Hukumu ya Chenge sasa baada ya Krismasi

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
266
HUKUMU ya kesi ya kuendesha gari kwa uzembe na kusababisha vifo vya watu wawili inayomkabili aliyewahi kuwa Waziri wa Miundombinu, Andrew Chenge, imeahirishwa hadi Desemba 29, mwaka huu.

Kesi hiyo iliahirishwa jana katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni mbele ya Hakimu Mfawidhi Kwey Rusema kwa kuwa Chenge hakuhudhuria mahakamani kwa madai yu safarini Mwanza kwenye msiba.

Chenge alitakiwa kupanda kizimbani jana ili kusomewa hukumu baada ya kukamilika kwa ushahidi uliotolewa kutoka pande zote mbili katika kesi hiyo iliyodumu kwa zaidi ya mwaka mmoja na miezi minane.

Awali, Wakili anayemtetea Chenge, Simon Mponda aliiomba Mahakama hiyo kutotoa hukumu hiyo jana kwa kuwa mshitakiwa hajafika kwa sababu amepata udhuru na kuwa amesafiri kwenda Mwanza kwenye msiba.

“Kutokana na maombi ya upande wa mshitakiwa na kwa kuwa mshitakiwa hayupo mahakamani, ninaahirisha kesi hii hadi Desemba 29, mwaka huu kwa ajili ya kutoa hukumu,” alisema Hakimu Rusema.

Chenge anakabiliwa na mashitaka matatu likiwemo la kuendesha gari kwa uzembe na kusababisha vifo vya wanawake wawili, kuharibu pikipiki ya matairi matatu pamoja na kuendesha gari lisilokuwa na stika ya bima.

Katika moja ya ushahidi wake mahakamani hapo, Chenge ambaye ni Mbunge wa Bariadi Magharibi mkoani Shinyanga, alidai shahidi wa tatu wa upande wa mashitaka, Fortunatus
Musilimu, ana ugomvi naye.

Chenge alidai shahidi huyo ambaye aliwahi kutoa ushahidi kuwa mabaki ya ubongo wa marehemu yalikutwa kwenye gari la Chenge na kuwa aliwasilisha bima batili, kuwa ni mwongo na ana ugomvi naye.

Ilidaiwa kuwa Machi 27, mwaka jana katika Barabara ya Haile Selassie Oysterbay, mshitakiwa akiendesha gari aina ya Toyota Hilux Pick Up namba T512 ACE, aliigonga

pikipiki ya matairi matatu (bajaj) yenye namba T 736 AXC na kusababisha vifo vya Beatrice Costantino na Vick George. (mwisho)
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom