Kiganyi
JF-Expert Member
- Apr 30, 2012
- 1,242
- 765
MBUNGE wa jimbo la Ludewa Deo Filikunjombe(pichani) amepinga vikali uamuzi wa mhandisi wa Halmashauri ya wilaya ya Ludewa Baraka Mkuya kuwatumikisha wananchi wa kijiji cha Masimbwe katika ujenzi wa barabara ya Halmashauri kwa ajili ya mbio za mwenge.
Mbunge Filikunjombe alifikia uamuzi huo wa kuzuia wananchi kuendelea kutumikishwa kazi za ujenzi wa barabara za wilaya bila malipojuzi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo baada ya wananchi kuhoji sababu za kutumikishwa kujenga barabara za wilaya bila malipo huku shughuli nyingine za uzalishaji mali zikiendelea kusimama.
Wakizungumza katika mkutano huo wananchi hao walisema kuwa pamoja na jitihada zinazofanywa na mbunge wao kupambana na vitendo vya ufisadi kwa ngazi ya Taifa ila bado kuna ufisadi wa kutisha ambao umekuwa ukifanywa katika ngazi ya vijiji ambao umekuwa ukiwatesa wananchi na kujiona kama ni watumwa katika nchi yao ukiwemo huo wa Halmashauri ya wilaya ya Ludewa kuwatumia wananchi kujenga barabara za wilaya ambazo kimsingi zinatengewa bajeti .
Mkazi wa kijiji hicho Jonh Mwasanga alisema kuwa katika kijiji hicho wananchi wamekuwa wakishindwa kufanya kazi zao za kilimo kutokana na kila siku kutakiwa kwenda kutengeneza barabara ya wilaya kwa ajili ya mbio za mwenge na kumtaka mbunge wao Filikunjombe kutolea ufafanuzi .
Mkazi huyo alisema pamoja na kuchangiswa michango kwa ajili ya mbio hizo za mwenge ila bado wananchi wamekuwa wakitakiwa kushiriki katika ujenzi wa barabara hiyo jambo ambalo wamedai kuwa ni kunyanyaswa na uongozi wa wilaya ya Ludewa .
Afisa mtendaji wa kata ya Mlangali Edward Makamba akizungumzia suala hilo alisema kuwa maeneo mbali mbali ya vijiji wananchi wamekuwa wakitumika kujenga barabara za wilaya .
Hivyo alisema kuwa kwa kuwa maofisa watendaji wa vijiji na kata ni watekelezaji wa maagizo ya mkurugenzi wa wilaya hivyo walikuwa hawajui kama kuwatumikisha wananchi katika ujenzi wa barabara ni kosa.
Mbunge Filikunjombe akijibu madai ya wananchi hao alisema kuwa ni kinyume na utaratibu kwa wananchi kutumikishwa kutengeneza barabara za wilaya na kuwa utaratibu uliopo ni wananchi kutengeneza barabara za vijijini na sio za wilaya ambazo zinatengewa bajeti.
Hivyo alisema suala hilo atalifuatilia kwa kina hata ikiwezekana kwenda kuonana na mkurugenzi ama waziri wa wizara hiyo John Magufuli.
Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Ludewa Monica Mchiro alipoulizwa juu ya suala hilo alisema kuwa atalifanyia kazi zaidi ili kujua ni bajeti kiasi gani ilitengwa kwa ajili ya barabara hiyo ya wilaya .
SOSI; Fransis Godwin!