Hotuba ya chadema kuhusu mswada wa fedha .

Mpaka Kieleweke

JF-Expert Member
Feb 27, 2007
4,132
1,571
HOTUBA YA MAONI YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI BUNGENI WIZARA YA FEDHA, MHE.CHRISTINA LISSU MUGHWAI (MB) KUHUSU MUSWADA WA SHERIA YA FEDHA, 2011
  1. UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani Wizara ya Fedha, Mhe. Kabwe Zuberi Zitto (MB), naomba kuwasilisha maoni ya Kambi rasmi ya Upinzani kuhusu Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2011, kwa mujibu wa kanuni ya 86 kifungu kidogo cha (6).

Mheshimiwa Spika, Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani Wizara ya Fedha na Uchumi wakati akihitimishahotuba yetu ya bajeti mbadala alisema maneno yafuatayo; ninanukuu; "Kila mtu akitimiza wajibu wake, Tunaweza.Tukiacha kuwa Taifa la walalamikaji, Tunaweza.Tukiendeleza Umoja wa Kitaifa, mshikamano na kulinda Haki za raia, Tunaweza.Ninaamini, Tunaweza!, mwisho wa kunukuu

.
Mheshimiwa Spika, kupitia hotuba yetu mbadala na michango yetu katika kamati za bunge na ndani ya ukumbi huu, Kambi rasmi ya Upinzani tuliweza kushauri na kujenga hoja za kutaka kuondolewa na kubadilishwa kwa mambo mbalimbali yaliyokuwa kwenye hotuba ya bajeti ya serikali na ambayo yangeweza kuwatesa wananchi; Hatimaye serikali imelazimika kuyaondoa; Tumetimiza wajibu wetu kwa kuleta bajeti mbadala, yenye mawazo mbadala na ya Kambi mbadala. Tumethibitisha kwamba Tunaweza.

Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani tulidai ada za leseni za biashara za Sh 10,000, 30,000 na 50,000 zilizokuwa zimewekwa na serikali zifutwe, ili zisiwaumize wananchi wengi wanaofanya biashara ndogondogo; na hatimaye serikali imelazimika kuzifuta. Tuliacha kulalamika na kuidai serikali iwatendee haki wananchi na hatimaye serikali imelazimika kufanya hivyo. Tumethibitisha kwamba Tunaweza.

Mheshimiwa Spika, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kiliongoza maandamano ya nchi nzima yaliyohudhuriwa na mamilioni ya Watanzania katika miji na vijiji mbalimbali vya nchi hii, kudai tozo na kodi mbalimbali katika bei ya mafuta na bidhaa nyingine muhimu zipunguzwe, ili kupunguza ukali wa maisha. Tulijenga mshikamano na wananchi na ndani ya Kambi rasmi ya upinzani na hatimaye serikali imelazimika kupunguza kodi na tozo hizo. Ni matumaini yetu kuwa sasa angalau bei za mafuta zitapungua. Tumethibitisha kwamba Tunaweza.

Mheshimiwa Spika, mbali na kupunguzwa kwa kodi na tozo kwenye mafuta kama tulivyotaka, Kambi ya Upinzani inaona bado ipo haja ya kuhakikisha bei ya mafuta inashuka zaidi na zaidi. Tangu mwaka 2008 serikali ilikuwa inasita kutekeleza kufanya uagizwaji wa jumla wa mafuta (Bulk Procurement), lakini kwa kuwa suala hili pia limesukumwa na Kambi ya Upinzani kabla hata ya kuanza kwa mkutano huu, hatimaye serikali imelazimika kutekeleza. Tumethibitisha kwamba Tunaweza.

Mheshimiwa Spika, ni matumaini yetu kuwa sasa kupitia uagizwaji wa jumla wa mafuta kupitia Shirika la Petroli Tanzania (TPDC), wafanyabiashara wa ndani wa mafuta watakuwa wakinunua mafuta katika shirika hilo, hivyo bei atakayonunulia mlaji inaweza kuwa nafuu.

Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani tulipinga ongezeko la faini ya makosa ya barabarani (Traffick Notification Fee) kutoka shilingi 20,000.00 hadi Shilingi 300,000.00 iliyopendekezwa na serikali, na hatimaye serikali imelazimika kupunguza faini hiyo mara kumi hadi kufikia shilingi 30,000.00. Tumethibitisha kuwa sisi ni Kambi Rasmi tunajali haki za watu wetu na kwa hiyo Tunaweza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa faini za makosa ya barabarani zimepunguzwa hadi kufikia Sh 30,000, bado Kambi ya Upinzani tunaitaka serikali ipunguze faini hiyo hadi kufikia Sh 20,000, kwani bado kuna ongezeko la Shilingi 10, 000 ambalo linaweza kuchochea rushwa.

Mheshimiwa Spika, izingatiwe kuwa katika mwaka wa fedha wa 2010/2011, serikali ilipata mapato ya kiasi cha shilingi bilioni 10, kutokana na faini hii ya makosa ya barabarani, lakini katika mwaka ujao wa fedha pamoja na kusudio la serikali kuongeza faini hiyo bado itapata mapato pungufu ya shilingi bilioni 8 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani tunaitaka serikali ijikite zaidi katika kuimarisha sheria na maadili yanayohusu usalama wa vyombo vya usafiri barabarani, badala ya kutumia faini ambazo zitachochea rushwa na kuongeza makosa ya uendeshaji wa magari barabarani

.
Mheshimiwa Spika, kwa mantiki hiyo tuliyoeleza, Kambi rasmi ya Upinzani tunapendekeza kifungu cha 23 cha Muswada wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2011, kifanyiwe marekebisho kwa kufuta kiasi kipya cha faini ya Shilingi 30,000 na kurejesha kiasi cha faini kilichokuwepo cha Shilingi 20,000.

Mheshimiwa Spika,
Kambi ya Upinzani kupitia taarifa rasmi ya vipaumbele vya bajeti mbadala tuliyoitoa siku chache kabla ya mkutano huu wa bunge kuanza, pamoja na mambo mengine, tuliitaka sehemu ya tozo ya kuendeleza ujuzi (Skills Development Levy) ielekezwe kwenye Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu; Na hatimaye kodi hiyo imeelekezwa tulikotaka. Tumethibitisha kwamba Tunaweza

Mheshimiwa Spika, hakikatunaweza, hiyo ndiyo raha ya Watanzania kuchagua wabunge wengi wa upinzani. Kwa kura zao, idadi ya wabunge wa Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni imeongezeka, na hivyo tumezidi kutimiza wajibu wetu wa kuibana serikali iliyoko madarakani katika kuhakikisha matakwa na maslahi ya wananchi yanaheshimiwa. Daima hatutarudi nyuma, tutaendelea kupigania wananchi wote wa taifa hili bila kujali jinsia zao, dini zao, makabila yao, na tofauti zao zozote zile.

Mheshimiwa Spika, Kwa niaba ya Kambi ya Upinzani, na kwa heshima na taadhima kubwa, nachukua fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza Watanzania wote kwa kutuchagua kwa wingi kuingia bungeni katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana. Tunaamini watatupa dola na kutufanya tuwe wengi zaidi mwaka 2015 ili tuzidi kusimamia matakwa yao kikamilifu, kwani bado yapo mambo mengi ambayo serikali imekataa kuyafanyia marekebisho, kama ifuatavyo;
  1. MAPENDEKEZO ZAIDI YA MAREKEBISHO
Mheshimiwa Spika, kifungu cha 4 cha muswada huu kinafanya marekebisho ya sheria ya kodi kwa kuongeza kifungu cha 56 A cha sheria ya kodi, kwa kuweka faini ya kulipa kwa riba iliyopo sokoni ya kodi ambayo haikulipwa kwa wakati pamoja na ziada ya asilimia 5.

Mheshimiwa Spika, katika hili, Kambi ya Upinzani, tunapendekeza kuondolewa nyongeza ya asilimia tano ya riba hiyo, kwani itatoa mwanya kwa watendaji wa mamlaka za ukusanyaji kodi kutumia vibaya mamlaka yao kunyanyasa wananchi na kujinufaisha binafsi.

Mheshimiwa Spika, katika kifungu hicho hicho cha 4 kwenye kifungu kidogo cha 5, Kamishna wa Mamlaka ya Mapato (TRA), amepewa mamlaka ya kutoza faini au kumpunguzia mlipaji riba inayotakiwa kulipwa zaidi kama mhusika atakuwa na sababu ya msingi ya kuchelewa kulipa kodi hiyo (good cause).

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani tunataka kifungu hicho kifanyiwe marekebisho kwa kuyawekea mipaka mamlaka hayo aliyopewa Kamishina wa TRA, kwani yanampa mwanya wa kufanya upendeleo kwa baadhi ya watu, kunyanyasa au kujinufaisha binafsi kwa sababu tu amepewa uhuru wa kuamua sababu ya msingi.

Mheshimiwa Spika, Kifungu cha 6 cha muswada huu kinafanyia marekebisho jedwali la nne la sheria ya kodi kwa kuongeza kodi katika bidhaa mbalimbali kama maji na vinywaji baridi

.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaona kuwa serikali haina nia ya dhati ya kushusha mfumuko wa bei za vyakula ambao pia unajumuisha maji na vinywaji hivyo.Waziri alishakiri kuwa mfumuko wa bei kwa kiasi kikubwa unasababishwa na ongezeko la bei za vyakula. Kwa hiyo, ongezeko hilo la kodi katika maji na vinywaji baridi, kwa vyovyote vile litasababisha kuongezeka kwa mfumuko wa bei katika vyakula na maisha kuzidi kuwa magumu.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu hizo, Kambi ya Upinzani, inapendekeza kifungu hicho kifanyiwe marekebisho kwa kuondoa ongezeko hilo la kodi katika maji na vinywaji baridi na kurejesha kodi iliyokuwepo zamani.
Mheshimiwa Spika, utafiti uliofanywa na Mtaalam Kankesu Jayanthakumaran wa Australia, kuhusu tathmini ya maeneo maalumu ya uwekezaji kiuchumi yaani Export Processing Zone (EPZ na Special Economic Zone (SPZ); uliochapishwa mwaka 2003, unaonyesha dhahiri kuwa nchi zinazoendelea bado hazifaidiki na uwekezaji katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, moja ya sababu ambazo Mtafiti huyo alizitaja kama sababu ya nchi kutokufaidika na uwekezaji katika maeneo hayo ni misamaha ya kodi na nafuu nyinginezo za kifedha.Kwa sababu hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani inapendekeza kuwa misamaha ya kodi ya miaka 10 inayopendekezwa katika vifungu 15, 19, 25 na 31 vya muswada huu kwamba wapewe wawekezaji katika maeneo hayo, tunataka ifutwe.

Mheshimiwa Spika, kifungu cha 30 cha muswada huu kinafanyia marekebisho jedwali la pili aya ya 8 la sheria ya kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa kuondoa Shirika la Nyumba la taifa katika msamaha wa kodi hizo. Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaona kuwa uamuzi huu wa serikali utawaathiri sana wapangaji wa nyumba za shirika hilo, kwani kwa sababu ya kutakiwa kulipa kodi hiyo ya VAT, shirika litalazimika kupandisha kodi kwa wapangaji wake na hivyo wapangaji wataathirika. Kwa mantiki hiyo, Kambi ya Upinzani tunataka kifungu hicho kifanyiwe marekebisho kwa kuurejesha msamaha wa kodi ya VAT kwa shirika hilo, ili kodi za nyumba hizo zisipande na kuwaumiza wananchi

.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani pia ilitarajia muswada huu uzingatie mapendekezo mengine tuliyoyatoa kwa maslahi ya wananchi lakini hayazingatiwa; Kwa hiyo, tukiweka mbele maslahi ya taifa, tunachukua fursa hii kusisitiza tena kuwa mapendekezo hayo yafanyiwe utekelezaji kama ifuatavyo;
  • Tunataka Sheria ya Kodi ya Mapato ifanyiwe marekebisho na kushusha kiwango cha chini kabisa cha kodi ya mshahara (PAYE) mpaka asilimia 9 na kiwango cha juu mpaka asilimia 27, ili kuwezesha wafanyakazi wabakiwe na fedha na hivyo kutumia katika uchumi na kukuza uzalishaji.
  • Tunataka Kodi katika misitu irekebishwe ili kuiongezea serikali mapato ya shilingi bilioni 100.
  • Tunataka Misamaha ya kodi kwa wawekezaji wakubwa ipunguzwe hadi kufikia asilimia 1 ili kuipatia serikali mapato ya shilingi bilioni 658.
  • Tunataka Kodi katika sekta ya madini irekebishwe ili kuipatia serikali mapato ya shilingi bilioni 240.
  • Tunataka Msamaha wa ushuru wa mafuta kwa kampuni za madini uondolewe ili kuipatia serikali mapato ya shilingi bilioni 59.
  • Tunataka pensheni ya shilingi 20,000 kwa mwezi tuliyotaka ianze kutolewa kwa kila mzee mwenye umri wa zaidi ya miaka 60, iingizwe katika muswada huu wa fedha, ili kuwapunguzia ukali wa maisha wazee wetu.
  • Tunataka posho za vikao (sitting allowances) zifutwe katika mfumo wa malipo ya ndani ya serikali.
Mheshimiwa Spika, Tunataka kuona Watanzania wakinufaika na kodi zao na raslimali zao zote walizojaliwa na Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo kazi waliyotutuma, na sasa tumeanza kuitekeleza.

Mheshimiwa Spika; Naomba kuwasilisha.
………………………………..CHRISTINA LISSU MUGHWAI (MB)NAIBU MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI -WIZARA YA FEDHA22/06/2011
 
Yaani serikali ya CCM ingekua inafanya kama wapinzani wanavyotaka na kuagiza, nina hakika wangetawala na kuwaongoza waTZ milele!!!
WaTZ wanataka unafuu na uhakika wa maisha. Mapendekezo mengi ya CHADEMA yanalenga kuleta unafuu na uhakika wa maisha; sasa CCM wangekopi na kupesti haya masuala, naamini wasingetoka madarakani.

Lakini kwa vile wao ni mabichwa magumu, anguko lao linawadia.
 
Christina Lissu Mughwayi Vs Tundu Lissu, kwenye chama kimoja cha CDM! Je hii imekaaje? Huyu ni dada au mkewe? Na alipataje kuwa mbunge? Au ndiyo indicator za ukabila? Wadau mtujuze maana CDM inalalamikiwa sana kwa ukabila
 
Mmhhh.. let me be objective kwa kweli mumejisifia sana mpaka mkasahau kujenga hoja....

Anyway mengine yanasikitisha... Ati
Mheshimiwa Spika, kifungu cha 30 cha muswada huu kinafanyia marekebisho jedwali la pili aya ya 8 la sheria ya kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa kuondoa Shirika la Nyumba la taifa katika msamaha wa kodi hizo. Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaona kuwa uamuzi huu wa serikali utawaathiri sana wapangaji wa nyumba za shirika hilo, kwani kwa sababu ya kutakiwa kulipa kodi hiyo ya VAT, shirika litalazimika kupandisha kodi kwa wapangaji wake na hivyo wapangaji wataathirika. Kwa mantiki hiyo, Kambi ya Upinzani tunataka kifungu hicho kifanyiwe marekebisho kwa kuurejesha msamaha wa kodi ya VAT kwa shirika hilo, ili kodi za nyumba hizo zisipande na kuwaumiza wananchi
Shirika la Nyumba lina wapangaji wangapi? na nisehemu gani ya watanzania mil. 43? na je wasiopanga shirika la nyumba wao hawalipo kodi kubwa.... hapa du! sijui mlikuwa mnafikiria nini?
 
Christina Lissu Mughwayi Vs Tundu Lissu, kwenye chama kimoja cha CDM! Je hii imekaaje? Huyu ni dada au mkewe? Na alipataje kuwa mbunge? Au ndiyo indicator za ukabila? Wadau mtujuze maana CDM inalalamikiwa sana kwa ukabila
we huna kabilla lisu ni kabila gani magamba na nyinyi
 
Nguvu ya uma ipo nyuma yenu makamanda komaeni dhidi ya maskini watanzani
 
Tunataka Kodi katika sekta ya madini irekebishwe ili kuipatia serikali mapato ya shilingi bilioni 240.

Hapa Chadema hamko specific, elezeni wazi, sekta ya madini irekebishwe vipi?, kodi katika madini itozwe Asilimia ngapi?, statement kama hii ya serikali kupata shilingi bilioni 240 is too general why not billion 500 au 1000 au zaidi?.
Chadema toweni msimamo wenu wazi kwamba Asilimia ya kodi iongezwe hadi iwe ngapi?, kwa sababu so far kodi ya madini yetu ni ndogo sana kiasi kwamba hatunufaiki na madini yetu!.
 
Back
Top Bottom