BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,007
Thursday, 05 July 2012 20:39 |
Mwananchi Bunge linaloendelea na kikao chake mjini Dodoma, juzi liliambiwa kwamba Serikali imetenga Sh9 bilioni kwa ajili ya kugharamia matibabu ya viongozi wakuu wastaafu. Akihitimisha mjadala wa hotuba yake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Menejimenti na Utumishi wa Umma, Celina Kombani alisema fedha hizo ni kwa ajili ya wastaafu wanaopaswa kutunzwa na Serikali. Bila kuelezea suala hilo kwa undani, Waziri Kombani alisema tu kwamba kiwango hicho kimepungua mwaka huu kutoka Sh10 bilioni zilizotengwa mwaka jana hadi Sh9 bilioni mwaka huu kutokana na idadi ya viongozi wastaafu wanaopaswa kuhudumiwa na Serikali kupungua. Wastaafu wanaoangukia katika fungu hilo ni marais Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa. Mawaziri wakuu wastaafu ni Joseph Warioba, Samuel Malecela, Cleopa Msuya, Salim Ahmed Salim na Edward Lowasa. Waziri Kombani hakuwataja viongozi wastaafu waliopungua, lakini sote tunafahamu fika kwamba Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere na Mzee Rashid Mfaume Kawawa tayari wametangulia mbele ya haki. Bila shaka takwimu hizo zitakuwa zimewashangaza wengi kutokana na wingi wa fedha zinazotengwa kila mwaka kugharamia tu matibabu ya viongozi, bila kutilia maanani fedha nyingine nyingi zinazotengwa kama mafao ya viongozi hao wastaafu. Kwa akili ya kawaida, fedha hizo ni nyingi mno kulinganisha na idadi ya viongozi waliokusudiwa na takwimu hizo zinaacha maswali mengi kuliko majibu. Tunasema hivyo kwa sababu hatuoni jinsi kiasi hicho kikubwa cha fedha kinaweza kugharamia matibabu ya idadi ndogo sana ya viongozi wetu wastaafu, kwani siyo siri pia kwamba wastaafu wetu wengi wamekuwa wakipatwa na maradhi ya kawaida ambayo siyo tu hayahitaji fedha nyingi kuyatibu, bali pia yangeweza kupata tiba hapa nchini. Ndiyo maana tunasema vifungu vikubwa vya fedha zinazotengwa kila mwaka kwa shughuli hiyo siyo tu vinatia shaka, bali pia vinaacha ukungu na kiza kinene vikiwa vimetanda. Sisi hatusemi kwamba viongozi wetu hao wastaafu hawastahili kupata matibabu kwa kodi zetu. Tunachosema hapa ni kwamba gharama za matibabu yao hazipaswi kuwa siri au kuacha shaka hata kama wastaafu hao walitutumikia vizuri wakati wa utawala wao. Ni sahihi kabisa kwamba walipakodi wangetaka kujua kodi zao zinavyotumika kuwagharimia viongozi wao. Bado tunasisitiza kwamba Sh9 bilioni kwa matibabu ya viongozi hao wastaafu siyo tu ni nyingi mno, bali pia ni kufuru na za kufikirika. Takwimu hizo hazijumliki hata kidogo. Ni matibabu yapi yenye gharama hata robo ya kiasi hicho kilichotengwa, hata ukiweka usafiri, malazi na gharama nyingine? Ni kichekesho kwamba fedha hizo zimepitishwa na Bunge. Kinachosikitisha ni Bunge kutohoji fedha zote hizo zinakwenda wapi. Bunge lisiloona umuhimu wa kuibana Serikali iboreshe mazingira na huduma katika hospitali zetu ili viongozi na wananchi watibiwe katika hospitali hizo badala ya kupeleka fedha zetu nje na kujenga uchumi wa nchi nyingine. Ebu fikiria hili: Mwaka uliopita, wagonjwa waliopelekwa India kutibiwa mwaka wa fedha uliopita walitumia Sh7 bilioni zikiwa kodi za wananchi. Kwa nini tusitumie fedha hizo kuleta vifaa na wataalamu kutoka nje kwa lengo la kuimarisha hospitali zetu na wataalamu hao kutusaidia kujenga uwezo wa wafanyakazi katika hospitali zetu na sekta ya afya kwa jumla? Lengo la kuweka sheria ya mafao ya viongozi ilikuwa njema ili viongozi wetu wasiishi maisha ya mashaka baada ya kustaafu. Bahati mbaya hakuna aliyejua kwamba baada ya kuzikwa kwa Azimio la Arusha viongozi wetu wangetupilia mbali maadili ya uongozi na kuwa matajiri wakubwa, wengine wakifanya biashara na kuanzisha makampuni hata wakiwa bado katika ofisi za umma. Ndiyo maana tunalazimika kusema kuwa, huko tuendako tutalazimika kuangalia upya mafao ya viongozi, hasa suala hili la kutumia mabilioni ya fedha kila mwaka kwa matibabu ya kufikirika ya viongozi wetu. |