Pdidy
JF-Expert Member
- Nov 22, 2007
- 50,720
- 21,779
Padri Privatus Karugendo
TUKIO la kutoeleweka kwa Bwana Iddi Simba, ambaye zamani alikuwa waziri wa serikali ya awamu ya tatu, lilijitokeza katika mkutano wa 17 wa hali ya siasa nchini, uliofanyika kwa siku mbili chini ya maandalizi na uratibu wa Mpango wa Utafiti wa Elimu ya Demokrasia Tanzania (REDET), Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, ambako mada kadhaa ziliwasilishwa, ikiwamo ya Iddi Simba iliyohusu Sekta Binafsi, Utawala na Maendeleo.
Kilichoibua kutoeleweka na mjadala uliokuwa na hasira na jazba nyingi, ni pale Iddi Simba, alipojitahidi kuyajibu maswali mawili ya msingi aliyoyauliza kwenye mada yake. Maswali yenyewe yalikuwa:
Kwa nini wananchi wa Tanzania baada ya miaka yote hii ya utawala wetu huru, bado ni maskini pamoja na neema zote zilizopo nchini mwetu; huku wageni wakifaidika zaidi kwa kusaidiwa na watawala wetu?
Kwa nini wasomi na wananchi wenye hali nzuri ya kimaisha, kwa muda mrefu sana katika historia ya nchi yetu huru walidharau na hata kuogopa kuingia katika harakati za siasa?
Akijibu maswali haya, alijaribu kushawishi na kuonyesha kwamba tatizo kubwa la taifa letu ni udumavu wa akili. Hoja hii ndiyo iliyoibua hasira. Wasomi wengi waliokuwa kwenye ukumbi wa Nkrumah pale Chuo Kikuu, walichukulia hoja hiyo kama matusi, kudhalilishwa na hawakuvumilia.
Wakati akijenga hoja yake ya udumavu wa akili, Iddi Simba alisema kwamba: Kwa mujibu wa Ripoti ya Mwisho ya Uchunguzi wa Kidemografia na Kiafya nchini Tanzania ya Mwaka 2004/2005 (Tanzania Demographic and Health Survey-2004/2005) asilimia 51 ya watoto wenye umri chini ya miaka 5 wanakabiliwa na udumavu, hususan udumavu wa akili, kutokana na sababu kadhaa zinazohusika na makuzi yao ikiwemo lishe duni.
Iddi Simba aliendelea kueleza kwamba kwa vile watoto wa jana ndiyo watu wazima wa leo, hivyo Tanzania kuna hatari tukawa tuna asilimia 51 ya watu waliodumaa kiakili na kwamba kimaumbile na kwa kuzingatia nadharia ya mtapanyo (diffusion), si kawaida kwa wenye akili za kawaida kuwaambukiza wenye akili zilizodumaa, bali kinachotokea ni wale wenye akili zilizodumaa kuwaambukiza kitabia wale wenye akili za kawaida. Ukifuata mantiki ni kwamba mbali na ile asilimia 51 ya watu waliodumaa kiakili kuna asilimia nyingine zaidi inayoongezeka baada ya waliodumaa kuwaambukiza wenye akili nzuri.
Maprofesa, waliishambulia hoja hii kwa nguvu zote. Kwa kusema kwamba kama hii ni kweli, basi wao wasingekuwa na uwezo wa kufundisha tena, maana kila mwaka wanaingiza chuoni wanafunzi wasiojua kitu, na mwisho wa masomo wanakuwa wameelevuka. Kwa mantiki kwamba walioerevuka wanawaambukiza wasiojua kitu.
Ingawa sina uhakika kabisa na hoja ya kwamba lishe mbovu inaleta udumavu wa akili, sikuwa na matatizo ya kumwelewa Iddi Simba. Labda ningekuwa ni mimi ninatoa mada hiyo, ningetumia Udumavu wa Fikra, badala ya Udumavu wa Akili. Nina imani Iddi Simba hakumaanisha kutokuwa na akili za kusoma shule na kushinda mitihani. Nafikiri alimaanisha upevu wa fikra, maono, uvumbuzi na ujuzi wa kuyaweka aliyojifunza mtu kwenye matendo.
Zaidi ya miaka 45 ya uhuru wetu, Tanzania tuna kitu gani cha kuuonyesha ulimwengu kwamba hatukudumaa kifikra? Tumevumbua nini? Tunatengeneza nini cha pekee katika viwanda vyetu? Tuna mchango gani katika dunia hii ya utandawazi? Madini yetu ya kipekee ya Tanzanite, yanaingia sokoni yakiwa na nembo ya Afrika ya kusini. Tumeshindwa kuendesha shirika letu la ndege, tumeshindwa kuendesha shirika letu la reli, tumeshindwa kuendesha viwanda vyetu na tumeshindwa kudhibiti rasilimali kila mtu anakuja na kuchuma na kuondoka. Kwanini mtu asifikiri kumedumaa kiakili? Ni neno gani zuri? Labda tuseme tumesinyaa kifikra?
Rais Robert Mugabe na Rais Mwai Kibaki ni wasomi wazuri, matendo yao ya kungangania madarakani ni dalili za udumavu wa fikra aliotaka kuuelezea Iddi Simba. Watu wamekufa na nchi zao zimeingia katika matatizo makubwa kwa sababu ya tamaa zao binafsi. Huu ni udumavu wa fikra. Hakuna njia nyingine ya kuelezea jambo hili. Kuna mifano mingine mingi ya viongozi wa Afrika, waliozifukarisha nchi zao kwa kuchota utajiri mwingi na kuwekeza nchi za Ulaya. Chanzo chake ni udumavu wa fikra.
Inawezekana neno hili ni la udumavu wa akili ni baya kwa wale wanaofikiria kwamba wana akili nzuri. Lakini watu hawa watatuelezea nini juu ya wasomi wanaosaliti taaluma zao kwa sababu ya kutaka kupata utajiri wa haraka na maendeleo binafsi. Madaktari wanaokubali kuingiza dawa bandia na kuzisambaza nchi nzima wanakuwa na akili nzuri au wamedumaa kiakili? Au madaktari wanaozikimbia nchi zao maskini na kwenda kutafuta mishahara mikubwa nchi za nje wana akili nzuri?
Mtu asiyekuwa na uzalendo, anakuwa amedumaa kifikra, vinginevyo hakuna namna nyingine ya kulielezea hili. Wataalamu wanaopitisha mikataba mibovu ambayo wanafahamu itawaathiri wao, watoto wao na vizazi vijavyo wanakuwa na akili nzuri au ni wadumavu wa akili?
Suala si kusoma, na si kuwa profesa, daktari. Unaweza kusoma, unaweza kuwa Profesa, lakini kama huna fikra pevu na maono ya mbali, unakuwa na udumavu wa fikra. Hadi leo bado kuna mjadala mkubwa wa kutumia lugha yetu ya Kiswahili katika kufundishia. Mtu akianza kujiuliza kutumia lugha yake ama kutoitumia, kunakuwa na kasoro fulani kwenye akili yake.
Baadhi ya Watanzania wanataka walipwe mshahara bila kufanya kazi. Ni Watanzania wangapi wanafanya kazi saa zinazotakiwa na kutambuliwa na serikali? Kila sekta kuna ugonjwa wa Ametoka kidogo. Na huyu mwenye ugonjwa wa kutoka kidogo na kuchelewa au kutofanya kabisa anataka alipwe mshahara mwisho wa mwezi. Je mtu huyu anakuwa na akili nzuri au ni mdumavu wa akili.
Kwa nini taifa tajiri kama ilivyo Tanzania, tuendelee kuomba misaada kutoka nje, hadi msaada wa kujenga vyoo? Na mbona tunapopata misaada hiyo, badala ya kuendesha miradi ya maendeleo tunakimbilia kununua mashangingi na kupanda daraja la kwanza kwenye ndege? Wanaotoa misaada wanapanda daraja la kawaida kwenye ndege; lakini sisi waheshimiwa wetu ili wawe waheshimiwa ni lazima wapande daraja la kwanza kwenye ndege kwa kutumia fedha za misaada. Je huu si udumavu wa fikra?
Wasabato masalia, ni wasomi! Lakini baadhi yao walitaka kusafiri hadi nchi za nje bila pasipoti, tiketi na visa. Waliamini kwa nguvu za Mungu, wangeweza kusafiri na kuongea lugha ngeni bila kujifunza. Kama huu si udumavu wa akili ni kitu gani? Lakini pia na wale wote wanaoamini kwamba mkate unaweza kugeuka kuwa mwili na divai kugeuka kuwa damu ya Yesu, au kupona malaria bila kutumia dawa, kutibu ukimwi kwa miujiza, wana matatizo yale yale ya udumavu wa akili. Tunaweza kutofautiana kwa maelezo, lakini hatimaye hoja ya Iddi Simba, ni ile ile ya kuwataka Watanzania kujikomboa kifikra.
Ni lazima tuwe na fikra pevu na maono; ni lazima kuijenga Tanzania yetu na ya vizazi vijavyo; mbali na ukweli huu ni kukubali bila aibu kwamba tuna ugonjwa wa kudumaa kifikra.