Ab-Titchaz
JF-Expert Member
- Jan 30, 2008
- 14,631
- 4,225
Mama akataa kuua mtoto wake mwenye jinsia mbili
*Familia yadai auawe kwa kuwa ni mkosi
*Ampeleka kwa mama yake kulinda ndoa yake
Na Mwandishi Wetu
MKAZI mmoja wa Kijiji cha Matare Kata ya Mugumu mjini, wilayani Serengeti, Anna Samson [22] anakabiliwa na wakati mgumu katika ndoa yake, baada ya kukataa kumuua mtoto wake aliyezaliwa na sehemu mbili za kiume na kike kwa madai kuwa ni mkosi kwa mila za kabila la Wakurya.
Uamuzi huo wa kikatili unadaiwa kutolewa na mume wa mwanamke kwa kushirikiana na mama yake mzazi, mara baada ya kuzaliwa kwa mtoto wao Baraka Marwa mwenye umri wa miaka miwili sasa. Mtoto huyo alizaliwa katika Hospitali ya Wilaya ya Nyerere akiwa na jinsia mbili ya kike na ya kiume.
Akizungumza na Mwananchi Jumapili kwa huzuni kubwa, Anna alisema kuwa matatizo hayo yalianzia hospitalini mara baada ya kujifungua na kwamba mume wake kwa kushirikiana na mama mkwe wake, waliamua mtoto huyo auawe kwa madai kuwa ni mkosi kwa familia hiyo na kuwa hatakiwi kukanyaga katika nyumba yao.
"Kwa kweli iliniwia vigumu kutekeleza uamzi huo wa kuua mtoto wangu kutokana na maumbile hayo,nilikataa na kuzuiwa kufika nyumbani kwangu kwa kuwa ni mkosi mkubwa kuwa na mtoto wa namna hiyo kwa mujibu wa mila na desturi za Kikurya, alisema huku akibubujikwa machozi.
"Niliamua kwenda nyumbani kwa wazazi wangu na kuwaeleza hali halisi ambako mama yangu alikubali kukaa na mtoto huyo, baada ya kumwachisha kunyonya ili niweze kurudi kwenye ndoa yangu ambako pia nina mtoto mwenye umri wa miaka minne,"alisema.
Alisema walikuwa wakiendelea kumpeleka hospitali kwa ajili ya matatizo yake, kwa kuwa wakati wa kukojoa anapata taabu sana kiasi cha kumvuta kwa mpira, ndipo wakafikia hatua ya kumtahili sehemu ya kiume kwa kuwa ndiyo iliyoonekana kufanya kazi kuliko ya kike.
"Pamoja na kumtahiri bado akinywa chai au vitu vya majimaji hupata shida kukojoa, nimempeleka Hospitali ya Bugando mjini Mwanza, mara mbili na wamesema watamfanyia upasuaji, nimepangiwa nirudi tena mwishoni mwa mwezi huu, tatizo ni kwamba sina fedha kwa kuwa mume wangu hayuko tayari kutoa fedha kwa ajili ya kazi hiyo, alisema na kuongezea; "Katika upasuaji unategemewa kufanywa kuondoa sehemu ya kike na kubakiza ya kiume kwa kuwa ndiyo imeonekana kufanya kazi,"alisema Anna.
Alisema mtoto huyo kwa sasa yuko kwa mama yake Matare alikomuacha huku yeye akiwa ameamua kurejea kwa mume wake ambako baada ya kurejea bila ya mtoto huyo alipokelewa bila shida yoyote.
Aliomba watu wenye uwezo na mashirika mbalimbali, wamsaidie ili aweze kufanikisha matibabu ya mtoto huyo na kunusuru ndoa yake iliyoko majaribuni kwa kuwa hakuna amani ndani ya ndoa baada ya kukataa kumuua mtoto Bahati.
Uchunguzi wa Mwananchi Jumapili umebaini bado baadhi ya jamii wanaendekeza mila ambazo zinakiuka haki za binadamu na kibaya zaidi ni kwamba mila hizo zinatekelezwa na vijana wadogo ambao wanatakiwa kuleta mageuzi katika jamii.
Akizungumza na Mwananchi Jumapili Mratibu wa Wasaidizi wa Kisheria na Haki za Binadamu Wilaya ya Tarime, Bony Mato kuhusiana na tukio hilo alisema mila kama hizo zinatakiwa kufanyiwa marekebisho kwa kuwa zinakiuka haki za binadamu ambazo mtu anazaliwa nazo.
"Nilistushwa sana na uamzi huo baada ya kuambiwa na Anna yaliyomkuta kwa kweli inasikitisha sana kuona watu wa karne hii bado wanaendekeza mambo kama hayo, niliamua kumtuma kuja ofisini kwako kwa msaada zaidi,"alisema
Mwananchi Read News