Hadithi - shujaa wa mashariki

Yona F. Maro

R I P
Nov 2, 2006
4,202
218
Na Michael Mngumi

“Nataka kuwa mpanzi katika nchi ya kigeni. Nataka kuipanda mbegu ya mtende katika shamba la ngano.” Nilikuwa nikiyakumbuka maneno aliyosema marehemu babu yangu asubuhi moja miaka mingi iliyopita, alipokuwa amesimama mbele ya nyumba yake kubwa ya mawe akiliangalia jua lililokuwa likichomoza mashariki mwa dunia.


Nami nikamjibu “amani,” kwa kuwa nilijua, mimi hasa ndiye nitakayekuwa mrithi wa shamba lile, nitakayeyavuna mazao na kuyaweka ghalani.Nami katika siku hizo sikujua maana ya maneno hayo wala tafsiri yake.


Wakati nikiyakumbuka maneno haya nilikuwa nimesimama karibu na mti mdogo uliokuwa katika bustani yangu, nikiwa nimevaa mavazi ya zambarau yenye kunakshiwa kwa mapambo mengi ya thamani. Kichwani nilivaa taji ya dhahabu.


Shingoni ulining’inia mkufu wa dhahabu wenye thamani kubwa. Mkufu ambao mng’aro wake ungeweza kumpa nguvu mtumwa aliyeelemewa na mzigo, na kumtia furahani mjane aliyeelemewa na masaibu ya dunia.


Nilionekana kama mfalme tajiri aliyesimama karibu na jumba lake la fahari, kasri ambalo halijapata kuonekana hapa duniani. Hata hivyo sikuwa mfalme ila nilikuwa mfanyabishara tajiri tu.


Nilisogea karibu zaidi na mti huu mdogo na kuuegemea huku nimetazama kusini. Hapa, mawazo yangu yakafurika kwa mambo yaliyopita, mambo ya zamani. Mambo haya yakaingia sana katika akili yangu hata sikuweza tena kuona wala kusikia mambo mengine yaliyonizunguka; hata nikamsahau binti yangu niliyekuwa naye bustanini, aliyekuwa karibu nami akiliangalia ua ambalo alilipenda sana kama alivyonipenda mimi babaye.


Nilikuwa nikiwakumbuka marafiki wapendwa. Mashujaa tuliosafiri pamoja zamani kwenda katika mwamba wa dhahabu. Safari ambayo sitaisahau.Tukaja kutengana katika pwani isiyojulikana ambayo baadaye niliipa jina la “Pwani ya Huzuni” kwa kuwa iliwatenganisha marafiki wapendwa. Marafiki walioanza urafiki wao tangu wakiwa watoto wadogo.


Wote nilizipata habari zao; mmoja alikuwa kama nyota ya kisiwani. Mwingine alikuwa ndiye mlima mrefu huko kusini ya mbali. Huyu alipenda makuu, alishakuwa mfalme. Hapana shaka pia walizipata habari za ustawi wangu na ukarimu wangu.


Nilitamani sana kufunga safari ndefu kwenda kuwatembelea huko mbali walipokuwa; lakini nilishindwa kufanya safari hiyo kwa kizuizi cha mwanangu mpendwa aliyekuwa angali mdogo, ambaye asingeweza kuandamana na mimi na kufanya safari ndefu.


Safari za nchi kavu na baharini, safari zenye zahama kubwa. Hivyo nilishindwa kwenda peke yangu na kumwacha mwanangu mpekwe, ‘kwani mama yake alifariki kwa kuumwa na nyoka wakati mwanangu angali amdogo. Akanizoea sana, tukawa tukiandamana pamoja kila mahali.


Basi kwa muda mrefu nilibaki na huzuni ya kukosa kuwaona marafiki wapendwa, pamoja na hayo niiluamini ule usemi usemao, “milima haikutani bali binadamu hukutana.” Kwa jambo hilo nikaazimu kusafiri siku za usoni wakati mwanangu atakapokuwa mkubwa.


Hata nilopokuwa nikiyawaza haya, tazama macho yangu yakatiwa kiwi cha macho. Mwanga mkubwa ukayapiga macho yangu. Macho yangu yakapoteza nuru. Mwangaza ule ulitoka katika dhahabu safi iliyokuwa imenakishiwa kwenye kaburi la marehemu babu yangu mpenzi aliyefariki siku nyingi zilizopita.


Nilimpenda sana hata nikaamua kulipamba kaburi lake kwa mapambo ya dhahabu nikijifariji kuwa pengine yangeweza kumkumbusha maisha yake wakati alipokuwa angali hai akiishi na mjukuu wake waliyependana sana, karibu na bonde.


Nikavuta hatua kuelekea kwenye kaburi hilo. Karibu na kaburi kilipita kijito kidogo. Nikakivuka kijito kile na kusimama mbele ya kaburi. Jua liliangaza kwa nguvu, anga lote lilikuwa jeupe.


Hata hivyo mwanga wa jua haukuunguza kutokana na upepo uliokuwa ukivuma kutoka kusini. Mwanga wa jua ulipoipiga kwenye kaburi ulifanya kutokee rangi rangi mithili ya upinde wa mvua. Rangi hizi zilitokea kwenye pande sita za kaburi. Mwanga ule ulipopiga kwenye kijito kidogo, maji yake yakawa ya samawati. Kuzunguka kaburi iliota mihamuni; na kando ya kijito iliota mikilua na minaraha iliyozongwa na milangamia.


Mahali hapa ndipo ilipokuwa pepo ya vigelegele ya ndege aina ya chozi na jamii zake walioiomba nyimbo za shangwe wakati wa kuchomoza na kuchwa kwa jua. Ilionekana mahali hapa ndipo lilipokuwa lango kuu la kuingilia mbinguni.


Napenda ieleweka wazi, sikuwa nikiabudu, kusujudu, kuyapiga magoti wala kuyafumba macho na kufanya fumbato ya mikono na kuomba msaada ama muujiza mahali hapa, bali nilikuwa nikifanya kumbukumbu, kumkumbuka mtu mashuhuri.


Nililitazama sana kaburi hili lililokuwa mbele yangu ambalo ndani yake ilikuwemo mifupa mitupu. Kweli, mwanadamu aaliumbwa kwa udongo na udongoni atarudi! Uzuri wote umekuwa chakula cha mchwa! Hata hivyo maneno yake ya hekima yamedumu hata leo. Kwa ajili hiyo najiandaa kuyasanifu maneno yangu ili nyakati zijazo yazidi kuwaongoa watu, kwani katika maisha, yote hupita, lakini maneno hudumu hata milele.


Siku hizo nilikuwa mtoto mdogo tu, sikuutambua vizuri upendo ule na hekima ile kubwa aliyokuwa nayo mzee yule, sikujua maisha yangu na mafanikio yangu ya baadaye alikuwa ameyabeba katika kichwa chake kilichokuwa kimejaa mvi.


Kamwe sikuyaelewa maneno yake mengi aliyokuwa akiniambia wakati wa jioni turudipo nyumbani baada ya kazi ya uvuvi. Kabisa, kabisa, sikumwelewa pale aliponiambia alitaka mimi nimtukuze hapa duniani kwa kulienzi jina lake (Jina lake likumbukwe mabondeni na milimani, hata ng’ambo ya nchi za mbali na kwenye visiwa vya bahari).


Alitaka kulijenga jina lake katika nchi aliyokuwa akiishi, maadamu hakuwa na ukoo akiwa Ajinabi: akiwa hana ndugu wa damu isipokuwa mtoto wake wa kike.


Alifanana na mbegu ya mtende iliyochukuliwa na maji ya mto hadi konde la ngano. Nakumbuka sana siku ile aliponiambia nilikuwa na sura ya kishujaa. Shujaa wa kuweza kuzitikisa falme kuu na kuijenga himaya itakayodumu karne na karne.


Nikiwa bado nimesimama mbele ya kaburi la babu yangu, niligeuka nyuma na kulitazama kasri kubwa. Jumba ambalo kwa karne nyingi litabaki kuwa mashuhuri. Nimetembea pande nne za dunia.


Nikasafiri katika bahari zenye visiwa vikubwa vilivyojengwa mfano wa paradiso, kote huko haikuonekana fahari ya kuvutia kama kasri na bustani yangu.


Watu mashuhuri toka pande nne za dunia, wakiwemo wafalme waliojijengea enzi kuu, na wafanyabiashara wa lulu, wote hawa huja kuliangalia jumba la fahari na bustani mashuhuri, pamoja na kumwamkia mfanyabiashara wa dhahabu akiwa na binti yake aitwae sheolomelo.


Kwa upande mwingine binti yangu, Sheolomelo, mwana Tausi, aliyekuwa fahari yangu kubwa, alikuwa kivutio kingine.


Awapo ndani ya kasri alikuwa akiuhamisha uzuri wote wa bustani ndani ya jumba kwa ajili ya urembo wake. Hata watumishi wangu walikuwa wakimwita. “Taa ya nyumba.” Uzuri wake ulimfanya ashindane na ndege tausi na kunipa taabu kubwa ya kumchagua kiumbe mrembo katika bustani yangu.


Leo naweza kumfananisha na Cleopatra, mwanamke aliyepata kunitia wazimu zamani. Nayaamini maneno ya wahenga waliposema;” Utajiri wa baba humfanya mwana kung’aa kama nyota.”


Wakati wa jioni tulipenda kutembea bustanini. Binti yangu akawa mashariki mwa bustani akiangalia maua ya manjano. Nami nikawa Magharibi mwa bustani nikiangalia maua ya zambarau. Tukiwa kwenye bustani hii tulikuwa tukijiona kama tuko pepo ya Edeni.


Basi maua katika bustani yangu yakawa mengi hata ndege wakatawanya mbegu zake nje ya bustani. Bonde lote likajaa maua. Siku moja nikamtuma mtumishi wangu kwenda kuupima ukubwa wa bustani hii mpya iliyooteshwa na ndege.


Akatembea mwendo mrefu hata akachoka na kurudi kwangu akisema; “Sikuuona mwisho wa bustani kila niliposonga mbele likatokea bonde kubwa la maua!”


Karibu na himaya yangu walikuwa wakiishi mbwa mwitu waliokuwa wakisubiri kula makombo kutoka katika karamu zangu nilizokuwa nikifanya.


Magharibi mwa jumba hili ulikuwepo mji mkubwa. Mji nilioujenga mimi mwenyewe. Mji uliojaa mahekalu meupe. Mji huu ulichipuka na kuwa mji mkubwa sehemu za mashariki.


Nilipata kuupima ukubwa wa mji huu. Urefu wake ulipata kilometa kumi na saba. Nao ulikuwa mji mraba. Nikaweka taa maelfu elfu kwenye mji huu. Usiku ukafanana na mchana katika himaya yangu.


Katikati ya mji huu ulikuwepo mnara wa dhahabu. Juu ya mnara huu ilikuwepo sanamu kubwa ya dhahabu ya mzee mkongwe aliyeishi zaamani. Chini ya sanamu hii liliandikwa jina lake kwa herufi za dhahabu. Mji huu niliupa jina letu “Umlele.”


Nami niliupenda sana uwindani na uvuvi. Siku nyingine nilitoka nyumbani na mwanangu kwa kazi hizo.


Wakati nilipokuwa nikiitazama himaya hii nilikuwa nikijiona nilikuwa, hasa, ile mbegu ya mtende iliyopandwa kwenye shamba la ngano. Mtende uliokuwa na kuiua ngano yote kondeni.


Tena nilikuwa nikijiona nilikuwa ile nyota ing’aayo iliyochomoza pande za Mashariki. Hata aliyewahi kuwa mpinzani wetu mkubwa siku za nyuma miongoni mwa wazee mashuhuri karibu na saa zake za mwisho aliipaza sauti yake na kusema:


“Tumeshindwa kuling’oa gugu kubwa lililoota katikati ya shamba la ngano. Ngano yote imekufa. Jina letu na ukoo wetu vimetoweka kama mvua jangwani. Imekuwa sawa na kupatwa kwa jua saa za asubuhi. Kupatwa kwa milele!”


Kwa ajili ya wazee leo nami naitwa mwanadamu; kwa ajili ya wazee leo sauti yangu yasikika kama baragumu mlimani; kwa ajili ya wazee leo vishindo vya hatua zangu vyasikika katikati ya habari; kwa ajili ya wazee leo masikio yangu yanasikia sauti za maombolezo ya chungu bondeni; kwa ajili ya wazee leo macho yangu yanatazama na kuona katikati ya giza.


Sauti ya babu yangu aliyoitoa zamani leo yautoa mwangwi kupitia maisha yangu. Maisha yangu yamejaa nakala za maneno yake watu wote wananijua kama mtu muungwana. Nimeamua kuitoa thamani kuu kwa watu wote. Utajiri wangu leo unafanana na chemchemi ya maji inayokata kiu ya mchovu.


Leo naamini uungwana ndiyo kiungo pekee kati ya tajiri na masikini. Nitabaki nikiwaogopa na kuwatukuza wazee, maneno yao yana nguvu kushinda mafuriko ya bahari. Nautia muhuri nikiipasisha hekima ya wazee.


Hekima yao imempa ufalme mtumwa katika nchi ya kigeni. Mbele ya kaburi hili na zito shukrani kubwa kwa marehemu babu yangu ambaye hekima yake leo imeniwezesha kuishi maisha maarufu.


Pamoja na yote niliyokwisha kusimulia kwa ujivuni, na yote nitakayosimulia, na yote yaliyopo kwenye ukuu wangu; si mimi wala babu yangu aliye na nafasi katika mambo hayo. Siku zote nitainyanyua mikono yangu juu, na macho yangu kutazama juu, na kukifunua kinywa changu kulisifu jina la Allah Muumba wa mbingu na nchi na vyote vilivyomo-Rabil alamina.


Pamoja na ukuu wote huu nilijiona sikuwa na bahati siku hizi zilinikuta mpweke zaidi. Baba yangu na mama yangu waliokuwa sehemu ya furaha yangu hawakuwa pamoja nami.


Hii ilikuwa ni kazi ya kifo; kuwatenganisha wapendwa. Nikatambua hapakuwa na furaha kamili hapa duniani. Ni kweli wahenga waliposema; ukisema ni nuru si nuru, ukisema ni giza si giza, mwisho huwa giza kamili-ndiyo adamah.


Ikawa kila mara nilitazamapo jumba hili na bustani yake, pamoja na mji mkubwa, na fahari yote, huzuni kubwa ikanipata. Nikamkumbuka mzee maskini ambaye mauti yalimkuta akiishi ndani ya nyumba ndogo ya mawe pamoja na umaskini aliokufa nao mimi nakubali alijaliwa fahari kuu ya fani katika wakati wake.


Vyovyote vile, kwake, yumkini huko mbali aliko ana huzuni kubwa inayomfanya asipumzike salama akidhani alifariki na kuzikwa pamoja na jina lake. Ndiyo maana nikaamua kuandika kitabu hiki nipate kumtukuza zaidi yumkini akapata amani zaidi huko alipo; kwani inasemekana kuwa yapo maisha baada ya kufa, lakini mimi naamini wafu hawajui neno lolote.


Nilishikwa na uchungu, nikajawa na nguvu kama niliyepagawa na pepo. Nikatamani kwenda kulivunjavunja kaburi lile na kumtoa mzee aliyefariki zamani, halafu nimwongoze kuelekea kwenye hasri kubwa.


Kisha nimlete mshairi mashuhuri na mpiga kinubi hodari wamliwaze kwa muziki. Mwisho nimtilie divai kwenye kikombe cha dhahabu. Maskini, Lilikuwa ni jambo lisilowezekana, kwani yeye alibaki akijilisha udongo akikazana afanane nao.


Karibu na kaburi kilikuwepo kijumba kidogo nilichokijenga kwa mawe meupe. Mlango wake ulikuwa wa kioo. Ndani ya kijumba hiki nilihifadhi kumbukumbu muhimu za babu. Moja ya kumbukumbu hizi ilikuwa ni nguo yake ambayo alikuwa akiipenda sana wakati wa maisha yake. Nguo hii nilikuwa nikiiangalia mara moja kila baada ya miaka sita.


Hii ni kwa sababu kila nilipoiona ilikuwa ikinitia simanzi kubwa kwa kunikumbusha dhahiri babu yangu na maisha yetu ya zamani tukiwa pamoja. Ulikuwa mfano wa njozi. Kwa kukumbuka hayo nilikuwa nikibaki kama mfu mbele ya kijumba kidogo hata nikamtia wasiwasi mkubwa binti yangu. Ni leo tu ninapozigundua siku hizo. Kumbe zilikuwa siku bora, zenye furaha tele! Nashika tama nikiyaamini maneno ya wahenga waliposema; furaha kamili huoneka siku ya kumbukumbu.


Kutoka mlango ule wa kioo niliweza kuiona nguo chakavu, ikionyesha kuwa awali ilikuwa ya hudhuriungi. Nguo hii ilikuwa juu ya meza ya mawe.


Nilipoiona nguo ile nilishindwa kuimudu akili yangu. Mawazo yangu yakazidi kuchukuliwa na kutopea kwa mambo yaliyopita, siku za zamani, miaka mingi iliyopita. Siku zangu za mwanzo kuishi na babu yangu.


BABU MAMA NA MJUKUU

Wakati bado ningali mdogo mama yangu alinisimulia habari za babu yangu (baba yake mama) aliyekuwa akiishi mji uliokuwa mbali kidogo kutoka mji tuliokuwa tukiishi na mama yangu.


Alinipa hamu kubwa ya kumfahamu mzee huyu. Wakati huu mimi sikuacha kumwota babu yangu. Kwa vile nilikuwa mvulana nilitaka kwenda nikaishi naye akanifundishe tabia za kiume, tabia za kishujaa.


Mama akaniambia, “Mwanangu subiri ukue, uwe na nguvu za kuweza kumuua simba. Nitakupeleka kwa baba yangu ukaishi naye. Naye atakupa wasia. Utampenda na kutamani kuishi naye milele.” Nikatamani miaka iende haraka ili niweza kufunga safari kwenda kumwona mzee huyu ambaye mimi Umlele nilirithi jina hili kutoka kwake.


Katika umri wangu huo mdogo sikujua kabisa kuwa nilikuwa nikilitafuta jambo muhimu: mwana awatafutaye wazee huitafuta hekima; hekima ya wazee humpa mwana mali na amali njema.


Miaka ya saburi kwangu ilionekana kuwa mingi. Hata hivyo, nilijua, siku zote heri huambatana na subira wakati ulifika ambapo nilipevuka vya kutosha, siyo mimi tu niliyeliona badiliko hili, bali hata mama yangu alionekana kuridhika kwa namna nilivyokuwa nimepevuka katika mwili na akili; akaniambia, “nitakupeleka kwa baba yangu sasa ukaishi naye.”


Tukaifunga safari ambayo kwa siku nyingi mimi nilikuwa nikiisubiri kwa hamu.Hii ilikuwa ndiyo safari yangu ya kwanza kufanya maishani.


Niliyastaajabia mandhari ya kupendeza ya dunia; jinsi vile vilima na mabonde ya kuvutia yaliyofuatana mfululizo, na jinsi vile mbingu zilivyoifunika dunia pasipo mwisho.


Niliona kama vile tulikuwa tunakwenda mwisho wa dunia. Baada ya safari ndefu tulikuwa tunakaribia mwisho. Mama yangu aliliweka vizuri kapu lake kubwa alilokuwa amejitwika huku akiendelea kutangulia mbele kunionyesha njia.


Tulikuwa tunapanda kilima kidogo. Baada ya kutembea kidogo niligeuka nyuma kulitazama bonde kubwa tulilolipita. Mama yangu alikuwa akionekana mchovu zaidi kuliko mimi, nadhani hii ni kwa sababu ya mzigo mzito wa kapu kubwa alilokuwa amejitwika mwendo wote wa safari yetu, mwendo wangu ulikuwa wa taratibu, mara zote nikakuta mama yangu ameniacha nyuma.


Giza lilikuwa limeshaanza kutanda wakati nilipoangalia mbele kumwangalia mama yangu aliyesimama kunisubiri.


Nilipomfikia nikatazama mbele zaidi. Giza lilinizuia kuweza kuziona vizuri nyumba tatu zilizokuwa mbele yetu zikifuka moshi.


Moyoni nilitambua lazima yale yalikuwa ni makao ya mzee mkongwe. Mama aliwahi kunisimulia kuwa kwa babu yangu uingiapo usiku nyumba zake hufuka moshi.


Nilimwangalia mama yangu, naye akatambua kuwa nilikuwa tayari nimeyatambua makao ya babu. Kabla hajatamka neno alinitolea tabasamu, kimaisha akasema,” haya ndiyo makao ya baba yangu ambapo mimi nilikulia kabla sijaposwa.” Hapa mimi nilitangulia mbele, naye mama alinifuata nyuma. Mara kwa mara niligeuka nyuma kumwangalia mama anielekeze njia.


Kitambo tulifika katika makao ya babu, hakuchelea kutukaribisha: “Karibu mjukuu wangu mpenzi. Nimekutarajia kwa miaka mingi.


Katika miaka hiyo kila siku asubuhi nimekuwa nikitoka nje na kuangalia upande wa Magharibi kumwangalia mjukuu wangu. Nikafanya hivyo hata jioni wala sikumwona. Nikaishi maisha ya upweke kabisa.


Leo nafurahi kukuona umekuja kulichukua zizi.” Mikono yake aliinyoosha, na miguu yake ilisogea taratibu wakati akisema mameno haya ya upendo. Mimi, hapa, nilikuwa nikiimba wimbo mmoja tu; “Babu, babu, babu…!” Baadaye nilikuwa chini ya miguu yake.


Ukaribisho huu zaidi ulionekana kuwa kwangu. Ni jambo ambalo halikunishangaza mimi, kwani mimi ndiye niliyekuwa bwana harusi na mama yangu alikuwa ni mpambe tu.


Mama alimwamkia baba yake kwa heshima zote. Naye babu alionekana mwenye furaha isiyo kifani.


Nilibaki nimetulia chini ya miguu ya babu. Pembeni alisimama mama yangu. Watu niliowategemea zaidi walinizunguka. Kwangu lilikuwa ni tukio kubwa. Tukio kama hili hutokea mara moja tu maishani.


Chini ya miguu yake nilianza kumchunguza babu. Pamoja na utando wa giza lililozidi kupevuka dhahiri niliubaini mwonekano wake. Alikuwa mrefu wa kadiri, akiwa amevaa vazi la hudhurungi lililokuwa mfano wa kanzu ya mfuto.


Kichwani alijifunga kilemba kilichonizuia kuziona mvi zake. Uso wake ulibeba hekima na heshima. Macho yake yalionyesha yalibeba siri nyingi. Niligundua sikufanana naye, lakini aliongea kwa utulivu kama mimi.


Nyumbani mwa babu yangu kulikuwa kimya. Moshi pekee ndiyo uliotoa ishara kuwa aliishi mwanadamu hapa. Niliambiwa mbele ulikuwepo mji, lakini makazi ya babu yalikuwa yamejitenga mbali na mji huu.


Ilionekana babu alinionea fahari kubwa. Akampongeza mama kwa kumwambia: “Umelizaa simba dume litakaloitawala nyika kubwa: kweli mwana aliyezaliwa neye huzaa!” kisha babu alinikazia macho:” ukizaa mwana wa kike umepata utajiri; hasa akiwa ni mweupe, unaweza ukamwoza kwa mahari ya ng’ombe arobaini. Siyo utajiri huo!?” Mimi nilibaki nikimwemwesa mwemwesa tu, nikikosa neno la kumjibu.


Nilikuwa na hamu ya kuingia ndani ya nyumba ya babu nikione chumba chake alichokuwa akilala na kukiangalia kitanda chake na vitu vyote vilivyokuwemo.


Sikujua ni kwa nini nilikuwa na hamu ‘na jambo hili? Labda ni kwa ajili ya hamu kubwa niliyokuwa nayo ya kuyafahamu zaidi maisha ya mzee huyu. Hata hivyo giza lililokuwamo ndani ya nyumba hii pamoja na baridi iliyokuwepo vilinifanya nishindwe kuingia.


Nikabaki chini ya miguu ya babu huku akiwa amenikumbatia. Nikajisikia salama zaidi.


Baada ya ukaribisho huu babu alitunyooshea mikono ya ukarimu akiielekeza mlangoni mwa nyumba yake. Sote wawili, mimi na mama yangu tulitembea kuelekea ndani ya nyumba hii chini ya uangalizi wa babu aliyesimama kama mlinzi kati ya lango la mji akiwakaribisha mahashamu katika harusi ya kifalme.. Kulikuwa na moto kidogo ukumbini. Moto huu ndiyo babu alioutumia kumulikia nyumba yake nilikaa karibu na moto huu kuondoa baridi. Babu na mama nao pia walikaa kuuzunguka moto wakiongea.


Nyumba ya babu ilikuwa na vyumba viwili mbali na ukumbi tuliokuwemo. Kisha mama alilivuta karibu yake kapu kubwa tulilokuja nalo. “nimekuletea mbegu ya mzabibu kama utakumbuka safari ya mwisho nilipokuja, uliniagiza nitakaporudi tena nikuletee mbegu hii.” Ndani ya kapu kubwa mama aliitoa mbegu ya mzabibu.


“Mara nyingine utanifundisha namna ya kutengeneza divai ya zabibu, “babu alimwambia mama.


Mama alibaki akivigeuza geuza vitu vingi vilivyokuwa ndani ya kapu. Halafu akaitoa chupa kubwa yenye divai na kumpa babu. Baada ya kufungua kifuniko na kugundua kilichokuwepo ndani, alisema,” wewe ndiwe mwana.” Mwanga mdogo wa moto ulitosha kuniwezesha kuuona vizuri uso wa babu. Alikuwa na tabasamu kubwa.


Japokuwa aliipenda divai ya zabibu ajabu hakuupanda mti wa mzabibu kwenye bustani yake ya miti ya aina nyingi ya matunda. Akaichukua tena kutoka ndani ya kibuyu alipokuwa ameiweka mbegu yake ya mzabibu na kuanza kuiangalia. “Japo miaka imesonga. Si kitu, nisipoyala mimi matunda yake atayala mjukuu wangu.” Babu alisema.


Nilitaka kuzungumza na babu. Lakini nilishindwa kwa sababu walifululiza kwa maongezi na mama. Waliponyamaa kidogo nilimuuliza babu anipe habari za mji huu aliokuwa akiishi. Kabla babu hajazungumza na mimi, mama aliingilia kati na kunitaka radhi, akisema nimpe nafasi ya kuongea na babu kwani yeye alikuwa na muda kidogo tu kabla hajaondoka. Nilipoona hivyo niliwaacha ukumbini waongee vizuri. Nikaondoka kwenda kuvikagua vyumba vya babu.


Chumba nilichoanza kuingia kilijaa giza tupu. Nikajaribu kupapasapasa bila kugundua kitu. Nikaamua kurudi ukumbini. Mara hii babu alikuwa ameondoka ukumbini, naye mama alikuwa akiupunguza moto uliozidi kuwaka. Kutoka chumba kingine nilimwona babu akitokea. Mikononi alikuwa na jungu kubwa lililoonekana kuwa zito hata likamfanya achechee.


“Tangu mwaka huu ulipoanza nimekuwa nikisikia harufu ya wageni. Kila siku nimekuwa nikiandaa chakula kizuri kuwaandalia wageni wangu mashuhuri,” alituambia haya wakati akilitua jungu kubwa.


Maneno haya ya ukarimu yalinifanya nitanabahi habari alizokuwa akinisimulia mama yangu kuhusu upendo mkubwa wa babu.


Halafu mimi na mama tulikaa kulizunguka jungu la chakula. Kwa vile nilikuwa na njaa nilikula harakaharaka. Mama yeye alikula taratibu. Ingawaje hivyo, mama alishiba mwisho wake akiniacha pale chini nikizidi kujiweka vizuri mbele ya jungu. Kitambo, mama alipatwa na mashaka huenda ningevimbiwa baadaye.


”kanitupia jicho mara kadhaa huku akinionya. Haikuwa rahisi kuliacha jungu la supu ya mamumunya. Babu yeye alisema kuwa nilipaswa kula sana ili niwe na nguvu nikawinde simba.


Baada ya hapa nilihisi usingizi mzito. Babu aliniingiza ndani ya chumba chake kilichojaa giza huku akimulika kwa kutumia kijinga ambacho mimi hakikunipa nuru kabisa. Nililala juu ya ngozi ya mnyama mwenye manyoya haba. Kisha babu alirudi ukumbini na kuzidi kuongea na mama.


Asubuhi kabla ya jua halijachomoza mama aliniamsha ili tuagane. Ulikuwa ni msimu wa zabibu hivyo alitaka kuziwahi zabibu zake.


Hapa sote watatu tulikuwa tunayaangaza maisha mpya. Mama aliyekuwa amezoea kuishi na mimi sasa alikuwa akienda kuishi pekee. Kwa babu maisha ya upweke yalikuwa yamefikia mwisho; kwani alikuwa amempata mjukuu ambaye atayafanya maisha yake ya mwisho yawe, hasa, yale yapatikanayo.


Nami nilikuwa nikiachana na mama yangu mpenzi niliyemzoea na kumpenda sana. Sikuamini hapa duniani kama alikuwako mtu mkamilifu kama yeye. Kwa ajili ya jambo hili nilitaka niambatane naye kurudi nyumbani.


”Jambo hili lilikuwa gumu mbele ya babu yangu. Baada ya purukushani zangu kushindwa kufaulu nilisema moyoni, “nitaishi naye muda kitambo tu, mara hadithi zake zitakapokwisha nitarudi nyumbani kwa mama yangu.”


Nilibaki nimesimama nikimwangalia mama aliyekaribia kutokomea kwenye upeo wa macho yangu ambaye aliondoka akiwa na majonzi mengi. Hata alipopotea kwenye upeo wa macho yangu mimi nilibaki bado nimesimama nikiwa nimetazama mbali alikoelekea.


Machozi mengi yalikuwa yakititika mashavuni mwangu. Nilipogeuka nyuma, nilimwona babu akiwa amesimama karibu yangu. Alinisogelea na kunishika mkono, “njoo huku,” aliniambia.


Jua lilikuwa limeanza kuchomoza. Niliweza kupaona vizuri mahali alipokuwa akiishi babu. Zilikuwepo nyumba tatu zilzojengwa kwa mawe zikiwa zimetazamana na kuacha uwanja katikati yake. Nyumba niliyolala ndiyo iliyokuwa kubwa zaidi.


Nilimuuliza babu anipe habari za zile nyumba mbili ndogo ambazo moja wapo ilionekana kuwa mpya kidogo, akaniambia nyumba kuukuu kidogo ilikuwa ni ya mama yangu wakati bado anaishi hapa. Ile iliyokuwa mpya mpya babu aliniambia ilikuwa ni nyumba yangu.


Nilianza kuijenga asubuhi moja, mara nilipopata habari kuzaliwa kwako”, babu alinisimulia. “Nilitamani sana kuijenga himaya yangu hapa, lakini bahati mbaya mwanangu pekee alikuwa binti ambaye mara wakati wake wa kuolewa ungewadia naye kupata mume yumkini angeniacha pakee akienda kujenga mji mpya.


Hata hivyo binti yangu aliposwa na mwana wa ajinabi kama mimi ambaye ahakuwa na maisha kwani muda si mrefu baada ya kumuoa binti yangu alifariki dunia akiwafuata wazee wake.


”Baadaye ndipo ulipozaliwa” wakati babu akisimulia juu ya kuzaliwa kwangu alinitazama.


Kisha aligeuza shingo na macho yake na kuendelea “Nilimshukuru Mungu. Hii kwangu ilikuwa ni zawadi kubwa. Nilijua jina langu lilikuwa limenirudia.


Kwa furaha nilichinja mwana mbuzi mweusi mwenye kichwa cheupe. Hii ilikuwa ni nadhiri yangu. Nadhiri hii ilihusiana na maisha yako. Awali maisha yako yatakuwa duni lakini baadaye utajua fahari na kutukuzwa.” Wakati akinisimulia haya tulikuwa tumesimama katikati ya uwanja wa nyumba tatu.


Kisha alinipeleka hadi kwenye bustani yake ya miti ya matunda. Mbele ya bustani hii, mbali, niliweza kuuona mji mdogo. Kabla sijamuuliza. Babu anipe habari za mji huu babu alianza kunipa habari za bustani yake ya miti ya matunda.


Akaniambia matunda kwenye bustani yake hupatikana majira yote ya mwaka. Niliyaamini maneno yake kwani ilikuwepo miti ya matunda aina aina iliyokuwa ikipokezana kuzaa toka majira ya kiangazi hadi masika, na masika hadi kipupwe.


Babu aliniambia majina ya matunda na asili yake. Nilizunguka bustanini na kuonja baadhi ya matunda na kupata ladha mbalimbali.


Baada ya kuizunguka bustani yote mwisho tulikaa chini ya shina la mti mkongwe. Hapa nilimuuliza babu maswali mengi. Babu alinisimulia habari nyingi za mambo mengi aliyoyashuhudia katika maisha yake marefu kisha tulijadiliana namna tutakavyoujenga ushirika wa maisha yetu.


Baadaye tulioondoka kwenda kupata chakula. Chakula kikuu cha babu kilikuwa ni matunda na nyama. Babu aliipasha moto supu ya mnyama pori ambaye aliniambia kuwa alikuwa ni mbogo.


Jioni tuliutembelea mji mdogo uliokuwa ukiitwa Somondra. Mjini tulizitembelea sehemu zote muhimu. Babu alinionyesha watu wengi mashuhuri. Yeye alikuwa ni mtu anayefahamika sana.


Usiku tulipomaliza kula tulitoka ndani ya nyumba na kukaa katikati ya uwanja wa nyumba tatu. Babu aliwasha moto. Tutaongea ziadi. Babu akaniambia namna ambavyo ningepaswa kuishi hapa duniani. Usiku ulipopevuka zaidi babu aliniacha na kuingia ndani ya nyumba yake kubwa. Kitambo alitoka nje.


Mkono wake wa kushoto alishikilia upinde na mshale. Aliniita na kuniongoza hata mbele ya nyumba ndogo. Alizitoa funguo za mlango wa nyumba ile na kunipa. Aliunyoosha na mkono wake mwishoni kunipa upinde uliokuwa na mshale.


“Hii ndiyo fimbo ya kichungaji,” aliniambia wakati nimeunyoosha mkono wangu kuupokea upinde ule. “nakupa ukalichunge zizi. Ng’ombe wakazaane na kuongezeka, ukaliongoze zizi ili kuihimili idadi ya ng’ombe. Siku moja ukawe mfugaji mkuu katika Somondra”. Hapa alikuwa akinihalalisha mimi kuishi naye na kuwa mrithi wake wa baadaye.


Niliufungua mlango na kuingia ndani. Ndani ya nyumba hii nilikuta kitu kimoja; ngozi ya mwana mbuzi iliyokuwa nyeusi na nyeupe. Niliona ngozi hii kupitia mwangaza wa moto uliokuwa unawaka nje. Niliuweka upinde wangu pembeni mwa nyumba.


Nilipotazama nje ya mlango nikakuta babu amekwishaondoka. Niliufunga mlango na kulala juu ya ngozi ya mwana mbuzi. Sikuweza kupata usingizi haraka. Nilikuwa nikifikiria mzee huyu ambaye sasa nilijiona nilikuwa na bahati ya kuishi naye. Baadaye usingizi ulinichukua.


Hata usingizi uliponitoka, katikati ya usiku nilimsikia babu akitoka nje mara kwa mara. Hali hii haikunipa amani. Mara ya nne alipotoka nilifungua dirisha taratibu na kuchungulia nje, lakini sikumwona.


Nilibaki pale dirishani nikiwa nimechungulia. Mara nikamwona babu anakuja akitokea bustanini mikononi alishikilia kitu. Aliposogea karibu nikakagundua kuwa alikuwa amekamata mnyama.


Nilikumbuka mitego yake aliyokuwa ameitega bustanini. Baadhi ya vimnyama hutembelea bustanini wakati wa usiku vikitafuta matunda, lakini mwisho wake hujikuta vinakuwa kitoweo cha babu. Nilitamani mapambazuko yaharakishe, kwani siku yake ingekuwa siku nzuri. Baada ya hapa sikumsikia tena babu kutoka nje. Nami nilishikwa na usingizi tena.


Asubuhi nilipoamka na kutoka nje nilimwona babu akiwa amechuchumaa kando ya njia tuliyojia mimi na mama yangu mkono wake wa kulia alishikilia kisu. Chini alikuwa amelala mnyama aliyekuwa akimchuna.


Babu alikuwa akiimba nyimbo taratibu. Nilipoungana naye niligundua alikuwa amekamata wanyama watatu. Akaniambia nikae pembeni yake nimwangalie na kujifunza namna ya kumchuna mnyama.


Alipomaliza kuwachuna wanyama, niliukusanya uchafu wote wa wanyama wale na kuuzika ndani ya shimo.


Kisha sote wawili tuliingia jikoni. Hapa tulikuwa na pilikapilika kubwa ya kutayarisha chakula chetu. Mara kwa mara babu alichugulia ndani ya jungu langu kubwa akiyaangalia mapishi yangu.


Baada ya muda ukumbi wote wa nyumba kubwa ya babu ulitakapaa vyungu vya nyama. Vilikuwepo vyungu vya nyama ya kuchemsha. Kukaanga, kuchoma na kubaika, hata supu ya makongoro ilikuwemo ndani ya jungu kubwa zaidi. Nilitamani mama yangu aje na kuviona vyakula hivi, na kuyashuhudia mapishi yetu ya hali ya juu.


Tulipomaliza kula niligundua kuwa lilikuwako jambo jingine zuri zaidi hata kuzidi nyama tunayoila. Babu yangu alikuwa ni mwindaji pia mvuvi.


Uwindaji na uvuvi ndiyo zilizokuwa kazi zake kwa mapokezano. Mchana kutwa nyumba zake kila siku zilikuwa zikifungwa. Akarudi karibu kuchwa kwa jua. Mara nyingine alirudi usiku. Lakini siku ya jumamosi alikuwa akipumzika akiitunza amri ya nne ya Mungu, kwani wakati mimi ninaanza kuishi naye alikuwa tayari amekwishaongoka.


Sasa, kazi hii ya uwindaji ambayo mimi nilikuwa nikiitamani, ndiyo kazi iliyokuwa inafuata asubuhi hii.


Babu aliingia ndani ya chumba chake cha kulala. Alipotoka alikuwa na vazi la ngozi mikononi. Akanipa na kuniambia: hili ni vazi lako la kuwindaji.”


Nililitwaa vazi lile la ngozi ya simba.

“Nataka ufanane na simba ukalitikise pori kwa muungurumo wako; aliniambia mara nilipolipokea vazi.


Nilipolivaa lilinipwaya kidogo.

“Unakua, siku si nyingi litakuwa sawa,” babu alisema.


Niliingia ndani ya nyumba yangu na kuuchukua upinde pamoja na mshale. Nilipotoka nje nilimwona babu akiwa amesimama mbele ya mlango wa nyumba yake kubwa akiliweka vizuri vazi lake la kiwindaji mwilini mwake. Mkononi alikuwa na upinde pamoja na mshale.


Kiunoni aliuchomeka upanga uliong’aa. Akanitazama. Macho yake yakaonekana kukumbuka jambo jingine. Akarudi ndani ya nyumba yake. Alipotoka alikuwa na upanga mwingine ambao alinipa. Niliuchomeka upanga ule kiunoni kama alivyofanya babu. Tukaondoka kwenda kuwinda, babu akiwa ametangulia.


Msituni babu alinifundisha kulenga shabaha. Baadaye alinifundisha namna mbalimbali za uwindaji; kuanzia uwindaji wa wanyama wadogo hadi wakubwa, hata wanyama wapole na wakali.


Katika siku ya kwanza tu niliupenda uwindaji. Jioni ilipofika tulirudi nyumbani. Mimi nilikosa mavuno, ila babu yangu alimpata kurungu mwenye manyoya ya kijivu.


Usiku ulipowadia kama kawaida tuliwasha moto uwanjani. Mara hii niliuwasha mimi. Tukakaa juu ya vigoda kuuzunguka moto. Tukatazama juu angani. Anga lilikuwa na nyota nyingi. Babu akanifundisha majina ya nyota na kunionyesha yule mwindaji. Mwisho babu alilitwaa zeze lake na kuanza kulipiga. Sote pamoja tukauimba wimbo wa kumsifu mfalme maarufu aliyeishi katika nchi ya asili ya babu.


Haya yakawa ndiyo maisha yangu ya kila siku nikiwa na mzee huyu. Nikayapenda sana maisha haya, pia nikampenda zaidi mzee huyu hata sikutaka kutengana naye tena.



NI MZEE WA KILINDONI

Ikawa kila mara nimtazamapo mzee huyu nikagundua jambo moja katika moyo wake. Lilikuwa pendo. Moyo wake ulijaa mapenzi makubwa kwangu. Alinipenda kwa upeo wa upendo wake.


Ijapokuwa moyo hauonekani ndani ya mtu, lakini kupitia upendo wake dhahiri niliweza kuuona moyo wa babu ukiwa mweupe. Kila nilipokuwa nikilifikiri pendo la babu yangu kwangu nilikuwa nikiahidi kumlea vizuri siku ambazo atakuwa hajiwezi.


Basi miaka ilivyozidi kwenda mbele maungo ya mwili wangu yakabadilika. Nikaonekana kama mwana simba anayetaka kutengana na mamaye. Akili yangu pia ikakua, nikawa mjanja kama sungura. Babu akayatambua haya, akawa na furaha kuu.


Katika kipindi hiki nilimkumbuka mama yangu. Mwanamke masikini aliyekuwa akiishi katika mji mdogo uliokuwa ukiitwa Baridos, uliokuwa miongoni mwa miji ya nchi tuliyokuwa tukiishi ya Somondra. Huko alikuwa akilima zabibu. Nilibaini kuwa kipindi cha miaka mingi ameishi maisha ya upweke. Niliyafikiria zaidi maisha yake ya kila siku yaliyokuwa:


Jua lilipochomoza lilikuwa likimkuta ameshafika shambani. Shambani alichuma zabibu zilizoiva. Akazitia ndani ya kapu lake na kurudi nyumbani. Kutoka katika zabibu hizi alikuwa akitengeneza divai.


Divai hii alikuwa akiitia ndani ya vibuyu, ambapo alienda hata mjini kuuza divai yake. Wakati wa kurudi nyumbani alipenda kununua badamu kumletea mwanae, lakini, sasa, mwana huyo alikuwa hayupo. Ni dhahiri jambo hili lilikuwa likimtia simanzi. Usiku ulipoingia kabla hajalala mama alikuwa akiimba nyimbo za kumsifu Mungu.


Katika kipindi hiki cha kuishi na babu yangu ndipo nilipojua namna nilivyozaliwa:


Nilizaliwa usiku wa manane juu ya jabali kubwa lililokuwa mlimani. Mama yangu alikuwa safarini. Usiku ulipoingia alipanda juu ya jabali ili kujilinda na wanyama. Wakati huu alikuwa na mimba ya miezi saba.


Uchungu mkubwa ulimshika mama yangu hata ulipotimia usiku wa manane nilizaliwa. Wakati mimi ninazaliwa baba yangu alikuwa amekwishafariki.


Babu aliyenisimulia haya aliniambia hata na maana ya kuzaliwa kwangu jinsi hii :


Kutokana na mila za nyumbani katika nchi ya asili ya babu yangu, mtoto anapozaliwa jinsi hii ni ishara kuwa atakuwa mtu wa kutukuzwa siku za usoni. Jina lake litakuwa kubwa kama bahari. Walakini mimi sikuielewa maana yote ya mambo haya.


Pia kutokana na maelezo haya nilipata kujua asili ya babu yangu. Ni hadithi iliyonisisimua na kunifanya nitambue kuwa babu yangu alikuwa ni mtu hodari tangu utotoni katika kisiwa cha Mafia.


Siku hizo kisiwa chote cha Mafia kilijazwa na upepo wenye harufu nzuri. Wenyeji wake waliamini kuwa upepo ule ulikuwa ukitoka visiwa vya mbali vilivyojazwa kwa mimea ya maua yenye harufu nzuri katika familia yoa walizwaliwa watoto kumi na saba.


Yeye alikuwa ni mwanaume pekee aliyebaki kwani ndugu zake wawili wa kiume walifariki mapema. Baba yake alikuwa ni jumbe wa Kilindoni. Kama mtoto pekee wa kiume babu yangu alikabiliwa na jukumu kubwa : jukumu la kuuendeleza na kuuenzi ukoo wa jumbe.


Kama tunda pekee lililokuwa limebeba mbegu ya mtende likadondokea ndani ya mto na kuchukuliwa mbali. Babu yanbgu hakukaa Kilindoni.


Katika ujana wake babu alipenda sana ubaharia. Alichonga majahazi na kufanya safari ndefu za baharini, akivitafuta visiwa vilivyokuwa na maua yaliyokuwa yanaleta harufu nzuri kisiwnai Mafia. Alisafiri katika visiwa vingi, lakini hakuviona visiwa hivi vilivyokuwa na maua. Akarudi nyumbani Mafia.


Baadaye tena alifanya safari nyingine nyingi. Hata katika safari ya mwisho akaenda mbali zaidi na kufika katika ksiiwa kikubwa walimokuwa wanaishi watu.


Aliishi kisiwani humu muda mrefu hata akampenda mwanamke mmoja waliyezaa naye mwana wa kike. Huyu ndiye aliyekuwa mama yangu. Pia ilikuwa ni katika kisiwa hiki ndipo babu yangu alipokutana na wamishonari na kuongoka, akaiacha dini yake ya Umizimu.


Wenyeji wa kisiwa hiki walimpa jina jipya babu yangu, wakamwita “Francis Drake” wakimfananisha na bahari a shupavu wa Kiingereza.


Baada ya miaka kupita babu alikumbuka nchi yake na watu wake. Akaamua kurudi nyumbani pamoja na binti yake. Siku tano tangu walipoanza safari yao bahari ilikumbwa na machafuko makubwa. Upepo wa kubisha uliipata bahari.


Upepo huu ulilisukasuka jahazi na kulichukua hadi maawio ya jua. Wakajikuta wanatokea pwani. Ilikuwa ni pwani ambayo haikuwa na mtu aliyekuwa anaishi bahari ya Pwani hii ilikuwa imejaa dhoruba; hivyo babu na binti yake walishindwa kurudi.


Katika Pwnai ile ulikuwepo mto ulioingiza maji yake baharini. Alimtwaa binti yake na kuufuata mto ule. Baada ya siku chache walitokea katika nchi mpya. Katika nchi hii babu aliufikiria uumbaji mkuu wa Mungu.


Mungu aliumba bahari, mimea. Wanyama, ndege, wadudu na vitu vbingi vinginevyo. Kisha aliumba mwanadamu kuvitawala vyote. Babu aliyaangalia mazingira yaliyomzunguka; yalikuwa na vitu vyote hivi. Akiwa kama wanadamu wengine wote aliona alistahili kuyatawala mazingira haya popote ambapo angefika.


“Nitafanya makao yangu katika nchi hii nami nitakuwa mwindani na mvuvi; lakini sitapasahau nyumbani Mafia ambako watu wote niwapendao wanaishi. Katika makao yangu mapya Mungu akanisaidie nikawe nyota ing’aayo iliyochomoza Mashariki.” Katika nyumba hizi tatu zilizozjngukwa na bustani ya miti ya matunda ndipo mahali babu yangu alipopachagua kuwa makao yake ya mwisho.


Hii ndiyo iliyokuwa asili ya babu yangu hapana shaka hii ndiyo iliyokuwa asili yangu pia. Hata hivyo, mimi najua, bado muda kidogo nitajulikana kama Mwanasomondra.


Wakati mmoja nilimuuliza babu; haikumpasa sasa kurudi nyumbani Mafia kuuchukua mji? Akanijibu, “ilinipasa kufanya hivyo, lakini kuchipuka mbali na nyumbani ilikuwa ni jambo la kishujaa zaidi. Siku zote lango kuu huwa mbali na mji.”


Basi miaka ya kuishi na babu ilivyozidi kwenda mbele babu yangu alizidi kubadilika. Akaonekana mzee zaidi, nywele zake zilijaa mvi na kuwa nyeupe kama sufi. nguvu zake pia zilianza kupungua.


Siku moja nilimuuliza alikuwa na miaka mingapi sasa? Akanijibu; “nimeishi misimu ya mvua karibu mia mbili. Kama ningeifanya safari ya kuizunguka dunia kwa miguu ningeishaizunguka mara kumi na mbili.” Hesabu yake ilikuwa ni kubwa, mimi sikuielewa, ila nilizidi kumheshimu kutokana na umri wake huo mkubwa. Hata harufu yake nilipokuwa nikimnusa alikuwa akinuka harufu ya gogo la mpioingo wa zamani.


Kipindi hiki babu yangu akawa mzungumzaji zaidi. Muda mwingi aliutumia akizungumza nami. Mara nyingi wakati wa kuchwa kwa jua tulionekana tukiwa tumeongozana tukirudi nyumbani baada ya uvuvi.


Yeye alikuwa akitangulia mbele akiwa na mkongoji wake. Akiniambia maneno kunionyesha njia nisiyoifahamui. Mara hii maneno yake yalikuwa yenye mafunzo mengi na mengine yaliyonekana kama maono.


“Nilikuwa mlima volkano mfu, mlima ambao ulikufa wakati kilele chacke kingali kifupi: lakini simba huzaa simba wala hawezi kuzaa ng’ombe. Leo umetokea ukiwa mlima volkano hai, mlima utakaokua hadi kilele chake kufika mawinguni,” alipenda hadi kuyhakariri maneno haya.


“Nikiziangalia siku za usoni, nauona mji mkubwa uliochipuka sehemu za Mashariki. Ndani ya mji kuna fahari ya jumba la kifalme na bustani iliyojaa ndege na wanyama wa kila namna.


’’Katika lango la mji kuna alama ya upinde ikimaanisha nguvu kubwa ya mji. Namwona kijana tajiri, akiwa katika kiunga cha mji kilichoko mashariki mwa mji, akiwa amevaa kaftani akijiandaa kwenda kuweka shada juu ya kaburi la mzee wa mji.” Alisema maneno haya siku moja mara baada ya kumaliza kuupima ukubwa wote wa mji wa Somondra.


Mimi nilifikiri alikuwa akitaka kuuteka mji wote wa Somondra ili kuiongeza himaya yake wakati alipokuwa akiupima mji; hata hivyho nilipata mashaka kwani hakuwa na jeshi ijapo kikosi kimoja.


“Sasa hata nikifariki si neno, kupitia kwako nitaishi tena”, aliniambia na kuzidi kunisisitizia nimuenzi.


Kutokana na babu yangu, kuzidi kuwa mzee mara nyingi nilikwenda mawindoni peke yangu. Nilipofika badala ya kuwinda muda mwingine niliutumia kuyatafakari maneno ya babu. Nikazifikiria nyumba tatu za mawe zilizokuwa zimefurika nyama pori.


Nikaifikiria na ile miti ya matunda. Nikashangaa vitu hivi vingewezaje kunipa heshima na ukuu wote alioutabiri babu! Nikamfikiria na mzee mwenyewe…! Alikuwa mzee, maskini, asiye na nguvu tena.


Angewezaje katika udhaifu ule kuitafuta mali na kuniridhisha! Nikauangalia na upinde wangu uliokuwa tegemeo langu kubwa, hata hviho upinde huu haukuweza kunipa kitu kingine zaidi ya kurungu na mbogo mwituni.


Kumbe hkatika mtazamo wangu wote kwa babu, na udhaifu wote uliomzunguka nilishindwa kutambua kuwa akili ni mali.


Kamwe sikujua mambo yote haya aliyoyatabiri babu yaliutegemea uta wangu. Asilani, sikujua siku zijazo uta ule ungeniongoza katika njia ngumu, hata heshima kuu!


Niligundua pia, kwa nini babu alipenda sana kuniambia maneno ya mausia katika kipindi hiki. Alijua siku alizoish9 zilikuwa nyingi. Hasa alipoiangalia miti mikongwe ya matunda aliyoipanda zamani. Miti iliyozaa matunda misimu isiyohesabika. Aliziangalia na nyumba zake alizozijenga zamani.


Nyumba alizozijenga kwa mawe meupe, lakini zikageuka rangi na kuwa nyekundu kwa ajili ya ukongwe.


Alipojilinganisha na miti na nyumba zake akaona wakati uliwadia. Alipogeuka kwangu akaniona nilishakuwa mwanamume. Akatambua ilimpasa kuitayarisha njia yangu bila kuchelea.


Nikaliona jukumu kubwa lililokuwa mbele yangu, jukumu la kumuenzi babu; hata hivyo jukumu hili kwangu bado lilikuwa gizani.


Mafikara haya yalipozidi sana akilini mwangu, babu alitambua, akaniuliza; “mjukuu wangu niambie fikara inayokusumbua akilini, kwa kuwa mimi ni babu yako. Mzee niliyeishi miaka mingi na kushuhudia mambo mengi. Nami ni mganga wa tiba zote.”


Mimi nikamjibu, “maneno uliyoniambia babu yangu yameuzidi upeo wa kili yangu. Akili ambayo bado changa. Jukumu ulilonipa ni kubwa.


Nashindwa nikalikuza na kulienzi vipi jina lako, kwani kmimi ni kijana maskini tu! Naona kama umenipa jukum u la kuumba dunia mpya. Kama ni uchawi kanionyeshe basi mimi mjukuu wako.”


“Usiogope,” babu alinituliza moyo. “Ninayo njia kwa mambo haya. Kitambo nitakuonyesha.”


Maisha ya uzee yawadiapo huenda haraka sana, sawa na mabadiliko yatokeayo wakati wa balehe. Ni kama kasi ya kijito kinachoikaribia pwani. Ndivyo ilivyokuwa kwetu. Kila asubuhi tulipoamka babu akaonekana amepungua nguvu, huku mimi nikijiona, kuongezeka nguvu. Katika kasi ya mabadiliko haya ndipo asubuhi moja babu yangu aliponiita.


Nilitoka ndani ya nyumba yangu nikiwa na upinde wangu na kuzunguka nyuma ya nyumba mahali sauti ilipotokea. Nilimkuta babu amekaa chini kwenye ubavu wa ukuta wa nyumba uliokuwa upande wa bustanini. Alivaa vazi lake alilolipenda, la hudhurungi. Pembeni kwake ulilala mkongoji. Nilikwenda na kukaa kulia kwake. Halarfu nikauweka chini upinde wangu.


“Mazungumzo niliyofanya hapo nyuma yalikuwa yanatayarisha njia ya mazungumzo haya ya leo,” alikifunua kinywa chake ambacho kwa sababu ya ukungu wa uamsho wa asubuhi kilitoa kitu mfano wa mvuke.


Akaendelea. “Siku nyingi nimekuwa nikiitafuta siku nzuri ya kutoa maneno haya kwako. Neno zuri hutolewa siku nzuri. Asubuhi ya leo nilimwona Kotwe bustanini. Ndege huyu huonekana kwa nadra. Tangu nilipojenga mahali hapa hii ni mara ya pili kumwona. Ndege huyu hubeba baraka. Neno utakalosema na kupanga siku hiyo halitaharibika.” Wakati wote alipokuwa anaongea maneno haya alikuwa ametazama chini. Mimi nilibaki nimemgeuzia shingo huku nimemkodolea macho, nikiitazama midomo yake namna ilivyochezacheza, ambayo sasa haikutoa mvuke tena.


“Zamani niliogopa,” babu aliendelea, “Nani angekuwa badala yangu wakati nitakapofariki! Nikaogopa ningekufa kama mbwa mwitu nyikani, nikisahauliwa kama chungu kilichovunjika. Sasa, hilo si jambo ninalohofu tena. Ni wewe utakayekuwa badala yangu. Mustakabali wangu wote uko kwako.


“Nakufa bila ya walimwengu kujua nilikuwa mkuu. Nilikuwa nyota kubwa yenye mwangaza hafifu. Najitolea kukuonyesha yote ili nyakati zijazo uliokoe jina langu, likakumbukwe vizuri.


‘’Jina langu likafanane na jua likavume kama tufani baharini, likiziangusha merikebu na mashua za vita, tena likatajwe kama jina la “babu” kati ya ulimi wa mjukuu. Mwanamume ni muhuri, na muhuri wa mwanamume ni jina kubwa. Mambo yaliyoonekana fumbo kubwa leo nayaweza wazi.”


Hapa nikaiweka sawa akili yangu kusikia fumbo kubwa likifumbuliwa.


“Tazama Kaskazini,” babu aliniambia. Nikayageuza macho yangu upande huu wa kaskazini. Upeo wa mambo yangu ulikuwa mdogo, haukuweza kufika hata robo ya nchi yetu ya Somondra.


“Mbali zaidi upande huu wa kaskazini ipo hazina kuu; mwamba wa dhahabu. Mwamba huu umo ndani ya msitu mnene uitwao “msitu wa giza.” Njia yake ni ngumu. Itachukua siku nyingi kufika huko. Zamani watu wengi walijaribu kwenda huko, lakini wote walipotelea huko. Katika siku za hivi karibuni hakuna mtu aliyejaribu kwenda huko.


“Habari hjii ya mwamba wa dhahabu hakuna anayeifahamu isipokuwa watu wachache wanaotoka koo za kishujaa; mashujaa wasafiri.


“Miaka ya nyuma wakati msitu huu bado ungali mdogo wasafiri waliopita karibu na msitu huu wakati wa ashudhuri jua lilipopiga kwenye dhahabu walikuwa wakiona mwangaza mfano wa zabarijadi angavu uliokuwa unapaa angani na kuwashangaza. Huu ni uthibitifu wa wingi wa hazina hii. Imekisiwa, mtu atakayefanikiwa kuupata mwamba huu atakuwa ndiye tajiri mkubwa duniani.


“Nilitia tamaa kubwa, kubwa mno, kwa habari hii ya mwamba wa dhahabu. Watu hujenga majina kwa ujemadari na ufalme, dhahabu nayo hujenga jina nikijua kupitia dhahabu jina lngu litakumbukwa kama nuru wakati wa giza, likitajwakati ya ndimi za watunyakati na milele. Imekupasa kujitolea kwa ajili yangu.


“Ngoja nikuambie jambo moja; mwanamume unapozaliwa chini ya jua ni kama dhahabu iliyofukuliwa mgodini, lazima ipitishwe ndani ya moto ipate kupasishwa.


“Vyovyote vile, wewe ndiye mnajimu wa nyota kubwa ing’aayo ijazo.”


Namna aliyokuwa anaongea alionekana kuniamini kushinda hata nilivyojiamini mimi mwenyewe. Kisha babu aliukamata upinde wangu na kuunyanyua juu.


“Upinde huu utakuongoza hata ushindi wa mwisho. Mababu zangu walishinda vite wakitumia upinde. Ukiukamata vizuri utakupa ufalme ugenini.” Aliuweka chini upinde wangu na kunyanyuka akiniacha pekee.


Alipoingia ndani ya nyumba yake na mimi ninyanyuka kutoka pale chini na kuingia ndani ya nyumba yangu. Ndani ya nyumba nilikaa juu ya ngozi ya mwanambuzi nikiegemea ukutani. Kwa muda mrefu nilikuwa nikiwaza habari za mwamba wa dhahabu.


Sikujua kama babu yangu alipanga ukuu wetu upatikane kwa njia hii!


“Wakati mwingine damu ni daraja liisiloepukika kuufikia ukuu.” Ndiyo imani kubwa aliyoiamini babu yangu. Nikiyatarajia kabisa mambo haya maishani, lakini kila mara babu alipoyataja niliyaona kuwba mageni.


Mno mno, nilijoina bado ningali mchanga kwa kila jambop, kiasi kwamba matarajio yote ya babu nisingeyatimiza. Jambo hili lilimtia wahaka mkubwa babu yangu aliyetamani kuuona ushindi wakati bado angali hai. Ulikuwa ni wasiwasi wenye maana.


Akiwa amening’ang’anizia kunishikisha mundu ilinipata kuupokea. Huyu alikuwa mtu mwenye hekima; ni dhahiri matarahjio yake yalibeba ushindi. Nikijua mavuno huwa hayaji kimuujiza ilinipasa kulichukua jembe na kuingia shambani katika wakati muafaka wa kilimo. Mvua ya kwanza ndiyo ya kupandia.


NAWAKUMBUKA MNYAMWEZI NA MIGILIMO

Kwa upande wake, babu yangu alikuwa akiukaribia mwisho. Ulikuwa ni mwisho mzuri. Akiwa na umri mkubwa na mambo mengi aliyoyashuhudia, alikuwa ameutoa ushuhuda mkubwa kwa kizazi chake.


Hakustahili lawama. Kwangu, daima atabaki kuwa mtu imara aliyekuwa na msimamo kamili. Hapana shaka pia atauthibitisha ule usemi kuwa mashujaa wengi hufa ugenini. Hata hivyo kwa upande wake lilikuwepo jambo moja lililoutia giza moyo wake wote; mashaka juu ya ukuu wake wa baadaye. Hapana shaka angefariki na mashaka haya.


Kwa upande wangu, nilikuwa kama askari anayeyavaa mavazi ya vita tayari kwenda kwenye uwanja wa mapam,bano; au kama nahodha anayefunga tanga za jahazi tayari kufanya safari ndefu baharini.


Niliyafikiria pia maisha ya mbeleni ya mama yangu. Alikuwa akitarajia nini? Bila shaka jambo moja tu; siku moja atakapokuwa mzee aishi tena na mwanae. Hapo atakaa na wajukuu wake na kuwapa simulizi.


Hiyo ndiyo itakayokuwa furaha yake katika maisha yake ya mwisho. Yumkini kipindi hiki pia atakuwa akijitahidi kutenda mema ili apate kukubaliwa katika pepo ijayo. Jambo baya, mwana huyu wa pekee aliyekuwa anamtegemea alikuwa akiyavaa mavazi ya vita na kuzitweka tanga za jahazi tayari kusafiri. Haikujulikana kama atarudi salama! Endapo angeyajua mambo haya angeaangua kilio kikubwa.


Habari za mama yangu zikaumeza zaidi moyo wangu kipindi hiki. Nikakumbuka zamani aliponileta huku mbali kwa babu. Nakumbuka pia, siku ile, alipotuaga. Aliponiangalia mara ya mwisho akadondokwa machozi nami nilipolia. Ni kweli mama na mwana hawatengani, wakitengana hulia.


Hamu ya kuonana naye iliujaza moyo wangu. Nikaamua kulit6imiza jambo hili. Nilikuwa na kila sababu ya kwenda kumwona. Pale tutakapokutana tena! Machozi ya ukiwa yaliyotutoka siku nyingi yatageuka na kuwa machozi ya furaha, ambapo mwisho tungefutana machozi haya.


Nilimweleza babu shauku hii iliyonipata. Nilikuwa siwezi tena kustahimili kwa jinsi nilivyompenda.


Babu aliniambia nifikapo nyumbani kwa mama yangu nisije nikamwambia habari ya mambo yote aliyokuwa amekusudia.


Ingawaje babu hakuniambia kwanini nisimweleze mama mambo haya; lile jambo lililolijua hata mimi ni kuwa wakati wa kumwambia mama habari hii ulikuwa bado kuja.


Niliufikia mji mdogo wa Baridos ambao wakazi wake wengi walikuwa ni wanawake na watoto. Wengi wa wanawake wakiwa ni wajane. Ulikuwa ni mwanzo wa usiku. Nilitembea kuelekea ndani zaidi ya mji huu. Mbali na giza niliweza kuikumbuka nyumba moja iliyokuwa mkabala na boma la mji.


Nilijawa na furaha kubwa kuiona nyumba hii. Akili yangu ilikuwa na kumbukumbu nzuri kwani wakati natoka katika nyumba hii nilikuwa mdogo kabisa. Nilipinda na kuelekea upande wa kushoto moja kwa moja kuifuata nyumba hii. Ilikuwa vigumu kupasahau mahali alipoishi mama yangu.


Mandhari ya mahali hapa sasa yalinijia wazi. Niliuona mti aina ya mbambakofi uliokuwa umeota kando ya nyumba, mti ambao wakati ninaondoka mahal hapa niliuacha ukiwa mdogo, sasa ulikuwa mkubwa. Nilikumbuka zamani namna nilivyopenda kupanda na kushuka katika mti huu. Moyoni sikuamini endapo nitamwona mama yangu tena, kwani ukimya mkubwa uliyatawala makao haya. Mbele ya nyumba hii ukimya mkubwa uliusadikisha moyo wangu.


“Je, alikuwa amehama? Au alikuwa amefariki?” niliwaza.


Pamoja na mawazo haya, akili yangu haikushikwa na bumbuazi, kwani moja kwa moja nilitembea kuuendea mlango wa nyumba. Nilifanana na ndama aliyetanga mbali na mamaye; na sasa alikuwa ameufumania mlango wa zizi alilolala mamaye.


Niliweza kuisikia sauti ndogo. Ilikuwa ni sauti ya mwanamke akiimba. Pamoja na udogo wa sauti wala sikuisahau. Kwangu ilikuwa ni sauti tamu, sauti ya upendo, sauti ya ukarimu, sauti ya mama yangu. Nilitaka kwenda kumwona mtu mwenye sauti ile; nikaipanda ngazi kuu ya mlango. Mbele ya mlango badala ya kubisha hodi niliita “mama…!”


“Wewe ni nani?” Sauti ile ya ukarimu iliuliza.


“Mimi mwanao”


“Ndiyo”


“Wewe ndiye yule mwana nimpendaye sana? Mwana mpotevu!”


“Ndiyo”


“Karibu mwanangu”


Muda kitambo, sote tulilishikilia komeo la mlango wa nyumba; mama akiuvuta ndani mimi nikiusukumiza kwa ndani.


Hapa, kati ya mlango ndipo tulipokutana. Machozi ya furaha yalitutoka wakati mwanga mdogo wa taa ya fanbusi iliyokuwemo ndani ulipoyakutanisha macho yetu.


Lilikuwa ni tukio la furaha na huzuni, huzuni ya kumbukumbu ya giza la dunia lililokuwa limetutenga, na furaha ya kukutana.


Kwa vile ulikuwa ni usiku ulikuwepo utulivu mkubwa. Nbiliweza kumsikia mama akipumua haraka haraka wakati tumekumbatiana.


Miaka mingi tuliyotengana haikumbadilisha mama yangu. Alionekana kama alivyokuwa zamani, isipokuwa tu alionekana kushupaa na mkakamavu zaidi. Nadhani hii ni kwa sababu ya kazi ya kuihudumia mizabibu kondeni miaka yote.


Wakati huu tulikuwa tumeachana. Wakati ninamwangalia kumchunguza alikuwa bado akitokwa machozi. Machozi haya yalinifanya nimwemwese pia.


Usingeamini kuwa nilikuwa mwanamume! Matone ya machozi yake yaliakisi mwanga wa taa, yakaonekana ya manjano mbivu.


Machozi yale yalinipa thamani kuu kwa kuitoa rangi ya dhahabu. Nilikuwa mtu wa kwanza aliyepata kupendwa hata kuliliwa kwa machozi ya dhahabu. Niliyapokea machozi yale kama ya dhahabu halisi. Mama yangu alionekana mwanamke mpweke kabisa.


“Najua umekuwa mpweke muda mrefu,” nilimwambia.


“Sasa nimekuja kuzungumza na kucheka nawe.” Niliyafuta machozi yake ili kumfariji.


Mapenzi yanapomwemea mtu ulimi huwa hausiti kusema “nakupenda,” nacho kiganja cha mkono huwa hakisiti kulifuta chozi.


“Umlele!” mama aliniita. “Ni wewe? Umenikumbuka!”


Mimi nilibaki nikiwa nimemwangalia tu.


“Umebadilika!” aliniambia.


“Miaka tuliyotengana imekubalisha sana umekuwa mkubwa kama tembo, na sauti yako kama ya simba!” Mama yangu alinisifu.


“Utanisamehe mwanangu. Nilifanya kosa. Watu husema; mwana hatengwi na mamaye katika miaka ya kuchwishwa ziwa, la sivyo atalisahau ziwa na mamaye,” mama aliniambia katika uso uliojaa haya.


Hakika sikuwa na la kusema, nilibaki nikimwangalia mwangalia tu mwanamke huyu, ambaye mbali na kufululiza kuzungumza hata yeye furaha ya ujio wangu ilimuelemea na kumfanya akose la kufanya, kwani nilimwona, mara kushika hiki, mara kile, mara aliacha vyote na kubaki akiongea; lakini mwisho wake aliandaa na kunikaribisha chakula.


Tulipotoka kwenda kulala ilikuwa yapata usiku wa manane. Chumba nilicholala kilitoa haruvu ya divai ya zabibu.


Nikayaangaza macho na kuona vibuyu kadhaa ambavyo hapana shaka vilikuwa na divai ndani yake. Nilitaka ninyanyuke kitandani kwenda kuinywa divai ile, lakini niliona uvivu kwa ajili ya uchovu, tena nilikuwa nimeshiba sana. Nikazima taa na kulala.


Mionzi mingi ya jua ilipenya moja kwa moja kupitia nyufa za dirisha ndani ya chumba nilichokuwa nimelala. Nikagundua mapambazuko yaliwadia. Nilipotoka nje niliona jua lilikuwa limechomoza zamani. Wakati natoka nje niliona aibu kidogo wakati namsalimu mama nikiwa nimechelewa kuamka. Walakini, hii ilikuwa ni sababu ya uchovu.


Mama alikuwa ameshatayarisha chakula. Nilipata tabu kidogo kuviepa vyungu vya chakula ukumbumini. Baadaye nilijumuika pamopja na mama kwa staftahi ile. Jungu kubwa nilipopigana nalo mimmi lilikuwa na uji mzito uliotiwa mafuta ya ng’ombe.


Muda uliofuata tulizungumza zaidi na mama yangu. Aliniambia mambo mengi kuhusu mji wa Baridos, na mimi nilimsimulia habari nyingi kumhusu babu yangu. Mchana jua lilipokuwa kali mama alinipa divai.


Siku ya tatu mama akawa na maongezi ya mashaka. Aliuangalia umaskini wake. Akaogopa juu ya mustakabali wangu. Angenirithisha nini? Hakuwa na kitu. Zaidi, baba yake ambaye mimi nilikuwa nikiishi naye hakuwa na mali mbali na upinde, na mtumbwi mchakavu!


“Tazama nyumba ndogo ni8nayoishi,” aliniambia. “Ndani ya nyumba kuna vibuyu vyenye divai ya thamani ndogo, tena vipo vyungu vyungu vipya na vya zamani. Vitanda vyangu ni vya mbao hafivu.


Ndani ya nyumba iko dari yenye nafaka kidogo. Mbele ya nyumba yangu, karibu na njia, yupo punda mmoja, mfugo wangu p0ekee. Mbali, mashgribi, katikai bonde la mierezi lipo shamba dogo la zabibu na njugu.”


Nilijua vizuri, mama yangu alikuwa mwanamke maskini. Angenirithisha nini? Hakuna walakini, alikuwa na kitu kimoja chenye thamani kubwa kwangu. Nilijua ulimi wa mzazi umejaa matendo. Nikakinyany7ua kichwa changu.


“Najua huna kitu. Huna nyumba huna ng’ombe, huna shamba, lakini unao ulimi. Neno lako moja ni bora kuliko mali nyingi. Mama nipe radhi dunia hii ni ngumu.


“Umeomba.” Mama aliniambia akimaanisha niliomba jambo jema. Ilionekana alishaitayarisha radhi yangu tangu zamani ni mimi tu niliyechelewa kuiomba.


“Kwa vile wewe ni mwanamume. Ukawe shujaa ili ukawe na mwisho wmzuri.” Haya ndiyo mambo aliyonipa.


Niliuhisi mwili wangu ukijawa nwa nguvu za ajabu kwa maneno yale. Moyoni nilishangaa kumsikia mwanamke akitamka maneno ya kikume. Kwa maneno yale nikajua niliipata njai salama.


Usiku baada ya chakula tulitoka nje ya nyumba, na kukaa ju ya jiwe kubwa lililokuwa ubavuni mwa nyumba yetu. Ulikuwa ni wakati wa kiangazi chenye joto jingi. Juu angani iling’ara mbalamwezi.


Mwanga wa mbalamwezi uliufanya mji wa Baridos uliokuwa na nyumba nyingi za tembe upendeze mno. Mahali pote mjini zilikuwa zikisi8kika kelele za watoto wakifanya michezo wakati wa mwezi mpevu. Ambao walikuwa wakiambatana nao tangu kuandama na ulipozama ulizama pamoja na michezo yao. Kwetu sisi wawili huu ulikuwa ni wasaa wa kuvutia sana. Tulijiona kama tulikuwa juu ya mwezi.


Hapa, niliwakumbuka marafiki wa zamani wakati bado sijaondoka kwenda kuishi kwa babu marafiki hawa tulicheza na kuwa pamoja kila mahali. Mama alinipa habari zao; na kwamba walikuwa na hamu ya kuniona.


Licha ya muda mrefu tuliotengana sote watatu tuliamini siku moja tutaonana tena. Nayo majina ya marafiki hawa ni haya: wa kwanza alikuwa akiitwa Mnyamwezi; niliambiwa huyu tulizaliwa usiku mmoja; wa pili alikuwa akiitwa Migilimo; lakini sisi watoto wa mji wa Baridos tulimpa la “Nguzo.” Huyu wazee walituambia sisi tulimtangulia kidogo kuiona nuru.


Babu yake Mnyamwezi alikuwa mfugaji mkubwa. Alimiliki makundi makubwa ya ng’ombe, kondoo na mbuzi. Kila siku asubuhi Mnyamwzi aliyaongoza makundi haya ya mifugo malishoni. Baadaye mimi na Migilimo tulimfuata.


Mara nyingi tulimkuta bado akiwa njiani. Tukaungana naye na kuwa watatu. Hapa tukayaonogza makundi ya mifugo hata nyika iliyojaa majabali. Katika nyika hii nyasi zilikuwa nyingi hivyo mifugo ilitulia. Nasi tulifanya michezo yetu.


Tuliupenda zaidi mchezo wa mielekea. Muda mwingi tuliutumia kuucheza mchezo huu hata mara nyingti tuliisahau mifugo yetu. Tukapigana mieleka tukipimana nguvu na uzito. Migilimo alionekana kuwa hodari zaid ikatika mchezo huu. Ni wakati huu tulipompa jina la “Nguzo” jinsi alivyokuwa imara wakati wa kupigana mielekea mfano wa kisiki cha mpingo.


Ikawa kila siku tuirudishapo mifugo babu yake Mnyamwezi alituangalia na kusema, “mnapendeza kama maua,” akitufananisha na maua ambayo huzidi kuchanua bila kujali mbele kilikuja kiangazi ama mafuriko. Tulipokwisha kuingiza mifugo yote mazizini alituita na kutuuliza swali. Kupitia mifugo tuliyoichunga alifahamu tuliipenda dunia.


“Mwaionaje dunia?” Hili ndilo swali alilotuuliza kila siku tuwarudishapo kondoo.


Alianza Migilimo kulijibu swali hili: “Naona dunia imekaa tenge lakini bado iko katika mhimili wake, tena imegeuka rangi, imekuwa ya kijani. Imefanya mirija pande nne… Mirija inayodondosha maji mfano wa asali.”


“Nifumbulie fumbo lako,” mzee alimwuliza Migilimo.


“Kwa usemi huu nina maana dunia ni tamu kama asali.”


Kisha mzee alimgeukia Mnyamwezi na kumuuliza swali hilohilo.


“Naiona dunia imefanana na mbingu saba yenye uzuri usioelezeka”


“Nifumbulie fumbo lako,” mzee alimuuliza Mnyamwezi.


“Kwa usemi huu nina maana dunia ina raha kama ilivyo pepo.”


Iliwadia zamu yangu kulijibu swali hili. Niliyakumbuka maneno ambayo mama yangu zamani alipenda kuyakariri. Nilijua maneno hayo yalikuwa jibu kamili jinsi vile dunia ilivyo.


“Naiona dunia imefanana na giza la usiku wa manane, usiku wenye nuru ndogo ya mwezi na nyota.”


“Nifumbulie fumbo lako,” mzee aliniuliza.


“Kwa usemi huu nina maana dunia imejaa tabu na raha kidogo tu.”


“U-mtoto mwerevu,” mzee alinisifu. Sifa hii ndiyo inayonikumbusha siku hizo. Kisha mzee aliwageukia Mnyamwezi na Migilimo.


“Majibu yenu yanafanana na hadithi ya vipofu walioambiwa wautoe wasifu wa tembo baada ya kuupapasa mwili wake…”


Sasa ngoja nikusimulie jinsi mji huu mdogo wa Barodos ulivyochipuka. Mji huu ulichipuka zamani zaidi ya miji yote katika nchi hii isipokuwa mji wa Somondra.


Karibu theluthi nzima ya wakazi wake ni watu wa nasaba za mataifa ya mbali, wengi wao wakiwa ni watu weusi, wasafiri mashujaa wadinasi.


Katika mto ambao babu yangu aliufuata hata akafika katika mji wa Samondra, nyuma, mto uligawanyika pande mbili; upande mmoja ulielekea sehemu ya Mashariki na ule upande mwingine ulielekea sehemu ya kaskazini.


Hivyo mabaharia wengi waliopotezwa na upepo walijikuta wakifuata mto huu.


Walipofika mahali ambapo mto uligawanyika wale walioufuata upande wa kaskazini ndiyo hatimaye awalitokezea hapa Baridos; na wale walioufuata ule upande wa mashariki ndiyo waliokuja kutokeza katika mji aliokuwa anaishi babu yangu; Somondra.


Inasemekana mgeni wa kwanza kufika Baridos alipofariki fuvu la kichwa chake lilichukuliwa na kuhifadhiwa ndani ya msitu uliokuwa karibu na mji. Baadhi ya wakazi wa Baridos huenda whuko na kuliabudu fuvu hili.


Ndivyo ilivyotokea kwa wazee wawili, ambao walitokea mashariki ya Afrika. Babu yake Mnyamwezi na babu yake Migilimo. Babu yake Mnyamwezi yeye alitokea karibu na ziwa kubwa la Tanganyika.


Huyu alikuwa Mnyamwezi, tena akitokea katika ukoo maarufu wa Mtemi Milambo. Alipofika katika nchi hii alijiita jina la “Mnyamwezi.”


Babu yake Migilimo yeye alitokea pwani, katika mji wa Tanga. Asili yake ikiwa ni nyanda za juu kusini, sehemu za Uhehe. Akakulia katika pwani hii akijifunza uvuvi na hatimaye aje kuwa baharia.


Wote walichukuliwa katika bahari yenye pepo kali wakati walipofanya safari baharini. Hatimaye wakaja kutua katika nchi hii ya Somondra.


Basi katika usiku huu niliyakumbuka maisha yangu ya mwanzoni kabisa mwautoto wangu. Nikaamini maisha ya utot yalikuwa maisha ya pekee hapa duniani; maisha mataqmu lakini yasiyoonekana kwa mtoto wakati anayakabili.


Maisha hayo, sasa, kwetu yalikuwa yamepita. Wakati huu nilitaka kuufanya urafiki wtu wa utotoni uwe msingi kwa mafanikio yajayo.


Siku iliyofuata nikiwa nimekaa juu ya jiwe lililokuwa ubavuni mwa nyumba yetu, jiwe ambalo lilionyesha kuwa awali lilikuwa ni jabali kubwa lililomomonyoka kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa, niliangalia mbele na kumwona kijana mweusi kama giza akiwa na sura iliyofanana na dubu akija kwa mwendo usio na papara. Nyumba yake alifuatana na kijana mwingine mweusi mwenye macho kama ya mbogo.


Mabadiliko makubwa yaliyotokea katika miili yetu hayakutufanya tusahauliane. Mazoea makubwa ya zamani yalitufanya tunusane kama mbwa.


Nilimsikia Mnyamwezi aliyekuwa ametangulia mbele akisema maneno, nikayataga masikiko yangu nipate kusikia;


“Nakumbuka hapo zamani Umlele uliposema; “Sisi binadamu si kama milima, siku moja tutakutana,” Leo hii mabarobaro watatu waliotengwa na gtiza la dunia wameonana tena katika asubuhi tulivu mbele ya jiwe lililomomonyoka. Wamekuja kuziandaa silaha zao za jadi, kwani huko mbele kuna vita inakuja.”


Niliwaangalia Mnyamwezi na Migilimo nikaridhika na kuyaamini maneno ya wazee waliyotabiri zamani. Matabiri yao waliytafanya kulingana na jinsi vijana hawa walivyozaliwa.


Mnyamwezi mara alipozaliwa tu aliishikilia kwa mkono wake nondo ya uzani wa juu na kuinyanyua juu. Wazee wakatabiri kuwa ile ilikuwa ni ishara kubwa Mnyamwezi atakuwa na nguvu za kuuzuia mlima mkubwa usianguke.


Naye Migilimo mara alipozaliwa tu aliinyoosha mkono wake akilia apewe upanga uliokuwa karibu yake. Wazee wakatabiri kuwa siku za usoni kila atakapopita Migilimo na upanga patanuka harufu ya vibudu.


Maongezi yetu ya awali tulikumbuka maisha yetu ya zamani. Baadaye kila mmoja wetu alikuwa na malengo makuu aliyopanga maishani. Alianza Mnyamwezi;


“Mwenda bure si mkaa bure; ndivyo walivyoniambia wazee. Nami nauliza; yawezekana kuisubniri bahati kama mvua? Naam, yawezekana; lakini, mbona, hata mbegu hukimbilia mabondeni mahali penye rutuba, sembuse mimi mwanadamu..."”


Naye Migilimo alikuwa na mambo makuu aliyoyapanga katika ujana wake:


“Tembea uone ndiyo maneno waliyonipa wazee. Nami nasema, msahamu kwao ni mtumwa. Lakini, yanipasa kuondoka, kwenda kuiona dunia; na katika miaka yangu ya mwisho mwisho nitarudi, nije nilale na wazee wangu katika udongo mweusi wa nyumbani.”


Maneno waliyoyasema Mnyamwezi na Migilimo yalinipa nguvu. Nikazidi kugundua sote tulikuwa na akili moja; na mimi nikasema:


“Nimeambiwa iko nyota ngeni sehemu za Mashariki; lakini milima, mabonde na mawingu vimeificha nyota hii ya kijani.


Nitauchukua mundu na farasi wangu kwenda kuitafuta nyota hii kwa kuwa mimi ni mnajimu, zaidi, Migilimo akatukumbusha maneno ya wahenga yasemayo; mtu husifiwa kwa matendo atendayo wala si kwa maneno asemayo.


Hapa, sote watatu tuliyavaa mavazi ya vita, huku tukiwa tumesimama kando ya jahazi lililopepea tanga, tayari kusafiri bahari kuu.


Habari ya mwamba wa dhahabu ilibaki kuwa siri yangu. Niliutunza wasia wa babu. Sikumweleza mama yangu, Mnyamwezi wala Migilimo. Hata hivyo nilijua, wakati ungefika mambo yopte yangekuwa hadharani.


Siku saba tulizokaa na mama yangu zilionekana kama siku moja; na siku moja tuliyokaa na kina Migilimo ilionekana kama nukta moja.


Tulitamani kuishi pamoja siku zote, lakini ilikuwepo nguvu isiyozuilika iliyotufanya tutengane kwa mara nyingine, na kuendelea na safari isiyojulikana; kwani jioni ya siku iliyofuata mbele ya Mnyamwezi na Migilimo waliokuwa wanashuhudia nilikuwa nimekumbatiana na mama yangu mpenzi tukitakiana heri nyingine kwa maisha mengine yajayo.



MBEGU MBAYA YAPANDWA

Nilimkuta babu amedhoofu zaidi. Mifupa ya mwili wake ilionekana waziwazi. Alipozungumza midomo ilimtetemeka.


Ngozi yake ilizidi kusinyaa, na uso wake ulizidi kuwa mweusi. Ilionekana kana kwamba alipitiwa na kiwavi mbaya wakati nimeondoka! Nikapata mashaka kuwa babu yangu alikuwa njiani kuelekea nchi ya mbali.


Nilimpa salaamu nyingi kutoka kwa mama yangu, na kwamba amtarajioe mama mara baada ya kumalizika msimu wa zabibu.


“Maskini!” babu alihuzunika. “Kama angeyajua ya kesho angefanya hima aje tuagane. Oh! Naweza kufariki bila kumwona mwanangu mara ya mwisho!” Sauti yake ilikuwa dhaifu.


Alionekana kana kwamba mguu wake mmoja ulishatumbukia kuzimu. Kwa sababu hii moyo wangu ukatuta zaidi kwa hofu Nikaogopa. Nikijiaona nilikuwa bado mdogo kuirithi himaya ya babu.


Katika simanzi hili nikamuuliza mzee, “waweza kunionyesha jambo jingine?”


“Tulia, kitambo nitakuonyesha jambo jingine kubwa,” babu alinijibu.


Pamoja na mashaka haya, nilijua mauti ya wazee hayafiki mpaka wameutoa wasia wote.


Siku chache zilizofuata babu alizungumza nami mambo makubwa. Katika mambo haya ndipo ilpomea mbegu mbaya ambayo baadhi ya wazee walitabiri zamani.


“Mara ulipoondoka, alirudi Somondra mzee mmoja mkongwe, ambaye kwa umri ni makamo yangu,” babu yangu alianza kunisimulia.


“Ukimwona jinsi alivyo, amekwishakumalizika kama mimi. Mzee huyu aliondoka mara ya mwisho hapa Somondra wakati mimi ndiyo nimeingai tu umri wa mtu wa makamo. Katika maisha yake alipenda kusafiri huku na huko. Katika nchi. Alianza kusafiri tangu ujanani. Awali alisafiri na kurudi Somondra. Lakini safari ya mwisho imemchukua miaka mingi hadi leo kurudi. Mtu huyu kichwa chacke kimebeba mengi.


“Mzee huyu ni miongoni mwa ma-asadi wa nchi hii. Mara baada ya kurudi jambo la kwanza alilolitaka ulikuwa ni kuonyeshwa wzee wakongwe waliokuwa wamebaki. Alipopewa habari zangu alistaajabu mno! Akatamani kuonana na mimi.


Alitambua lazima lilikuwepo jambo kubwa lililoyavuta maisha yangu jambo ambalo nilichelea kuwaambia warithi wangu.”


Hapa, marafiki wa zamani walikutana. Wote wakiwa wazee sasa. Zamani, enzi ya ujana wote walipenda kusafiri. Mara hii walijikuta wakiwa pamoja katika njia nyingine safari ya mwisho.


Wakataka kuutayarisha usuhuba wao huko kuzimu. Wakaambiana yote waliyokuwa nayo mioyoni. Babu yangu hakuacha hata neno moja! Alimwambia jinsi ambavyo kupitia kwangu alipanga kulienzi jina lake; na kwamba mim ikUmlele nilikuwa njiani kuuendea mwamba wa dhahabu. Loo!


Walakini, roho ya uhasimu kwa mtu hasidi huchipua kwa neno lisilo hilo yoyote kumbe ulimi ndiyo adui mkubwa wa nafsi ya mtu! Hulitoa neno likasikika kati ya sikio la hasidi na kuuleta uhasimu.


Kumbe mtu hasidi ana umbo la kadiri, macho maangavu, na uso wa tabasamu! Neno tu ndilo huifichua roho yake ya ubinafsi. Hasidi hana sababu.


Maneno yale kidogo kutoka ulimi laini usio hata na mfupa yaliuleta uhasimu mpya. Ulio imara kama mwamba. Uhasimu mkuu baina ya wazee wawili. Uhasimu ulioendelea mpaka huko kuzimu walikokwenda na kubaki pia katika vizazi vyao vilivyokuwa hai. Njia nzuri waliyokuwa wakiitafuta kwa uhusiano mwema milele iligeuka na kuwa njia mbaya kwa uhasama milele.


Ukoo aliokuwa akitokea mzee huyu ambaye kwa jina alikuwa akiitwa soyelo, lakini kwa ajiilo ya kupenda kusafiri alipewa jina la “Msafiri.”


Ulikuwa ni miongoni mwa koo mbili maarufu za kifalme katika nchi hii ya Somondra koo ambazo hapo zamani. Zilipigana vita mfululizo kuwania madaraka.


Vita baina ya koo hizi vilikwisha baada ya makubaliano kuwa nchi itaongozwa kwa mapokezano ya madaraka kati ya falme mbili hizi; kwa kipindi cha miaka minne minne.


Wakati huu ndipo ulipokuwa ukiwadia muda kwa ukoo wa mzee huyu kuishika hatamu ya nchi.


Ukoo wa wadalaki aliokuwa akitokea mzee Soyelo ulikuwa ndiyo ukoo wenye nguvu zaidi.


Ulikuwa ndiyo chimbuko la majemadari wengi wa vita katika Somondra, wakaazimia siku moja kuitawala Somondra yote ki-imla. Miongoni mwa majemadari wakuu wa ukoo alikuwa ni Abobo ambaye pia alikuwa ni mjukuu wa mzee Soyelo. Huyu ndiye aliyekuwa shujaa wa vita,


Zamani, kabla ya mzee huyu mpenda safari hajaondoka kwa safari yake ya mwisho alikuwa mzee mmoja kikongwe zaidi: Inaaminika hadi leo hajatokea mtu aliyepata kuishi muda mrefu namna hiyo katika Somondra yote.


Kutokana na umri wake mkubwa ndiye mtu aliyeifahamu viozuri Somondra. Alivijua vizazi na vizazi; tangu koo kubwa na maarufu hata koo ndogo zaidi.


Yeye alikuwa anatokea katika ukoo duni usiotambuliwa na wasomondra. Ikawa kila mgani aliyefika na kuishi Somondra mzee huyu akapenda kumfahamu zaidi. Akabashiri kuwa siku moja Somondra itaongozwa na mgeni.


Kwake, wageni walikuwa kama taa ya mshumaa iliyo maarufu hata kushinda karabai yenye mwangaza mkubwa. Labda ubashiri huu ndiyo uliompa nguvu zaidi babu yangu! Bahati mbaya sikuwahi kumuuliza juu ya jambo hili; hata hivyo hoja ya babu haikuwa juu ya mamlaka!


Si babu yangu mzee Umlele, ambaye hakuwa mzalia halisi wa Somondra, ambaye mzee Msafiri, Soyelo, alimpigia upatu, sik umoja mkuu katika Somondra, akasema; “Watu hawa watakuwa mashahidi tu katika mapambano makubwa ya koo mbili mashuhuri kuwania uku wa Somondra;”


Basi kwa vile mzee Soyelo muda mrefu wa maisha yake aliutumia akiwa ughaibuni alikutana na watu wengi; hivyo alijua mengi; hata habari ya mwamba wa dhahabu aliifahamu.


Akaazimu moyoni kuwa kabla hajafariki dunia atarudi katika nchi ya baba zake na kukiambia kizazi chake kilichobaki habari ya hazina ile kuu. Alijua miongoni mwa watu katika ukoo wake wangemudu kwenda katika msitu ule hata kuutwaa mwamba wa dhahabu. Huo ungekuwa ni mwanzo wa fahari mpya ya ukoo wake mashuhuri.


Alijua, nilikuwa nikijitayarisha kuuendea mwamba wa dhahabu. Je, iwapo ningeitwaa dhahabu na kurejea nayo, ni yepi yangejiri? Alifikiri…, babu yake alifariki na kuzikwa hapa Somondra; na mababu wa mababu zake wote walizikwa katika udongo huu. Yakini, yeye ndiye mtu pekee aliyepaswa kustawi na kushamiri katika Somondra.


Alimfikiria na babu yangu… ijapokuwa alikuja zamani hapa Somondra, bado alikuwa akihesabiwa mtu mgeni. Halikuwepo kaburi hata moja la ukoo wake! Halikuwepo baba, mama wala nasaba yake yeyote mahala hapa! Kwake atabaki kuwa mtu mgeni siku zote.


Akijua mambo ambayo yangejiri endapo ningeitwaa dhahabu, alisema; “Hatutauache mtende uote na kuchanua kwenye shamba la ngano. Tutaungoa na kuutupa mbali, nje ya shamba ungali mdogo.”


Babu alifahamu nilikuwa mtende uliotakiwa kung’olewa na kutupwa nje ya shamba; na yeye aakasema:” Kati ya wakulima wote wa Somondra sijamwona mkulima stadi, mwenye jembe imara la dhahabu, jembe pekee liwezalo kuung’oa mtende wenye mizizi ya chuma.”


Hapa, mikono yangu mielekevu, mikoiliyo na macho, iliyojaa pendo ilishurutishwa kutakabari, kupata upofu, na kuwa na ukatili usio kifani. Hata hivyo hii ilikuwa ni nyota inayochomoza; na hii ndiyo iliyokuwa njia yake! Ilikuwa ikipigana na wingu zito ipate angaza ng’ambo ya pili, siku zote wingu hupita ukiacha nyota iking’aa.


Bado ninakubuka siku ile, wakati mzee Soyelo alipoyasagasaga meno yake kw ahasira pale babu yangu aliposeham kuwa wakulima wa Somondra wasingeweza kuung’oa mtende wake.


Hapa ndipo nilipomjua mwanadamu; kwa kiasi kikubwa amejawa na ubaya. Ninayaamini maneno aliyoniambia mzee wangu mapema; “Si wazuri Binadamu duniani; wana vituk vya sumu kali kushinda ya nyoka; kicheko chao kikubwa kimeficha maovu makubwa; moyo wao wa tamaa umejaa hila na hadaa!”


Wakati mmoja nalifikiri kuwa matendo yote atendayo mtu ndiyo huleta jumla ya hesabu kamili ya matendo alotenda mtu maishani; lakini kumbe tendo moja atendalo mtu kabla ya mauti ndiyo huleta jumla ya hesabu kamili ya matendo yote aliotenda mtu maishani! Kwangu mzee Soyelo, daima atafanana na nyoka mwenye sumu kali aliyetaka kuniangamiza.


Hapa uhasimu uliota mizizi na kuchanua. Ukapokewa na kizazi cha babu yangu na cha mzee Soyelo; hata hivyo wazee hawa hawakukishuhudia kilele chake.


Ndani ya ukoo wa wadalaki, kurudi kwa mzee Soyelo kulifanya ukoo ufanye tamasha kubwa, kwani mzee aliyeyabeba mambo mengi ya ukoo alikuwa amerejea. Walimtarajia awape mambo mapya ya mwisho ili waujenge ukoo hata hatamu ya juu.


Akimtumaini Abobo, jemadari mkuu, na shujaa wa vita, mzee Soyelo hakutia mashaka kwa ushindi huu thabiti wa mwisho.


Sasa, jemadari huyu mkuu pamoja na majemadari wengine walikuwa wanauongoza ukoo maarufu wa Wadalaki kwenda kumwangamiza mjukuu wa mzee Muungwana; wakiyachukua majembe na sululu kwenda kuifukua mbegu ya mtend iliyosiwa katikati ya shamba la ngano.


Kwa ajili ya mambo haya yote babu yangu akaniambia,. “Umlele, huu ni mwanzo wa mabaya; na hii ndiyo njia ya ukuu wetu. Nasimama katika vita hii nikiwa dhaifu ingawa. Wewe ndiwe ngano na upinde wangu. Najua Mungu anao upendeleo kwa watu waungwana.”


Sikuweza kusema neno ila tu nilishangaa, jinsi gani ningeweza kusimama na kukaniliana na jeshi imara kama lile! Nikaona kana kwamba babu yangu alikuwa akinitoa kafara.


Nikamtazama mara kadhaa nikifikiri pengine angeyatangua mawazo yake; lakini alionekana hakuwa na jambo jingine mbali na njia aliyonionyesha. Hata hivyo moyo wangu ulikuwa na jambo jingine bado kutoka kwake.


Hapa niliwakumbuka akina Migilimo na Mnyamwezi. Walikuwa hasa, wanaume wakazi waliotatikana. Nikafikiri, endapo ningewaambia habari hii wangenishika mkono wa pongezi, kwani kama kilikuwepo kitu walichokitamani sana basi ilikuwa ni vita. Tungeufanya mpambano mkubwa na kufa kiume. Nikapanga kuondoka kwenda kuwajulisha habari hii.


NAPITA KATIKA DARAJA

Kama nilivyokwisha kusimulia huko nyuma kuwa katika nchi hii ndogo ya Somondra ulikuwepo mto mkubwa. Mto huu ulikuwa karibu kabisa na mahali tulipokuwa tunaishi na babu yangu. Mto huu ulikuwa ukiitwa Merei.


Wakazi wengi wa nchi hii walikuwa ni wavuvi. Waliendesha maisha yao ya kila siku kwa kutegemea uvuvi kwenye mto Merei, mto uliofurika samaki.


Katika nchi hii uvuvi ulianza zamani, ukawa maarufu hata nchi yote ya Somondra ikajulikana kama nchi ya kivuvi. Kutoka chemchemi kuu ya mto huu, mto ulienda mbele ukiizunguka karibu nchi yote ya Somondra.


Merei, jina la mto huu lilikuwa na maana ya “nguvu nyeusi.” Inaaminika kuwa katika mto huu ndimo ilipokuwemo siri ya utajiri.


Hakuna mtu aliyeweza kutajirika bila ya kuvua kwanza kwenye mto huu. Inaaminika matajiri wote wa Somondra utajiri wao ulikuja baada ya kufanya uvuvi kwenye mto Merei. Imani hii babu yangu hakuiamini.


Watu wengi wakaanza uvuvi tangu utotoni. Baada ya hapo wengi waliiacha kazi hii, lakini wakiwa tayari wamekwishakupitia sehemu muhimu waliyoiamini kuwa ilikuwa ni daraja lililowaunganisha na utajiri.


Siku ile alipokuwa akija katika nchi hii, babu yangu aliutazama mto ule na kuuona ulijaa samaki. Akatamani siku moja kuwa mvuvi kwenye mto huu. Miaka michache baadaye alikuwa mvuvi mashuhuri.


Wakati babu yangu anaanza uvuvi mama yangu alikuwa bado jajakuwa msichana; hata hivyo aliweza kumsaidia baba yake kuwatayarisha samaki kabla ya kuwahifaddhi na hata kuwauza.


Utashangaa, vipi babu yangu aliweza kuzimudu kazi mbili kwa pamoja! Kazi ya uwindaji na kazi ya uvuvi! Ndiyo, alizimudu barabara. Baada ya mawindo mazuri alikuwa na desitry ya kupumzika siku kadhaa bila ya kwenda mwituni. Ndipo alipokuwa akiutumia muda huu kwa shughuli ya uvuvi.


Alikuwa na mitumbwi mitatu, aliyoitumia kuvulia, akitumia nyavu. Yeye alikuwa akitumia mtumbwi mmoja, na mingine miwili alikuwa akiikodisha kwa malipo ya samaki.


Wakati mto ulipofurika alitega hata migono ili kujipatia samaki wengi zaidi. Wakati mmoja zamani alifanikiwa sana katika kazi hii.


Zamani, wakati babu yangu ndiyo anauanza uvuvi alikuwa akivua peke yake kwenye mtumbwi.


Baadaye aliwapata vijana wa Kisomondra, akaandamana nao akiwafundisha uvuvi, kabla sijakuja mimi na kuwa mshirika wake mkubwa. Wakati mimi ninaanza kuishi naye alikuwa amebaki na mtumbwi mmoja tu.


Tukawa tukitoka nyumbani wakati wa Magharibi kwenda mtoni. Tukatega migono, na usiku ulipoingia tuliingia ndani ya mtumbwi na nyavu zetu na kuupeleka mtumbwi mbali mtoni sehemu iliyokuwa na samaki wengi.


Asubuhi tulirudi nyumbani na samaki wengi. Kipindi cha mwezi mpevu hatukuvua usiku, badala yake tulikwenda wakati wa asubuhi kuiangalia migono yetu tuliyoitega. Mara moja moja tulivua wakati wa mchana.


Miaka ya uzee ilipowadia babu yangu alipungua nguvu. Mtumbwi na migono yote niliimiliki mimi. Kwa vile babu yangu alikuwa ni mvuvi mashuhuri nilimpata mshirika mwingine.


Huyu alikuwa ni mzee mmoja ambaye awali aliwahi kutumia moja ya iliyokuwa mitumbwi ya babu. Nilifanya hivi kwa vile katika ujana wangu nilipenda sana kuwa pamoja na wazee.


Walakini, sasa, mambo yamebadilika, msimamo na matarajio yangu ya kuwa mvuvi na mwindaji aliyefanikiwa zaidi vinaonekana kutofaulu.


Yanibidi kuziacha kazi hizi mbili nilizozipenda. Naziacha kazi hizi ili niitetee heshima yetu na jina zima la Umlele. Mabahaluli wa Kidalaki wanaiwinda roho yangu sawa na jina letu wapate kuviangamiza. Sijui kama huko mbele nitajarejea tena kuzifanya kazi hizi!


Je, itajawezekana kwa mfanyabiashara tajiri kuuchukua upinde na kwenda mwituni kuwinda Kurungu? Au kuupanda mtumbwi na kwenda kuvua? Mapenzi yana nguvu kubwa, wala hakuna kitu kinachoweza kuizuia nguvu hiyo. Nami katika siku hizo nitaipima nguvu kubwa ya mapenzi.


Jioni moja nilikuwa mtoni kwa ajili ya uvuvi. Kama kawaida hali ya hewa ilikuwa ni ya upepo uliokuwa unavuma taratibu na kuongeza utulivu wa mto.


Nikiwa ufukwendani nilitazama juu na kuyaona mawingu mazito meusi yaliyokuwa yamelijaza anga lote. Hali hii iliupa msisimko mwili wangu; msissimko ambao sikuweza kuubainisha.


Nilinyanyuka kutoka chini nilipokuwa nimekaa karibu na mtumbwi. Nikajaribu kuusukuma mtumbwi wangu kuelekea kwenye mchanga lakini ulikuwa mzito kwa ajili ya kujaa samaki wengi.


Niliuacha mtumbwi ule na kutembea mbele kando ya mto nipate kuuona upande mwingine wa mto aliokuwepo mzee wangu aliyekuwa mshirika wangu katika kazi hii.


Alikuwa akitega migono. Mara nyingi nyakati za jioni kama hizi wavuvi huwa ndiyo wanaanza kufika mtoni. Hata wakati huu walikuwepo wachcahe tu ambao niliwaona ng’ambo ya pili ya mto.


Wengi wao walikuwa ni wale wazee ambao uvuvi kwao yalikuwa ni mapenzi yaliyokithiri. Haikupita hata siku moja bila ya wazee hawa kufika mtoni, japo kuuangalia mwelekeo wa upepo tu.


Ni ajabu kubwa sana katika nchi hii jinsi vile watu walivyokuwa wakiuhusudu uvuvi! Walikuwepo baadhi ya wazee waliouhusudu uvuvi hata wakatoa wasia kuwa watakapofariki sharti wazikwe pembezoni mwa ufukwe.


Upande wa mashariki wa ufukwe wa mto huu yalikuwepo makaburi matatu ya wazee wavuvi wa zamani ambao waliagiza kuwa sehemu hii kuwa mahali pao pa kuzikana, ili kudhihirisha kwamba wao walikuwa koo maarufu za kivuvi.


Kabla sijafika ng’ambo mahali ambapo pangeniwezesha kumwona mzee, alitokeza karibu mbele yangu.


“Zamani,” mzee alizungumza “tulivua samaki kwa ajili ya chakula tu; hapakuwa na soko kubwa, hivyo samaki walizaana na kuongezeka sana. Siku hizi mambo yamebadilika. Watu wameongezeka, na kufanya idadi ya wavuvi kuongezeka pia. Ndiyo maana samaki wamepungua mtoni.”


Pamoja na upungufu huu ambao wazee waliuelezea, mimi bado niliwaona samaki walikuwepo wengi mtoni. Lazima siku za nyuma mto hu ulifurika samaki!


Ilikuwa ni kawaida baada ya shughuli ya uvuvi mwishoni tuligawana samaki. Nilitengeneza mafungu mawili kutoka samaki waliokuwa ndani ya mtumbwi.


Nikishamaliza niliwatia samaki kutoka lundo moja kati ya mawili ndani ya Jumu langu maalumu la kubebea samaki. Nikauchukua na upinde wangu ambao wakati hu sikuacha mbali nami. Nikaondoka nikimwacha mzee akiukarabati mgono mmoja.


Nilitembea taratibu kutoka ufukweni, nikipi8ta katikai njia nyembamba kuelekea mjini. Baadaye nilifika sehemu iliyokuwa na mianzi mingi.


Njiani kote nilikuwa nikiwaza jisni vile Wadalaki walivyokuwa wananiwinda sasa. Waliniwinda kama vile mimi na babu tulivyokuwa tunamwisnda mbogo aliyejeruhiwa mwituni. Baada ya mianzi kwisha, njia ilitokeza kilimani.


Mbele ya Kilima hiki ilifuata tambarare iliyojaa changarawe. Kutoka mahali hapa sehemu kubwa ya mto ilikuwa inaonekana waziwazi. Nilisimama na kugeuka nyuma kuangalia mtoni.


Japo giza liloishatanda, niliweza kumwona vizuri mzee mvuvi akiwa bado amekaa ufukweni juu ya mchanga akiurudisha vizuri mgono wake. Kisha niliendelea mbele. Bado wavuvu wanaovua wakati wa usiku walikuwa hawajaanza kupita kwa wingi. Nilikutana na wawili, watatu wakishuka taratibu.


Ukiondoa wavuvi hawa wachache niliokutana nao njia yote ilikuwa kimya. Hata ndege walishatulia matunduni mwao. Kwa ajili ya utulivu huu hatua zangu za taratibnu zilizsikika zikifanya kishindo kikubwa. Nilihakikisha upinde wangu ulikuwa mgongoni.


Upinde ambao babu yangu aliupa jina la “Bnamanyala,” akiufananisha na pinzi zilizowapa sifa kubwa mababu zake kule Mafia.


Niliendelea mbele tatiabu; lakini kitambo, macho yangu yalikutana na kitu kigeni kilichokuwa mbele yangu. Nikatazama vizuri huku nikisaidiwa na mwanga wa mbalamwezi na kuona kitu mfano wa mwamba mdogo mweusi ukiwa umesimama pembeni mwa njia, kushoto kwangu.


Nilihakikisha, mwamba ule ulikuwa ni mgeni mahali hapa. Sijapata kuuona bado! Kutoka mahali ulipokuwa mwamba huu hadi mahali nilipfoka sasa ilikuwa yapata hatua zangu hamsini.


Mwamba ule uligeuka na kuanza kusogea karibu na njia. Mbele ya jiwe moja kubwa lililokuwa kando ya njia, mwamba ule ulisimama na kukaa juu ya jiwe hilo.


Nilitambua, kitu kile haukuwa mwamba, bali mwanadamu. Mwendo wake ulidhihirisha. Bila shaka alikuwa akijitayarisha kusalimiana na mvuvi. Kutokana mahali alipokuwa amekaa ju ya jiwe uso wake aluelekeza njiani.


Hatu zangu bado zilikuwa zinatoa kishondo, mfano wa kishindo cha simba mwenda pole,. Nilipomkaribia niligundua alikuwa amevaa mavazi ya kipiganaji akiwa na silaha mikononi.


Nilikigeuza kichwa changu na kumtazama, kisha nikamsalimia. “Amani na iwe kwa mpiganaji na kwa mvuvi mpita njia.” Mtu huyuya libaki kimya bila kuitikia salamu yangu.


Nikamchunguza vizuri; kichwani alivaa kofia ya ngozi ya chui; vazi lake lilikuwa la ngozi ya simba; kiunoni alijifunga mkanda wa ngozi ya Chui. Mkono wake wa kushoto alikuwa na ngao, na kwenye mkono wa kuume alishikilia fumo. Kiunoni aliuchomeka upanga. Vazi hili lilikuwa linavaliwa na wapiganaji vijana wa Kidalaki.


Mimi nilikuwa nimevaa nguo zangu za kivuvi nikiwa na upinde mgongoni.


Nilikuwa karib ukumpita mpiganaji huyo wakati aliponisemesha.


“Wewe unayejiita mvuvi, simama. Muda huu ninapozungumza nimeushikilia uhai wako.”


Nilijifanya kiziwi na kundelea mbele. Mungu pekee ndiye aliyeushikili auai wangu.


“|Wwe ni kiziwi!” Alifoka. “Iwapo hutaitii amri yangu nitakukamata na kuikata hiyo shingo yako. Nimetumwa nikukamate na kukupeleka ukiwa hai; na mim indivyo ninavyotaka; lakini ikiwa hutaki nikupeleke ukiwa hai, basi nitakupelekea ukiwa mzoga! Damu yako ataulizwa mzee Umlele,” alikuwa na sauti nyembamba iliyoukata mithili ya kiwembe kwenye kiganja cha mkono utulivu huu mkubwa wa usiku.


Wakati huu alikuwa amenyanyuka na kuanza kunifuata.


Nilijua huyu alikuwa ni mpiganaji mzuri. Akiwa ameaminiwa na majemadari wake ilimpasa aupate ushindi apate kutuzwa nishani katika jeshi lao. Mimi ndiye niliyekuwa kipimo kwake apate kwa nishani yake hiyo ya juu!


Sauti yake na mwndao wake vikanifanya nimwondolee mzaha mtu huyu. Nikasimama. Nikaamua kumpandisha hasira. “Wewe ndiye mwari uliyetolewa kwangu nikupose? Karibu, njoo nikupeleke kwa babu yangu mzee Umlele akakuone.” Maneno yangu machafu yalimtia jazba.


Akavurumka kama nguruwe mwenye watoto. Nikageuka vizuri kumkabili nguruwe huyu aliyekuwa hatua chache tu mbele yangu.


Nilimsikia anaanza kuunguruma, akijaribu kunitisha.


Mimi nilibaki nimesimama, Banamanyala akiwa bnado mgongoni huku mkono nikiwa na jumu langu la samaki.


Kutokana na maelezo yake nilijua hakupewa idhini ya kuniua.


Alinisogelea karibu kabisa, akajifufutua na kunisukuma kwa ngao yake. Misuli ya mikono yake ilijaa nguvu. Nikapepesuka na kuanguka juu ya mawe. Jumu langu lililokuwa na samaki likadondoka huku samaki wwengi wakitapaa chini.


Niliupeleka mkono mgongoni na kumkuta Banamanyala bado yupo. Nikasimama na kumwona adui yangu akijitayarisha kunishambulia tena, huku akiniamuru niongoze njia kuelekea ngome kuu ya Wadalaki.


Hapa, sikusita tena, nilijua shambulio lake jingine litakuwa kubwa litakalonilewesha. Nikarusha teke na kuipiga barabara kwa uwayo wa mguu wangu ngao yake. Teke langu lilipimwa kwa uzani wa juu.


Ngao ile ilichomoka toka mkono wake na kutua kwenye paji la uso wake. Pigo lililomfanya aione mbingu ilikuwa na miezi saba. Akaweweseka na kuanguka mbali na ngao yake lakini bado alikuwa na fumo mkononi na upanga kiunoni.


Pigo langu llimtia aibu kubwa akataka kuifuta aibu. Hapa, alionekana hakuijali tena amri aliyokuwa amepewa na waku uwake ya kunipeleka nikiwa hai. Kutoka chini alipoanguka akanyanyuka na kuvurumka, huku akiwa amelikamata fumo lake barabara kwenye mkono wake wa kuume.


Mwili wangu ulishapata joto. Nilikuwa mwepesi. Nikanesa. Fumo lake likanikosa na kwenda juu ya jiwe lililotoa cheche za moto. Ilimbidi adui yangu afanye kazi ya ziada. Kosa alilotarajia kulifuta lilizaa mtoto.


Sasa adui yangu alibaki na silaha moja; upanga uliokuwa kiunoni. Wakati hu alikuwa ameshasimama imara. Akavuta hatu mbili nyuma na kusimama. “Nilitumwa nikupeleke ukiwa hai, lakini kwa ajili ya ukaidi wako. Sasa nitakupeleka ukiwa mzoga,” alijipa matumaini ya ushindi.


Niliyatazama makosa yangu ambayo yangewza kuutoa ushindi rahisi kwa mtesi wangu na kuyarekebisha. Nikasimama imara kwa utetezi.


Akauchomoa upanga wake toka kiunoni na kujiandaa kunishambulia. Bahati mbaya hakuwa na shabaha kabisa! Au pengine ni kwa ajiil ya ustadi wangu! Upanga wake ulinikosa na kupiga chini ambapo ulizama na kubaki ampini tu.


Hapa nikamkamata Banamanyala. Nilijua hata yeye alikuwa akiwashwa kwa hasira. Nikavuta hatua tatu nyuma. Nikajikunja huku macho yangu yameutazama moyo wa adui yule. Nifanyapo hvi huwa sikosi shabaha mwilini. Vazi lake la ngozi ya simba halikuwa kiziizi kwa Banamanyala. Mshale ule ulizama katikat5I ya moyo wa audi huyu. Akatoa yow3e refu wakati anabisha hodi kuzimu, wanyama wa mwitu walikuwa wameishaitia ganzi mikono yangu. Nikauchomoa upanga wake toka ardhini na kukikata kichwa cha Mdalaki huyu.


Mara hii huruma ilikuwa mbali na moyo wangu; katika masikkio sikuisikia; katika macho sikuiona; katika miguu sikuikanyaga; na mikono ulikuwepo upanga. Ilikuwa imekimbia hadi mbungu ya saba mahal pasopofikika. Nilishangaa kabisa jinsi vile huruma na msamaha vilivyouamsha uadui dhidi ya moyo wangu! Uwanja wote ulitapakaa damu. Damu hii ilinibadilisha ilinigeuza shetani.


Nilikichuku akichwa kile ambacho ulimwi wake ulikuwa umetoka mdaomoni na kuburzika ju ya mchanga.l Nikakiweka juu ya jiwe alilokuwa amelikalia awali; na mwili wake niliulaza chihi ya jiwe hili.


Ulikuwa ni ushindi mdogo na hatua yangu ndogo ya awali ya kuchipuka kwangu. Ingawaje: ilikuwa ni hatu athabiti. Damu hii ilibaki kuwa kubukukmbu mbaya katika maisha yangu ya awali ya ujana wangu.


Niliweza kuuona mchuruziko wa damu uliokwenda moja kwa moja na kutakapaa kwenye samaki wangu hata kwenye jumu. Nikawaacha samaki wale na kuondoia.


Njiani niliikumbuka damu ile. Mwili ulinisisimka. Nikaona baridi kali. Usiku huu niliuogopa. Dhahiri nilijiona nikianza kupita katika daraja la babu; “Wakati mwingine damu ni daraja usiloepukika kuufikia ukuu.”


Nilipofika nyumbani moja kwa moja nilikwenda kwenye nyumba kubwa, nyumba aliyokuwa analala babu yangu. Nilikwenda hata nikaukaribia moango,. Nihlijua muda huu alikuwemo ndani akiwa amelala kwani katika uzee wake huu alipenda kulala.


Sijui katika muda huu alikuwa anawaza mambo gani? Labda alikuwa akiyawaza maisha yake ya zamani kule kilindoni.


Mafia, mpaka alivyokuwa mzee sasa mwenye mvi tele! Bila shaka pia alimkumbuka baba yake, jumbe wa Kilindoni. Jumbe aliyeheshimiwa na kupendwa sana.


Hapana shaka pia alimkumbuka mjukuu wake mpenzi ambaye muda huu alikuwa ameishikilia mundu kulitetea jina lake. Walakini mimi nilikuwa nikiliwaza jambo moja; daraja hili kubwa la babu! Nikiliona lilikuwa ni daraja kubwa lenye kina kisichokuwa na mwisho!


Nilifika katika mlango wa nyumba yake uliokuwa wazi. Ndani ya nyumba ilikuwa ikiangaza taa chakavu ya kandili. Nilitaka kwenda kumsimulia jinsi vile nilivyokutana na Mdalaki yule na namna nilivyompiga hata kumchinja pengine angenipa mkono wa pongezi, na kuizidisha imani yake kwangu.


Nilishangaa kutomkuta babu ndani ya nyumba yake. Ndani ya nyumba hii sikuiona dalili ya uwepo wake. Ingawaje hivyo,. Sikuacha kuchakura chakura vitu ndani ya vyumba kumtafuta/. Nikadhani kuwa pengine akili yangu ilipatwa na jinamizi lililoyazuia macho yangu yasimwone babu yangu. Nikayakodoa macho yangu juu ya ngozi yake aliyokuwa analalia, wala sikumwona nikashangaa wapi alikwenda babu yangu?


Nyumba zote zilikuwa shwari, na vitu vyote vilibaki salama. Niliuona hata upinde wake uliokuwa kulia mwa ngozi.


Upande wa kushoto wa ngozi ulikuwepo upanga wake mkubwa uliokuwa umeegemezwa ukutani. Pia kilikuwepo na chungu alichokuwa anahifadhia dawa zake. Chungu hiki kilikuwa wazi, nikaenda na kukifunika.


Awali, sikujishughul;isha kwenda kumwangalia ndani ya nyumba hizi, kwani zilibaki zikiwa zimefungwa; isitoshe wakati hu hakuwa na mazoea ya kuingia humo. Ilinibidi nikahakikishe.


Nikatoka kwenda kwenye nyumba iliyokuwa ya mama. Nikaingai dnani lakini kulikuwa na giza tupu! Nijaribu kumwita lakini hakuitika. Nikarudi kwenye nyumba kubwa kuchukua taa, kisha tena nikarudi kwenye nyumba ile na kumulika ndani mwote. Bado sikumwona. Hata kwenye nyumba yangu nilimwangalia na kumkosa.


Zamani, katika miaka yanguy ya mwanzo ya kuishi naye, alipenda kutoka saa za magharibi akaenda hata mjini mahali palipokuwa na uwanja ambako watu wengi walikusanyika na kutoa mihadhara. Hata hivyo ulikuwa umepita muda mrefu tangu alipoacha kuhudhuria mihadhara hii.


Isitoshe, usiku ulikuwa mpevu sasa, hakuna mhadhara ambao ungedumu mpaka muda huu. Vile vil esikutaraji tena endapo angethubutu kwenda huko na kutoa mhadhara, kwani huenda angejikuta anavuka mpaka wa maneno kama ilivyotokea kwa mzee Soyelo; hivyo akazidi kufanya mwaliko wa sherehe asijue kuwa sherehe yenyewe ilikuwa ni ya matanga ya mjukuu wake!


Nikafikiria zaidi…! Je, iliwezekana kuwa aliuawa? Nani angemuua? Jambo hili halikuwa rahisi. Umri mkubwa aliokuwa nao hakuna mtu ambate angethubutu kumdhuru. Wadalaki waliamini kuwa mtu ambayte angeyafupisha maisha ya mtu mzee hata yeye asingekuwa na maisha marefu. Wadalaki waliwaogopa wazee.


Sasa ilikuwa yapata katikati ya usiku nikiwa bado sijamwona babu yangu.


Nikakumbuka wakati wa mchana nilipomwona akijikiokot kwenda kutega mitego kwenye bustani. Nikatoka kwenda kumwangalia huko, lakini pia hakuwako. Nikamtafuta kila mahali katika makao haya bila kumwona.


Sasa nilichoka na kukata tamaa. Nikaenda kwenye chumba chake na kukaa juu ya ngozi nikimsubiri. Nilikaa hapa mpaka nikachoka. Hakika nilishindwa kutulia sehemu moja. Nikatoka nje na kuanza kumwita, sehemu zote zilibaki kimya. Nikafikiria labda hii ilikuwa ndiyo namna wazee wakongwe wanavyotoweka.


Nikawaza… sasa nitabaki pekee katika himaya hii maarufu. Nitabaki nikiitegemea akili yangu kuniongoza. Akili iliyojaa upofu! Nikaogopa.


Nikarudi ndani ya nyumba yangu. Mara nilipoingi nikaanza kulia; nikalia kwa sauti kubwa nikimlilia babu yangu.


Niliponyamaza ilikuwa yapataq usiku wa manane. Nikatoka nje na kusimamk akatikati ya nyumba hizi. Katikati ya usiku huu na nyumba hizi nikaon kitu kigeni katika macho yangu na himaya hii.


Mbele yangu niliona mfano wa shetani mweusi akija kuelekea nyumba hizi. Niliyakodoa macho yangu yapate kunisadikisha katika jambo hili geni.


Awali nilifikiri akili yangu ilipatwa na uchakaramu kwa ajili ya kumpoteza babu yang, lakin bado ilikuwa timamu. Sikukosea hata kidogo. Jitu hili kubwa ambalo katika mbalamwezi hii lilizidi kuonekana jeusi lilikaza mwendo kuelekea himaya hii.


Nilijua kuwa ni shetani mnyongaji tu ndiye ambaye huonekana katikati ya giza, nilijiona nilikuwa katika hatari nyingine. Niliuona usiku huu ulikuwa usiku mkuu.


Nisingekimbia. Mimi ndiye niliyemiliki himaya hii. Ilinipasa kuilinda.


Nilibaki nimesimama katika giza nene macho yangu yakiwa yamemtazama mgeni huyu mkubwa aliyezidi kuvuta hatua kunisogelea.


Nilijua mtu huyu hakuwa mwema. Nilijiandaa kukabiliana naye. Ijapo ubaya hulipwa kwa wema, wakati mwingine ubaya shariti ulipwe kwa ubaya.


Alipofika karibu nami nikakifunua kinywa changu kumkarbisha; “Karibu jemadari mkuu katika himaya hii maarufu yenye nyumba za mawe na bustani ya matunda.


Karibu kwa vita, kwani, kamwe simkiabishi jemadari usiku wa manane nba kumkumbatia kumbatiao la kirafiki. Daima mtu wa aina hii ni adui.” Sauti yangu ilifanana na sauti ya radi jnsi inavyozilinda mbingu.


Pasipo kutamka neno lolote mgeni huyu wa ajabu alizidi kunijongelea akizidi kujikaribisha. Mimi nilibaki nimesimama nikimsubiri mgeni huyu ambaye kimya chake kikubwa kilishanitangazia vita kuu.


Mwanzo wa bustani, kuzifikia nyumba zangu mgeni huyu aliongea:

“Abobo Abobo! Jemadari mkuu,” na jemadari wa majemadari.


Jemadari wa jeshi la Kidalaki linaloitwa “meno ya mamba” Leo nami nimekuja kwa sonara wala si sonara wa kukata dhahabu na lulu bal isonara wa kukata vichwa vya watu.


Nafurahi kumkuta sonara huyo akiwa nje ya nyumba zake za mawe katika usiku huu mkuu, akimsubiri Abobo, mimi Abobo nasema nipo tayari kwa mapambano. Je ee sonara utavihimili vishindo?”


Sauti yake ilikuwa nzito na ya kijasiri, ilikaribia kuzitikisa nyumba zangu.


Hata kabla halijajitambulisha, tayari nilikuwa nimeshatambua jitu lile lililoitwa Abobo Mdalaki, jemadari mkuu wa jeshi la Wadalaki nililitambua kutokana na mwendao wake uliofanana na mwendo wa simba mkongwe.


Abobo lilikuwa ni jitu la miraba minne iliyopindukia. Nguvu zake zilirandana sawia na umbo lake. Lilikuwa na nguvu nyingi. Kilikuwa ndicho kipaji chake.


Zamani wakati Abobo angali mdogo alionekana kuwa alikuwa na nguvu zisizo za kawaida. Wakati mmoja aliwaua simba wengi vichwa vyao alivitwaa na kuviweka kuizunguka nyumba yake.


Aliingizwa jeshini angali mdogo kamwe hajawahi kujeruhiwa vitani. Alipotimu hirimu la ujana Abobo aliondoka na kundi dogo la askari kwenda katika nchi jirani iliyokuwa adui mkubwa wa nchi ya Somondra. Akafanya vita huko na kuleta maafa makubwa tokea hapo aliogopwa. Ndipo wazee wa Kidalaki walipoamua kumfanya jemadari mkuu wa jeshi lao.


Uso wake ulibeba tabia yake ya kikatili. Jambo alilolipenda katika maisha yake lilikuwa ni vita. Alipokaa nyumbani macho na masikio yake alivitega kusikia tetesi ya vita. Kwa kumtumia jemadari huyu Wadalaki walikuwa wwanapanga kuitawala nchi yote ya Somondra, kisha wasonge mbele zaid hata kuziteka na kuzitawal anchi zote jirani.


Sasa mtu huyu mwenye sifa kubwa hizi alikuwa hatua chache tu kutoka makao yangu, akininyooshea mkono wa vita, akidhamiria kuniangamiza adinasi kama mimi!


Labda huu ndiyo ulikuwa mwisho wangu! Nguvu zangu zilikuwa ndogo kuweza kuhimiloi vishondo vya Abobo. Sikudhani mauti yangu yangetokea katika muda nisioturajia na kwa urahisi hivi! Kweli, kifo kijapo hakipigi hodi: Wakati utakapowadia nitaondoka katika usiku mnene nisioujua.


Ijapokuwa ni hivho, wanaume hhuyakabiloi mauti kiume. Nami nilikuwa mwanamume, ilinipasa kufa kiume.


Niliyakumbuka maneno aliyoniambia mama yangu siku moja;"”kwa vile wewe ni mwanamume ukawe shujaa ili ukawe na mwisho mzuri. "”Kwangu, kufa kishujaa ulikuwa ni mwisho mzuri. Maneno haya yamekuwa yakinitia nguvu wakati wote.


Niliapa kuwa kabla sijatangulia kuzimu itanipasa nimwachie kumbukumbu dubwana huyu; kumbukumbu itakayobaki kaitka maisha yake yote ya kipiganaji.


Niliupeleka mkono wangu mgongoni ili nimchukue Banamanyala; lakini Banamanyala hakuwepo mgongoni. Tayari, alikuwa ndani kujipumzisha. Hakika muda hu hakupaswa kulala. Ilikuwa ni afadhali nilale mimi kuliko yeye.


Nikavuta hatu akuelekae ndani ya nyumba yangu kwenda kuuchukua uta wangu. Nilipokwenda hatua mbili nimwona Akijikunja na fumo mkononi. Nilifarijika kugundua kuwa hakuwa na shoka lake, shoka lililotela makiwa makubwa. Bila shaka alikuwa amenipuuza. Niligundua zaidi kuwa hakuna na silaha nyingine zaidi ya fumo alilokuwa amelishika mkononi.


Hatua nyingine kuelekea ndani ingempa shahaba nzuri Abobo. Nikasimama dakika moja ilipita tukiwa tumesimama huku tumetazamana.


Muda mfupi uliofuata nianguka na kulala bata kama chatu mwenye njaa, huku fumo la Abobo likipita juu ya kiwiliwili changu.


Akiwa bado ameinama huku mkono wake wa kulia akiwa ameuelekeza chini kwa ajiil ya nguvu kubwa aliyoitumia, akayakodoa macho yake huk umdomo wake ameukenua na ulimi kumtoka nje, ulimi uliozungukwa na meno makubwa. Alionekana kama chatu aliyeponyokwa na paa.


“Kijana, unafanana na kirisa” (yule ndege ambaye huikwepwa shahaba nzuri ya jiwe la manati). Auid yangu alinisifu “Tangu utoto wangu mkono wangu haujakosa shahaba. Lakini mara ya pili hakika hutosimama.”


Shabaha, ilikuwa ni sifa nyingine ya Abobo. Aliweza kulenga na kupiga kitu kilichokuwa mbali huku amefumba macho.


Wakati yeye akinisifu, mimi nilikuwa nimeshapiga hatu kuliendea fumo lake. Nilitaka nimpe pigo kwa kutumia fumo lake. Nikalifikia fumo lile na kulikamata barabara katika mkono wnagu wa kuume.


Hapa niliupata wasasa mzuri wa kuupima umaridadi wa Abobo katika uwanja wa mapambano. Nikavuta hatua tatu zaidi kumwendea audi yangu, aliyebaki akiwa amesimama kama vile hapakuwa na hatari yoyote iliyokuwa inamkabili.


Nikamvurumishia fumo lake lililokwenda kutua juu ya kichwa chake kikubwa na kuifanya barabara kuu itakayozizuia nywele kuota milele. Hi indiyo kumbukumbu niliyoitaka.


Kwa Abobo hii ndiyo ailiyokuwa mara yake ya kwanza kujeruhiwa. Akatoa mguno mkubwa mguno ambao ungemfanya mtu mwingine apige yote.


Nilimsifu audi yangu na kukiri kuwa alikuwa shuja amkubwa asiyeshindika kirahisi, kwani sijapata kukosa shahaba namna ile tangu nilipomwua kurungu wa kwanza mwituni; hasa akiwa adui mkubwa kama Abobo! Nikamwogopa zaidi Abobo.


Nikamwona Abobo akiinua mkono wake wa kuli ajuu na kushika kichwani. Alipou7teremsha mkono waotwe ulikuwa umelowa damu kutokana na jeraha nililompa. Akautazama mkono ule wenye damu kisha akanitazama na mimi.


Akakitikisa kichwa chake kwa hasira huku ameyakaza meno yake na kuitamba damu ile mkononi. Nilimpa aibu isiyosetirika.


Mimi nilitumbukia ndani ya nyumba kuuchukua upinde wangu.


Nilipotoka nikakutana uso kwa uso na Abobo mlangoni. Akalikaba kioo langu kwa mimono yake. Alikuwa ametega mithili ya chatu kando ya kijia. Wakati amenikaba kooni niliutazama vizuri uso wake wa kutisha; ulijaa damu. Nikagundu apigo nililokuwa nimempa lilikuw akubwa.


N ikampiga teke zotei kwenye korodani (mapumbu), teke ambalo kwa mtu mdogo lilitosha kumtia wazimu. Akairamba midomo yake kwa utamu na kujitikisa huk akiyakaza meno yake kuupunguza uchungu, na kuzidi kuikaza mikono yake kweny ekoo langu.


Nilijitutumua kwa nguvu zangu zote nipate kutoka kwenye mtengo huu ulioninasa, bila mafanikio ilionekana vidole vyake vilishikana na kutiwa kufuli kwenye koo langu na funguo zake kutupwa kuzimu.


Hapo niliziamini habari nyingi zilizosimuliwa kuhusu Abobo. “Ana nguvu za ajabu!”


Aliendelea kunjikaba. Nilipoona siwezi kujinasua nilitulia na kusubiri punzi ya mwisho initoke. Nilianza kukoroma mbele ya uso wa Abobo.


Alipoona nilishakuwa nusu mzoga alinivutia chiin ya kwapa la ena kunitia kabari ilionekana ulikuwa mfano wa chatu mkubwa akimsulubu mwana mbuzi. Hapa uhai wnagu ulimtegemea Abobo.Mtu dhalimu! Chini ya kwapa za Abobo nilimfikiria babu yangu aliyekuwa mwasisi wa vita hii.


Nisingeweza kumlaumu; yeye alikuwa ni jemadari nami nilikuwa askari. Askari hawezi kumlaumu jemadari wake kwa kumweka mstari wa mbele wa mapambano; ila tu nilisikitika kuona kuwa vita hii ilikuwa imeanza wakati babu yangu hayupo.


Akiwa bado amenikaba kabari, Abobo alianza kuondoka kuelekea njia aliyojia. Pasipo kupenda nikamfuata kila sehemu anayokwenda bado nilikuwa na upinde wangu katika mkono wngu wa kushoto.


Kisha nilimwuliza Abobo aniambie mahali alipokuwa ananipeleka na kwa nini?


Akanijibu kuwa alikuwa ananipeleka nikauawe, na sababu ya kuuawa kwangu mimi nilijua, n akwmaba yeye ndieya liyepaswa kuniuliza.


Baadaye alipatwa na haku ya kunieleza.


“Kamwe sitokusamehe wakati bado naishi. Lazima nikupe kifo cha tabu mimi mwenyewe nitahakikisha ninafanya hivyo.


‘’Haikunipasa mimi nije kukimata kikaragosi kama wewe, ninao vijana wengi ambao ningeweza kuwatuma, lakini ulinipa hasira sana ndiyo sababu nikaamua nije mimi mwenyewe.


’’Ndiyo maana nilikwambia sababu ya yote haya wewe unaifahamu. Au siyo wewe yliyemuua kikatili askari wangu? Hakuna mtu anayemuua Mdalaki bado akaishi. Nitahakikisha unapata kifo kibaya.


“Kama vile haikutosha umenitia jeraha.” Umenipa aibu kubwa. Nitaiweka wapi aibu hii? Nitasimulia nini habari ya aibu hii? Labda kifo chako kibayta kitanipa nguvu ya mwanzo ya kusimulia kisa hiki. Itakuwa ni habari mbaya kwangu kusikia kuwa umekufa mbali na mikono yangu.”


Wakati akimaliza kunieleza haya tulikuwa tumeshaingia mjini. Mji wote ulikuwa kimya ni wazi8 hata hiyo, kuwa watu majjumbani waliweza kvuvisikia vishondo vya hatu zetu wakati Abobo akinikokota kutokana na maelezo aliyokuwa amenipa yule mpiganaji niliyemuua usiku mchanga, nilishgatambua kuwa Abobo alikuwa ananipeleka kwenye ngome ya wadalaki iliyokuwa ikenjengwa mwisho wa mji. Alikuwa ananipeleka huko ili nikahukumiwe kifo cha aibu.


Nimamuuliza nanipe habari za babu yangu.


“Habari za babu yako utazipataq huko kuzimu unakokwenda.” Alinijibu huku akionekana hakuwa na muda tena wa kuongea na mimi.


Tulikuwa tunaukaribia mwisho wa mji huku sehemu tuliyokuwa tunapita sasa ilikuwa ni ya makazi ya Wadalaki. Ngome yao ikiwa haiko mbali kutoka mahali hapa. Nilijua ningekufa kifo kibaya katika ngome ile iliyozungukwa na watu madhalimu. Haitakuwa vizuri kwangu kwenda kuziona nyuso zile chafu Nikakumbuka mielekea tuliyopigana zamani. Nilizijua mbinu nyingi za kumwangusha adui.


Abobo akiwa bado amekaza mwendo kuelekea ngome yake nikateaga miguu yangu kwenye miguu yake. Sote pamoja tukaaruka na kuanguka kifudifudi. Mimi nilitangulia chini. Kabari lake kali alilokuwa amenikaba bado halikutoka. Matokeo yake akajaa hasira na kuinyonga shingo yangu. Nikaliona giza nene likiyafunika macho yangu. Kitambo nilikuwa katika dunia sisiyoonekana kwa macho. Wala kusikika kwa sikio, wala kutambulikana kwa mawazo. Ilikuw ani dunia kiwa.


Itaendelea
 
shy jaribu kufupisha mana kwa jinsi ilivo ndefu balaa....

uongo mbaya hata sijamaliza!!!!!! ngoja niendelee lakani...
 
shy jaribu kufupisha mana kwa jinsi ilivo ndefu balaa....

uongo mbaya hata sijamaliza!!!!!! ngoja niendelee lakani...
 
Thanx shy,.kumbe wewe ndie mtunzi wa hii hadithi,.,nilishawahi kuisomakwenye magazeti ya nyumbani ,.ni nzuri.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom