Faida ya tunda la Mkomamanga kitiba kwa waathirika wa UKIMWI

Tareeq

JF-Expert Member
May 3, 2010
828
407
Mkomamanga (Punica granatum)ni mmea ambao asili yake ni katika nchi za Mashariki ya Kati (Middle East) na umetajwa sana katika vitabu vya kale vya historia ya eneo hilo. Kwa mujibu wa kamusi ya Kiswahili Sanifu iliyoandikwa na Taasisi ya Utafiti wa Kiswahili (Institute of Kiswahili Research) ya Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam-Tanzania, mkomamanga ni mti unaozaa matunda ambayo maganda yake huchemshwa na kufanywa dawa ya kufunga kuhara (TUKI, 1981).

i inaonyesha kuwa wenyeji wa Upwa wa Afrika Mashariki wamekuwa na uzoefu wa kutosha kuhusiana na uwezo wa tiba wa mmea wa mkomamanga kwa muda mrefu hasa ikizingatiwa kuwa wamekuwa na mfungamano wa kihistoria na wageni toka Mashariki ya Kati kwa kipindi kirefu.

Mkomamanga una dawa mbalimbali kama vile Tannis (punicalin na punicalagin), Flavonoids, Alkaloids, Steroids, Triterpenes na Polyphenols. Dawa hizi hupatikana katika magome, majani, mbegu, maganda ya matunda, juisi ya matunda na katika maua ya mkomamanga. Tunda la komamanga pia lina vitamini C na E kwa wingi pamoaja na madini ya potassium na copper.

Faida za kitabibu za mmea-dawa huu
Katika majaribio ya kisayansi imethibitika kuwa juisi ya komamanga na fukuto ya mmea huu husaidia kudhibiti kasi ya kuzaliana kwa virusi vya UKIMWI namba 1 [HIV-1]. Hii ni kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Neurath A. R pamoja na wenzake na kupewa kichwa kisemacho “Punica granatum juice provides an HIV-1 inhibitor and candidate tropical microbicide”.

Utafiti huu ulichapishwa katika jarida la kisayansi la BMC infectious diseases (4) 41-45(2004). Matokeo yanayofanana na hayo pia yalithibitika katika utafiti mwingine uliofanywa na Kun Silprasit na wenzake mnamo mwaka wa 2011 na kupewa jina la “Anti-HIV-1 Reverse transcriptase activities of hexane extracts from Asian Medicinal Plants”. Utafiti huo ulichapishwa katika jarida la kisayansi la “Journal of Medical Plant Research Vol. 5 (17), pp. 4194-4201, 9 Sept 2011”.


Dawa zinazopatikana katika maganda na majani ya mkomamanga husaidia katika matibabu ya hali ya tumbo kujaa gesi na kudhibiti tindikali (acid) tumboni. Mkomamanga pia husaidia katika matibabu ya kuhara damu na kutibu uambukizo katika kibofu cha mkojo (Cycititis).

Lojo ya mbegu za matunda ya komamanga ikichanganywa na maziwa, husaidia katika tiba ya kuondosha mawe katika figo. Fukuto ya Mkomamaga husaidia katika tiba ya minyoo aina ya tegu (Tapeworms) lakini pia husaidia katika matibabu ya uvimbe wa wengu (Spleen). Dawa-lishe hii pia husaidia kwa kiwango kikubwa katika uponaji wa vidonda vya tumbo.

Katika jaribio moja lililofanywa kwa wanyama, dawa hii ilionyesha uwezo mkubwa sana (97.4%) wa kuponya vidonda vya tumbo. Kazi hii hutokana na uwezo wa dawa hii wa kudhibiti bakteria aina ya Helicobacter pylori ambao kwa kiasi kikubwa huchangia kutokea kwa vidonda vya tumbo (70 -80% ya vidonda vya mfuko wa chakula na 90% ya vidonda katika utumbo). Hii ni kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Hu W. na wenzake mnamo mwaka 2006 na kupewa kichwa kisemacho “Study of in-vitro inhibition effect of Pomegranate rind on H.pylori”. Utafiti huu ulichapishwa katika jarida la Academic Journal of Kunming Medical College 27, 25-27.

Utafiti mwingine uliofanywa na H.R. Rahimi na wenzake mnamo mwaka 2011 ujulikanao kwa jina la “Punica granatum is more effective to prevent Gastric Disorders Induced by Helicobacter pylori or any other stimulator in humans” uliochapishwa katika jarida la kitabibu la Asian J. of Plant Sciences 10 (7): 380-382, 2011; pia ulithibitisha uwezo wa mkomamanga katika tiba ya vidonda vya tumbo. Lakini pia uwezo wa dawa hii wa kupunguza uzalishaji wa tindikali tumboni, huchangia katika uponaji wa haraka wa vidonda vya tumbo.


Katika mfumo wa damu, komamanda hutoa msaada mkubwa wa kuzuia na kutibu magonjwa yanayoshambulia mfumo huo nyeti. Komamanga ni dawa nzuri ya kuzuia na kutibu shinikizo la damu, magonjwa ya nyama za moyo, kiharusi (Cerebrovascular Accident) na magonjwa ya mishipa ya damu. Komamanga lina madini aina ya potassium na copper kwa wingi, pamoja na faida zingine mwilini, madini haya husaidia kusharabiwa (kufyonzwa) kwa madini ya chuma kutoka katika utumbo kwenda mwilini kwa urahisi na hii husaidia katika matibabu na kinga ya tatizo la upungufu wa damu mwilini.

Komamanga pia ni mahili katika tiba na kuzuia magonjwa ya kusendeka (magonjwa ya muda mrefu) kama vile saratani ya tezi ya prosteti ya wanaume, saratani mbalimbali, kisukari, baridi yabisi na uvimbe wa maungio ya vidole (gout). Komamanga husaidia mwili kuondosha sumu na uchafu utokanao na kemikali na mabaki ya vyakula mwilini kama vile asidi ya uriki (uric acid). Sumu hizi ni chanzo kikuu cha magonjwa mengi ya kusendeka.

Komamanga pia husaidia katika jitihada za kukabiliana na tatizo la unene wa kupindukia (Obesity). Husaidia katika matibabu ya tatizo la ini pale linapolemewa (Liver congestion). Dawa ndani ya komamanga licha ya kuwa na uwezo wa kudhibiti aina kadha wa kadha za bakteria wanaosababisha magonjwa mwilini, pia zina uwezo wa kukabiliana na virusi wa aina mbalimbali wanaosababisha magonjwa kwa binadamu.

Kwa mujibu wa wasomi na wanazuoni wenye shahada za uzamivu, Dk. Navindra Seeram na Dk. Risa Schulman, komamanga kwa hakika ni dawa asilia inayotamba katika tiba za kisasa (Modern Medicine) kwenye karne ya 21.

Kipimo
Dawa-lishe hii hutumiwa kwa kunywa fukuto inayotokana na sehemu za mmea kiasi cha gram 3 hadi 9 kwa siku inatosha kwa ajili ya tiba ya magonjwa mbalimbali. Kwa ajili ya minyoo ya tegu magome au mizizi ya mkomamanga kiasi cha gram 50 huchemshwa katika lita 1 ya maji ili kupata fukuto.

Juisi ya matunda yake pia inaweza kutumiwa kiasi cha bilauli moja kila siku ili kukinga magonjwa mbalimbali. Kwa mujibu wa tafiti mbalimbali dawa hii ni salama kama itatumiwa kulingana na kipimo sahihi. Tahadhari ichukuliwe kuhusu matumizi ya dawa hii kwa wanawake wajawazito na kwa watoto chini ya umri wa miaka 12 kwani hakuna taarifa za kutosha kuhusiana na usalama katika makundi haya.

Madhara yanayoweza kutokea kwa kutumia dawa-lishe hii (Adverse reactions)
Matumizi ya kipimo kikubwa cha dawa hii ikiwa katika hali yake ya asili (zaidi ya gram 80) kinaweza kusababisha kizunguzungu, maumivu makali ya kichwa, kushindwa kufumbua macho, kutapika, kuzimia na wakati mwingine inaweza kusababisha kifo. Dawa hii pia inaweza kusababisha mwili kunyong’onyea, kutokuona vizuri, kushitukashituka kwa misuli na kutetemeka kwa mikono kama mlevi (tremors).

Onyo:
Ni vizuri kuepuka matumizi holera ya dawa hata kama ni dawa za asili. Si kila dawa ya asili ni salama kama itatumiwa bila kufuata ushauri wa mtaalamu aliyesoma na kuelewa vizuri sayansi ya tiba asilia na lishe. Mimea ina kemikali za asili hivyo inapotumiwa ni lazima tahadhari zichukuliwe kuzuia madhara yanayoweza kujitokeza.Kumbuka mimea ni dawa.
 

Similar Discussions

1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom