefika shingoni.