Hivi ndivyo vitabu vyetu, inatisha!!!

AHAKU

Member
Jan 28, 2010
26
1
Wakuu naomba mpitie hiyo makala hapo chini muone naomna sekta ya vitabu ilivyovamia Bongo. Ni makala kutoka gazeti la Mwananchi leo jumanne tar 26 2010


Mkanganyiko vitabuni
Kitabu chafundisha mbu anasababisha kipindupindu
Na Abeid Poyo
UJIO wa mfumo wa kiuchumi wa soko huria umeleta athari katika nyanja mbalimbali nchini ikiwemo sekta ya elimu.
Mfumo wa elimu Tanzania umevurugika baada ya elimu kugeuzwa kuwa bidhaa inayonadiwa sokoni.
Mojawapo ya athari ya mfumo huu wa kiliberali ni kuzuka kwa waandishi wengi wa vitabu vya masomo shuleni wanaopotosha maarifa katika vitabu wanavyotunga.
Kukosekana kwa udhibiti wa vitabu kutoka mamlaka husika, kumesababisha idadi ya watunzi kuzidi kukua huku baadhi wakichapisha vitabu na kuvipeleka sokoni bila ya kuwa na sifa stahiki kitaaluma.
Uchunguzi wa Mwananchi umebaini baadhi ya vitabu vinavyotumiwa na wanafunzi wa shule za msingi vina kasoro za ukweli wa maarifa katika matini zake, makosa ya uchapaji na uhariri.
Cha kushangaza baadhi ya vitabu hivi ni vya kiada huku vikiwa na baraka zote kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kupitia Kamati ya Kuthibitisha Vifaa vya Elimu (Emac).
Vipo vitabu hata majibu ya maswali ya mazoezi kwa wanafunzi yamekosewa jambo linaloshadadia ukweli kuwa waandishi wanalipua kazi. Wachapishaji waliotarajiwa kubaini makosa ya kiufundi nao wamekosa umakini.
Uchunguzi ulipitia vitabu vitatu tofauti vya shule za msingi ambavyo licha ya waandishi kuzungumzia mada zinazofanana katika somo la Historia, kuna mkanganyiko mkubwa wa ukweli wa baadhi ya maarifa katika mada hizo. Vitabu vyote ni vya kiada vilivyoidhinishwa na Kamati ya Kuthibitisha Vifaa vya Elimu Tanzania (Emac) kutumika kwa wanafunzi wa darasa la nne. Vitabu hivi ni pamoja na Tujifunze Historia Darasa la Nne kilichopewa ithibati na Emac Desemba 17 mwaka 2007.
Vingine ni Historia Shule za Msingi (4) kilichoidhinishwa Desemba 21 mwaka 2007 na Historia: Kitabu cha Mwanafunzi 4, kilichopitishwa Desemba 24 mwaka 2007.
Mkanganyiko umejitokeza katika mada ya ‘Binadamu na mabadiliko ya kimaumbile’ huku kila kitabu kikiwa na idadi tofauti ya hatua za mabadiliko hayo na hata majina ya hatua hizo.
Kwa mfano, ukurasa wa tano na sita wa kitabu Historia Kitabu cha Mwanafunzi, kupitia kichwa cha maneno ‘Mabadiliko ya umbile la binadamu katika nyakati mbalimbali’ kinataja hatua tano kwa mfululizo ufuatao: (1) Chimpanzee (2)Australopithecus (3)Zinjantropasi (4)Homo habilisi (5) Homo sapiens.
Historia Shule za Msingi (4) katika kurasa za saba na nane kinasema mwanadamu alipitia hatua sita huku hatua za mabadiliko hayo zikitofautiana kiorodha na kitabu cha awali.
Chenyewe kinaanza na hatua ya Australopithecus kisha Homo habilis, Zinjanthrophus, Homo erectus, Homo sapiens na Homo Sapiens Sapiens!
Kwa upande wake, Tujifunze Historia darasa la nne kinataja hatua saba huku baadhi ya majina ya hatua zikiwa tofauti na majina ya vitabu vingine.
Orodha ya hatua hizo inayopatikana ukurasa wa tisa na 10, inaonyesha hatua ya kwanza kupitia mwanadamu ilikuwa Pliopithecus kisha Ramapithecus, Zinjanthropus, Australopithecus robust, Homo habilis, Homo erectus na Homo sapiens.
Tofauti ya kimaarifa pia imejitokeza katika mada ya ‘Mifumo ya Kiuchumi na Kiutawala katika jamii za Watanzania’. Wakati Historia kitabu cha mwanafunzi kikisema mfumo wa Ubugabire ulikuwa maarufu katika maeneo ya magharibi mwa Tanzania hasa Mkoa Kigoma, kitabu cha Historia shule za msingi kinaeleza kuwa mfumo huo wa kikabaila ulishamiri zaidi kaskazini magharibi hasa katika jamii za Wahaya ambazo vitabu vingine vinasema vilikuwa vikifuata mfumo wa Unyarubanja.
Pamoja na tofauti ya maarifa hususan nadharia za wasomi katika taaluma mbalimbali kuwa jambo la kawaida na linalokubalika kisomi, kwa mtazamo wa haraka, waandishi wa vitabu hivi wanawakoroga wasomaji wao ambao kimsingi hawajapevuka kiuoni.
Aidha, japo mada ya mabadiliko ya umbile la mwanadamu inapingwa vikali na waumini wa dini walio na mtazamo tofauti kuhusu asili ya mwanadamu, hivi ndivyo mtalaa unaofuata mtazamo wa kisayansi unavyotaka wanafunzi wafundishwe na hatimaye kuja kuulizwa katika mitihani.
Hata hivyo, ni vigumu kwa mwanafunzi wa darasa la nne kung’amua ukweli wa idadi halisi ya hatua za mabadiliko ya mwandamu na majina ya hatua hizo. Ajibu nini endapo ataulizwa kuhusu idadi na majina ya hatua za mabadiliko ya umbile la mwanadamu? Nani katika waandishi hawa yupo sahihi, Haya ndiyo maswali yanayowachanganya baadhi ya watu.
Aidha, ni kwa kiwango gani watunzi wa maswali ya mitihani ya kitaifa wanatambua kuwepo kwa tofauti hizi za kimaarifa? Je, miongozo ya usahihishaji imetengenezwa kukidhi mahitaji ya majibu tofauti?
Vipi walimu darasani ambao kimsingi wanabanwa kufuata mihutasari na maelezo ya vitabu vya kiada kama hivi vinavyokanganya? Wako wapi wataalamu wa Emac waliopewa dhamana ya kuhakiki na kupasisha maarifa vitabuni kama yanarandana na maelezo ya mitalaa.
Mwaka 2009, mzazi aliyejitambulisha kwa jina la Lola Opanga alitoa taarifa kupitia magazeti tando (blogs) kuhusu kuwepo sokoni kwa kitabu hicho ambacho majibu ya maswali mengi yamekosewa. Kitabu hiki kinaitwa Primary Science Workbook: Fountain of Tests and Examination.
Taarifa hiyo ambayo Mwananchi inayo, imeorodhesha jumla ya maswali 16 kati ya 50 ambayo majibu yake yamevurundwa jambo ambalo kwa kiasi kikubwa limewapotosha watumiaji wa kitabu hicho.
Katika moja ya maswali ambayo mwandishi amepotosha ni lile lililouliza ‘Which of these diseases is caused by the mosquito? (Maradhi gani kati ya haya yanasababishwa na mbu?) Mwandishi alitoa chaguzi nne kama majibu ambayo ni (a) Tuberculosis (b) Influenza (c) Cholera na (d) Malaria. Akachagua Cholera (kipindupindu) kama jibu sahihi!
Swali jingine linauliza: A child took a meal of ugali, biscuits and soda. This meal has far too much. (Mtoto alikula ugali, biskuti na soda. Chakula hiki kina wingi wa) Chaguzi za swali zikawa (a) Carbohydrates, (b) Proteins, (c) Vitamins, (d) Fats. Jibu la mwandishi likawa Proteins!
Muda mfupi baada ya taarifa kutoka mtandaoni, juhudi za Mwananchi kukipata kitabu hicho katika maduka yaliyotajwa kukiuza ziligonga mwamba baada ya nakala za kitabu hicho kuyeyuka katika maduka husika yaliyopo Upanga jijini Dar es Salaam.

Wajibu wa Emac
Kwa mujibu wa Waraka wa Elimu Namba saba wa mwaka 2005, uliofuta Waraka Namba mbili wa mwaka 1998, machapisho ya kielimu yanayotumika kwa kufundishia ama kujifunzia katika shule za msingi, sekondari na vyuo vya ualimu, hayana budi kupata ithibati ya Emac.
Aidha, waraka namba saba wa 2005 umetoa miongozo na vigezo ya jinsi ya kuhakiki na kutathmini machapisho haya. Wadau wa elimu wanauliza kulikoni vitabu kuwa na makosa hata yale ya uchapaji?
Ni dhahiri kuna uzembe wa makusudi unaofanywa na kamati kwa kuwa kile kinachopaswa kufanywa kwa mujibu wa miongozo ya kimaandishi sicho kinachotekelezwa kivitendo na wajumbe ambao kimsingi wanatakiwa kuwa wataalamu mahiri katika somo husika.
Kwa mfano, chapisho liitwalo Emac Manual of Procedures la Agosti, 1999 linataja sifa za watathmini zikiwemo ujuzi wa somo, uzoefu wa kufundisha somo husika. Linaongeza kusema:
‘’Zaidi ya yote, watathmini lazima waonyeshe kiwango cha juu cha taaluma na uadilifu… Watapokea mafunzo fulani kabla hawajaanza kazi yao.’’
Kwa upande mwingine, hiki kinachojiri Emac kinaweza kutumika kama mojawapo ya misingi ya hoja wanazotoa baadhi ya watu kuwa mchakato wa kutoa ithibati kwa vitabu una harufu ya rushwa.
Wizara nayo?
Aprili 14 mwaka huu, wakati wa kikao cha 19 cha Bunge, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mwantumu Mahiza alisema wizara imeshang’amua kuwa baadhi ya vitabu vina kasoro kitaaluma hasa vile vilivyokuwa vikitumika wakati wa sera ya vitabu vingi vya kiada ambayo iligubikwa na changamoto kadhaa.
“Kutokana na changamoto hizo, serikali imeamua kubadili utaratibu huo na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imeunda tume ya wataalamu ambayo miongoni mwa majukumu yake ni kupendekeza utaratibu wa kupata Standard Texbook(s). (vitabu vyenye kiwango bora).’’ alisema.
Hii ndiyo hali halisi ya vitabu nchini. Serikali imeshatamka bayana kuwa utaratibu wa kutumia kitabu kimoja kwa shule zote utandelea kutumika katika shule za msingi.
Baadhi ya watu wanahoji mwelekeo wa elimu wa taifa hili ikiwa vitabu vinavyoweza kuchaguliwa kutumika baada ya kuidhinishwa na serikali vina sifa hii ya maarifa yake kuchakachuliwa!
mwisho
 
UCHAMBUZI YAKINIFU INGAWA NI NDEFU INAHITAJI UMAKINI


The Following User Says Thank You to AHAKU For This Useful Post:

Masika (Today)​
 
Aaah ndugu yangu wao watajali nini wakati watoto wao wanasomeshwa nje, kazi kwa watoto wa akina kajamba nani!
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom