Elections 2010 Hivi ni vyama vya siasa au ni usanii?

Anold

JF-Expert Member
Jul 15, 2010
1,456
613
Kuna vyama vya siasa mbavyo bado sijajua nia yao hasa katika Taifa hili. Nimesikitishwa sana na chama kimoja siasa (hivi ambavyo havina majina) ambacho kimemsimamisha mgombea ambaye ni Barmaid. Inawezekana wanasababu za msingi za kumsimamisha mgombea huyo ila kitu ambacho kimenisikitisha ni kauli za mgombea huyo alizokuwa anazungumza wakati naongea naye. Mgombea huyo nilimsikia kwa masikio yangu akisema kuwa anachotafuta ni hizo hela tu za kampeni na si vinginevyo, hapo ndio nikaanza kupata ufahamu kuwa kumbe kuna hela wagombea wanapewa ili ziwasaidie katika kampeni. Nilipo muomba anipe japo sera za chama anachokiwakilisha alikiri wazi kuwa hana analojua kuhusu hicho chama aliniambia kuwa yeye alielezwa kuwa asiwe na wasiwasi kwani kunawatu maalumu wameandaliwa kufanya kazi hiyo.

Kwangu mimi hili nalichukulia kama mzaha wa wazi ambao hauna tija kwa chama husika wala taifa, sitaki kuamini kuwa kuna watanzania ambao bado wanafanya mzaha na kebehi kwa mambo ambayo yana maslahi kwao na kwa Taifa kwa ujumla. Hivi mgombea huyo kwa bahati kama atapita atakuwa na lipi la maana kwa Taifa na hao waliomchagua?

Suala la kusimamisha wagombea inavyoelekea sio jambo linalohitaji umakini kwenye baadhi ya Vyama, ni suala la bora mgombea na sio mgombea bora, huu ujinga unaofanywa na hivi vyama ambavyo ni vingi, ndio unaofanya vyama vikongwe vilale usingizi,maana vinajua fika kuwa ushindi ni lazima.

Mgombea huyo ambaye nimemtaja hapo juu kuwa anagombea kiti cha ubunge kupitia chama fulani hapa jijini ni mfano tu, ila wamejitokeza wagombea wengi ambao kimsingi hawana sifa wala uwezo wa kuwa kiongozi kwa namna yeyote ile. Kwa ishara hizi ni dalili tosha kuwa kama sheria zetu za uchaguzi hazitakuwa makini basi huko tuendako tutashuhudia hata watu wa hovyo wakipata nafasi za uongozi katika nchi yetu. Tokea lianze zoezi la kuchukua na kurudisha fomu za wagombea katika kiti cha urais tumeshuhudia watu wa ajabu wakichukua na kurudisha fomu hizo kwa mbembwe na vituko, Pamoja na ukweli kuwa wana haki ya kikatiba lakini siamini kuwa hawajui kuwa hakuna uwezekano wa kupata nafasi hiyo, pamoja na ukweli kuwa hiyo ni demokrasia lakini mimi nafikiri huo ni uhuni na usumbufu unaosababisha taifa liendelee kupata hasara kwa kutumia hela za walipa kodi kwa ajili ya watu ambao hawana nia njema kwa Taifa.

Nafikiri kuna haja ya kuwa na udhibiti wa wagombea bila kuathiri suala zima la Demokrasia, haiwezekani suala la siasa liwe kama soko huria, kama mambo yataenda hivyo basi siku moja nchi yetu itapata viongozi mateja na hilo litadhalilisha sana Taifa letu ambalo limejijengea heshima kubwa kwa siku nyingi.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom