JK anatugombanisha na viongozi wa dini kwa nini?

Isango

R I P
Jul 23, 2008
295
450
Inafaa sasa Serikali ya Jakaya Mrisho Kikwete itafute majibu ya kutosha, kama haina majibu iombe radhi haraka sana. Serikali iombe radhi viongozi wa dini kwa Kikwete kusema kuwa wanajihusisha na madawa ya kulevya, halafu ikashindwa kuwataja. Serikali ina mdomo lakini imeshindwa kusema. Serikali ina mikono lakini haikamati kwanini?

Wabunge wanasisitiza kuwa wanaouza madawa ya kulevya wanyongwe, kweli watanzania wengi wameathirika na madawa haya, hivyo hatutegemei kuwa serikali ina urafiki na wauza madawa ya kulevya. Tayari tangu kipindi chake cha kwanza cha utawala Rais alisema ana orodha ya wauza madawa ya kulevya, sioni kwanini anachelewa kuwataja, anachelewa kuwachukulia hatua mpaka sisi watanzania tuendelee kuathirika?

Serikali ya Jakaya Kikwete itaje ni Sheikh yupi anauza madawa ya kulevya, itaje ni Askofu yupi, au Padre yupi au Mchungaji yupi anauza madawa ya kulevya. Kutuacha hewani vile bila kuonyesha majina, kwanza kunatuweka katika mahusiano mabaya na viongozi wetu wa dini.

Tunaacha kuwaamini kuwa wanatutakia mema, tunawaona kuwa ni wadanganyifu, sio waaminifu, hivyo hawapaswi kuendelea na majukumu waliyonayo ya kuchunga kondoo wa Mwenyezi Mungu na kuonya Roho za wanadamu ili baadaye tukamwone Mungu.

Kwa sasa kwa ujumla wake tunawaona viongozi wa dini wote, (Masheikh, Maaskofu, Mapadre na Wachungaji) wote sasa ni Wauaji, waharibifu wa watanzania, na kila wanachotuhubiria ni kiini macho ili waendelee kutuangamiza. Sasa ikiwa suala hili ni la kweli Kikwete taja, acha utani.

Kama sio kweli labda ulitaja kwa bahati mbaya, ukajivua nguo omba radhi, serikali ipo uchi kwenye hili, chuchumaeni, mfikirie rapu rapu la kuvaa!. Nimeandika mara nyingi sana, na ninarudia mara kwa mara, sielewi kwanini Jakaya Kikwete na wasaidizi wake hawakumbuki.

Kila tamko lina gharama, na hili sasa linagharimu heshima ya Rais na Baraza lake la Mawaziri. Washauri wa Kikwete kama mlimshauri vibaya, rudini sasa mwambieni "Mzee watake radhi viongozi wa dini".

Ilikuwaje Rais ukatoa tamko hujafanya utafiti wa kutosha? kama umefanya utafiti mbona usiwaseme? tunasikia kuwa wapo waliojisalimisha, mbona na hao hawajulikani? kwanini usiwataje? na hili limekuwa kama dili la EPA, kila anayejisalimisha unamsitiri? kama haujawasitiri mbona hatuwasikii?
 
Back
Top Bottom