Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,316
- 33,112
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, amewataka watumishi wa umma waliotangaza nia ya kuwania uongozi katika Uchaguzi Mkuu ujao, kuomba likizo ili kuepuka ukiukwaji wa sheria.
Ghasia aliyasema hayo wakati akifunga mkutano wa Baraza Kuu la Wafanyakazi katika utumishi wa umma, mjini Dodoma jana.
"Kama umeshatangaza nia ya kugombea katika nafasi mbalimbali za uongozi, omba likizo ili kujiepusha kuchanganya kazi na masuala ya kisiasa,"alisema.
Pia aliwaasa watumishi wa umma wasihusike katika kushabikia vyama vya siasa, ili kuepuka kukiuka misingi ya sheria za kazi.
Aliwataka kusoma waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma namba moja wa mwaka 2000, unaofafanua utaratibu unaosimamia ushiriki wa watumishi wa umma katika siasa.
Akizungumzia kuhusiana na programu ya kuleta mabadiliko katika utumishi wa umma, Ghasia alisema serikali inasisitiza utendaji wa kazi unaozingatia matokeo.
Pia alisema programu hiyo, inaimarisha uwajibikaji wa maadili ya watumishi wakati wakiwahudumia wananchi.
Hata hivyo, alisema utumishi wa umma unakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo baadhi ya watumishi kutokubali mabadiliko ya kifikra na ukosefu wa maadili.
Alisema kutokana na hali hiyo masuala ya uwajibikaji na tija yataendelea kuwa sehemu ya ajenda pana ya kuimarisha utumishi wa umma.
Ghasia alisema umuhimu huo unafanya masuala hayo kuendelea kuwa moja ya maeneo ambayo yatashughulikiwa na baraza lijalo.
Mmoja wa wajumbe hao, Edna Mwaigomela, alitaka serikali kutilia umuhimu ushauri wa baraza hilo lililomaliza muda wake, wa kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi.
Alisema mazingira mazuri ama mabovu yana uhusiano katika utoaji huduma kwa wananchi.
CHANZO: NIPASHE