House Girl akaleta kisirani “Trial marriage” yangu ikaota mbawa………!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398
Ilikuwa ni Mwaka 1997, ndipo mimi na mpenzi wangu wa awali tuliamu kufanya kile wazungu wanachoita Trial Marriage, yaani kuishi kinyumba kabla ya ndoa ili kupima kama tutaweza kumudu maisha ya ndoa. Tulikubaliana tuishi pamoja kwa muda wa mwaka mmoja ili kupima kama tabia zetu zitaendana kabla ya kuingia huo mkataba wa hiyari. Tulikuwa tukiishi Kinondoni Mkwajuni tukiwa tumepanga upande mmoja wa nyumba na upande mwingine ukiwa umepangishwa na familia nyingine. Alikuwa ni dada mmoja ambaye alikuwa hajaolewa lakini alikuwa na mpenzi wake dereva wa malori ambaye alikuwa anakuja pale mara chache kutokana na kusafiri mara kwa mara. Pia yule dada alikuwa ni mfanyabiashara wa Vinyago na huwa anasafiri sana kwenda nchini Afrika ya Kusini kupeleka Vinyago, na alikuwa kila akisafiri anakaa huko kwa wiki moja hadi mbili wakati mwingine hivyo mara nyingi tunajikuta tukiwa peke yetu katika nyumba hiyo.

Baada ya kuishi pamoja kwa muda wa miezi 9 ikiwa imebaki miezi mitatu mwaka utimie ili tuweze kuulizana kama ingefaa sasa tufunge ndoa au la, mpenzi wangu alipata taarifa kuwa mama yake yu mgonjwa sana na kwa sababu ni mtoto pekee wa kike katika familia yao ya watoto wanne alilazimika kwenda kwao mkoani Tabora kwa ajili ya kumuuguza mama yake. Kwa kuwa alikuwa ni muajiriwa serikalini, aliomba likizo bila malipo na kuondoka na kuniacha mpweke. Siku tulipokuwa tunaagana pale stesheni tulikumbatiana kwa huzuni na wote machozi yalitutoka kwa majonzi ya kutengana.

Nilikuwa na kawaida ya kuwasiliana na yeye kila nikiwa ofisini kwa kutumia simu ya ofisi, na alikuwa ananipa matumaini kuwa mama yake atapona na atarudi ili tuendelee na mipango yetu ya kufunga ndoa. Alinijulisha kuwa mama yake (baba yake alishafariki siku nyingi) na ndugu zake wamenipenda sana baada ya kuona picha zangu na kuwaeleza tabia zangu. Tulifurahi pamoja na tulikubaliana atakaporudi tufunge ndoa rasmi na kuishi pamoja kama mke na mume.

Siku moja yule dada mpangaji mwenzetu alileta house girl, aliniambia kuwa analazimika kuwa na msichana wa kazi kwa sababu tumebaki peke yetu tusije tukaibiwa. Yule house girl alikuwa ananiheshimu kweli na alikuwa akinisaidi kazi za nyumbani kama kufua kudeki na kupika wakati mwingine, lakini alikuwa akinisaidia wakati yule mwajiri wake akiwa amesafiri, hata sijui kwa nini nilimruhusu kunisaidia kazi zangu na uhuru wa kuingia ndani mwangu. Lakini nilijua labda ni binti ambaye amefunzwa kuwaheshimu wakubwa huko kwao. Alikuwa ni binti wa Kimwela kutokea mkoani Lindi, na alikuwa na heshima ile ya kijijini hasa.

Siku moja nilirudi jioni lakini sikukaa, nilitoka kidogo kwenda kumtembelea rafiki yangu aliyekuwa akiishi maeneo ya Kinondoni Biafra. Wakati natoka aliniomba nimuachie funguo ili anisaidie kupika, nilisita kwanza kumpa, lakini aliponisisitiza, nilijikuta namuachia funguo. Hata hivyo nilimtahadharisha asije akaacha mlango wangu wazi, kama akitoka kwenda popote, hata dukani. Nilitoka na kwenda kwa rafiki yangu na huko nilikaa hadi saa nne usiku na nikala chakula cha usiku huko huko ndio nikarudi nyumbani. Nilipofika nilikuta mlango wangu umeegeshwa na nilipofungua mlango nilikuta yule binti kaandaa chakula mezani, lakini nilisikia kama mtu anayeoga huko chumbani, nikashtuka kwani mpenzi wangu niliongea naye jioni hiyo alikuwa bado yuko kwao Tabora, sasa ni nani anayeoga huko chumbani kwangu, nilishikwa na udadisi. Nililazimika kuingia chumbani kwangu, na kukutana na yule binti akiwa uchi wa mnyama akijifuta maji kwa kanga yake, alikuwa amevaa chachandu nyingi kiunoni, nilibaki pale mlangoni nikimkodolea macho, alikuwa amegeukia ukutani na alionekana kutojua kabisa kama kuna mtu ameingia ndani, nilibaki nimeduwaa. Alikuwa ni binti aliyeumbika hasa, sikuwahi kudhani kama ana umbo zuri vile, kwani alikuwa akijitanda kanga mara nyingi. Aligeuka ghafla na kuniona, alishtuka sana na kukimbilia kanga yake, aliyokuwa ameitupa pale kitandani wakati akijiangalia kwenye kioo cha kabati. ‘Sasa unaficha nini wakati nimeona kila kitu' nilimwambia kwa utani. Hakunijibu aliendelea kujifunga kanga zake huku uso wake ukiwa umetawaliwa na aibu, kisha akataka kutoka. Ibilisi alishaniingia, nilijikuta nikimzuia na kilichofuata ni kumtupa kitandani. Zoezi halikuwa gumu kwani alionyesha ushirikiano wa hali ya juu, kama vile alikuwa anajua kitakachotokea. Nilijikuta nikimsaliti mpenzi wangu kwa mara ya kwanza!

Baada ya kitendo kile na yule binti kuondoka, nilijilaumu sana, na sikulala kwa kuwaza. Kesho yake niliwahi kazini na kitu cha kwanza nilimpigia simu mpenzi wangu kumjulia hali na kujua hali ya mgonjwa, tuliongea kidogo, lakini kabla sijakata simu aliniuliza kama niko mzima, nilimwambia kwamba mimi ni mzima. 'Kwani vipi' nilimuuliza. Aliniambia kuwa sauti yangu iko tofauti sana na siku zote na inaashiria kama naumwa. Nilimwmbia kuwa mimi ni mzima wa afya na nilijifaragua kwenye simu ili kumtoa wasiwasi. Jioni niliporudi nyumbani yule binti alikuja tena akitaka kunisaidia kazi, safari hii nilikataa, yule binti alionekana kushtuka kwa kitendo changu cha kukataa kumruhusu kuingia ndani. Nilijifungia ndani na kujitupa kitandani, niliamua kutopika na kutoka kwenda kula chipsi kwenye Bar ya jirani na baada ya kula nilirudi nyumbani. Nilimkuta yule binti kakaa nje ya mlango wao akiwa amejiinamia, sikumsemesha, niliingia ndani kwangu na kujitupa kitandani.

Niliamka asubuhi lakini bado nikiwa na mawazo na kujilaumu sana. Wakati naondoka kwenda kazini alitaka nimuachie funguo, nikakataa. Nilipofika kazini majira ya mchana mpenzi wangu alinipigia simu na kunijulisha kwamba ameamua kuja na mama yake huku mjini ili apatiwe matibabu, alinijulisha kwamba mama atafikia kwetu kwa muda lakini atahamia wa mjomba wake baadae, nilikubaliana na yeye lakini aliahidi kwamba watakuja wiki ijayo. Baada ya mazungumzo yangu na mpenzi wangu kwenye simu. Nilijikuta nikiwaza juu ya tukio lile la juzi kutwa nzima na hata kazi hazikufanyika pale kazini. Jioni nilipotoka kazini nilikwenda kwa yule rafiki yangu aishie Biafra na nilimweleza juu ya ugeni unaokuja na kile kilichotokea na house girl wa mpangaji mwenzangu. Yule rafiki yangu pamoja na kunilaumu lakini alinishauri nihame haraka sana kwenye nyumba ile kabla mpenzi wangu hajarudi. Nilitafuta nyumba haraka haraka na hazikupita siku mbili nikapata nyumba maeneo ya Kijitonyama na nikahamia bila kumfahamisha mpenzi wangu, nilitaka kujifanya namfanyia surprise. Siku nahama nilimuaga yule house girl wa mpangaji mwenzangu kwamba nahamia Dodoma kikazi, nikamuacha akiwa ameduwaa, akiwa haamini kile kinachotokea.

Baada ya wiki tangu kuhama mpenzi wangu alirudi nikaenda kumpoke pale stesheni na ndipo nilipomjulisha kuwa tumehamia Kijitonyama, alitaka kujua sababu ya kuhama ghafla na kwa nini sikumjulisha juu ya mpango wangu huo, nilimwambia kwamba ni kutokana na ugeni aliosema anakuja nao niliona ile nyumba ni finyu na pia nilitaka kumfanyia surprise. Alionekana kushangaa kidogo, lakini alinisifu kwa maamuzi yangu, kwani nilimjulisha pia kwamba nimechukua nyumba kubwa ili mama aishi na sisi badala ya kwenda kwa mjomba. Tulikubaliana binti mmoja wa mjomba aje tuishi naye ili awe anamwangalia mama tukiwa hatupo. Na kweli mjomba alimruhusu binti yake mmoja akaja kuishi na sisi ili kutusaidia kumuangalia mama.

Baada ya kama mwezi mmoja tangu mke wangu arudi, siku moja aliporudi kutoka kazini aliniambia kuwa alikutana na yule mpangaji mwenzetu wa kule Kinondoni Mkwajuni, na alishangaa alipomweleza kuwa tunaishi Kijitonyama, kwani eti mimi niliacha ujumbe kwa house girl wake kuwa tumehamia Dodoma kikazi, nilishtuka kidogo, lakini nikaipotezea kwa kumwambia kwamba nilimdanganya tu yule binti kwa sababu huwa namtaniaga. Mke wangu alinijulisha kwamba alimwelekeza yule mpangaji mwenzetu mahali tunapoishi na akaahidi kwamba kuna siku atakuja kututembelea. Hazikuwa taarifa nzuri kwangu kwani sikutaka ukaribu na yule mpangaji mwenzetu kwa hofu kwamba anaweza kuja na yule house girl wake hapo nyumbani. Mwezi mmoja baadae nikiwa nimejipumzisha nyumbani siku ya jumapili majira ya jioni, nikiwa na mke wangu, mama yake, binti wa mjomba wake pamoja na mjomba na shangazi na wageni wengine waliokuja kumuona mgonjwa, tulisikia mlango wa geti ukigongwa, binti wa mjomba alikwenda kufungua.

Hivi mnadhani wageni wenyewe walikuwa ni akina nani?

Hawakuwa wengine bali ni yule aliyekuwa mpangaji mwenzetu wa kule Kinondoni Mkwajuni na alikuwa amefuatana na yule house girl wake, nilipoangalia sura zao, zilionyesha dhahiri kuna jambo lisilo la kawaida limetokea. Nilishtuka kidogo na kujifanya kuwachangamkia, na kuwakaribisha wakae. Hawakutaka kukaa kwani yule dada aliniomba tutoke nje kwa mazungumzo ya faragha. Nikajua nkondo igwa. nilijikuta nikijisemea moyoni, 'hapa lazima kutazuka kimbwaimbwai.'

Nilitoka nje na kusimama nao upenuni mwa nyumba yetu, na hapo ndipo yule dada mpangaji mwenzetu akanijulisha kwamba yule binti ana ujauzito wa miezi miwili na kasema ule ujauzito ni wangu kwa sababu nilimbaka na ndio chanzo cha mimi kuhama na kusingizia nahamia Dodoma kikazi. Kijasho chembamba kilianza kunitoka na miguu iliishiwa na nguvu, nikataka kukaa chini lakini nikashindwa, nikabaki nimewakodolea macho. Yule dada alinishtua kutoka kwenye lindi la mawazo, kwa kuniambia kwamba anamuacha yule binti pale nyumbani kwangu, kwani wazazi wake waishio Mbagala wamemwagiza amlete kwangu nimtunze mpaka akijifungua ndio nimrudishe kwao.

‘Lakini we binti mimi si nilitumia kondoma siku ile!' nilijikuta nikiropoka.

‘Wee koma, uwe umetumia kondom au sijui kifuko cha ashikirimu hiyo mie sijui, mimba ndiyo hiyo imeingia, na sasa unalo bwana wewe.' Yule binti aliongea kwa kupaza sauti kama vile tunagombana. Nilijaribu kumfanyia, Shiii, ili kumtuliza lakini haikusaidia kwani aliendelea kupayuka, ‘Mwenyewe ulijua kunidanganya kuwa unahamia Dodoma ndio ujaaanja, kumbe huna lolote, sasa leo ndio utaeleza kama Kijitonyama ndiyo Kizota.' Hakuishia hapo aliendelea kunishutumu kwa kumkimbia baada ya kumbaka, alionekana kunipania kweli, nikajikuta nimeishiwa maneno. Ghafla mke wangu akaja kule tulipo baada kusikia zogo akiwa ameongozana na mjomba na shangazi yake pamoja na wale wageni waliokuja kumona mgonjwa na kumkuta binti wa Kimwela kanifungia kibwebwe akinishambulia kwa maneno makali nay a kudhalilisha. Mke wangu alipotaka kujua kulikoni, ndipo yule dada akamweleza kuwa eti nilimbaka house girl wake na kumuachia ujauzito na ndio chanzo cha mimi kuhama katika nyumba ile na kudanganya kuwa nahamia Dodoma ili kukimbia soo.

Je mnataka kujua kilichotokea baada ya hapo………………….

Kwa kifupi uchumba ulivunjika na yule house girl tulikubaliana arudi kwao Mbagala na kuahidi kwa maandishi mbele ya mjumbe kupeleka matunzo ili kuepuka kufunguliwa kesi ya kubaka. Lakini katika hali ya kushangaza alijifungua mtoto chotara wa Kiarabu. Kumbe alikuwa pia na uhusiano na kijana mmoja wa kiarabu aliyekuwa akiishi pale jirani na tulipokuwa tumepanga na ndiye aliyempa ujauzito, lakini soo likaniangukia mimi, na kunisababishia ‘Trial marriage' yangu kuota mbawa.

Hata hivyo niliamua kusamehe na kumuachia Mungu.
 
mmmmh mtambuzi gustova duuh!
una mastoriii balaa, huu mji uliuvamia haswaaa.....
hii story inachekesha na kufundisha, pole mwaya kwa maswahiba hayoo duuh! eti trial marriage mmh!
 
Kisa kireefu. Kichekesha. Kinafunzo kinaelemisha pia.
Pole mdau.
Mjini shule, ulilelea mimba isokuwa yako mda wote huo!
 
mmmmh mtambuzi gustova duuh!
una mastoriii balaa, huu mji uliuvamia haswaaa.....
hii story inachekesha na kufundisha, pole mwaya kwa maswahiba hayoo duuh! eti trial marriage mmh!

Hii stori alinisimulia afki yangu na wala siyo mimi yaliyonikuta......................LOL

 
This is our dady Gustavo a.k.a Bruc lee,kaka wa hiari wa dada glady aliemchungulia utukufu wake,baba cantalisia .....!
 
nini hao wa mwaka 1997, ma housegirl wa siku hizi wanakuja na mawili kichwani...
wengine wanadiriki kuuliza kama kuna "baba"
baba ukiwa legelege mpenda vya bure kwishney
 
Lakini ni funzo kwa kina baba wanaotake advantage kwa wadada wa kazi, sio wote ni honest au naive kiasi hicho!

Hongera kwa utunzi, hiyo inafaa kuwa movie tosha, kwa waandishi wazuri wa script
 
Back
Top Bottom