JK Hana dawa!

Sumaku

Member
Feb 17, 2009
53
1
Na Andrew Mushi

KWa muda sasa tangu nimekuwa nikiandika makala na mada nyingine katika vyombo vya habari , nimekuwa nikipokea maoni mengi sana kwa njia ya barua pepe, simu, ujumbe mfupi wa simu na hata ana kwa ana. Wengi wa wanaotoa maoni wanakimbilia kunyooshea vidole viongozi wa vyama vya siasa na zaidi chama tawala, na taasisi nyingine za utawala ndio wanawajibika kuchukua hatua ili kuleta mabadiliko na maendeleo ya nchi yetu.

Kitu kimoja kinachojitokeza wazi ni kuwa viongozi ndio wanapaswa kuwa wabunifu, kupangilia vizuri mipango ya maendeleo. Zaidi tegemeo limewekwa kwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na baraza la mawaziri na kwa mbali kidogo wabunge. Kwa mtizamo wangu, hapo ndio tunapokosea.

Mbaya zaidi, ni taasisi za kitaifa ndio zinazotazamwa kuwa ndio zenye nafasi ya kuleta mabadiliko. Taasisi kama kijiji, kata au hata wilaya hazionekani kuwa nafasi ya kuwa chachu ya kuleta mabadiliko tunayoyatamani kila kukicha. Pia, kuna asasi na taasisi kama makanisa, misikiti, hospitali, mashule, vyuo na nyinginezo nyingi zina nafasi kubwa sana katika kujenga jamii iliyo tayari kuhamia katika dunia ya kwanza.

Katika mawawasiliano yote hayo niliyotangulia kusema hapo juu hakuna nafasi anajipa mtu wa kawaida -yaani mimi na wewe, katika kuwa sehemu ya ufumbuzi wa haya masahibu yanayotukwamisha kusonga mbele kimaendeleo. Ninaamini kabisa, kuwa matatizo yanayotukabili yamesabishwa na mimi na wewe. Sio viongozi. Usianze kusema nimeongwa na mafisadi niseme hivi. Subiri nifafanunue. Kwa kifupi ni mimi na wewe ndio tunapiga kura. Tunaridhika na t-shirt na pilau ya siku moja, na kuwa radhi kusota kwa miaka mitano. Hili la pilau sitaliongelea leo.

Kwa kutumia nafasi aliyo nayo mtu mmoja mmoja katika kutumia mianya mingi iliyomo katka nafasi na sehemu mbalimbali tunamoishi, kufanyia kazi, kusali ua kuabudu, kusoma, kutembelea, tunaweza kuitumia ikawa chachu ya kupanga mipango mizuri ya maendeleo, kuwa na mitaala bora ya elimu itakayotupa uwezo mkubwa wa kupambana na mazingira yetu. Pia utaweza kuitumia kupiga vita na kuondoa ufisadi, rushwa na uchafu mwingine wowote katika jamii yetu.

Nitajaribu kutumia mifano halisi zaidi kuliko kuongea kinadharia ambayo itakuwa ngumu kueleweka. Kuna walimu wameweza kuleta mbadiliko makubwa na kutisha katika shule zao bila kusubiri wizara ya elimu au Taasisi zinazomiliki hizi shule. Mfano mzuri ni shule za sekondari za Jitegemee na Makongo za Jijini Dar Es Salaam. Jitegemee inamilikiwa na Jeshi na Kujenga Taifa na Makongo inamilikiwa na Jeshi la Wananchi. Miaka ya 1980 hizi shule zilikuwa ovyo kabisa. Mkuu wa shule ya Jitegemee Kanali Massawe aliweza kuwa mbunifu akaigeuza Jitemee ika shule inayofaulisha sana na kubwa na tena yenye mazingira bora ya kusomea. Kanali Kipingu naye alifanya Maajabu Makongo mpaka ikawa inatisha. Hawa wakuu wawili wa shule hawakuishia kuulaumu uongozi wa Jeshi-waliamua kuwa wabunifu.

Miaka ya 1993-96 alisoma bwana mmoja pale Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam. Anaitwa Emmanuel Makundi, huyu jamaa alikuwa anapenda maua sana. Mbele ya chumba chake akaotesha maua pakapendeza sana. Aliishi chumba cha chini na si ghorofani. Wakati huu ndio mazingira ya chuo yalikuwa yameharibika sana na hayatunzwi vizuri.

Wakati anakaribia kumaliza masomo mwaka 1996 Uongozi wa Chuo ukamuuliza amewezaje kutunza maua na mazingira yakapendeza hivyo. Kwa kifupi akawa amepata mwanya wa kuwasimulia na kuanza kushirikiana na uongozi wa chuo. Kwa hizo jitihada za Makundi ulianzishwa mradi mkubwa sana wa kuotesha maua na miti pamoja na utunzaji wa mazingira pale Chuo Kikuu. Bahati nzuri huu ndio wakati pia chuo kimeanza mkakati maalumu wa kuboresha majengo ya chuo ili kiweze kuchukua wanafunzi wengi zaidi.

Ili kuweka mambo vizuri zaidi, kwa kushirikiana na wanafunzi wengine pamoja na chuo wakaanzisha asasi ijulikanayo kama JEMA- Joint Environmental Management Action. Taasisi kwa kushirikiana na chuo kikuu walibadilisha mazingira ya chuo yakawa ya kupendeza na kuvutia sana. Kama Makundi hakuona mwanya na kuchukua hatua ninaamini, labda ule uoza wa Chuo Kikuu wa katikati ya miaka ya 1990 ungekuwepo mpaka leo.

Kwenye miaka ya 1980, kijiji cha Nronga Wilayani Hai kilipoteza watoto watatu kwa kuzama mtoni wakati wakienda kuuza maziwa katika kijiji cha jirani cha Foo. Kijiji cha Nronga ni wafugaji wakubwa wa ng'ombe wa maziwa. Kati ya hivi vijiji viwili kuna mto mkubwa sana, ambao wakati wa masika hufurika. Kuona hivyo akina mama wakasema hatuwezi kukubali watoto wetu waendelee kufa. Wakaanzisha ushirika wao wa kuuza maziwa. Huu sio sawa na ule ushirika ambao serikali inasisitiza vijiji vianzishe. Ni ushirika uliotokana na watu kuamua wenyewe kwa kuona shida na mahitaji yao.

Wakawa wanakusanya maziwa yote kijijini wakaenda kuuza Moshi mjini na Arusha. Leo hii huu ushirika una wanachama zaidi ya 400 na hata vijiji vya jirani wamejiunga nao. Sasa hivi kijiji kina uhakika wa soko la maziwa na hali za wanakikiji ni nzuri sana. Kuna mtu alipata kunisimulia juu ya hiki kijiji, kwamba nyumba za wanakiji zote ni za matofali na kuezekwa kwa bati.

Cha kufurahisha zaidi, wameanzisha mpango ambapo watoto katika shule mbili za Msingi hapo kijijini, shule za Naluti na Nronga, wanakunywa maziwa mara mbili kwa wiki. Tangu wameanza kunywa maziwa, maendeleo yao darasani yamekuwa mazuri sana. Hii ni kwa mujibu wa Hellen Usiri, Mwenyekiti wa huu ushirika wa kina mama. Pia watu waliotembele hiki kijiji wanathibitisha hili.

Kuna huyu Mbunge Zitto Kabwe. Kabwe tangu anasoma Chuo Kikuu cha Zanzibar na baadaye kuamia Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam alisimama imara kupiga vita uoza ndani ya Chuo na hata ndani ya Umoja wa wanafunzi, yaani DARUSO. Kwa kuelewa ujasiri wa Zitto, Wananchi wa Kigoma Kaskazini wakampa ubunge katika umri mdogo tu wa miaka 29 . Na mpaka leo kila mtu ni shahidi kuwa wananchi wa Kigoma kaskazini wamelamba dume.

Nimalizie kwa kusema ndani ya makanisa, misikiti, vijiji, kata, baraza la madiwani, mashuleni, NGOs, vyuonm, viwandani, Mitaani tunao akina Zitto wengi sana wa kuung'oa uovu. Usiogope, chukua hatua na utashangaa utakavyopata jeshi kubwa nyuma yako. Akina mama wa Nronga wametuonyesha inawezekana, kina mama na vijana tuamke.

Pia tunao kina Makundi na Kipingu wengi sana ambao ni wabunifu na wanaweza kubadilisha sehemu mbalimbali na kukawa na mabadiliko makubwa sana. Tutazame ndani ya nafsi, dhamira, roho, na akili zetu. Kuna chachu Mungu amekuwekea ndani yako, ukiitumia vizuri na mimi nisipojidharau, tutaibadilisha Tanzania. Sio mafisadi, wala wenye akili mgando watakaoweza kutuzuia. Sijakata tamaa, na najua wewe hujakaa tamaa. Tuamke, tukaze buti na tusonge mbele. Tusimsubiri Rais Kikwete, hatutafika!


CHANZO: kwanzajamii.com
 
Na Andrew Mushi

KWa muda sasa tangu nimekuwa nikiandika makala na mada nyingine katika vyombo vya habari , nimekuwa nikipokea maoni mengi sana kwa njia ya barua pepe, simu, ujumbe mfupi wa simu na hata ana kwa ana. Wengi wa wanaotoa maoni wanakimbilia kunyooshea vidole viongozi wa vyama vya siasa na zaidi chama tawala, na taasisi nyingine za utawala ndio wanawajibika kuchukua hatua ili kuleta mabadiliko na maendeleo ya nchi yetu.


Kuna huyu Mbunge Zitto Kabwe. Kabwe tangu anasoma Chuo Kikuu cha Zanzibar na baadaye kuamia Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam alisimama imara kupiga vita uoza ndani ya Chuo na hata ndani ya Umoja wa wanafunzi, yaani DARUSO. Kwa kuelewa ujasiri wa Zitto, Wananchi wa Kigoma Kaskazini wakampa ubunge katika umri mdogo tu wa miaka 29 . Na mpaka leo kila mtu ni shahidi kuwa wananchi wa Kigoma kaskazini wamelamba dume.

Nimalizie kwa kusema ndani ya makanisa, misikiti, vijiji, kata, baraza la madiwani, mashuleni, NGOs, vyuonm, viwandani, Mitaani tunao akina Zitto wengi sana wa kuung'oa uovu. Usiogope, chukua hatua na utashangaa utakavyopata jeshi kubwa nyuma yako. Akina mama wa Nronga wametuonyesha inawezekana, kina mama na vijana tuamke.

.....
CHANZO: kwanzajamii.com

Huyu ni Mzee wa Dowans hamna kitu.
 
Back
Top Bottom