Hatua za kupata udhamini ughaibuni (5) - makulilo, jr.

MAKULILO

Member
May 30, 2010
84
94
NA: ERNEST BONIFACE MAKULILO (MAKULILO, JR.)
CALIFORNIA, USA

Makala nne zilizopita zimekuwa zikichambua hatua za kupata udhamini ughaibuni. Hatua hizi ni nyingi, na makala ya leo inaendelea kufanya uchambuzi wa kina. Mpaka sasa tumeshaona kwa kina hatua zifuatazo: Ada ya Maombi (Application Fee), Barua ya Mapendekezo (Recommendation Letter), Barua ya Motisha (Motivation Letter/Statement of Purpose), Sampuli ya Maandiko (Writing Sample) na Insha ya Udahili (Admission Essay). Leo hii tunaangalia Mitihani/Majaribio ya Udahili (Admissions Tests).

Mitihani/Majaribio ya Udahili ni muhimu sana, na bila vyeti vya kuonesha kuwa umefanya mitihani husika na kufaulu vyema huwezi kudahiliwa na kupata udhamini. Mitihani hii imegawanyika katika makundi mawili makubwa. Na makundi haya yanatokana na hatua ipi ya masomo ambayo unaaomba ili uweze kudahiliwa, yaani mitihani ya udahili kwa upande wa Shahada ya Kwanza na Shahada ya Uzamili au Uzamivu ni tofauti. Pia sehemu unayoomba kwenda kusoma kama ni Ulaya au Amerika itakufanya ufanye mtihani fulani. Hivyo ni vyema kujua kila mtihani na falsafa yake ipoje.

Mtihani wa kupima uwezo wa lugha ya Kiingereza (English Proficiency Test). Katika makala moja niligusia kuhusu mtihani huu. Kwa ufupi ni kwamba, kwa kuwa Tanzania lugha ya Taifa ni Kiswahili (si Kiingereza) japokuwa elimu ya juu hutumia Kiingereza kama lugha ya kufundishia, mwombaji lazima aoneshe vyeti kuwa anajua lugha ya Kiingereza kwa ufasaha na ana uwezo wa kusoma shahada anayoomba. Hakuna mtihani wowote ule au cheti chochote kile kinachotakiwa isipokuwa kimoja kati yah ii mitihani miwili: International English Language Testing System (IELTS) au Test of English as Foreign Language (TOEFL). Huu IELTS ni wa Waingereza na unafanyikia pale British Council, na TOEFL ni wa Wamarekani unafanyikia University Computing Center – UCC tawi la University of Dar es Salaam, Mlimani.

Ni mara chache sana kupewa ruhusa ya kutuma maombi yako bila kuwa na cheti cha mtihani mmoja wa lugha kati ya hiyo. Udhamini wa Norway (Quota Scheme) wao huruhusu waombaji ambao wamesoma masomo ya sekondari na chuo (elimu ya juu) ambapo lugha ya Kiingereza ilitumika kama lugha ya kufundishia, kutowasilisha cheti cha aidha TOEFL au IELTS. Kwa vyuo vingine ni lazima uoneshe cheti cha lugha ya Kiingereza.

Ushauri wangu: Usisibirie mambo ya bahati ya mtende kuota jangwani kwa kutofanya mtihani huo wa lugha ya Kiingereza. Watu wengi hawafanyi mtihani huu, na wakiomba vyuo wakikosa wanaanza kulaumu, mara kuna upendeleo nk. Wanasahau kuwa VIGEZO NA MASHARTI KUZINGATIWA inapokuja suala zima la udahili na udhamini wa elimu ughaibuni. Ni vyema ufanye mtihani huu uwe katika nafasi nzuri ya kuwa mshindani mkubwa kuondokana na kuwa mshiriki au msindikizaji. Japokuwa ni gharama kulipia na kujiandaa kufanya mtihani huo, ni uwekezaji mzuri kwani unalipa, na faida yake ni kupata udhamini na kutimiza ndoto yako ya kielimu ughaibuni.

Mitihani mingine ni American College Testing (ACT), Scholastic Aptitude Test/Scholastic Assessment Test (SAT), Graduate Record Examination (GRE), Graduate Management Admission Test (GMAT) na mingineyo. Mitihani hii yote ni kwa ajili ya kusoma Marekani, kwa upande wa Ulaya na nchi zingine hawana mitihani hii ya udahili. Hivyo kama unawaza kufanya maombi na kutegemea kupata udhamini hakuna njia ya mkato ni lazima ufanye mitihani hii. Si mitihani yote unatakiwa kufanya, nitakueleza inakuaje.

Kwa waombaji wa Shahada ya Kwanza (Bachelor’s Degree) Marekani ni lazima wafanye mtihani mmoja kati ya ACT au SAT. Na kwa wale wanaotaka kusoma Shahada ya Uzamili au Shahada ya Uzamivu nchini Marekani ni lazima wafanye GRE au GMAT. GRE ni kwa wale wanaotaka kusoma kozi ambazo si za biashara na usimamizi (business and management), na kama unataka kusoma biashara au usimamizi (business or management) ni lazima wafanye GMAT. Mitihani hi yote ACT, SAT, GRE na GMAT kwa Tanzania inafanyikia University Computing Center – UCC tawi la Chuo Kikuu Mlimani, UDSM.Ushauri wangu: Huwa ni gharama zaidi kama unataka kupata udhamini wa kusoma Marekani maana ukiachilia kufanya mitihani ya lugha (TOEFL au IELTS) ni lazima ufanye mitihani mingine ya udahili (ACT, SAT, GRE au GMAT) kutegemea na hatua uombayo na masomo uombayo pia. Kitu kingine kwa Marekani na Canada kuna ada ya uombaji udahili (application fee) ambayo ni ghali pia. Hivyo basi huwa ni vyema mtu kuanza na kuwa na wazo la kuomba vyuo vingi na udhamini Ulaya kulikoni Marekani au Canada sababu Ulaya wao ni mtihani huo mmoja wa lugha tu, na nchi kama Norway sio lazima kufanya mtihani wa lugha ya Kiingereza. Pia Ulaya wao hawana hiyo mitihani mingine, na hawana ada ya malipo ya uombaji chuo (application fee).

Ni matumaini yangu kuwa umeweza kuelewa mambo ya msingi katika hatua za uombaji udhamini ughaibuni. Makala zijazo zitajikita zaidi kwenye vitu vingine za msaada na kurahisisha uombaji wa vyuo na udhamini ughaibuni.

Kwa maswali au maoni, niandikie Makulilo@makulilofoundation.org

MAKULILO​
 

Attachments

  • 101_0097.jpg
    101_0097.jpg
    39.8 KB · Views: 81
Thank u alot!!
Let me make use of this advice, i hope one day i will get a chance to study abroad!!!
 
Back
Top Bottom