Hivi huu ni mfano bora wa mbunge bora?

AMARIDONG

JF-Expert Member
Jun 24, 2010
2,502
180
JANA katika gazeti hili kulikuwa na habari zinazowaelezea wabunge wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuanza kutekeleza mikakati yao.
Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika, yeye ameanza kutekeleza ahadi zake kwa kutenga asilimia 20 ya mshahara wake kwa ajili ya kuchangia mfuko wa elimu wa jimbo hilo.
Wakati Mbunge wa Musoma Mjini, Vincent Nyerere, ameleta kontena moja la vitabu vya masomo ya kuanzia shule ya awali hadi chuo kikuu.
Vitabu hivyo ambavyo vitasambazwa kwa shule zote za sekondari za kata jimboni humo ni vya msaada uliotolewa na wahisani kutoka Marekani ambao pia ni marafiki wa Vincent.
Tunawapongeza wabunge hawa, kwa kuanza kutekeleza ahadi zao mapema, badala ya kusubiri wakati wa uchaguzi.
Tunasema hivi, kwa sababu ipo tabia ya baadhi ya wabunge wa vyama vyote vya siasa ambao wamekuwa wakisubiri wakati wa chaguzi ndipo waanze kutekeleza ahadi zao.
Hatua hiyo tumekuwa tukiitafsiri kama ni moja kati ya njia za kutoa rushwa kwa wananchi ambao nao wamekuwa wakipumbazwa na misaada hiyo.
Tunaamini kwamba suala la kuondoa kero, iwe ya maji, huduma za afya, barabara na nyingine kadha wa kadha si jukumu la mbunge bali ni la serikali.
Lakini inapotokea mbunge akaamua kutoa pesa zake mfukoni kwa ajili ya kulisaidia jimbo lake ni suala la faraja hata kwa wananchi anaowaongoza.
Ukweli ni kwamba mbunge ni mwakilishi wa watu na wa jimbo lake katika kutetea maslahi kwa mtizamo wa wananchi wake pamoja na kusimamia masuala yanayowagusa.
Sote tumeshuhudia wabunge wengi walioangushwa sababu kubwa inayotajwa ni kushindwa kwao kuwatumikia wananchi wao ipasavyo.
Tunawapongeza wabunge Mnyika na Nyerere kwa kuona kero zinazowakabili wananchi wao ni zao na hivyo kuamua kutumia nafasi walizopewa kuhakikisha wanawapunguzia makali.
Jambo hili linatia faraja, si tu kwa misaada bali wananchi nao wanaona wako karibu na watu waliowatuma kuwawakilisha.
Sisi Tanzania Daima tunasema kuwa kitendo cha wabunge hawa wawili walichoanza kukionyesha ni cha kuingwa na wabunge wengine.
Tunaamini kuwa Tanzania itajengwa na Watanzania wenyewe kwa kila mmoja kutumia nafasi yake vizuri kuhakikisha maendeleo ya nchi hii yanapatikana.
Kwani kwa hakika kabisa katika baadhi ya majimbo, wananchi hawajawahi kuwaona wabunge wao tangu walipowachagua na badala yake kuonana nao kunakuwa wakati wa uchaguzi.
Wabunge wa aina hii hawatufai, kwani wapo kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao binafsi na si ya wananchi ambao wamewatuma.
 
Back
Top Bottom