Haya ndiyo makosa ya Masha kisheria

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,991
Na. Lula wa Ndali Mwananzela (Raia Mwema)

Sipendi kuonwa mjinga. Sipendi kudhaniwa kuwa sina akili. Na kwa hakika sipendi binadamu mwingine mwenye kufa na kuoza kama mimi kunichukulia kuwa mimi ni punguani. Lakini zaidi sipendi mtawala anayefikiria taifa zima ni mazumbukuku na watu waliopigwa zindiko la bumbuwazi. Sitaki, tena sipendi kwa Watanzania kuonekana hamnazo! Na ninakataa kabisa, mara moja daima na milele kwa Waziri Lau Masha kuwachukulia Watanzania kuwa ni watu wepesi wa kufikiri na wasiona uwezo wa kuchambua mambo!

Jambo hili lingekuwa katika uwezo wangu Bw. Masha ambaye ni Waziri wa Mambo ya ndani leo hii angekuwa anasota Keko na kule Nyamagana wangekuwa wanajiandaa kwa uchaguzi mdogo wa Ubunge. Ningehakikisha siyo yeye tu bali wale wote ambao wamesimamia mradi huu wa vitambulisho hadi hivi sasa wanasimama kizimbani na makampuni yote ambayo "yamepitishwa" kuondolewa na mchakato mzima huu kusitishwa hadi upite uchaguzi Mkuu mwakani! Hata hivyo hilo ni somo la siku nyingine.

Leo hata hivyo nataka nioneshe pasipo shaka yoyote kuwa kwa Waziri Masha kuandika barua kwa Waziri Mkuu kulalamikia mchakato wa utoaji tenda ya uchapishaji wa vitambulisho amekiuka maadili ya kazi na kwa hakika amevunja sheria ya manunuzi ya serikali na kwa sababu hiyo amevunja kiapo chake cha Uwaziri na kile cha Ubunge na hivyo kupoteza sifa zote zakuendelea na nyadhifa zote mbili. Fuatana nami.

Bila ya shaka umeshasikia kuhusu hii barua ambayo tumeambiwa kuwa imeandikwa na Bw. Masha na yeye mwenye kukiri kuwa ndiyo ni ya kweli. Hakuna ushahidi mzuri na mkukbwa wa uvunjaji wa sheria wa Bw. Masha kama maneno yake mwenyewe yaliyomo kwenye barua hii (kama tutakavyoona hivi punde).

Lengo la sheria ya Manunuzi
Kwa muda mrefu manunuzi ya serikali yalikuwa yanafanywa kiholela mno, huku kila taasisi ikiwa ina taratibu zake na mtindo wake wa manunuzi. Kulikuwa hakuna usimamizi mzuri wa kisheria wa manunuzi ya vitu mbalimbali. Jambo hili kwa kiasi kikubwa lilikuwa linapoteza sana fedha za serikali kwa fedha hizo kuishia mikononi mwa wajanja huku bidhaa na huduma mbalimbali zinazodaiwa "kununuliwa" kutoonekana.

Hata baada ya sheria hii kuandikwa bado kumekuwa na matatizo katika manunuzi ya serikali (angalia ripoti ya Mkaguzi wa Serikali) na utaona bado kuna ugumu mkubwa sana wa kuifuata sheria hii. Licha ya mapungufu yake mengi sheria hii ilipoandikwa ilikuwa na lengo la kuunganisha taratibu mbalimbali za manunuzi, kuweka usimamizi wa mchakato wa ununuzi na zaidi ya yote kuhakikisha kuwa kuna haki, uwazi na uwajibikaji katika manunuzi ya serikali.

Hivyo, kwa kiasi kikubwa tumetarajia kuwa watumishi na watendaji wa serikali walioapa kulinda Katiba na sheria zake wanatakiwa kuwa wa kwanza kuhakikisha kuwa hadi nukta ya mwisho ya sheria hiyo inatakiwa kulindwa na kuheshimiwa.

Bw. Masha inaonekana alifikiri au alijiambia na kuamini kuwa kuitii sheria hiyo ni suala la uchaguzi tu (optional).

Barua ya Masha kwa Waziri Mkuu
Nitajaribu kuichambua barua hii na vielelezo vilivyomo ndani yake kuonesha ni kwanini ninaamini kwa asilimia 100 kuwa Bw. Masha ameivunja sheria ya manunuzi na kama kuna mtu yeyote yuko timamu, huyu ndugu yetu leo hii angekuwa amerudia kazi yake aliyosomea kwani hili la uongozi kwa uhakika limemshinda. Angalia sana matumizi ya maneno yangu kwani nimeyachagua vizuri kumaanisha ninachotaka kusema.

TATIZO LA 1. – Masha siye mtu sahihi kulalamika.

Katika ufunguzi wa barua yake hii Bw. Masha anasema hivi katika kifungu cha kwanza cha barua yake hiyo "Mheshimiwa Waziri Mkuu, ninakuandikia barua hii kuelezea kutoridhishwa kwangu na hali halisi ya mchakato wa kupata mzabuni wa kutekeleza mradi wa Vitambulisho vya Taifa".

Sheria ya manunuzi ya fedha kifungu cha sita kuanzia ibara ya 77 inaelezea kwa kirefu ni taratibu gani na wapi malalamiko ya kuhusu mchakato wa tenda yatolewe. Ibara hiyo inatangaza uwepo wa Mamlaka ya Rufaa ya Manunuzi ya Serikali ambapo mtu, mgavi, mshauri n.k ambaye kwa namna yeyote ile anaona kuwa hakutendewa haki au kwamba katika mchakato au utoaji wa tenda kuna kutokubaliana kwa aina fulani.

Msomi wetu wa sheria Bw. Masha anatambua kabisa kuwa yeye si mmoja wa watu wanaoweza kulalamikia mchakato huo lakini la pili ni kuwa katika sheria hiyo Waziri Mkuu siyo chombo au mtu wa kupokea rufaa ya mambo haya ya tenda kwa mujibu wa sheria ya Manunuzi. Tunajiuliza (na kwa kweli tunamuuliza Masha) ni kwanini Masha "hakuridhishwa" na mchakato ambao yeye siyo sehemu yake na iweje alalamike kwa mtu ambaye hana uwezo wa kisheria kuingilia mchakato huo?

Yawezekana alikuwa na sababu ya kulalamika (kama watu wengine) lakini hakuwa katika nafasi ya kutoa malalamiko hayo.

TATIZO LA 2. - Kwa maneno yake amejishtaki
Kwa mtu ambaye ni mwanasheria kauli inayofuatia katika barua yake ile inashangaza na kwa hakika ni kama mtu kujichongea yeye mwenyewe. Ni sawa na mtoto anapomkimbilia baba yake (au mama) akitoka kazini na kujitetea kwa kusema "baba mimi sijalamba sukari!". Anasema hivyo huku chembe chembe za sukari zimezunguka kingo za mdomo! Mara mbili anajichongea yeye mwenyewe.

Masha anasema hivi, "jambo hili linatokana na ukweli kwamba, sina mamlaka wala madaraka kisheria kuingilia mchakato huu.." Ninajiuliza kama Masha alijua kwamba hana mamlaka wala madaraka kisheria kufanya alichokuwa anafanya ni kitu gani kilimpa kiburi cha kufanya hivyo? Masha anafahamu tatizo lililoko kwenye (1) kwamba hakuwa katika nafasi ya kulalamika kuhusu suala lakini pamoja na ujuzi huo anaendelea kulalamika vile vile. Kwa maneno mengine Waziri Masha alijua sheria inasema nini lakini ujuzi wake huo haukumzuia kuivunja.

Jambo la pili ambalo anajichongea nalo ni pale anaposema kuwa "Lakini, kama Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye ninabeba ‘political responsibility' ninalo jukumu la kulinda maslahi ya serikali na Taifa hasa pale ambapo ninaona uamuzi ndani ya Wizara ninayoiongoza unaweza kuathiri mtizamo wa wananchi dhidi ya wizara yangu na serikali kwa ujumla".

Ukiangalia kwa haraka unaweza kufikiria kuwa Bw. Masha anasema kuwa anaamua kuandika kwa sababu anataka kulinda maslahi ya taifa kutokana matumizi mabaya ya fedha, kukwepesha vitendo vya ubadhirifu au kuliokolea mabilioni ya shilingi. Unaweza kufikiri kwamba amesema kuwa lengo lake ni kuhakikisha kuwa mradi huu unafanyiwa mabadiliko makubwa ili ulingane kweli na mahitaji ya Watanzania.

Hapana! Kitu kilichomsukuma kuandika barua hiyo ndefu ni kuwa anaingilia kati kwa sababu ameona kuwa uamuzi ndani ya wizara yake "unaweza kuathiri mtizamo wa wananchi dhidi ya wizara yanggu na serikali kwa ujumla!". Kwamba kwake kilichomfanya aamue kuandika barua hiyo ni kuwa wananchi wanaweza kuiangalia wizara yake vibaya na hata serikali!

Mimi najiuliza kati ya mauaji ya Albino na suala la vitambulisho vya utaifa ni kitu gani kinafanya wizara ya Bw. Masha ionekane vibaya na hata serikali kwa ujumla? Hivi kweli Bw. Masha anaamini kuwa watanzania wanaweza kushangazwa na mchakato mbovu au wenye matatizo kwenye suala la vitambulisho wakati wananchi hao hao wameshuhudia IPTL, Buzwagi, Richmond, Rada, Ndege n.k? Serikali imechafuka mbele ya wananchi si kwa sababu ya suala la vitambulisho, bali suala hili ni uthibitisho wa jinsi gani serikali imechafuka!

TATIZO LA 3: Kuambatanisha barua ya mambo ya tenda kwenda kwa Waziri Mkuu

Katika barua yake hiyo Bw. Masha anafanya kitu kingine ambacho kinahitaji kutolewa maelezo. Yeye akiwa ni Waziri anapata nakala za barua toka kwa Katibu wake Mkuu, Naibu wake na maafisa kadhaa wa ngazi za juu. Hilo siyo jambo geni. Linapokuja suala la tenda hata hivyo kuna sheria tofauti kidogo, sheria ambayo Bw. Masha hakuijali hasa pale alipoamua kuambatanisha barua ya mambo ya tenda kwenda kwa Waziri Mkuu.

Bw. Masha ameambatanisha barua hiyo yenye kumbukumbu CAB 214/364//01iliyotoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara wakati huo Bw. Mohammed Muya kwenda kwa mwenyekiti wa bodi ya zabuni Bw. Malisa. Masha anaweza na anapaswa kuwa na nakala ya barua hiyo, tatizo ni kwa yeye kuipeleka barua hii kwa Waziri Mkuu.

Sheria ya manunuzi ya serikali Ibara 42:2 inasema wazi kuwa ni kosa kwa mtu yeyote mwenye nakala ya nyaraka yeyote ile inayohusiana na masuala ya tenda kupitisha au kujaribu kupitisha nyaraka kwa mtu mwingine yeyote isipokuwa wale wanaotajwa kwenye kifungu hicho. Waziri Mkuu si mmoja wapo!

Kitendo cha Bw. Masha kupitisha barua hii kati ya Katibu Mkuu wa Wizara kwenda kwa Mwenyekiti wa Bodi kupeleka kwa Waziri Mkuu ni ukiukwaji mkubwa wa sheria. Bw. Masha haruhusiwi hata kupeleka nyaraka hiyo kwenye kikao cha Bunge au kamati ya Bunge isipokuwa kama sheria imebadilishwa!

Mtu mwingine anaweza kusema "huyo ni Waziri Mkuu bwana anaweza kuona lolote" jibu langu ni kuwa "hapana hawezi". Waziri Mkuu kama vile Masha wameapa kulinda Katiba na kwa hilo kulinda sheria zinazotokana na Katiba hiyo. Haijalishi kama mtu huyo ni Waziri Mkuu au Amiri wa Majeshi ya Mbinguni hata Rais hatakiwi kuona mawasiliano hayo kwani sheria inakataza yote hayo. Mwanyika yuko wapi hapa?

TATIZO LA 4: Kukutana na waombaji na kupokea malalamiko yao
Nimeshaonesha kwenye tatizo la kwanza kwamba Masha hayuko katika nafasi yoyote ya kisheria ya kulalamika kuhusu mchakato wa tenda, lakini pia hayuko katika nafasi ya kulalamikiwa kuhusu mchakato huo. Katika ukurasa wa tatu wa barua yake Bw. Masha anasema kitu kimoja ambacho kungekuwa na mtu mwenye kufanya maamuzi kwenye taifa letu Bw. Masha angetakiwa kujiuzulu wiki kadhaa zilizopita.

Anajishuhudia mwenyewe kwa kusema hivi "Baada ya kupitia taarifa ya Kamati ya tashtmini (evaluation committee) na hasa kutokana na malalamiko niliyopokea toka Kampuni ya SAGEM SECURITE niliona ipo haja ya kupata ufafanuzi". Mistari china yake anarudia hilo na kudokeza kitu ambacho kitakuja mgeuka baadaye kama nitakavyoonesha katika tatizo la tano.

Katika mahojiano yake na vyombo mbalimbali vya habari Bw. Masha amekubali kukutana na watu wa SAGEM ingawa amekana kukutana nao Uswisi au "nje ya nchi". Katika barua hii amekiri kuwa na mawasiliano na kampuni hii wakati mchakato unaendelea na siyo tu kuwa na mawasiliano bali kupokea malalamiko ambayo aliyapa uzito wa kutosha hadi kuwaita Katibu Mkuu na wenzake kuyafikisha kwao. Alifanya hivyo akiamini anatetea maslahi ya taifa.

Tatizo ni kuwa katika sheria ya Manunuzi ya Serikali ya mwaka 2004 ambayo unaweza kuisoma kwenye mtandao wa mwanakijiji.com au jamiiforums.com utaona kuwa sheria iko wazi kabisa kuhusu mikutano ya aina hii. Ibara ya 73:1(b) ya sheria hiyo iko wazi kabisa.

Ibara hiyo inakataza kwa mwombaji yeyote yule au hata asiye mwombaji kujaribu kuwasiliana na mtu yeyote ambaye katika nafasi yake au ofisi yake anaweza kuhusika na mchakato wa masuala ya tenda. Siyo tu kuwasiliana naye kuhusu jambo hilo bali pia kutoa kitu chochote kinachoweza kutafsiriwa kama zawadi, motisha au rushwa au hongo ya aina fulani.

Sheria hiyo inasema taasisi hiyo au kampuni ambayo itafanya jambo hilo inaweza kufungiwa kupata tenda yoyote kutoka serikali ya Tanzania kwa miaka 10!

TATIZO LA 5: makampuni mangapi yalilalamika kwa Masha?
Kama utakuwa umemsikiliza Waziri Masha kwenye mkutano wake na waandishi wa habari au katika mahojiano na Clouds FM utaweza kuamini kuwa makampuni matano yalilalamika kwake. Hili la haya makampuni yote kulalamika kwake tunalirejesha kwenye tatizo la kwanza kwamba kwanini hawa wote walalamike kwake na kwa nini yeye akijua kuwa sheria inakataza kukutana na waombaji hawa wakati mchakato unaendelea alikubali (entertain) kuwasikiliza?

Lakini cha kushtua zaidi ni kuwa sasa hivi Bw. Masha anadai kuwa makampuni manne mengine yalileta malalamiko kwake. Hadi hivi sasa (kwa kadiri ninavyojua) hajayataja makampuni hayo. Hata hivyo kama nilivyodokeza hapo juu tukiingalia kauli yake moja tunaweza kufikia mahitimisho kadhaa.

Bw. Masha kwenye kuelezea malalamiko aliyoyapokea anasema hivi "Baada ya kupitia taarifa ya Kamati ya tashtmini (evaluation committee) na hasa kutokana na malalamiko niliyopokea toka Kampuni ya SAGEM SECURITE niliona ipo haja ya kupata ufafanuzi." Chini yake anarudia wazo hili anaposema kwamba "katika kikao hicho niliwafahamisha kuwa nimepokea malalamiko toka mojawapo ya waombaji." Sasa tuangalia membo fulani kwa haraka tukizingatia kuwa hii barua inaenda kwa Waziri Mkuu.

- Hadi anaandika barua hiyo Masha alikuwa amepokea malalamiko toka kampuni moja na si zaidi.
- Malalamiko mengine yoyote yatakuwa ni baada ya barua hii. Hivyo, tungependa kujua alipokea malalamiko hayo lini na kutoka kwa kampuni gani?
- Kama alipokea malalamiko hayo manne mengine kabla ya kuandika barua hii ni kwanini ameamua kutaja kampuni moja?
- Jibu la swali hilo hapo juu ambalo amelitoa hadi hivi sasa ni kuwa alitumia SAGEM SECURITE kama mfano. Hata hivyo mtu yeyote mwenye akili timamu akisoma barua hiyo ataona kuwa Bw. Masha hakutumia lugha ya mifano. Angeweza kusema "nimepokea malalamiko toka makampuni mbalimbali kama vile SAGEM SECURITY na X,Y".

Lakini kubwa hapa ni kuwa Masha anadaiwa kukutana na SAGEM huko Uswisi (kitu ambacho anakikanusha) lakini wakati huo huo anasema kuwa alienda Uswisi baada ya kutoka Dubai. Swali ambalo halijajibiwa au kuulizwa ni huko Dubai alienda kwa shughuli binafsi au za serikali? Hata kama shughuli hizo zilikuwa ni binafsi je alikutana na kampuni yoyote au mtu yeyote ambaye anahusiana na kampuni ambayo imo kwenye mchakato huu wa tenda ya vitambulisho (tukizingatia kuwa kampuni mojawapo kati ya sita zilizopo inatokea Dubai!)?

Naweza kuendelea zaidi na zaidi lakini nina uhakika mtu mwenye macho hawezi kuambiwa tazama. Ukweli uko mbele yetu na Waziri Masha wakati umefika wa kupima uzito wa tuhuma dhidi yake na ajiwajibishe yeye mwenyewe au chombo kilichomteua kiamua kumuwajibisha au Bunge liamue kumwajibisha.

Hata hivyo hiyo ni ndoto ya mchana na sitarajii kuna kiongozi yeyote mwenye ujasiri wa kuchukua maamuzi hayo mazito kama ilivyokuwa vigumu kwa kuwawajibisha watu wengine wakiwa madarakani. Sitarajii sikio la kufa kusikia na hivyo basi mimi kama Watanzania wengine nimejisalimisha mbele ya nasibu na kukubali watutawale wapendavyo. Mpaka siku hiyo tutakaposema "inatosha"!

lulawanzela-at-yahoo.co.uk
 
Nawakubali wachambuzi wa mada nyingi sana hapa JF kwa kweli lau has to go....go go lau go..hilo moja ni kubwa sana inatosha uwezo wako bado mdogo rudi imma ukasubiri kufungua kampuni za deal ule commisin yako hapo ulipo hupawezi.
 
Mshikaji kanywa mambo/chambuzi kibao kutoka JF........idumu JF!!...udumu Lulawanzela!!
 
Nakubaliana na wewe MMKJJ. Hizi pia bado ni kelele za mlango ambazo hazimkoseshi usingizi Mwenye Nyumba.
Mkulu haoni wa halisikii la muadhini wala la mnadi sala.

Nikija kwa Mh. Masha, namuunga mkono kwa barua aliyoindika kwa PM only if deep down his concious, it was in a good faith na sio maslahi binafsi. Ninaamini hao Sagem wamentip kuhusu mchezo mchafu kenye zabuni hiyo.

Mchezo huo mchafu unachezwa kwa kutumia PPRA procedure za elimination every possible serios contenders. Kwa mtaji huo hata kama walalamikaji wangefuata taratibu za kulalamika, isinge saidia kitu.

Hata hizo kampuni 8 zilizopita, mshindi wanamjua na wengine ni wasindikizaji tuu. Kama kweli Masha alikuwa ana nia njema ya kuokoa jahazi, there ware only two ways. Moja ndiyo hiyo kumjulisha PM wasiwasi wake, lakini naamini pia lazima alikwenda kwa Mkulu for tete-a-tete.

Kisheria ni makosa aliyokuwa akiyafanya, lakini (if in good faith), aliyayafanya kwa makusudi na pia kwa kuelewa, lakini alikuwa na imani barua yake ni siri.

Kwenye barua za siri, hakuna cha sheria, taratibu na kanuni, kila aina ya madudu yanafanyika, leakage is ambarasment ya kuexpose punje moja too ya mchele iliyopenya kimakosa toka ndani ya gunia.

Mimi nimemuona akizungumza na TBC na kumsikiliza Clouds FM. Its pitty kulikuwa hakuna wauliza maswali yanayomata, it was just a PR Stunt!.

Baada ya kumuona Gotham, nimeconect the dots. Hata kelele zipigwe vipi, mradi huu ni lazima upite na utekelezwa mapema sana. Baada ya Masha kupiga kelele hata kama ni kwa nia njema, ameitwa na wahusika wakuu, wakamuhakikishia usalama wa kibarua chake.

Sasa mtaona kila press briefings kuhusu developments za deal hili, zitatangazwa na Masha mwenyewe. 2010, atasimama tena, na kwa mtindo ule ule wa t-shirt, kanga na pilau ya shibe ya sikumoja. Atapita na utapewa wizara nyingine, ili Membe akipokea kijiti 2015, Masha analetwa Foreign kusubiri 2025 by then he will be in his Fifties!.
 
Mshikaji kanywa mambo/chambuzi kibao kutoka JF........idumu JF!!...udumu Lulawanzela!!

unajuaje kama naye si member hapa JF?, na huitumia JF kuweza kuandika hayo kwa kuchochea mijadala ili apate la kuandika.
 
Nakubaliana na wewe MMKJJ. Hizi pia bado ni kelele za mlango ambazo hazimkoseshi usingizi Mwenye Nyumba.
Mkulu haoni wa halisikii la muadhini wala la mnadi sala.

Nikija kwa Mh. Masha, namuunga mkono kwa barua aliyoindika kwa PM only if deep down his concious, it was in a good faith na sio maslahi binafsi. Ninaamini hao Sagem wamentip kuhusu mchezo mchafu kenye zabuni hiyo.

Mchezo huo mchafu unachezwa kwa kutumia PPRA procedure za elimination every possible serios contenders. Kwa mtaji huo hata kama walalamikaji wangefuata taratibu za kulalamika, isinge saidia kitu.

Hata hizo kampuni 8 zilizopita, mshindi wanamjua na wengine ni wasindikizaji tuu. Kama kweli Masha alikuwa ana nia njema ya kuokoa jahazi, there ware only two ways. Moja ndiyo hiyo kumjulisha PM wasiwasi wake, lakini naamini pia lazima alikwenda kwa Mkulu for tete-a-tete.

Kisheria ni makosa aliyokuwa akiyafanya, lakini (if in good faith), aliyayafanya kwa makusudi na pia kwa kuelewa, lakini alikuwa na imani barua yake ni siri.

Kwenye barua za siri, hakuna cha sheria, taratibu na kanuni, kila aina ya madudu yanafanyika, leakage is ambarasment ya kuexpose punje moja too ya mchele iliyopenya kimakosa toka ndani ya gunia.

Mimi nimemuona akizungumza na TBC na kumsikiliza Clouds FM. Its pitty kulikuwa hakuna wauliza maswali yanayomata, it was just a PR Stunt!.

Baada ya kumuona Gotham, nimeconect the dots. Hata kelele zipigwe vipi, mradi huu ni lazima upite na utekelezwa mapema sana. Baada ya Masha kupiga kelele hata kama ni kwa nia njema, ameitwa na wahusika wakuu, wakamuhakikishia usalama wa kibarua chake.

Sasa mtaona kila press briefings kuhusu developments za deal hili, zitatangazwa na Masha mwenyewe. 2010, atasimama tena, na kwa mtindo ule ule wa t-shirt, kanga na pilau ya shibe ya sikumoja. Atapita na utapewa wizara nyingine, ili Membe akipokea kijiti 2015, Masha analetwa Foreign kusubiri 2025 by then he will be in his Fifties!.

Pasco, utetezi wa "nia njema" ni utetezi mgumu sana. Endapo tutaukubali tutajikuta tunatakiwa kuwafutia kesi kina Mramba na Yona, na kuwaomba radhi kina Lowassa, Karamagi na Msabaha, kwani wanaweza kabisa kudai kuwa yote waliyoyafanya katika nyadhifa zao ilikuwa katika nia njema.
 
unajuaje kama naye si member hapa JF?, na huitumia JF kuweza kuandika hayo kwa kuchochea mijadala ili apate la kuandika.

....aise sijui........ila yote yawezekana........member/guest.......good strategy though.....hakatazwi mtu........
 
Well explained Mkjj. But you know wht this guy will remain mum, so will be the govt, the parliament, The tz GOP and the people of the republic. But wait if Lau will be deemed disobidient/threat by the GOP bigwigs that is when these paragraphs of this thread will be of utmost important.

That is how it has been, how it is and how it will usually be.
 
Pasco, utetezi wa "nia njema" ni utetezi mgumu sana. Endapo tutaukubali tutajikuta tunatakiwa kuwafutia kesi kina Mramba na Yona, na kuwaomba radhi kina Lowassa, Karamagi na Msabaha, kwani wanaweza kabisa kudai kuwa yote waliyoyafanya katika nyadhifa zao ilikuwa katika nia njema.

Nia njema ninayo izungumzia hapa ni ile nia njema ya dhati from deep down ones concious mind kwa hapa kuna mchezo mchafu, nalipua bomu na liwalo na liwe.
Hii nia njema ndiyo itakayomuokoa mhusika as a man of integrity beyond any reasonable doubt.

Masha alipata tip ya mchezo mbaya and made an attempt to fight them kwa matumaini yafike kwa wakuu huko juu, akaitwa mahali na watu higher above ambao hakuwategemea kuwa watakuwa part and parcel. Angekuwa ni kweli mpigania haki na maslahi ya taifa, angeshauri "stop this nonsense or I quit".

Masha is not that bold, anapigania tumbo lake, ndipo akaamua kutumia ile formular ya "if you can't beat them, join them". Masha ndio sasa amejiunga nao na ndiye msemaji wao.

Hii mambo ya Gotham kufanya press conference naye anataka kuharibu, naye kesha itwa na kuambiwa funga mdomo. Naamini hata ongea tena mpaka taarifa rasmi za Masha.

Defence ya kwa nia njema, it can only work katika nia njema ya kuzuia ulaji. Ulaji ukishafanyika, nia njema is redundunt,

Ila pia kwa maoni yangu, hizi kesi za PCCB ni weak at the face of it. Hata hii ya Mahalu will be thrown out at appeal level kwa kutumia inadimissible evidence through ICT, where by Tanzania has not enacted any law/legistlation to accomodate such use.
 
Back
Top Bottom