JK ageuzwa mradi

Msharika

JF-Expert Member
May 15, 2009
947
69
• Watoto wa vigogo CCM wamponza

na Martin Malera na Sauli Gilliard


amka2.gif

OFISI ya Rais (Ikulu) na jina la Rais Jakaya Kikwete, yameingizwa katika mvutano wa kibiashara ambao unahusisha taasisi moja ya Marekani inayojihusisha na kampeni za kutokomeza malaria, iitwayo, Malaria No More.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima Jumatano kwa siku kadhaa sasa umebaini kuwa mzozo huo unatokana na kile kinachoonekana kuwa ni jitihada za kundi la watu kutumia urais wa Kikwete kutimiza haja binafsi za kibiashara.
Tukio la hivi karibuni kabisa ambalo linaweza kuchafua taswira ya Ikulu ni lile lililoibuliwa na Mkurugenzi wa Kampuni ya Deiwaka Entertainment, Joseph Mbilinyi (Mr. Sugu), anayeinyoshea kidole Ofisi ya Rais Kikwete na hususan mmoja wa wasaidizi wake wa karibu, Januari Makamba na kile anachokiita njama za kumpora mradi wa mamilioni ya fedha wa kampeni dhidi ya malaria, uliozinduliwa jijini Dar es Salaam na Kikwete mwenyewe.
Ili kuuzindua mradi huo, Rais Kikwete alilazimika kusafiri kwenda Dar es Salaam na kuuzindua akitokea Dodoma na kurejea tena siku iliyofuata kuendelea kuongoza vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya CCM.
Mbali ya Januari, vijana wengine wawili ambao majina yao yanatajwa katika sakata hilo ni William Mungai na Ruge Mutahaba.
Mbilinyi, maarufu kwa jina la kisanii la Mr. Sugu, kutokana na umaarufu mkubwa alioupata akiwa msanii mwanzilishi wa muziki wa kizazi kipya nchini miaka ya 1990, anasisitiza kuwa mradi huo ni wake, kwa madai kuwa ndiye aliyeingia mkataba na taasisi ya Malaria No More ya Marekani iliyouleta hapa nchini.
Akizungumza na Tanzania Daima Jumatano, msanii huyo mwenye makazi yake nchini Sweden, alidai licha ya kuingia mkataba, Januari aliwasiliana na viongozi wa taasisi hiyo na kufanikiwa kuupora na kuupeleka mikononi mwa kampuni nyingine kwa faida yake.
Mbali na kuzungumza na Tanzania Daima Jumatano, Sugu amepata kukaririwa na vyombo mbalimbali vya habari kwa zaidi ya wiki mbili sasa akisema kuwa wazo la taasisi hiyo kutumia wasanii wa kizazi kipya kwenye kampeni zake za kudhibiti malaria nchini ni lake na alilifanyia kazi kwa miaka miwili.
Alisema mara ya kwanza alikutana na wawakilishi wa kampuni hiyo kwenye ndege na kupeana mawasiliano yaliyozaa kuanzisha mradi huo. Msanii huyo ambaye anaonekana kuchanganyikiwa baada ya kile anachodai kuwa ni mradi wake kunaswa na wajanja, alisema hatakubali kunyamazishwa hadi hapo atakapolipwa fidia.
Januari Makamba apasua jipu

Wakati Mr. Sugu akilalamika kupokwa mradi huo, Januari aliiambia Tanzania Daima Jumatano kuwa anashangazwa na madai hayo kwamba amehusika kumpora msanii huyo.
Januari alisema mara ya kwanza aliusikia mradi huo kutoka kwa aliyekuwa Balozi wa Marekani nchini, Mark Green, ambaye kwa sasa ni mmoja wa wakurugenzi wa taasisi hiyo ya ‘Malaria No More’.
“Kwa hiyo wakati Balozi Green anaondoka nchini kurejea kwao, alisema angependa kuona taasisi hiyo ikizindua mradi huu nchini baada ya kufanya hivyo kwa mafanikio nchini Senegal, kwa kutumia wasanii maarufu nchini humo, akiwamo Youssou N’dour,” alisema Januari akionyesha kwamba hoja ya kutumia wasanii si ya hapa nchini pekee.
Kwa mujibu wa Januari, mwaka 2008 wawakilishi wa Malaria No More, waliwasili nchini na kukutana naye na kujadili kwa kina juu ya mpango wa uzinduzi wa mradi huo, huku wakiomba Rais Kikwete awe mgeni rasmi.
“Lengo la serikali ilikuwa kuhakikisha rais anauzindua mradi huo, lakini nilipokutana nao, jukumu langu lilikuwa kuwaelekeza kampuni kubwa zinazoweza kufanya kazi ya uzinduzi wa kampeni hiyo kwa kutumia wasanii.
“Mimi niliwapa kampuni tatu za kufanya nazo kazi. Niliwatajia Kampuni ya Prime Time Promotion, hasa kutokana na umahili wake wa kuandaa matamasha makubwa ya Fiesta kila mwaka, niliwatajia pia Kampuni ya Round Trip na Benchmark Production inayojihusisha na uandaaji wa mashindano ya urembo na usakaji wa vipaji vya wasanii, ‘Bongo Star Search.’
“Kuhusu wasanii watakaotumika kwenye uzinduzi huo, niliwashauri waangalie chati za wanamuziki wa bongo kupitia vituo vya redio na walifanya hivyo. Baada ya hapo sikujihusisha na kitu kingine chochote na sijapata hela yoyote na sikupaswa kulipwa,” alisema Januari.
Januari alisema alilazimika kuingia kwenye hatua hiyo, kwani lengo lilikuwa kuhakikisha rais anafungua mradi huo ili kudhibiti malaria inayoua nguvu kazi ya taifa kila mwaka pengine kushinda hata ukimwi.
Kuhusu Mr. Sugu na malalamiko yake, Januari alisema aliyajua siku tano kabla ya uzinduzi baada ya kukutana na wawakilishi wa Malaria No More na kwamba walikuwa na wasiwasi kama rais angeweza kufungua mradi huo.
“Waliniambia kuwa Sugu alikusudia kuishitaki taasisi ya Malaria No More nchini Marekani, nami nilipoangalia malalamiko yale sikuona kama yanaweza kuathiri uzinduzi wa kampeni hiyo, hivyo tuliendelea na maandalizi ambayo yalifana,” alisema.
Wakati Januari akitoa madai hayo, taarifa nyingine zinaeleza kuwa kampuni iitwayo Round Trip ambayo ndiyo iliyouratibu uzinduzi wa mradi huo hapa nchini ilipata fununu za kuwapo kwa kitu cha namna hiyo kupitia kwa mkurugenzi mwingine wa Deiwaka Entertainment, aitwaye William Mungai.
William ni mtoto wa Mbunge wa Mufindi Kaskazini, Joseph Mungai, aliyepata kuwa waziri wa wizara mbalimbali nchini kabla ya kustaafu alipokuwa Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika. Habari hizo zimefikia hatua ya kudai kuwapo kwa uwezekano wa William kuwa na mkataba wa malipo na Round Trip kwa kazi hiyo.
Kauli ya William Mungai

Tanzania Daima Jumatano haikuishia hapo, bali ilimtafuta Mungai kueleza namna anavyolijua sakata hilo na iwapo alihusika katika kuchota au kupokea fedha zozote kwa niaba ya Deiwaka.
Mungai alisema hakuwahi kuchota fedha hizo na asingeweza kuzichota kwani wazo la kuandika mchanganuo ambao yeye alishiriki lipo katika hatimiliki ya Kampuni ya Deiwaka.
“Sijachukua kiasi chochote kile cha fedha…mimi ni rafiki wa karibu wa Sugu, huwa nashirikiana naye katika kumshauri katika masuala mbalimbali…isitoshe nimekuwa miongoni mwa watu wanaoshirikiana na wasanii kuhakikisha wananufaika na kazi zao.
“Watu wanasema sijui William kachukua dola 2,000, sijui 200,000 si kweli, kwanza kwa nini nichukue wakati ile ni mali ya Deiwaka? Siwezi kufanya hivyo…Sugu mwenyewe hanitaji kwenye madai yake,” William alizungumza kwa makini.
Alisema jambo analofahamu juu ya mradi huo ni kwamba Sugu aliandaa mchanganuo kuonyesha namna wasanii watakavyotumika kutoa elimu ya kujikinga na ugonjwa wa malaria.
Alisema, Sugu akiwa nchini Marekani alipata kuzungumza na aliyekuwa Balozi wa Marekani nchini, Green na kumthibitishia kwamba mradi huo unatekelezeka na hata Rais Jakaya Kikwete, anaweza kushiriki.
William alisema katika uandaaji wa mchanganuo huo, Sugu alikuwa akimtumia kwa kufanya utafiti wa mambo kadhaa na kampuni zinazoweza kufanya kazi katika maeneo fulani.
“Hapa ndipo watu wanapojichanganya. Makampuni mengine yanataka kuniletea hela kwa kupata mradi ule…lakini sikupokea kwa sababu zinatakiwa ziende Deiwaka…wanataka kutoa shukrani kwa kupewa kazi ile lakini fedha hizo ni ndogo sana ikilinganishwa na kiasi na gharama alizoingia Sugu,” alisema.
Round Trip ni moja ya makampuni yaliyoshiriki katika maandalizi ya uzinduzi wa kampeni ya malaria na inahusishwa na kupewa kazi hiyo kutoka kwa Mungai, jambo ambalo amesisitiza kuwa si kweli.
Alieleza kuwa msanii huyo aliyevuma zaidi katika miaka ya 1990 alifungua madai dhidi ya taasisi ya Malaria No More kudai fidia ya gharama alizotumia kuandaa mchanganuo, hatimiliki na muda alioupoteza kuandaa, kitu ambacho baadaye hakuja kukifanya.
Alieleza wakati akisubiri majibu kutoka Marekani, Sugu aliletewa barua ya kuitwa mahakamani, siku ya Ijumaa (kabla ya uzinduzi) na kutakiwa kutokea mahakamani. Chanzo kingine cha kuaminika kilichodai kinalifahamu sakata hilo kwa undani kilieleza kuwa ‘mchezo mchafu’ ulianzia Ikulu wakati wa kumtafuta Rais Kikwete ili ashiriki katika uzinduzi huo.
Ruge Mutahaba naye aguswa

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa THT anayetajwa kuhusika katika mradi huo, Rugemalila Mutahaba, alisema alipata kazi ya kusaka wasanii, kuweka ulinzi na kupamba jukwaa siku ya uzinduzi huo na Round Trip iliyoingia mkataba na taasisi hiyo ya Marekani.
“Mimi sihusiki na chochote, maana kazi yangu ilikuwa kusaka wasanii, walinzi na jukwaa, lakini nashangaa Sugu anakwenda kwenye vituo vya redio na kunitaja kwamba nimempora, hiyo si kweli afanye uchunguzi atajua,” alisema Ruge.
Hata hivyo, Ruge ambaye pia ni Mkurugenzi wa Radio Clouds, alisema huenda Sugu ana malalamiko ya msingi, lakini anashindwa kuelekeza malalamiko yake kwa watu sahihi. Hii ni mara ya pili kwa Rais Kikwete kuzindua mradi na baadaye kuibuka utata katika mradi huo huo. Hivi karibuni akiwa mjini Arusha, alizindua hoteli moja ya kitalii, lakini siku iliyofuata wakala wa barabara nchini Tanroads waliamua kubomoa uzio wa hoteli hiyo baada ya kubainika kuwa ulikuwa umejengwa eneo la barabara.
 
And the saga continues......

Round Trip ni nani na ya akina nani?

Inaonekana Ruge sasa anabadilisha story, au.......

Imewekwa wazi kwamba Sugu anawashitaki MNM, sasa Ruge aliingiaje/anaingiaje humu?

.....and the beat goes on..........
 
Back
Top Bottom