Jaji Kiongozi azipiga kombora kesi za ufisadi

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,005
Date: 9/23/2009

*ASEMA ZINAENDESHWA KWA UKATA, ZANA DUNI, ATAKA WANAOLALAMIKA WAFANYE UCHUNGUZI

Na Ramadhan Semtawa
Mwananchi


WAKATI baadhi ya watendaji wa vyombo vingine vya dola wakiituhumu mahakama kuwa kikwazo katika vita ya ufisadi kutokana na kuchelewesha kesi, Jaji Kiongozi Fakhi Jundu, amejibu mapigo akisema, mhimili huo sio kikwazo na kutaka watu wasikurupuke kutoa tuhuma bila utafiti.

Ingawa Jaji Kiongozi hakumtaja mtu, hivi karibuni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Dk Edward Hoseah, aliishutumu mahakama akisema inachangia kupunguza kasi ya kesi za ufisadi.

Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili ofisini kwake jijini Dar es Salaam wiki iliyopita, Jaji Kiongozi Jundu alisema, watu wanapaswa kufanya utafiti kabla ya kutoa tuhuma hizo nzito dhidi ya Mahakama hadharani.

Kauli ya Jaji Kiongozi Jundu inakuja wakati kukiwa na wingu zito kuhusu kesi tatu za ufisadi zinazotarajiwa kufunguliwa ambazo tayari, Rais Jakaya Kikwete, alidokeza alipojibu maswali mbalimbali ya wananchi Septemba 9 mwaka huu.

Kwa msisitizo, Jaji Kiongozi Jundu alisema; "Watu wafanye utafiti kwanza, mahakama haijawezeshwa na kuandaliwa vema kukabiliana na kesi za dharura za ufisadi tangu mwanzo, bajeti yake ya mwaka huu ni Sh21 bilioni, fedha ambazo zinazidiwa hadi na bajeti ya mkoa (baadhi ya mikoa ilipata bajeti takriban Sh 43 bilioni kila mmoja), halafu watu wanataka tuendeshe kesi kwa kasi kwa fedha hizi, kesi nyingi zimeingia bajeti imeshapita."

"Angalia na taasisi nyingine, zenyewe ziliandaliwa vema kukabiliana na kesi hizo kwani ziliwezeshwa tangu wakati wa upelelezi, wewe (mwandishi) si unaenda Kisutu mara kwa mara, angalia tu hata maeneo ya waendesha mashtaka utakuta samani mpya, lakini angalia kwa mahakimu kulivyo na hali mbaya."

Jaji Kiongozi huyo alifafanua kwamba, mahakama ni mhimili mkubwa na muhimu wa dola, lakini wakati wa mchakato mzima wa kesi za ufisadi ambazo ni za dharura, haikuweza kushirikishwa vema na kuandaliwa kwa kuwezeshwa kuanzia miundombinu.

"Leo hii, ile Mahakama ya Kisutu pale ipo tangu miaka ya 1950, kesi nyingi za ufisadi ziko pale utaona mahakimu wanapaswa kupishana katika chamber (chumba) moja, mbali ya kesi hizo kuna kesi nyingine, mahitaji ya tangu miaka ya 1950 na sasa ni tofauti," alisisitiza na kuongeza:

"Watu wanataka tuendeshe kesi kwa kasi wakati bado tupo Primitive (katika mfumo wa ujima), tunataka mahakama iwe modern (ya kisasa) tuweze kuendesha kesi kwa kasi kwa kutumia mfumo wa digital, lakini uwezeshaji haupo, wakati huo kuna kesi za mauaji na nyingine nyingi za jinai bado hazijatolewa maamuzi."

Kesi kubwa za ufisadi zilizopo Mahakama ya Kisutu na nyingine Dar es Salaam, ni pamoja na kesi za wizi katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), matumizi mabaya ya madaraka ya umma zinazowakabili mawaziri wa zamani Basil Mramba na Daniel Yona na Katibu Mkuu mstaafu Wizara ya Fedha na Uchumi Gray Mgonja.

Kesi nyingine ni ile inayohusu kashfa ya Majengo Pacha ya BoT inayomkabili Mkurugenzi wa zamani wa Utawala na Utumishi (DPA) , Amatus Liyumba na mwenzake.

Jaji Jundu alisema; "Mazingira yaliyopo yakiwemo ya nguvukazi hayawezeshi kesi kwenda kwa kasi, kumbuka zipo kesi nyingine nyingi tu zinazopaswa kuendeshwa kwa kasi pia, au watu wanataka hizi nazo zisimame?"

Jundu alisisitiza: "Jaji wa Dar es Salaam ana wastani wa kesi 300 peke yake, bado mazingira ya utendaji kazi hadi sasa ni ya kizamani kwa kutumia mfumo wa kuandika kwa mkono badala ya kurekodi kwa njia ya digital."

Aliweka bayana kwamba, angalau Mahakama ya Biashara imeingia katika mfumo huo wa digital ambao ni rahisi kwa majaji kuweza kuendesha kesi kwa kasi na kutoa hukumu.

Kiongozi huyo wa majaji, aliweka bayana kwamba, wabunge ni watu ambao wanatakiwa kutambua hilo la uwezo mdogo wa mahakama katika kuhudumia kesi mbalimbali kwa kasi.

"Kwa kweli, nawapongeza sana wabunge wao walitambua hili kwamba, mahakama bado haijawezeshwa vema kuweza kuendesha kesi kwa kasi," alisisitiza.

Alisema mahakama imekuwa na kiu ya kutaka kuona kesi nyingi zinaendeshwa kwa haraka na kukamilika na kuongeza kwamba, serikali pekee ina majukumu mengi, lakini anaamini, siku zijazo hilo litaangaliwa kwa umakini.

Jaji huyo alifafanua kwamba, hata wanaharakati wanapaswa kuisaidia mahakama kwa kueleza bayana matatizo yanayoikabili kama mhimili muhimu wa dola katika kutoa haki.

Katika kuonyesha matatizo yanayoikabili mahakama, alisema hata mahabusu nyingi ziko hoi na kutoa mfano: "Angalia Gereza la Njombe, lile lina uwezo wa kuchukua watu 100, lakini lina watu 350, haya ni matatizo makubwa ambayo yanaikabili mahakama."

Aliongeza kwamba, Mwanza chumba kimoja kinaweza kutumiwa na mahakimu wanne na kusisitiza kwamba, :"Wanaotutakia mema waje watukwamue wasilaumu tu."

Kuhusu uwezekano wa mahakimu na majaji kuhongwa na mafisadi, alisema ndiyo maana wako makini kusimamia taratibu na kupanga majaji na mahakimu wa kuendesha kesi.

"Ndiyo maana, utakuta kesi inaweza kuwa na jopo la majaji watatu au mahakimu wanaopangwa ni watu wanaoangaliwa kwa karibu, si rahisi kufanya hivyo kwani tunafanya kazi kwa umakini kusimamia maadili," alisisitiza.

Hata hivyo, alisema mahakama inaweza kuwa na udhaifu wake katika kuendesha kesi ambao ni wa kawaida kiutendaji, lakini akasisitiza matatizo yaliyoelezwa juu ndiyo ya msingi.

Alisema katika kuchelewa kwa kesi wakati mwingine pia kunatokana na upande wa mashtaka na kuweka bayana: "Mara unaweza kusikia upelelezi haujakamilika n.k."

Tangu kuanza kwa kesi kubwa za ufisadi, baadhi ya watu wamekuwa wakiinyoshea kidole Mahakama kama kikwazo cha kuziendesha kwa kasi.

Tayari kesi nyingi za ufisadi ziko Mahakama ya Kisutu na nyingine Ilala huku kukiwa na taarifa za kuwepo kesi zaidi za ufisadi zitakazohusisha vigogo mbalimbali.
 
..."Kwa kweli, nawapongeza sana wabunge wao walitambua hili kwamba, mahakama bado haijawezeshwa vema kuweza kuendesha kesi kwa kasi," alisisitiza....

Jaji atawapongeza vipi wabunge hao. Kama kweli wabunge wanatambua matatizo ya mahakama si ndio haohao waliopitisha ile bajeti finyu kwa kuunga hoja kwa asilimia mia moja!
 
kelele za wananchi zinachangikiwa pia na elimu finyu yas sheria.Wananchi wao wanachotaka ni kila wakisikia kiongozi fulani kapelekwa mahakamani,basi lazima ana hatia bila kujali kwamba ushahidi wakuridhisha ni kitu cha muhimu sana katika maamuzi ya mahakama.
 
Well, ni attempt mzuri ya Judiciary katika kuonyesha kuwa it is not part ya usanii katika kesi za ufisadi
 
Ukweli ndo huo, pale kisutu pana msongamano sana na pia sijui hata mafaili wana manage vp, the guy was so angry na ameamua kuwambia ukweli, its difficult. Hizi kesi za albino zinaenda haraka na tunafurahia lakini ziko kisiasa zaidi, do you know kesi moja hadi inaisha kama hiyo ni over 200million zimetumika? na kesi zipo zaidi ya 50, fanya calculation mwenyewe ndo utaelewa maana Judge per day anapewa kama laki 3 per diem, na ujue ni kitengo kizima cha mahakama kuu kinaamia huko. halafu mnasema Tanzania haina hela.
 
Back
Top Bottom