Elections 2010 Gharama ya Tamko la JK Kwa TUCTA!

Buchanan

JF-Expert Member
May 19, 2009
13,199
1,969
TAMKO lina gharama, tamko la Jakaya Kikwete kwa wafanyakazi limemgharimu uwezo wake kiuongozi, tamko hilo limemgharimu heshima, tamko hilo sasa linamgaharimu kisiasa, pia tamko hilo linamgharimu afya yake ya akili na afya ya mwili pia.
Je, anaweza kudhani kuwa kuwabeza wafanyakazi hawa ni suala lililohitaji muda mrefu kupata majibu yake?

Tangu Rais Jakaya Kikwete azungumze kwa jazba na hamasa kubwa akibeza juhudi za wafanyakazi wa Tanzania chini ya TUCTA (Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi) kudai haki zao watu mbalimbali walitoa majibu yao.

Wapo waliotoa majibu kulingana na walivyoguswa kihisia hasa wale walioumizwa na namna hotuba hiyo ilivyotolewa na lugha iliyotumika.

Kwanza alitumia jazba, vitisho na kebehi, takwimu alizopewa ni za kughushi na tatu akujibu madai mengine ya TUCTA.

Kiongozi yeyote awaye na mwenye mamlaka ya juu kiutendaji ana wajibu wa kuchagua maneno yenye hekima kwa kuwa "hekima ni uhuru". Hivi hiyo ilikuwa kauli kweli ya rais mzalendo kuwatamkia wafanyakazi katika jamhuri ya nchi ya kwao Tanzania? aliwadharau kwa kiasi gani? kwanini rais aliwadharau wafanyakazi kiasi hicho? alijiamini hivyo hakujua kuwa waliomweka madarakani ndio wafanyakazi hao hao aliowatukana?

Swali la msingi ambalo ninataka kuwauliza wafanyakazi, je wafanyakazi wa Tanzania ni wa muhimu lini? je wakati wa uchaguzi tu? kwa sasa wafanyakazi wanaonekana wa muhimu kisa eti tu uchaguzi umekaribia.

Kauli ya 'tusi' kebehi na dharau waliyopewa na mwajiriwa mwenzao, yaani rais sasa inapambwa kwa maneno tofauti ionekane kuwa haikusemwa, au kama ilisemwa haikumaanishwa vile.

Tuchukulie kebehi nyingine ya hivi karibuni iliyotolewa na Naibu Katibu wa propaganda, Tambwe Hiza, eti kusema kuwa Kikwete hakukataa kura za wafanyazi, au makundi fulani ya kijamii. kauli hii tena inaongeza dharau kwa wafanyakazi na jamii ya watanzania kwa ujumla.

Ina maana watanzania walisikia vibaya wote? Tangu TUCTA hadi wananchi wengine hatukusikia Rais amesema nini? au kama alisema ina maana wafanyakazi au watanzania hawakuelewa? Mbona CCM wanadharau vile? ina maana sisi watanzania hatuna uwezo wa kuelewa, au uwezo wetu wa kuelewa ni mdogo? Tambwe Hiza haoni aibu kutetea uovu wa aina hii kinagaubaga?.

Ifike mahali kama tabia ya dharau ya CCM kwa watanzania ikome, kama ni mazoea basi yaishe. Hii ndiyo ilikuwa kauli ya Rais mwenyewe bila kushinikizwa, au kama alishauriwa basi alishauriwa vibaya, naye bila kuona uovu wa kauli hiyo basi alisimama bila woga akasema "nakama wanavyodai kwamba watampigia kura kiongozi na chama atakayewapa fedha hizo, kura hizo sisi tunahesabu tumeshazikosa. Ni afadhali kuzikosa kura za akina Mgaya kuliko kuwaumiza wananchi walio wengi kwa kutumia fedha zote za nchi kuwapa akina Mgaya wagawane na kuwakosesha wananchi huduma muhimu. Jambo hili sitalifanya."

Je, hapa Kikwete alikuwa anaomba kura za wafanyakazi? Kisingizio cha kukosa pesa kuwapa wafanyakazi maslahi mazuri hakina mashiko katika nchi yetu maana wapo wachache wanaonufaika na ufisadi, wamejikusanyia pesa zetu walipa kodi, na zingine kidogo tulizonazo wanatuumiza kwa kodi kubwa ili wao waendelee kuvinjari.

Kikwete aliona heri kukosa kura za wafanyakazi, je watanzania wana mashaka? au wafanyakazi nao hawaamini kuwa Rais hataki kura zao? mnadhani angetoa kauli gani kwa hali ya kuridhika aliyo nayo kwa sababu ya kura zetu? mnadhani angesemaje kwa kuridhika na madaraka tuliyompa sisi? ailijichukulia hata mamlaka ya kutamka kuwa yeye ni mwajiri namba moja, wala sio wananchi waliomwajiri yeye na wafanyakazi wengine.

Kuwa Rais alikataa kura za wafanyakazi hiyo ni kweli, kuwa alizungumza kwa kebehi sana kuwakebehi na kuwakejeli wafanyakazi hilo nalo ni kweli. Je, Watanzania wanahitaji mwekezaji toka ulaya kuelezea kuwa wanadharauliwa? mbona kama hili lipo wazi sana hata darasa la chekechea linafundishika.

Wafanyakazi wa Tanzania ni wa muhimu lini? hilo ni jambo la kutafakari. Kila tamko lina gharama, kama Kikwete alikuwa anafanya utani, sasa tamko lake limemgharimu. na inafaa akubali makosa, maana kujidai kujinasua katika tamko hili kwa kutoa visingizio viingine ni kama kuficha moto katika majani makavu. Na kamwe haitawezekana katika hali ya kawaida.

Dharau ya Tamko la Kikwete gharama yake ni wakati huu. Tanzania ni yetu wote, hata bila Kikwete na bila CCM itabaki Tanzania tu.

Tunapswa wote kuheshimiana na kusaidiana, wala sio kudharauliana, maana cheo ni dhamana tu. Kikwete katika hili alikosea, na hapa anathibitisha kuwa washauri wake wamechoka kufikiri kwani wamemwingiza mkenge hilo halina shaka.

Lakini kama anaendelea kuwatunza wafanyakazi wanaomshauri hayo, sisi hatuna shida. Tunakubali kuwa mchuma janga hula na wa kwao. Waliomshauri Kikwete awadharau wafanyakazi waendelee kumfariji pia katika uchungu wa kuzikosa kura hizo.

Si jambo jema kuukwepa ukweli japokuwa unasemwa na mtu anayeonekana "duni" na "dhalili."

Mate ni mate tu, hayawezi kuwa mvua hata kama Kikwete alitema. Dharau yake na kauli yake vinaendelea kumgharimu.

Ukweli utabaki kuwa ni silaha ya jasiri na uongo ni silaha ya mwoga! Mwalimu Julius K. Nyerere aliwahi kuandika hivi:

"Ukweli una tabia moja nzuri sana. Haujali mkubwa wala mdogo; haujali adui wala rafiki. Kwake watu wote ni sawa. Pia ukweli una tabia ya kujilipiza kisasi kama ukipuuzwa…. Ukweli haupendi kupuuzwa puuzwa...


Source: Tanzania Daima.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom