Hukumu Yanga, Simba Machi 5

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) jana lilitoa ratiba ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Tanzania Bara ambapo watani wa jadi Yanga na Simba watakutana Machi 5 kwenye Uwanja wa Jamhuri Morogoro.

Katika mechi ya mzunguko wa kwanza iliyofanyika Oktoba mwaka jana kwenye Uwanja wa CCM Kirumba Mwanza, Simba ambayo ilikuwa mwenyeji wa mechi hiyo ilichapwa bao 1-0 lililofungwa na Jerryson Tegete.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, mzunguko huo wa lala salama wa Ligi Kuu unatarajiwa kuanza Januari 15 na utamalizika Aprili 10, 2011.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Ofisa habari wa TFF Boniface Wambura alisema, ratiba imepangwa kuzingatia ushiriki wa Simba na Yanga kwenye michuano ya Kimataifa.

Wambura alisema, ratiba hiyo pia imezingatia maandalizi ya timu ya Taifa, Taifa Stars kwa ajili ya mechi za awali za kuwania fainali za Kombe la Mataifa Afrika dhidi ya Afrika ya kati itakayochezwa Machi 26 pamoja na mechi za kirafiki za kalenda ya Fifa.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, Simba na Yanga hazitaanza Januari 15 badala yake zitaanza kucheza Januari 21 ambapo Simba itakuwa nyumbani CCM Kirumba Mwanza ikiikaribisha Azam na Yanga itakuwa nyumbani Jamhuri Morogoro ikiikaribisha AFC.

Siku ya kuanza kwa duru hilo la pili, Azam itakuwa nyumbani Uwanja wa Mkwakwani Tanga ikimenyana na Kagera Sugar, Toto African itakuwa CCM Kirumba Mwanza ikimenyana na Polisi Dodoma, Majimaji itakuwa mwenyeji wa JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Majimaji na AFC itaikaribisha African Lyon kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha.

Aidha ratiba hiyo inaonesha kuwa kabla ya Yanga kukutana na Simba, itacheza na Ruvu Shooting Februari 28 na Simba itacheza na Mtibwa Sugar Februari 27.

Simba ndio bingwa mtetezi wa ligi hiyo na ilimaliza raundi ya kwanza ikiwa inaongoza kwa pointi 27 ikifuatiwa na yanga yenye pointi 25 na Azam inashika nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi 20.

Kuhusu timu za Dar es Salaam kutumia Uwanja wa Uhuru, Wambura alisema haitawezekana kwani mpaka jana Serikali ilikuwa haijajibu maombi yao.

Simba na Yanga kupitia TFF ziliomba Serikali iruhusu watumie Uwanja wa Uhuru na ule wa Taifa ili kuwapa mazoezi wachezaji wao wanaokabiliwa na michuano ya kimataifa na pia kupunguza katika hatua nyingine, Wambura alisema Kamati ya Utendaji ya TFF itakutana ili kuthibitisha tarehe ya kuanza kwa fainali za Ligi Daraja la Kwanza na kuchagua kituo kitakachofanyika ligi hiyo baada ya kutotokea mkoa ulio tayari kuandaa.

Awali TFF ilitangaza kuwa mkoa wowote unaotaka kuandaa fainali hizo unaruhusiwa ilimradi tu uwe na Sh milioni 20 za maandalizi, lakini mpaka sasa hakuna mkoa wowote uliojitokeza.

Timu zilizofuzu hatua hiyo ni Coastal Union ya Tanga, JKT Oljoro ya Arusha, Morani ya Manyara, Moro United ya Dar es Salaam, Polisi Morogoro, Rhino ya Tabora, Prisons ya Mbeya, TMK United ya Temeke na Villa Squard ya Kinondoni.

Timu nne za kwanza zitapanda kucheza Ligi Kuu msimu ujao.
 
Back
Top Bottom