Edward Lowassa arushiwa kombora

Geza Ulole

JF-Expert Member
Oct 31, 2009
59,185
79,368
3rd December 09
Muhibu Said


Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa (CCM), ‘amerushiwa kombora’ jipya, akituhumiwa kumwaga fedha na simu za mkononi kwa wananchi jimboni humo, zikidaiwa kuwa ni sehemu ya kampeni zake za kutetea kiti hicho katika Uchaguzi Mkuu mwakani.

Tuhuma hizo nzito zimetolewa na Mwenyekiti Mstaafu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Arusha, Daniel Ole Porokwa, alipokuwa akichangia mjadala kwenye kongamano la kujadili mustakabali wa taifa, kumbukumbu ya miaka 10 ya kifo cha Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Kongamano hilo la siku tatu lililohitimishwa jana, liliandaliwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF), katika ukumbi wa Karimjee, jijini Dar es Salaam.

Wakati Porokwa akitoa tuhuma hizo, Waziri wa zamani, Mussa Nkangaa, alikikosoa CCM akisema kwamba, imepoteza hadhi yake na kusababishia kushikwa na kigugumizi katika kuwashughulikia wanachama wake wanaotuhumiwa katika kashfa ya ufisadi unaoihusisha kampuni ya Kagoda Agriculture Limited na kampuni hewa ya kufua umeme wa dharura ya Richmond Development LLC ya Marekani.

Porokwa, ambaye kwa sasa ni Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Wilaya ya Monduli, alitoa tuhuma hizo bila kutaja jina, lakini matamshi yake yaliashiria dhahiri unaoihusisisha Lowassa na kashfa hiyo.

“Hivi sasa chama kimetekwa, huku Takukuru (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini) ikiangalia tu. Imefikia hata wale wanaosema hatukukutana na Rais barabarani, kwenye majimbo yetu fedha na simu zinatawanywa, lakini Takukuru inaangalia tu,” alisema Porokwa.

Hivi karibuni, Lowassa alikaririwa na baadhi ya vyombo vya habari akiwakemea watu waliokuwa wakidai kwamba, ana mpango wa kumpinga Rais Jakaya Kikwete kwenye kinyang’anyiro cha kuwania urais kupitia CCM mwakani.

Katika taarifa hiyo, Lowassa alisema watu wanaoeneza uvumi huo, wanataka kumchonganisha na Rais Kikwete kwani uhusiano na urafiki wao haukutokana kwa kukutana barabarani.

Porokwa pia, alidai hivi sasa chama kimekuwa kikiendeshwa bila kufuata utaratibu kinyume na ilivyokuwa enzi za Mwalimu Nyerere.

Alisema yeye ni miongoni mwa waathirika wakubwa na tatizo hilo na kutolea mfano jinsi alivyoondolewa kwenye nafasi ya Katibu Msaidizi wa CCM Wilaya ya Hanang, kwamba aliandikiwa na kiongozi mmoja wa chama hicho ujumbe mfupi wa simu ya mkononi (sms), kwa vile tu hakuwa ni mwanamtandao.

Alisema kiongozi huyo wa CCM, ambaye hakumtaja moja kwa moja, katika sms hiyo alidai kuwa uamuzi wa kumvua wadhifa huo umetokana na maelekezo ya Mwenyekiti wa Chama hicho Taifa, Rais Jakaya Kikwete wakati haikuwa kweli.

“Nilibahatika kukutana na Mwenyekiti nikamuuliza hilo akaniambia kuwa hahusiki,” alisema Porokwa.

Akichangia mjadala kwenye kongamano hilo, Nkangaa, ambaye amewahi kuwa Waziri wa Wizara za Maji na Tamisemi , aliishauri Taasisi ya Mwalimu Nyerere kuchukua jukumu la kuandaa sifa za viongozi na kushauri kuwa wanaojihusisha na rushwa hawafai kuwa na sifa ya kuwa viongozi.

Nkangaa, ambaye amewahi pia kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na Morogoro, alisema CCM imepoteza sifa ya kuwa chama cha wakulima na wafanyakazi na sasa kimekuwa chama cha wafanyabiashara wakubwa.

“Wamebaki wanatetea maslahi ya matajiri wakubwa kiasi ambacho wanapata kigugumizi kwamba, Kagoda na Richmond ichukuliwe hatua gani,” alisema Nkangaa.

Mateo Qares akichangia mjadala huo, aliwataka wafanyabiashara wakubwa waliomo ndani ya CCM kuondoka kwenye chama hicho.

“Hao kazi yao kubwa ni kujitengenezea maslahi yao binafsi na si maslahi ya chama, ndiyo wanayumbisha chama. Kwanza hawana itikadi ya chama, pili, historia yao haijulikani alikotoka napengine nina shaka kuwa wengine si raia wa Tanzania,” alisema Qares ambaye alikuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Baraza la Mawaziri) na Menejimenti ya Utumishi pamoja na mkuu wa Mkoa wa Mbeya wakati wa uongozi wa awamu ya tatu. na kuongeza:

“Hawa ndio waliomfikisha Rais mahali hapa tulipo, je anaweza kufanya maamuzi magumu?

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Askofu Peter Kitula, alisema Halmashauri ya CCT imewasilisha mapendekezo serikalini kuomba siku inayotengwa kwa ajili kupiga kura, ambayo mara zote huwa Jumapili, ibadilishwe na kuwekwa siku, ambayo haitakuwa Jumapili na siku hiyo iwe ni siku ya sikukuu, ili kuwapa fursa waumini wa Kikristo kushiriki katika zoezi hilo.

Alisema miongoni mwa sababu zinazochangia kuwapo na idadi ndogo ya wapigakura siku ya zoezi hilo, ni waumini wa Kikristo kutoshiriki kikamilifu katika zoezi hilo na kuwafanya wanaokwenda kanisani kushindwa kumuabudu Mungu kwa roho na kweli.

Nape Nnauye, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, alisema Takukuru imefanya vitu vya aibu lakini Mkurugenzi wake Mkuu, Dk. Edward Hoseah, amegoma kuwajibika na aliyemuweka madarakani hajamuadabisha.
Aliwauliza wajumbe wa kongamano nini kifanyike?.

Chanzo: NIPASHE

http://www.ippmedia.com/frontend/functions/print_article.php?l=10727
 
Lowassa lazima ataukamata ulaisi siku moja na ole wao waliomnyima kitumbua cha U-PM. Kama NEC imejaa mapamdikizi ya MAFISADI na Kamati KUU nalikadhalika sasa watashindwa kumpitisha 2015? Atafanya juu chini ili mwakani apewe ubunge ili kuonyesha anakubalika na baadaya hapo ndo ulaisi. Yupo radhi CCm ivunjike lakini ulaisi aukwae.
 
Lowassa lazima ataukamata ulaisi siku moja na ole wao waliomnyima kitumbua cha U-PM. Kama NEC imejaa mapamdikizi ya MAFISADI na Kamati KUU nalikadhalika sasa watashindwa kumpitisha 2015? Atafanya juu chini ili mwakani apewe ubunge ili kuonyesha anakubalika na baadaya hapo ndo ulaisi. Yupo radhi CCm ivunjike lakini ulaisi aukwae.

Nadhani ulais anaweza kuwa nao hata sasa, ila kuna kazi ngumu kwake kuupata urais.
 
Kama lile kombora la richmond aliweza kulipangua then hakuna kombora linaloweza kummaliza EL, tanzania ni rahisi kwa mtu kujisafisha, hizi zote ni sababu ya shida na hali duni za wananchi ndo maana mtu akiharibu anawadanganya vitu vidogodogo..pia watanzania husau mambo ya nyumba hichi ndo kitu kinachowapa kiburi viongozi wetu.
Nchi nyingine ukiharibu ndo ushaharibu..
we have to change
 
Back
Top Bottom