BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,011
Date: 6/15/2009
EWURA watangaza ongezeko la bei ya mafuta karibu maradufu
EWURA watangaza ongezeko la bei ya mafuta karibu maradufu
Na Fredy Azzah
Mwananchi
Mwananchi
WAKATI Mamlaka ya Kitengo cha Taifa cha Takwimu (NBS), kikitangaza kushuka kwa mfumuko wa bei kutokana na kushuka kwa bei ya mafuta, nauli na bidhaa nyingine, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), imetangaza kupanda kwa bei za mafuta kwa wastani wa asilimia 46.
NBS ilitangaza jana kuwa kushuka kwa bei ya mafuta, umeme, maji na nauli kumesababisha mfumuko wa bei kuteremka kutoka asilimia 12 iliyokuwa mwezi Aprili, hadi asilimia 11.3 kwa mwezi Mei.
"Mfumuko wa bei uko katika mwendo wa asilimia 11.3 kutokana na kushuka kwa bei za bidhaa ambazo si vyakula," Ephraim Kwesigabo, mkurugenzi wa kitengo cha idadi ya watu wa NBS aliieleza Reuters jana.
Lakini wakati NBS ikitangaza hayo, mkurugenzi wa Ewura, Haruna Masebu alikuwa na mkutano na waandishi wa habari na kutangaza kuwa bei ya petroli imepanda kwa asilimia 46.31, dizeli 11.98 huku mafuta ya taa yakipanda kwa asilimia 13.3.
Masebu alizitaja sababu zilizosababisha ongezeko hilo kuwa ni pamoja na kupanda kwa bei ya mafuta katika soko la dunia pamoja na kushuka kwa thamani ya shilingi dhidi ya dola ya Marekani.
Alisema kulinganisha bei walizozitangaza Mei 27 mwaka huu, petroli imepanda kwa asilimia 5.47, dizeli kati ya asilimia 2.38 na 2.64 na mafuta ya taa asilimia 3.79.
Kutokana na ongezeko hilo, bei mpya kwa jiji la Dar es Salaam, petroli itakuwa ni kati ya Sh1,418 hadi 1,524 huku dizeli ikiwa Sh1,338 hadi Sh 1,473 na mafuta ya taa kati ya Sh 860 hadi Sh 924.
Kwa kipindi cha mwezi Januari hadi Juni mwaka huu, bei za mafuta zimekuwa zikipanda japo siyo kwa kiasi kikubwa kama ilivyokuwa mwaka jana. Bei zitaendelea kupanda kutokana na kuimarika kwa uchumi wa dunia na hasa Marekani, alisema Masebu.
Ewura imebaini kuwa bei za mafuta ghafi kwenye soko la dunia imefikia dola 70 za Marekani kwa pipa. Wadadisi wa masuala ya mafuta wanabashiri kuwa huenda bei zikafikia ukomo wa dola 75 za Marekani na hatimaye kushuka kabla ya majira ya baridi Ulaya, Septemba 2009.
Pamoja na wasiwasi huu, bei za hapa nchini haziwezi kufikia bei za Julai 2008.
Hata hivyo, wauzaji wa mafuta wamekuwa wazito kupunguza bei za bidhaa hiyo wakati inaposhuka kwenye soko la dunia, wakisingizia kuwa wanalazimika kuuza kwa bei kubwa kwa sababu bado wanatumia shehena walizoagiza kwa bei kubwa.
Mapema mwaka huu, bei ya mafuta duniani ilishuka hadi chini ya dola 40 za Marekani kwa pipa, lakini bei iliendelea kupanda hapa nchini kwa kisingizio kuwa meli za mafuta zinashindwa kuvuka pwani ya Somalia kutokana na maharamia kuziteka. Serikali ililazimika kuingilia kati na kuanza kudhibiti bei ya nishati hiyo.
Kwa mujibu wa Ewura, bei za mafuta katika Mkoa wa Kigoma, dizeli ni Sh1,538 hadi Sh1,688 huku petroli ikiuzwa kwa Sh1,618 hadi Sh1,739.
Katika Mkoa wa Arusha, petroli itauzwa kwa Sh 1,502 hadi Sh1,614 huku dizeli ikiuzwa kwa Sh1,422 hadi Sh1,528.
Mwanza petroli itauzwa kwa Sh 1,567 hadi Sh1,685 huku dizeli ikiuzwa kwa Sh1,487 hadi Sh1,634.
Masebu alisema kituo cha mafuta kitakachobainika kuuza mafuta kwa bei ya juu kuliko iliyotolewa na Ewura kitachukuliwa hatua kali za kisheria.
Katika hatua nyingine, Masebu alisema mchakato wa kuandaa utaratibu wa kuagiza mafuta kwa pamoja unaendelea na kuwa tayari kampuni ya ushauri wa kitaalamu ya Petrol Development Consultants Ltd ya Uingereza imeshakabidhi rasimu ya pili ya mchakato huo.
"Kilichobakia ni wadau kuanza kuijadili kwenye mjadala unaotarajiwa kufanyika Juni 23 mwaka huu," alisema.
Alisema mfumo huo unalenga kupunguza hitilafu zilizobainika kwenye tafiti iliyofanywa Agosti 2007.
Utaratibu wa sasa wa kila kampuni kuagiza mafuta yake unasababisha gharama kubwa za usafirishaji, msongamano wa meli bandarini; na hivyo kusababisha ada za ucheleweshwaji wa meli, alisema Masebu.