How to 'kill' mwananchi!

IsangulaKG

JF-Expert Member
Oct 14, 2010
706
385
Salamu baba yangu,

Natumaini U mzima baba yangu mpendwa'

Kijana wako naendela kutafuta Maisha huku mjini na usiwe na wasiwasi kwani barua yako kuhusu kibanda chako cha majani kuvuja niliipata na kwakweli najikusanya ili baada ya siku kadhaa nikutumie ‘vijifedha' japo upige kaslopu.

Hata hivyo, hongera sana kwa kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa kijiji kwa mara ya nne mfululizo. Natambua pengine juhudi zako za kubandika picha ya Rais wetu hapo mlangoni kwenye mlango wako wa bati lenye kutu na matobi kadhaa, kujitahidi kuibadili kila inapoharibika kwa kunyeshewa na mvua kutokana na kibanda chako kuvuja, kubandika picha za maraisi woote waliopita toka uhuru hapo ndani ambapo sebule inashirikiana na chumba cha kulala na zizi la ndama wako na kuku ambao huwachinjia wageni wanapokuja. Nakumbuka wakati wa mbio za mwenge nikiwa mdogo uliwahi kutoa jogoo mkubwa uliyekuwa umeahidi kuwa ni wangu na ukawachinjia viongozi wa Mwenge, japo nilifaidika kwa kasumba ile ya ‘mgeni njoo wenyeji wapone' bado nakudai jogoo wangu (teh teh teh). Ningeweza kukuuliza maswali ambayo nakuuliza kila siku; mfano:
Viongozi hao uliobandika picha zao ukutani mwako toka enzi za uhuru, wanayafahamau mapenzi yako makubwa kwao?
Wanatambua imani kubwa uliyonayo kwao?
Natambua pia kuwa wanakutumia mara nyingi kugawa sabuni, mikate, vitenge, pombe kwa wazee wakati wa uchaguzi , je wanakutafuta baada ya uchaguzi?

Hata hivyo tuyaache hayo;
Baada ya kusoma barua yako kuwa umechaguliwa tena kuwa mwenyekiti wa kijiji, na japo ulikuwa na upinzani wa vijana kutokana na umri wako ; naomba nikufundishe jinsi ya ‘Kuwaua' wananchi kifikra. Najua wewe ni mwalimu wangu mkuu hapa duniani japo, mwanafunzi aweza kuwa na elimu zaidi ya mwalimu na pengine hata akamfundisha Mwalimu kwa mfumo huu wa elimu mpaka uzeeni;

Nakupa mbinu; za kuwaua kifikra
Uwatawale; hadi utapofariki;

Baba mwenyekiti,
Kumuua mwananchi, huitaji atomiki
Fikra Zake zipanchi,Itawale yake haki
April hadi Machi, atalala hazinduki
Ukizama kwenye pochi, sana Utammiliki,
Kwa vinoti mishikaki,
Visivyomaliza dhiki!

Ili umuue mwananchi kifikra baba mwenyekiti ;
Kwanza , endelea hali ile ile ya kuwajengea hofu iliyokuwepo toka enzi za Uhuru.
Hofu ambayo imekufanya wewe binafsi uendelee kubandika picha za maraisi wako ukutani mwaka kila mwaka.
Hofu ambayo ilikufanya ukachinja ‘jogoo' wangu wa urithi kwa viongozi wa mwenge.
Hofu ambayo inakufanya unatetemeka kuwakusanya wananchi wakati wa uchaguzi ili wapokee ‘vifadhira'
Hofu ambayo inakufanya uchukie vyama vya upinzani na kuwaona kama ni wakorofi,
Hofu ambayo inakufanya uwaogope vijana kwamba watakiyumbisha kijiji iwapo watatawala
Hofu inayokufanya ushindwe kukubali kuwa sasa huwezi kuwaletea wanakijiji wako maendeleo kwa kuwa fikra zako ni zile zile.

Ukimjaza hofu hii mwananchi baba mwenyekiti;
Utakuwa bosi wake,
Tapoteza wezo wake,
Takuona malaika,
Uchaguzi ukifika,
Ahadi za kusadikika,
Endelea kutamka,
t shirt kimvika,
Japo suruali viraka,
Fikraze tazishika!

Yaani kama nilivyosema awali utakuwa ‘Umemuua'

Pili, Baba Mwenyekiti; Mnyime nafasi ya kupanga mikakati ya maendeleo yake mwenyewe, mpangie wewe au wataalamu toka huko wizarani.
Toka uhuru au hata kabla ya uhuru, na vile kilivyoanzishwa kile kitengo cha Mipango kule wizarani , basi ‘wataalamu' wa wizara wataenda Bagamoyo au Kunduchi Beach. Wakapanga:
Mipango ya Elimu ya mwananchi wa kijijini ambako hawajui hata sura ya darasa
Mipango ya afya kijijini, wakati hawajui hata ndani ya dispensary kuna nini
Mipango ya kilimo kijijini wakati hawajui hata mashamba yana sura gani
Wanapata kiyoyozi
na upepo wa baharini
Wanawapangia mikakati
Wananchi kijijini
Kuundoa umasikini
Kwa mikakati ‘makini'
Ikisomwa Bungeni,
Bajeti ikawini,
Inafungiwa kabatini,
Ukiuliza kwa nini,
Serikali haina uwezo!

Hata ile inayokuja huko kijijini
Kila ngazi inapopita
Inapingwa Panga na wajanja
Hata kamati yako
Nayo inapata Nyanja
Kuwadhulumu wananchi wako!

Kwa kuwa umewatawala akili, yaani umewaua kifikra, hakua atakaye hoji.
Kwa kuwa hawakushiriki kuandaa mikakati ya kushughulikia umasikini ‘WAO' . Hawa jamaa wa wizarani wanapokuja na mikakati yao , hakuna mafanikio. Unabisha? Jiulize mafanikio ya MEM, MMEM, Mabadiliko ya sekta ya Afya kadhaa…na kadhalika. Imekusaidia nini hapo kijijini?


Tatu, namna nyingine ya kuwaua wananchi kifikra; wala usiwape taarifa za maendeleo ya kijiji hasa fedha zinazopatikana wala usijiudhuru wakikulaumu. Suala la kuwajibika kwa viongozi kwa wananchi japo ndiyo waliompa mamlaka halipo katika nchi zetu hizi. Kiongozi ni mtumishi wa wananchi pale tu anapoomba kura, baada ya hapo, kiongozi yuko juu ya serikali, yuko juu ya bunge na zaidi kabisa yuko juu ya Wananchi! Unabisha? Umesikia madaktari wamegoma hivi karibuni lakini viongozi wameng'ang''ania madarakani. Umesikia kiongozi mkubwa anayemiliki silaha za kivita (halafu ati mnasema nchi ina amani) amepoteza nyaraka za serikali wakati akila raha na kimada wake, bado anaendelea kuongoza?. Kiongozi anayeamini kuwa siraha ni ‘mtaji wa maisha' kwa tafsiri rahisi ukiwa na siraha wewe ni tajiri……ujambazi? Bado yuko madarakani!

Nne,kwa kuwa mkuu wa kituo cha polisi pale wilayani na askari wa sungusungu wako chini yako; kamata kila mmoja mwenye kiherehere. Yeyote Yule anayejifanya kutaka kuwafufua wananchi toka katika kifo chao cha fikra, KAMATA, WEKA JELA, HUKUMU! Tumia ule mfumo maarufu wa ABP-ACUSE, BLAME, PUNISH. Mfumo huu wa ABP ndiyo wanaoutumia viongozi wako huku juu na kwa kuwa unawaamini sana ni vema ukatumia mbinu hii. Uitumie mbinu hii kwa kila mwananchi;
Utamtumikisha, bila swali kuuliza,
Utamplelekesha, Kukupinga hatowaza,
Utamnyenyekesha, Sautiye hatopaza!

Anza sasa kutumia mbinu hizi kama ulikuwa bado hujaanza
Na UTAKUWA UMEMUUA KIFIKRA! Kwa kikoloni nasema.This is HOW TO 'KILL' MWANACHI!
Wasalaamu!
Mwanao Mlosi K. Mtulutumbi (MKM)
 
Kwa maudhui ya barua hii tayari kumbe "TUMEISHA KUFA!!"
You're a real GT!!! THANKS!!
 
Back
Top Bottom