Mungi
JF Gold Member
- Sep 23, 2010
- 16,975
- 9,566
JAMBAZI sugu Pokea Kaaya `Steven Kaunda aliyekuwa anasakwa na Polisi kwa kumpiga risasi na kumwua askari kanzu na kumjeruhi kwa risasi begani Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Arusha (OC-CID), ameuawa kwa kupigwa risasi. Kaaya amefikwa na mauti hayo kwa kumiminiwa risasi na polisi baada ya kugundulika akiwa kwa mganga wa kienyeji akitibiwa majeraha. Kifo cha jambazi huyo ambaye Januari 3 alimuua Kijanda Mwandu (35) na kumjeruhi Faustin Mafwele wakati wa tukio la kurushiana risasi eneo la Shangalai wilayani Arumeru mkoani hapa, limethibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Thobias Andengenye. Kamanda Andengenye alisema jana kwamba Kaaya aliuawa jana saa 12.45 alfajiri akiwa kwenye boma la Anna Roshilari katika kijiji cha Orarashi, kitongoji cha Lengine wilayani Arumeru. Alisema baada ya kupata taarifa za jambazi huyo kuwa eneo hilo, walituma kikosi cha kuhakikisha wanamtia mbaroni. Alisema: Askari wangu walizunguka boma hilo usiku kucha na ilipofika saa 6.45 walimwona akichomoza ndani ya boma na kukimbia, askari wakamfukuza umbali wa kilometa mbili na ghafla akamgeukia askari namba E. 9912 Konstebo Wito na kumngata vidole ili aachie silaha aliyokuwanayo. Andengenye aliendelea kusema, kwamba baada ya kumngata vidole, askari huyo aliachia silaha, jambazi akaichukua, lakini wakati akijiandaa kuitumia, askari wengine walimwahi kwa kumpiga risasi akaanguka chini na baada ya muda mfupi akafa. Alisema jambazi huyo alifika nyumbani kwa Anna Roshirali kutibiwa kwa mganga wa kienyeji jeraha alilokuwanalo. Aidha, jeshi hilo linaendelea kuwatafuta washirika wa karibu wa jambazi huyo, akiwamo Augustine Shine Baba Mzungu, mkazi wa Sakina Juu, mjini hapa. Pia kuhusiana na tukio hilo, watu wanne wanahusishwa na Kaaya ambao ni Agnes Silasi (40) ambaye ni mke wa marehemu aliyekamatwa eneo la tukio, Josephat Haule (33) mkazi wa Shangarai, Juma Masamaki Twalibu (46) wa Ngarenaro na Daines Masawe (19) wa Nambala. Hata hivyo, polisi wanaendelea kuwashikiliwa watoto wa marehemu ambao ni Alex Parumina (13) na Daines Masawe (9), waliokamatwa siku ya tukio la mauaji ya Polisi Shangarai. Mwingine anayeshikiliwa ni Rehema Ally ambaye siku ya tukio alikamatwa na silaha akiwa ameificha chooni. Kamanda huyo alisema kabla ya jambazi huyo kuuawa, polisi wakishirikiana na wananchi, Januari 6 saa 4 asubuhi, eneo la Moshono, mtaa wa Letera, walipata silaha za jambazi huyo alizotumia kumwua polisi na kumjeruhi askari mwingine. Silaha hizo ni bunduki SMG namba 1016188011 yenye risasi 20 na magazini mbili na shotgun moja aina ya Model namba 88-12GA yenye risasi nne. Alisema silaha hizo zilikuwa zimehifadhiwa ndani ya mfuko wa sandarusi, huku juu yake umefunikwa jaketi jeusi, na kufichwa kichakani. Mwili wa mrehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru, ambako kabla ya kuhifadhiwa katika majokofu, uliwekwa nje ya jengo hilo, kwa saa nane ili wananchi waushuhudie. Hata hivyo, habari kutoka kwa baadhi ya askari waliokuwa kwenye tukio la mauaji ya jambazi huyo ambao hata hivyo hawakutaka kutajwa majina yao, walisema wanachoamini uchawi upo, kwani walipomwona jambazi huyo kwa karibu kabla ya kukimbia, walifyatua risasi ikagoma. Yaani nakwambia tulifanya kazi kubwa, kila tukikoki wapi, mpaka tukaanza kuomba ila nikakumbuka jinsi babu yangu alivyonifundisha, ikabidi niwaelekeze wenzangu ndipo chuma kikaachia, vinginevyo tungemalizwana huyu jamaa, alisema mmoja wa askari hao. Aliongeza kuwa pia jambazi huyo wangemwua mapema lakini, kila walipokuwa wakipata taarifa ya mahali alipo na wao kufika eneo hilo, lakini huwa tayari ameondoka kwa pikipiki. |