Jeshi la Polisi lilipojaribu kuandika ‘Injili’ bila ya mafanikio

Consigliere

JF-Expert Member
Sep 9, 2010
12,037
24,595



Na Thaddeus Musembi

Katika mafundisho ya Bibilia na yale ya Katoliki neno injili humaanisha masimulizi yahusuyo maisha na habari za Yesu Kristo. Katika uasilia wake neno injili humaanisha habari njema. Awali habari kuhusu Yesu zilikuwa zikisimuliwa na watu waliomfahamu au waliopata kumsikia wakati ule anaishi, lakini kadiri miaka ilivyokuwa ikienda, habari kuhusu Yesu zilianza kupungua. Hali hii ilitokana na ukweli kuwa watu waliozifahamu habari zake pia walipungua kwa sababu mbali mbali zikiwemo kuhama toka eneo moja kwenda lingine au baada ya kupatwa mauti au sababu nyingine zilizopelekea wapoteze uwezo wa kuendelea kuzieneza, aina hii ya utunzaji na uenezaje wa habari inafahamika kwa wataalamu wa Kiswahili kama fasihi simulizi.
Hapa ndipo wanafunzi wake wakaona kuna haja ya kutunza habari zake katika fasihi andishi ili ziendelee kuishi na kudumu katika jamii kwa muda mrefu bila ukomo. Najua utajiuliza kwa nini nimelihusisha jeshi la polisi na injili ya Luka, tuwe pamoja. Jumla vitabu vya injili ambavyo kanisa linavyo mpaka sasa ni vinne. (Nitaegemea zaidi katika mafundisho ya katoliki), ambavyo vimeandikwa na Marko, Luka, Yohana na Mathayo.
Ukiagalia Injili tatu za mwanzo hakuna ubishi kuwa kuna kufanana kwa maneno na upangiliaji kwa kiasi kikubwa, Japo Yohana ndiye anaeonekana kutofautina kwa kiasi kikubwa na wenzake, mimi nitaongelea namna Luka alivyokuwa akijaribu kujitofautisha kwa makusudi na hapa ndipo msingi wa makala yangu ulipo.
Ukisoma katika utangulizi wa Injili ya Luka katika Bibilia ya katoliki, tunaambiwa kuwa katika uandishi wake Luka anaacha maneno yanayoweza kuumiza moyo wake au mioyo ya wasomaji.
Msingi wa tofauti hizo zinazojitokeza unaweza ukatokana na ukweli kuwa Luka natofautitiana kitaaluma na kiasili na waandishi wengine tofauti ilivyo kwa waandishi wengine wa Injili Luka hakuwa Myahudi, pia kitaaluma alikuwa ni daktari wa mambo ya tiba. Uandishi wake ulilenga zaidi wasomaji wasio wayahudi hivyo akaacha kuandika juu ya mambo yasiyoeleweka kwa wasio wayahudi (mila,lugha n.k) pia alihakikisha kwa makusudi anailinda taaluma yake aliyoipenda kwa kuacha kuandika mambo ambayo aliona kama yana dharirisha taaluma yake ya udaktari (mwanamke aliyetokwa damu kwa muda wa miaka kumi na miwili (Marko 5:26)).
Huyo ndiye Luka, ambaye jeshi Polisi limeamua kumuiga ili nao waandike injili yao.
Kwa muda mrefu jamii imekuwa ikililalamikia utendaji wa jeshi la polisi wengine wakaenda mbali zaidi na kupendekeza kuwa lifumuliwe ili lindwa upya. Binafsi nathubutu kusema pamoja na malalamiko hayo, nimewahi kushudia baadhi ya mafanikio ya jeshi hilo, mafanikio ambayo ukiangalia kwa makini hupatikana tukio husika linakuwa halina maslahi kwao au kwa wakubwa fulnani, na wakati mwingine mafanikio haoyo hutokana na utashi binafsi wa askari wake na si muundo (chain of command). Katika siku za karibuni utendaji wa jeshi la polisi umeibua maswali mengi yasiyo na majibu kiasi cha kuwafanya watu wajihisi kuwa labda uwezo wao wa kufikiri umeanza kupungua.
Ya karibuni zaidi yalianzia Arusha walipoamua kuyavunja kwa kutumia nguvu maandamano ya amani yaliyokuwa yakifanywa na CHADEMA na wafuasi wao, wakitumia taarifa za kiintelijensia ili kuhararisha amri yao, ikumbukwe kuwa CHADEMA walikuwa na barua ya polisi ikiwaruhusu kufanya maandamano hayo.

Taarifa hizo za kiintelijinsia zilisema kuwa maandamano hayo yangekuwa na uvunjifu wa amani, matokeo yake wao ndiyo wakavunja amani, baada ya kelele na mbinyo kutoka kila kona ya nchi, polisi wakawa hawana jinsi zaidi ya wao kujitetea na ili kujisafisha katika uso wa jamii wakaamua kuingia 'hollywood', huko wakatengeneza filamu waliyoipenda wao, wakaacha matukio yatakayowaumiza mioyo yao na ile ya watazamaji na kweli ingeumiza mioyo kwa namna watu walivyouawa na kujeruhiwa, wakaunganisha vipande vya picha ili wapate picha kwa ajili ya wasio wayahudi(wasio wakaazi wa Arusha). Wakajitetea zaidi kuwa walijaribu bila mafanikio kuwasihi CHADEMA bila mafanikio kwani ilionekana CHADEMA wameamua kufanya jambo na walikuwa wanaelekea kituo kikuu cha polisi kuteka kituo (Station Attack), ambacho kilikuwa na silaha nzito-nzito, wakawa hawana jinsi ikabidi watumie taaluma yao ya udaktari(mbinu za kipolisi).

Nadhani mpaka hapo umeona namna polisi wanavyojaribu kuandika injili yao kwa kufuata nyayo za Luka bila mafanikio, Luka alifanya jambo sahihi ambalo kila mtu alilielewa na asiyeelewa alipoelekezwa naye alielewa, ndiyo maana hakuhangaika kuweka utetezi, lakini wao wanaahangaika kujengea hoja maelezo yao, hoja ambazo pia hawanazo. Wengi hawakuwepo Arusha wameyaona na kuyasikia hayo kupitia waandishi na vyombo vyao vya habari, cha ajabu polisi inawaita waandishi hao hao na kuwaonyesha senema yao waliyoitengeneza bila shaka kwa kuunganisha unganisha picha hizo hizo za waandishi.
Watu wakauawa, wengine wakajeruhiwa, wengine wakakamatwa na kufunguliwa mashitaka. Nilitegemea mashitaka yaliyofunguliwa yangekuwa ni ya uvunjifu wa amani, ikawa sivyo wakashitakiwa kwa kosa la kufanya maandamano bila ya kibali ambacho hata hivyo wanacho, je si kweli kuwa polisi ndiyo walisababisha uvunjifu wa amani kwa kutoa katazo lisilo na maandishi?. Ziko wapi taarifa za kiintelijensia tulizoambiwa? mbona hatuzioni katika hati za mashitaka je hazithibitishiki?

Katika jitihada za kujisafisha polisi wanaonyesha usugu wao wa kuvunja sheria kwa kuongelea kwenye vyombo vya habari suala ambalo wao wenyewe wamelipeleka mahakamani na kesi yake ikiwa imeshafunguliwa na washitakiwa kupandishwa kizimbani. Wakiwa nje ya mahakama wanaongeza madai mengine ambayo hayapo kwenye hati ya mashitaka kuwa CHADEMA walitaka kuteka kituo cha polisi, hii yote ni katika kurutubisha utetezi wao wanatumia nguvu zote kuusambaza, hawajali tena kuwa nguvu hiyo waitumiayo inazidi kuondoa kabisa imani ya wananchi juu ya jeshi hilo lenye majukumu nyeti.

Mimi ni mwana-CCM makini, hai na imara, ni lazima nikilinde chama changu mapema, kwani huko tuendako na kwa mwamko na demokrasia ya sasa huenda wao wakaja kuwa madarakani na matokeo yake bila ya kuwa na polisi adilifu shida wazipatazo wao sasa, zikatugeukia sisi kwa kuwa tutakuwa nje ya madaraka.
Wakati jamii ikijadili injili iliyoandikwa na jeshi la polisi, huko Mwanza jeshi hilo likaibuka na kituko kingine kituko hicho kilihusiana na faru George maarufu kama kifaru wa JK mwenye umri wa miaka kumi na mbili, idara ya wanyama pori iliripoti kuhusu kuuawa kwa faru huyo na watu wasiojulikana ambao pia walitoweka na pembe zake, ndani ya muda mfupi polisi wakapata maneno ya kurefusha injili yao wakasema wamekamata pembe za mnyama huyo na wanamshikilia mhusika ambaye ni muajiriwa wa idara ya wanyama pori, hiyo ndiyo intelijensia ya polisi.
Idara ya wanyamapori ikaenda kuhakiki kama uintelijensia wa polisi, baada ya idara ya wanyama pori kufanya uintelijensia wao wa kweli, ikagundua mambo mawili:

  1. Idara yao haina mfanyakazi mwenye jina hilo
  2. Pembe zilizokamatwa si za 'Faru George' na ukiacha mbali Faru George si za faru kabisa, kwani ni mchanganyiko wa pembe za ngombe, gundi na sement.
Hao ndiyo polisi wetu, hawana muda wa kuhakiki ili kuthibitisha mambo, wana haraka ya kutaka kuonekana mbele ya vyombo vya habari wakiongea porojo, nashindwa kuelewa hizi intake za siku hizi sijui zikoje.
Je hiyo ndiyo intelijensia ya polisi wetu? Intelijensia ya kubunibuni mambo na kukimbilia kuyatoa kwenye vyombo vya habari? Intelijensia haifanywi na watu wavivu wa kufikiri na kutenda wala haifanywi na wapenda sifa wa kiwango chao, ni muda sasa wa kuanza kubadilika, japo mlitakiwa kuwa muwe mumebadilika muda mrefu uliopita.

Nimeliongelea jeshi la polisi katika ujumla wake lakini nawajua na najua wapo wachache ambao wanatimiza majuku yao kwa uadilifu na uaminifu uliotukuka, japo kwa uadilifu wao huo unayafanya maisha ya utumishi wao ndani ya jeshi hilo kuwa mgumu, ni kama wanatembea bila viatu katika njia yenye miiba na vipande vya chupa hawa nawaomba wasiukatie tama uadilifu wao huo, wasijione kuwa ni wachache sana kuweza kubadilisha hali ya mambo, wakumbuke ukubwa wa meli na gari unavyopelekwa huko na huko kwa usukani mdogo.

Polisi hapa wanajaribu kuandika injili kwa kufuata utaratibu aliotumia Luka lakini hawatafanikiwa. Kwani dhamira ya Luka na ile ya Polisi hazifanani na wala kukaribiana kufanana, wakati, Luka alikuwa na dhamira ya kueneza habari njema, zenye upendo na uzima, polisi wapo kwenye mchakato wa kuficha ukweli, kueneza matumizi ya mabavu, manyanyaso na kujenga chuki ndani ya jamii.
Luka alijitoa kwa ajili ya jamii, polisi wamesahau viapo vyao vya utumishi na uadilifu na kufanya kujiingiza katika aina ya utendaje wenye mashaka.
Japo aliyaacha baadhi ya mambo hiyo ilikuwa ni baada ya kuridhika kuwa waandishi wenzake wameshayaongelea na hivyo yatosha, Luka hakutunga mambo na kuyapendezesha ili kuwavutia watu kujiunga na imani yake mpya bali aliongea ukweli, juu ya kile alichokishudia na alichofundishwa..

Copied & Pasted from Thaddeus Musembi
 
Ur real a great thinker! Even a slow learner like Wasra understands or tabular rasa like Tambuu Hizo
 
Waraka wako unaeleweka vizuri sana mkuu, walengwa waufanyie kazi ama wakipuuza basi waendelee kundika injili zao.
 
Dah,hamjambo? Nitarud ngoja nikale maana una umuhimu huu wakala na kwa njaa niliyonayo nitashndwa kuumaliza!
 
Kwa anayetaka kujua tofauti ya JF na FACEBOOK basi anaweza kuijua tofauti hiyo kuanzia hapa.I salute you mwanaccm unayesimamia ukweli.
 
Kwa anayetaka kujua tofauti ya JF na FACEBOOK basi anaweza kuijua tofauti hiyo kuanzia hapa.I salute you mwanaccm unayesimamia ukweli.

Sikubaliani na wewe, kwani mabadiliko tunayoyashuhudia huko Mashariki ya kati leo mengi yameletwa na Facebook,Twitter na YouTube.
Tatizo ni jinsi ya kutumia tu!!!!!
 
Back
Top Bottom