Food 4 Thought!! from Tanzania Daima by Paschally Mayega

654

Senior Member
Feb 1, 2012
172
40
Paschally Mayega​
RAIS wangu maneno nitakayoyaandika hapa, si maneno yangu. Ni moja kati ya nukuu nyingi zilizoandikwa katika mabango tofautitofauti yaliyokuwa yamebebwa na wanaharakati. Walikuwa wakiandamana kukushinikiza umalize mgomo wa madaktari.
Mengine yaliandikwa, “Rais wetu watu wanakufa uko wapi? Rais gani anang’ang’ania Ikulu? Spika Anne Makinda acha blabla aibuuu, achia ngazi, maisha ni muhimu kuliko kanuni!” na mengine mengi.
Wakati haya yakiendelea Dar es Salaam, Mwanza kulikuwa shamrashamra na sherehe za kukata na shoka. CCM ilikuwa inatimiza umri wa miaka 35. Tunaambiwa lilipikwa mpaka pilau. Magunia ya mchele 1,000 na ng’ombe 35 waliangushwa.
Wenye malori na vibasi waliogelea katika mafuta ya petroli na dizeli. Kubali tu kama utabeba watu kuwapeleka kiwanjani, unajaziwa tanki. Mabilioni ya shilingi yakateketea. Kwa hakika tatizo katika nchi hii si fedha. Zipo nyingi! Lakini kwa wateule wachache!
Rais wangu sikulaumu, najililia tu mwenyewe nafsini mwangu. Ni Watanzania wangapi walikuwa wanakufa kila siku kutokana na mgomo wa madaktari? Ni madhara makubwa kiasi gani yamesababishwa na mgomo ule kwa Taifa. Ni kiongozi gani alionyesha kujali? Hukuonekana hata siku moja kwenye mahangaiko na vifo vya watu wako! Lakini watu walikuona Mwanza kwenye ‘kipunga’ (wali na nyama).
Nikiangalia vifo vya wagonjwa mahospitalini vikiendelea kwasababu ya mgomo wa madaktari na wakati huohuo nikiwaangalia viongozi wetu wa CCM walivyokuwa wanajichana kule Mwanza, nikamkumbuka marehemu mama yangu, aliniambia, “Mwanangu elewa kuwa Mwenyezi Mungu wakati anaumba, aliumba watu akaumba na vitu.”
Kufanya sherehe msibani kunamwondolea mtu utu na kumfanya awe kitu. Nikajiuliza ni mimi kitu au ni wale ninaowaona wakijirusha Mwanza ndiyo vitu?
Umati ulioonekana Mwanza ulikuwa mkubwa. Yawezekana vipi umati mkubwa kama ule utokee kwenye sherehe za bure badala ya kuomboleza msiba uliokuwa umelikumba taifa? Watu wamekusanywa kutoka vijijini hata hawajui kuwa kuna Watanzania wenzao wanakufa kwa sababu hakuna fedha ya kuwalipa madaktari stahili zao. Wangelitafakari hili nina hakika wengi wangeondoka na pilau yao wangewaachia wenyewe.
Kuangusha sherehe kubwa namna ile katikati ya maafa yaliyochukua maisha ya watu kwa mgomo wa madaktari kuna hitaji mtu mwenye moyo mkubwa kama wa mwendawazimu na katili kama wa mchawi!
Ukikosa baba hata vile ambavyo ungekuwa naye asingekufanyia unadhani angekufanyia, lakini kuwa na baba ambaye anakuona unakufa badala ya kukuokoa anaendelea na kilevi chake inauma sana.
Mgomo wa madaktari ulidumu kwa takriban wiki tatu. Maisha ya watu wengi ambayo bila mgomo yangeokolewa yalipotea.
Wengi waliathirika zaidi kwakukosa matibabu kwa wakati! Kipindi chote hicho baba hukuwahi kutamka hata neno moja kuonyesha angalau kuwa unajali. Na hata ulipolihutubia Taifa katika kilele cha sherehe za miaka 35 ya CCM jambo zito kama hili, lililogharimu maisha ya watu wako hukulisemea kabisa.
Kama hata watu walio karibu yako hawakuona kuwa ni muhimu kwako kuwaeleza wananchi nini serikali yako ilikuwa inafanya kuwaokoa katika janga hili basi baba, madhali limetulia usilisemee hili popote! Baki nalo tu kama haupo vile!
Akizungumza katika maandamano ya wanaharakati mwanamwema Ananilea Nkya, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, alisisitiza kuwa maandamano hayo ni ya wananchi. Akaeleza kuwa ujumbe wao walioutuma kwa serikali usipotekelezwa watawaambia wananchi waingie mitaani kudai haki yao yakupata matibabu. Alisema, “Tunatoa saa 24 kwa hatua za haraka kuchukuliwa kuhusu mgomo wa madaktari la sivyo, kesho (siku iliyofuata) tutawaeleza wananchi jinsi ya kuingia barabarani ili kuishinikiza serikali ijiuzulu.”
Kwa maneno mepesi anasema maandamano ni ya wananchi ambao kupatiwa matibabu ni haki yao. Kama serikali inashindwa kuwapatia haki ya kuishi ambayo ndiyo inayofanya haki nyingine zote zitekelezwe basi waishinikize ijiuzulu!
Serikali ni Rais. Kuitaka ijiuzulu ni kukutaka wewe baba ujiuzulu. Hapa ndipo tulipofikia. Mizaha imewakifu wananchi. Wamefikia wakati wakufanya uamuzi. Tusingojee hukumu ya wananchi. Majuto yake ni makali mno! Kama unaweza kusema sema sasa, tena sema mambo matatu tu si zaidi! Watu wako wanaokupenda watakusikia.
Kwanza wafukuze kazi wote waliohusika katika kuurefusha na kuuacha ukue mgomo huu, ukianza na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Waziri wa Afya, Haji Mponda na Naibu wake, Lucy Nkya. Wakemee polisi wanaotumia pingu na bunduki zaidi kuliko busara katika kazi zao. Waamrishe wawaachie wanaharakati haraka na bila masharti yoyote.
Chuki wanayoiunda ndani ya mioyo ya wananchi haiwi dhidi ya shingo zao, bali inakuwa juu ya kichwa chako. Baba polisi wamelifanya jina lako liwe kero katika masikio ya watu wako. Halafu malizia kwa kuwaomba radhi Watanzania.
Ulipotoka nje ya nchi walikuona kama uliona bora uende katika uzinduzi wa tawi la benki mojawapo ya kigeni, badala ya kushughulikia roho za wananchi. Hili wanalo katika vifua vyao. Hata Mwanza kwenye kujirusha kwa CCM wananchi walikuona. Baadhi yao waliokuona ni wagonjwa wenyewe waliokuwa wametelekezwa na madaktari katika vitanda vyao vya mauti.
Baba wengine kati yao hivi sasa ni marehemu! Kwa udhaifu wetu wanadamu tunadhani kama usingeenda Mwanza au kule kwingine na badala yake ungeenda Muhimbili, kwa busara zako madaktari wangerudi kazini. Baadhi ya hawa ambao hivi sasa ni marehemu, kwa msaada wa madaktari wangevuta siku zao na tungekuwa nao hadi leo! Lakini hilo halikuwa! Tumwachie Mungu kwa sababu ni yeye tu mwenye mamlaka ya kuhukumu!
Usiongeze maneno mengine mbele ya watu wako baba, kwa sababu wao wamekwisha kutoa hukumu. Hatma yetu na ya nchi yetu tumwachie Mwenyezi Mungu mwenyewe!
Rais wangu madaktari wamerudi kazini kwa sharti kwamba watekelezewe madai yao katika kipindi cha mwezi moja. Wametaka pia wanaharakati waliokamatwa waachiwe mara moja tena bila masharti yoyote. Lakini kwa utendaji ulioonyeshwa na serikali wakati wa kipindi cha mgomo, haitarajiwi madai ya madaktari kutekelezwa katika kipindi cha mwezi mmoja. Mgomo unaweza kurudi.
Tukiruhusu mgomo huu kujirudia madhara yake yatakuwa makubwa. Hawatagoma madaktari peke yao. Na walimu nao watagoma. Wafanyakazi watagoma. Wanafunzi watagoma. Wagomaji watakuwa ni wengi. Wananchi watakapogoma nchi itazizima! Naijutia siku hiyo ikilazimishwa kutokea. Kitabu tulichoanza kukisoma tangu 2005 kitafikia mwisho. Mwisho mchungu kama shubiri!
Waziri mkuu Mizengo Pinda alitumia saa chache sana kumaliza mgomo uliodumu kwa wiki tatu. Aliyoyatamka yakamaliza mgomo angeyatamka siku ya kwanza yangemaliza mgomo mapema na hivyo kupunguza ukubwa wa maafa. Vitisho vyake kuhusu matumizi ya vyombo vya dola katika kushughulikia mgomo wa madaktari nchini, viliwaongezea hasira madaktari na hivyo vikachochea maafa zaidi. Hakukuwa na sababu kwa Pinda kutoa vitisho kwa madaktari. Badala yake alipaswa kuwatia moyo madaktari na kuonyesha kuhusika kwake katika madai yao kama alivyofanya baadaye na kujikuta akitoa kauli mbili tofauti katika suala moja. Kwetu tunasema, ‘Yamleka zipita nga masala yawazana’.
Kuna watu hupata fahamu baada ya mambo kuharibika. Kushindwa kuupatia mgomo huo suluhu ya haraka, kumeonyesha jinsi waziri mkuu alivyoshindwa kuwajibika katika nafasi yake. Serikali imeonyesha udhaifu mkubwa katika kushughulikia mgomo wa madaktari. Imefanya uchukue muda mrefu na hivyo kusababisha maafa kwa watu wasiokuwa na hatia. Aidha mgomo huo umeonyesha jinsi serikali ilivyodhaifu na inavyoshindwa kujisimamia.
Rais wangu huko nyuma Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliwahi kuliambia Bunge kuwa hakuwa na uwezo wakumwondoa kazini katibu mkuu David Jairo. Leo kamwondoa kazini katibu mkuu Blandina Nyoni na kuacha maswali kuwa uwezo huo sasa kaupata wapi? Kama ikithibitika kuwa alikuwa na uwezo huo toka mwanzo, je, ichukuliwe kuwa alilidanganya Bunge?
Ndugu Rais, kama unaona huruma kumfukuza mtu kazi basi vunja baraza lote la mawaziri. Jitengenezee kabaraza kadogo ka mawaziri wasiozidi 15 kakusaidie kumalizia vizuri hii miaka yako miwili ya utendaji 2013/2014 iliyobaki.
Mawaziri ulionao sisemi wote lakini hawakusaidii. Ni kwasababu ya utendaji wao mbovu na wengine hawatendi kabisa na hao ndiyo wanaowafanya wenzetu wengine wakuone umepwaya. Achana nao. Kama fadhila umewafadhili inatosha.
Wala usitegemee hawa waje wakuambie asante. Bado uko madarakani na wengine wanajifanya fyatu wanakupinga hadharani. Hao ndiyo watakuwa wakwanza kusema tulikuwa tunamwambia lakini alikuwa hasikii.
Usitafute hifadhi yako ya baadaye kwa kumtengeneza Rais ajaye. Kwa utendaji huu wananchi hawana shida na yeyote kutoka CCM tena. Migomo, malalamiko, shida zimewajaa wananchi kila kona ya nchi, utamuuza nani kwa wananchi 2015 akubalike? Tafuta hifadhi yako ya baadaye kwa watu wako. Wananchi wakiridhika na wewe ndiyo hifadhi ya kweli. Achana na Waswahili ambatana na watendaji mahiri na wenye fikra pana. kina Tibaijuka, John Pombe, Januari na wenzao wana uwezo wa kulisafisha jina lako. Kumbuka wakati wa uwaziri mkuu wa Edward Lowassa nani aliyaona mapungufu yako? Ulikwenda kila mahali nani aligundua? Nchi ilikuwa inatembea! Mapungufu yote haya yasingejulikana. Na mwaka 2015 utakuwa na pilikapilika nyingi za kisebusebu. Kumbuka mwaka 2005 ulivyoizunguka dunia kujitambulisha. Ukiizunguka tena dunia 2015 kuwaaga uliokuwa unajitambulisha kwao kuna ubaya gani?
Rais wangu nitaendelea kuililia nchi yangu na Watanzania wenzangu waponda kokoto, wamachinga, mama na baba lishe, wapaa samaki na wanuka jasho wenzangu wote mpaka pumzi yangu ya mwisho itakapotoka katika mwili wangu.


 
..kwenye nchi za wenzetu vyama vya upinzani vingekuwa vimeilinyaka tukio hilo na kulitengenezea matangazo ya tv, na makala kwenye magazeti.

..ndiyo maana wakati mwingine nasema vitengo vya habari na uenezi vya CDM,CUF,NCCR, vimelala usingizi mzito.
 
ni ujumbe mzito sana kwa raisi na viongozi wetu. Kwa wasaidizi wake wanaomtakia mwema huwa wanampa taarifa km hizi km ushauri bora ila wengi wanamwibia kwa uongo.
 
..kwenye nchi za wenzetu vyama vya upinzani vingekuwa vimeilinyaka tukio hilo na kulitengenezea matangazo ya tv, na makala kwenye magazeti.

..ndiyo maana wakati mwingine nasema vitengo vya habari na uenezi vya CDM,CUF,NCCR, vimelala usingizi mzito.

Sasa wenzangu chadema ukiwaambia wamelala hawakuelewi, fedha zilizotakiwa kurusha matangazo kwenye TV na redio ndio zinatafunwa vizuri sana makao makuu
 
Back
Top Bottom