Pdidy
JF-Expert Member
- Nov 22, 2007
- 50,872
- 21,950
- Atoboa uadilifu umeporomoka
- Sasa chaanzishwa kitengo maalum
- Asema Ze Utamu bado wanasakwa
Jeshi la Polisi nchini lipo katika mkakati madhubuti wa kujisafisha ili kulirejeshea maadili kutokana na baadhi ya askari wake kulichafua baada ya kubobea katika vitendo vya uhalifu.
Kupitia mkakati huo, Jeshi la Polisi linatarajia kuanzisha kitengo maalum kitakachokuwa kikifuatilia maadili ya ya askari.
Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Said Mwema, alidokeza kuhusu mkakati huo wa kuwarejesha katika maadili baadhi ya askari wake wakati akizungumza na gazeti hili jana jijini Dar es Salaam katika mahojiano maalum.
Mwema alisema kuwa hatua ya kuanzishwa kwa kitengo hicho kinatokana na baadhi ya askari wake kukosa maadili na kujihusisha na vitendo vya kihalifu kinyume cha maadili ya jeshi hilo.
IGP Mwema alisema hataweza kuvumilia askari wake yeyote atakayejihusisha kwa namna yoyote katika vitendo hivyo ambavyo vimekuwa vikilishushia heshima jeshi hilo mbele ya wananchi.
"Kwa kawaida askari ni mlinzi wa raia, lakini pindi inapotokea anakuwa mhalifu kwa kweli maadili ya kazi yanakuwa hayapo, na mara nyingi inapotokea askari wangu anajihusisha na vitendo hivi hatua huchukuliwa mara moja ambazo ni za kukiuka maadili na baadaye hufikishwa mahakamani," alisema IGP Mwema.
Alisema kuwa askari wote wa jeshi hilo waliodaiwa kuhusika katika matukio ya ujambazi wiki kadhaa zilizopita katika mikoa ya Mara, Mwanza, Rukwa na Arusha watachukuliwa hatua kwa mujibu wa vipengele viwili vya makosa vya ukiukaji wa maadili na makosa aliyoyafanya askari.
Aliongeza kuwa, pamoja na kuwepo kwa kanuni za maadili, lakini baadhi ya askari wake wamekuwa wakizikiuka na kujihusisha na vitendo vya uhalifu.
Mwema alisema mkakati wa kuanzisha kitengo hicho wameamua kuuanzisha kutokana na kubainika kuwa baadhi ya askari wanajihusisha na uhalifu hivyo kurudisha maadili ya jeshi hilo.
Alisema mkakati mwingine ni Jeshi la Polisi kuwa na uwezo wa kimafunzo katika kupanga mikakati, mbinu za kuzuia na kuthibiti uhalifu wa aina zote nchini.
IGP Mwema aliongeza kuwa mkakati mwingine ni jeshi kuwa na mpango wa mafunzo ya maadili ambayo yatawahusisha askari wake wa vitengo tofauti.
"Haya yote ni kuhakikisha ile dhana ya ulinzi shirikishi na polisi jamii inaendelea kufanikiwa zaidi na jeshi linapokea taarifa mbalimbali za kihalifu kupitia wananchi wake.
"Tunahitaji kuwa karibu na wananchi na sio kuwa maadui, ikiwa maadili hayatarudishwa, nchi itaendelea kuwa na matatizo ya kiusalama na kiuchumi," alisema.
Hata hivyo alisema ukosefu wa uadilifu si tatizo kwa Jeshi la Polisi pekee, bali ni la taifa zima.
"Uhadilifu unatakiwa kuanzia kwenye ngazi ya familia na maeneo mengine kama mashuleni.. inakuwa ni kurekebishana, lakini kama huko chini mtoto anakua hana maadili basi hata anapoanza kazi tabia huwa ya aina hiyo," alisema IGP Mwema.
Katika hatua nyingine, Mwema alisema mpaka sasa Jeshi hilo halijafanikiwa kumtia mbaroni mmiliki wa Mtandao wa Ze Utamu, ambaye anatuhumiwa kuwadhalilisha viongozi kadhaa nchini.
IGP alifafanua bado jeshi lake linaendelea kumfuatilia kwa kushirikiana na nchi nyingine kutokana na makosa ya kimtandao kuhusisha zaidi ya nchi moja.