Kakke
JF-Expert Member
- Dec 4, 2010
- 1,883
- 1,482
[h=1][/h]Posted on June 26, 2012 by zanzibaryetu
SUALA la Muungano limezidi kutawala mijadala katika kikao cha baraza la wawakilishi kinachoendelea huku baadhi ya wajumbe wakitamka wazi kuwa hawataki Muungano. Katika kikao hicho ambacho tayari kimepitisha bajeti kuu ya serikali ya Zanzibar wajumbe wa baraza hilo jana walijadili bajeti ya ofisi ya makamo wa pili wa rais wakitaka serikali isimamie kupata uhuru zaidi wa kiuchumi katika muungano.
Ofisi ya makamo wa pili wa rais ndio inayotambulika kuwa msimamizi mkuu wa shughuli za serikali ndani ya baraza la wawakilishi.
Mheshimiwa Naibu Spika mimi niseme wazi kwanza kwamba sitaki muungano na katika kitu ambacho nakichukia sana basi ni huu muungano maana kwa miaka 48 ya muungano huu kila siku tunaambiwa kuna kero wala hazitatuliwi basi ni uvunjike tu alisema Mwakilishi wa Jimbo la Wawi (CUF) Saleh Nassor Juma.
Juma alisema kupigania haki ya Zanzibar haimaanishi chuki katika muungano na kwamba muungano uliyopo ni wa nchi mbili huru ambazo lazima kuwepo na haki sawa kwa pande zote mbili.
Naye Mwakilishi wa Jimbo la Kitope (CCM) Makame Mshimba Mbarouk alisema Lazima mheshimiwa makamo wa pili wa rais tuamke muungano huu, siwo tunataka maslahi ya Zanzibar na tunataka haki zetu zote kuanzia mapato ya gesi. Nitazuwia bajeti hii mpaka niambiwe katika accounti ya Zanzibar imepata kiasi gani kwa mapato ynayotokana na gesi maana ni haki yetu alisema Mbarouk.
Abdallah Juma Abdallah Mwakilishi wa Jimbo la Chonga (CUF) alisema viongozi wa serikali na vyama wamewekwa madarakani na wananchi hivyo sio sahihi kubeza maoni ya wananchi ambayo hawautaki mfumo huu wa muungano na kuahidi kusimama pamoja na wananchi wa jimbo lake iwapo waamua kuukataa.
Kiongozi yeyote kuanzia rais, wabunge na hata sisi wawakilishi tumewekwa hapa kwa kuchaguliwa na wananchi na tunasimama kuwasilisha maoni ya wananchi sasa ikiwa wananchi watasema hawataki muungano, mheshimiwa naibu spika lazima tusimame nao alisema Mwakilishi huyo na kuongeza.
Mimi kama mwakilishi wa chonga nasema wananchi kama watasema hawataki muungano basi nitasimama nao na nitakuwa bega kwa bega na kwa sababu wamenichagua kwa kuniamini na pia nahitaji tena kurudi katika nafasi hii na nikidharau maoni yao au matakwa nayo hawatanirejesha tena alisema Abdallah.
Mwakilishi wa nafasi za wanawake Asha Bakari Makame (CCM) kwa upande wake aliwaambia wajumbe wa baraza hilo kutoka CCM na CUF kwamba wanadhamana kubwa ya kuwatetea wazanzibari bila ya kuhofia nafasi zao na kwamba wazanzibari wanawatazama wao kwa kuwaamini.
Mheshimiwa naibu spika ni CCM na CUF pekee tuliyopo humu ndani wananchi wanatuamini na lazima turejesha imani kwa wananchi wetu ikiwemo suala kuu la kutetea Zanzibar ndani ya muungano kero gani hizi zisizokwisha? alihoji Asha ambaye aliwahi kuwa waziri wakati wa SMZ .
Asha Bakari ambaye ni naibu mwenyekiti wa umoja wa CCM Tanzania (UWT) alisema ni umoja na mshikamano miongoni mwa wazanzibari ndio silaha pekee itakayoweza kuwavusha wazanzibari katika kudai maslahi yao ndnai ya muungano.
Mimi siogopi chochote na kwa umri huu tena naona lolote litakalonifika ni sawa tu lakini nawaambia wenzangu kwamba tuiteteni Zanzibar na tusiwe na woga maana wengine wamezowea kututisha alisema kwa kutoa tahadhari.
Mwakilishi wa Jimbo la Mji Mkongwe (CUF) Ismail Jussa Ladhu alisema serikali ya Zanzibar inafanya makosa makubwa ya kuridhia kila kitu ambacho kinatolewa na serikali ya muungano.
Ni muda mrefu wimbo ndio huo huo wa ahadi ya kushughulikia kero za muungano na kero zenyewe hazishi kwa sababu hata hizo kamati hazipo kisheria za kutatua kero alisema.
Jussa alitaka viongozi wa serikali kuwaunga mkono wananchi katika madai yao ya msingi kwa kuwaelekeza nini waseme wakati wa kutoa maoni ya katiba mpya ya jamhuri ya muungano wa Tanzania na kwamba bila ya kutoa muongozo wananchi watababaika.
Mimi nina imani kubwa na serikali yangu ya umoja wa kitaifa na ninaipenda lakini naomba itoe msimamo hapa katika kuwaelekeza wananchi wakadai nini wakati wa tume itakapokuja kukusanya maoni alisema Jussa na kupigiwa makofi na wajumbe wenzake.
Aidha mwakilishi huyo aliwataka wananchi na viongozi wa siasa kutokuchanganya misimamo ya siasa pamoja na dini katika kutoa maoni kwani inaweza kuharibu na kuwagawa wazanzibari.
Awali akiwasilisha hutuba ya bajeti ya makamo wa pili ya kuomba kuidhinishiwa shilingi billioni 12.3 kwa mwaka wa fedha za 2012/2013 Waziri wa nchi Ofisi hiyo Mohammed Aboud Mohammed alisema juhudi zimekuwa zikiendelea katika kutatua kero za muungano na kwamba wajumbe wa baraza la wawakilishi wawe wavumilivu.
MWISHOUJENZI WA BANDARI
SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar imesema itatumia kiasi cha dola za kimarekani 400 millioni kwa ajili ya mradi wa bandari ya Mpigarudi Visiwani Zanzibar.Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Mawasiliano na Miundombinu, Issa Gavu alipokuwa akijibu suali la msingi la Mwakilishi wa Jimbo la Mji Mkongwe (CUF) Ismail Jussa Ladhu aliyetaka kujua mradi wa ujenzi huo utagharimu kiasi gari cha fedha.
Kwa gharama ambazo zinakisiwa kulingana na concept paper ya wizara, mradi huu usingeweza kuzidi USD$ 400 millioni. alisema Naibu Waziri Alisema hata hivyo kwa vile gharama hizo zilikisiwa miaka mitano iliyopita ingewezekana akuweka ongezeko la asilimia 10% ambapo mradi usingezidi dola za kimarekani millioni mia tano. (USD$ 500).
Akijibu suali la la fedha hizo zitatokea wapi na zina masharto gani, Gavu alisema fedha hizo hazijapatikana na hivyo masharti ya fedha yasingeweza kupatikana vile vile.
Awali Jussa alitaka kujua bandari hiyo iliyokusudiwa kujengwa ambayo ni ya kisasa pendekezo hilo limefanyiwa kazi kwa kiasi gani na limefikia hatua gani, ambapo Naibu Waziri alisema ni ya ujenzi huo upo na serikali inaendelea na mchakato wake.
Akizungumzia pendekezo hilo Naibu alisema linaendelea kufanyiwa kazi na kwa sasa serikali imeshakamilisha upembuzi yakinifu uliofanywa na kampuni ya CRB- ya China.
Naibu huyo aliwaambia wajumbe wa baraza la wawakilishi kwamba baada ya kuipitia wataalamu wameona bei iliyopendekezwa na kampuni hiyo ni millioni 800 fedha za kimarekani.
Millioni 800 ni nyingi sana na hiyo bado serikali imo katika kutafuta njia mbadala ya kufanikisha suala hili alisema Naibu waziri huyo.
Aliwaambia wajumbe wa baraza hilo kwamba licha ya baadhi ya wajumbe wameonesha wasiwasi wao juu ya kampuni ya kichina lakini bado serikali ina matumaini na ufanyaji wa kazi ya kampuni hiyo kwa mujibu wa mkataba waliofunga.
Mheshimiwa mwenyekiti haina maana kwa kuwa kampuni moja ya kichina imefanya vibaya na hii itakuwa imefanya vibaya kwa zile kampuni ambazo zimefanya vibaya za kichina ni nyengine lakini hii ni nyengine na bado serikali ina matumaini ya kufanya kazi yetu vizuri alisisitiza naibu huyo.
MWISHOUKOSEFU WA WALIMU YA SAYANSI
WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar imekiri kuwepo kwa uhaba wa walimu wa sayansi katika visiwa vya Unguja na Pemba.Naibu Waziri wa wizara hiyo, Zahra Ali Hamad aliwaambia wajumbe wa baraza la wawakilishi kufuatia suali la msingi la Mwakilishi wa Jimbo la Muyuni (CCM) Jaku Hashim Ayoub aliyetaka kujua ni sababu gani zinazochangia kuwepo kwa uhaba wa walimu wa sayansi nchini.
Zahra alisema uhaba wa walimu wa sayansi katika skuli za Unguja na Pemba unatokana na wanafunzi wengi kutofaulu masomo ya sayansi katika mitihani ya kidato cha nne na kidato cha sita na hivyo kupelekea vijana wachache wenye sifa za kujiunga na mafunzo ya ualimu kwa masomo ya sayansi.
Akijibu suali la kwa nini wizara ya elimu imeshindwa kulipatia ufumbuzi tatizo hilo Zahra alisema Ni kweli waheshimiwa wajumbe wizara iliahidi kulipatia ufumbuzi suala hili lakini ufumbuzi huo hauwezekani kupatikana mara moja na inahitaji muda wa kuweza kulitatua tatizo la upungufu huo.
Alisema wizara imepata vibali vya uajiri wa walimu wapya katika mwezi wa Aprili 2012, amabpo wizara iliajiri walimu 197 wenye shahada na stashahada mbali mbali wakiwemo walimu wa masomo ya sayansi.
Katika mwezi wa juni 2012 alisema wizara imepata kibali chengine cha uajiri wa walimu 111 wenye shahada na stashahada za ualimu wakiwemo walimu 48 wenye shahada ya kwanza ya masomo ya masomo ya sayansi.
Naibu waziri huyo alisema kukosekana kwa walimu hao kunaweza kuchangia katika kushindwa kwa wanafunzi kufnaya vizuri katika mitihani yao ya kidato cha nne na cha sita.
Aidha kushindwa kwa wanafunzi hao pia kunachingiwa na wanafunzi kutopendelea kusoma masomo ya sayansi kwa dhana ya kuwa ni masomo magumu au wanafunzi huliogopa somo la hisabati ambalo ndilo somo la msingi.
Ni kweli skuli ya Muyuni na skuli nyengine zina uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi. Uhaba huu unatokana na wanafunzi wengi kushindwa kufaulu masomo yao na kujiunga na vyuo vikuu alisema Naibu huyo.
Zahra alisema wengi wa waombaji wa mafunzo ya ualimu wamefaulu katika masomo ya sanaa kuliko sayansi na hivyo masomo ya sayansi hukosa walimu na tatizo hilo ni sio kwa skuli za zanzibar peke yake bali ni Tanzania nzima.
Hata hivyo alisema wizara imeandaa mafunzo ya ualimu kazini kwa walimu wasio na sifa za kufundisha masomo ya sayansi ili kuinua uwezo wao na hatimae waweze kudumu kuyafundisha masomo hayo.
Akizungumzia mikakati ya wizara yake katika kuhakikisha tatizo hilo linapungua Naibu Waziri alisema mpango wa wizara yake ni kuajiri vijana waliomaliza kidato cha sita na kufaulu masomo ya sayansi ili kusaidia kupunguza uhaba wa walimu wa sayansi.