FFU wavamia kijiji, watembeza mkong'oto

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,080
igp-mwema.jpg
IGP, Said Mwena

Mahija Mpera
WATOTO wawili hawajulikani waliko huku watu kadhaa wakiwa wamejeruhiwa na mali zao kuharibiwa baada ya kundi la askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), kuvamia na kuwashushia kipigo kikali wananchi kwenye Kijiji cha Msongola.

Habari zilizolifikia gazeti hili jana zimeeleza kuwa tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia jana kijiji hicho kilicho Kata ya Msongola, Ilala jijini Dar es Salaam.

Lakini, kamanda wa polisi wa Ilala, Faustine Shilogile alikataa kuzungumzia tukio hilo akieleza kuwa litatolewa ufafanuzi na kamanda wa Kanda ya Dar es Salaam.

Ofisa mtendaji wa Kata ya Msongola, Oliver Mwashikia aliiambia Mwananchi kuwa “askari hao waliingia nyumba moja baada ya nyingine na kuwapiga watu waliowakuta bila kujali ni wazee, vijana au watoto na kuharibu kila kitu walichokiona mbele yao”.

Ofisa huyo alisema kuwa chanzo cha tukio hilo ni askari wenzao wawili kupigwa na wanakijiji hao usiku wa kuamkia Jumanne iliyopita.
Aliendelea kueleza kuwa askari hao walipigwa usiku wa manane baada ya kufika kijiji hapo wakimsindikiza mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaa, aliyefika kumdai fedha zake mkazi wa kijiji hicho waliyemtaja kwa jina la Mwinga Chacha.

Kwa mujibu wa mtendaji huyo, askari hao walifika nyumbani kwa Chacha majira ya saa 6:00 na mkazi huyo wa Kimara aliyekuwa akimdai Chacha fedha baada ya kumkopesha dawa za kuku.

Alisema: "Baada ya mdai huyo kufika, askari walimtaka afungue mlango, lakini Chacha akakataa. Ndipo purukushani zilipoanza na kusababisha majirani kuamka na kuanza kupambana na askari hao."Mwashikia alisema baada ya kuona wamezidiwa nguvu, askari hao walikimbia na kurudi kesho yake na wenzao hao wakiwa na magari manne.

"Wakavamia kijiji hicho na kuanza kuwachapa wanakijiji," alieleza.Mwashikia alisema baadhi ya wanakijiji walijeruhiwa katika tukio hilo ambalo pia lilihusisha uharibifu wa mali nyingi na kusababisha watoto wawili kutoweka na hadi sasa hawajulikani walipo.Watoto waliopotea ni Mwita Mohano na Kasaya Mohano ambao ni wa familia moja.

Habari zaidi zilieleza kuwa askari hao wanadaiwa kutoka kituo cha polisi Sitakishari, Ukonga na kwamba walivamia kijiji hicho wakiwa na magari manne aina ya Lanrover Defender juzi asubuhi.

Mmoja wa wanakijiji hao, Subira Mwita alilieleza gazeti hili kuwa askari hao walifika nyumbani kwake na kumuulizia baba na mama yake.Alisema, alipowajibu kwamba wote wawili wako kazini, walimtishia kwa silaha kisha wakaingia ndani na kuvunja redio.

Mkazi mwingine ambaye hakutaka kutajwa gazetini alieleza kuwa asubuhi ya siku ya tukio hilo, aliondoka na kwenda kazini kwake ambako ni karibu tu na nyumbani.

"Ilipofika saa 4:00 asubuhi, nilisikia sauti za risasi zikilia na baadaye kidogo akasikia mtoto wake akilia,"alisema.

Alisema baada ya matukio hayo aliamua kurudi nyumbani ambako aliwakuta askari hao wakiwa ndani ya nyumba yake na wakivunja ndoo."Mpaka nimefika tayari walishavunja ndoo tatu na kuchukua fedha taslimu Sh100,000. Waliponiona wakaanza kunipiga virungu," alisema.Akieleza kwa uchungu, mama huyo alisema kuwa anashangaa maaskari hao kuwafanyia unyama wanakijiji hao hasa watoto na kinamama ambao hawana kosa lolote

“Ndugu mwandishi hicho kipigo nilichokipata nikikufunulia nguo utanionea huruma. Mwili umeharibika kwa kipigo na walikuwa wananiambia twende huku nikawaambia nina mtoto mdogo wa miezi sita ndipo waliponiachia,”alisema mama huyo.

Mwanakijiji mwingine ambaye pia hakutaka kutajwa jina lake gazetini alilaani kitendo hicho akikiita cha kinyama na kinyume na dhamana waliopewa askari ya kuwalinda wananchi.

Chanzo: FFU wavamia kijiji, watembeza mkong'oto
 
Back
Top Bottom