Heri kaburi chakavu la shujaa kuliko nyumba angavu ya muongo na mnafiki

Vox Populi

Member
Oct 23, 2010
23
0
Mwanazuoni mmoja liwahi kusema kwamba ukitaka kukmbukwa siku zote baada a kufa ama ufanye mambo ambayo wengine wanweza kuyaandika au uandike mada ambazo wengine wanaweza kuzisoma.

Mtu awaye yote aweza kutengeneza historia ya maisha yake kwa namna yoyote apendavyo. Lakini historia njema ni tunu na lulu kwa vizazi vyote. Lakini kuna wengine ambao huacha fahari ya majuto na mateso kwa wale ama aliowaongoza au waliomzunguka.

Kuna watu ambao kwao faraja yao ni kuona wengine wanaishi katika mateso na kunyanysika kusiko na kikomo. Hutawala fikra za watu, na kutawala utashi wao kwa manufaa yao binafsi. Kwao matunda ya mafanikio ni kunufaika huku wakiwa wamekaa na kunyonya hata kile kidogo ambacho mwingine angepata.

Wengine ushujaa wao unatokana na urafi na unafiki wao. Hili ni daraja la wale ndumila kuwili, wamejaa uongo na unafiki nao hula na kufanikiwa sana kutokana na hayo. Hupata madaraka kutokana na uongo na unafiki naam hao hujiimarisha kutokana na ujinga wao waliopumbazwa na kupumbazika kwa vitu vipitavyo kama upepo na au viyeyukavyo ka mshumaa au barafu katika joto kali.

Kuna wale waamuao kuipiga ncha ya mkuki kwenzi, naam hao ni wachache sana, ambao hufa na kupotelea katika vumbi la uharibifu, historia yao huishia hapo, lakini hukumbukwa na wale tu waliotegemea wokovu na ama nafuu toka kwake. Hili ni kundi la wachache ambao historia ya maisha yao huanzia saa ile tu anapothubutu kupiga kwenzi ncha ya mkuki, na huishia pale ncha ya mkuki inapomrudi na kummaliza.

Mwandishi Walter Rodney katika kitabu chake “How Europe Underdeveloped Africa” aliwahi kuandika kwamba kama tunataka kujua juu ya mambo yaliyopita, tunapaswa kuangalia mambo ya sasa, na kama tunataka kujua juu ya mambo yajayo tunapaswa kuangalia juu ya mambo ya kale na mambo ya sasa.

Historia ni mwalimu mzuri naye aweza kutuongoza katika kweli. Tatizo lililo kubwa ni usahaulifu, na kuendelea kutawaliwa na fikra za ukale, “fikra za mwenzetu huyu”. Mwenzetu huyu kaja leo aondoka kesho, na kesho yake ndio leo yangu, ni fikra ambazo zinaweza kufanya yale mambo yanayopaswa kufanywa yasifanyike au kufanywa kiduchu tu.

Kuna kundi la watu ambao wao ni watu wasio tafakari hata kidogo, hawa ni watumwa wa kutafakari, na mara nyingi hili ni kundi la watu ambao huleweshwa kwa tamaa ya makombo yanayobakia mezani pa hao wakubwa. Ni heri mkate mkavu katika amani kuliko karamu nono katika fedheha, aibu na manyanyaso.

Kwa mwenye njaa, akipewa hata uvundo hufurahia, ndivyo ilivyo kwa wananchi wengi ambao kwao suala la nitakula nini leo ndio dua ya asubuhi. Inashangaza sana, ni nini kilichotufikisha hapa, mahali ambapo tunategemea misaada isiyo na tija toka kwa wahisani? Tumekuwa ombaomba hata kwa mambo ambayo nchi hii imebarikiwa lukuki!

Inashangaza sana, ombamba hubaki mtumwa dhaifu umaini wa ampatie ridhiki na kamwe akinyanyaswa hukosa sauti ya kujitetea. U wapi uzalendo, u wapi uhuru tunaoweza kujivunia, u wapi utaifa ambao tunaweza kusimama mbele ya watu wa mataifa mengine na kupaza sauti zetu kwa kishindo huku tukijivunia? Yote hayo yalikwisha zama na hakuna tumaini tena.

Ni hatari sana kuzoea taabu, watu wametabuishwa na kuridhika, heri maskini jeuri kuliko tajiri mpole anyonyaye jasho la watesekao, naam hiyo ni sawa na kumnyonya maiti damu. Ole wao viongozi wajionao kuwa wao ndio wao katika ulimwengu wa kutawala. Wamejilimbikizia mamlaka na kujihakikishia kutawala milele kwa sababu wamewapumbaisha wanaowatawala, saa inakuja ya kizazi kitauinuka juu ya kizazi kingine, tabaka moja juu ya tabaka jingine, naam ndipo watu wengi watakapotamani wangeyashuhudia hayo mapemazi zaidi lakini kesho yao itakuwa imepita kama mwanga wa radi.

Natamani Wasukuma wote pamoja na Wanyamwezi kwa ujumla wao ndio wangekuwa Wakurya wa Tarime na zaidi ninatamani sana kama Tarime ingekuwa ndio jumuisho la mikoa ya Pwani,Morogoro, Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga na Mwanza. Naimani nchi hii isingeongozwa kwa mbwembwe kama ilivyo sasa.

Ninatamani siku moja nione simba na chui kwa aina zao wanamrarua mmoja wa wale waliofikisha nchi hii katika dimbwi hili la umasikini tena umasikini wa kujitakia kabisaa ili iwe ndio mwanzo wa safari ya ukombozi halisi wa kiuchumi na kimaendeleo.

Ninatamani kipimo cha ukweli kuhusu mafisadi na ufisadi ingekuwa ni kudumbukizwa katika kreta ya Ngorongoro ili atakayetoka salama basi afananishwe na nabii Daniel aliyetupwa katika shimo la simba lakini kwasababu hakuwa na kosa akatoka mzima kati ya simba wenye njaa kali.

Ninatamani sana kama siku moja mahakama zetu zingetoa adhabu ya viboko hadharani kwa viongozi wasio waadilifu. Labda viongozi wangekuwa na nidhamu.

Kuna shida kubwa ambayo kwa nchi kama Tanzania ikawa inachangia nchi kuendelea kupiga hatua kuelekea kwenye uchumi tegemezi. Pamoja na mambo mengine ni kutokuwepo na nidhamu ya madaraka. Viongozi wengi wameendelea kuwepo madarakani toka kupatikana kwa uhuru na wamejihakikishia kuwepo madarakani mpaka wanapoamua wao wenyewe kung’atuka au kufa. Wengi wao wametumia ufukara wa wanaowatawala au kuwaongoza. Naam ukitaka kumtawala mtu vizuri na abaki mtumwa wako siku zote mnyime mafanikio na umuhakikishie njaa.

Kwasababu hiyo viongozi wengi wanauhakika wa kuendelea kutawala hata kama ni wafujaji na wababaishaji. Laiti kama wananchi wangekuwa wepesi wa kutathmini mambo sidhani kama uchaguzi ungefanywa kuwa ni chombo kinachowahakikishia watawala wabovu kurudi madarakani.

Fikra mgando za viongozi wengi ndizo ambazo zimeshindwa kuzaa matunda ya ukombozi wa kiuchumi wa taifa. Kila mmoja anaangalia kwanza maslahi yake na familia yake badala ya kuangalia maslahi ya taifa.

Viongozi wengi wamekuwa warafi na wanafiki, hakika heri kaburi chakavu la shujaa kuliko nyumba angavu ya mwongo na mnafiki.Tazama unafiki huu ambao hufanywa na viongozi wengi, kwamba ni katika kipindi hiki aifa linapoelekea kwenye uchaguzi mkuu ndipo wanakuja na hadaa zilezile za kuanzisha miradi ya hapa na pale.

Tuwaulize walikuwa wapi hawa hata wanakuja leo na hadaa zao za kupulizia watu vumbi machoni ili waingiwe upofu ili wawachague tena. Ni wakati mzuri wa kuuliza wakati wote huo tulikuwa na njaa kwanini hamkuleta chakula? Wakati wote huo wa miaka mitano tulikuwa tunaumwa walikuwa wapi kutupatia tiba wanakuja leo na aspirini ya kutuliza maumivu?

Ifike wakati tuseme tumechoka kudanganywa, na sasa tuamue kubadilisha mfumo wa kuwapatia madaraka viongozi waongo na wanafiki ambao ufikapo wakati wa uchaguzi huja kwa mgongo wa nyuma wakiomba fadhira. TUAMUE, TUNAWEZA, HATUNA SABABU YA KUOGOPA ILA KUOGOPA KWENYEWE.
 
Well said,

Mahojiano ya jana yamewafungua wengi. Tueneze neno, bado siku saba tu.
 
Tuwaulize walikuwa wapi hawa hata wanakuja leo na hadaa zao za kupulizia watu vumbi machoni ili waingiwe upofu ili wawachague tena. Ni wakati mzuri wa kuuliza wakati wote huo tulikuwa na njaa kwanini hamkuleta chakula? Wakati wote huo wa miaka mitano tulikuwa tunaumwa walikuwa wapi kutupatia tiba wanakuja leo na aspirini ya kutuliza maumivu?

Hapo ndipo umeufunga mjadala huu kiutu uzima na asiyesikia la mkuu huvunjika guu
 
Back
Top Bottom