DR Lwaitama anena kuhusu Chadema; Nimeipenda sana

ibange

JF-Expert Member
Dec 31, 2010
1,543
550
Nimekutana ha hii huko Mwanabidii Dr Lwaitama akimjibu Mjengwa. Soma maoni ya Mjengwa na majibu ya Dr Lwaitama, safi sana nimeipenda.

Ndugu yangu Mjengwa
Mawazo yako yamenigusa sana. Uliyoyatafakari baada ya kushuhudia uliyo yashhudia Iringa ni mambo wengine tumeanza kuyatafakari kwa kitambo kidogo hususani tangu Chama cha Chadema kilipomtangaza Dr. Slaa kuwa ngombea wake wa kiti cha Uraisi katika Uchaguzi Mkuu mwaka jana. Wewe umesema hivi: "Nimeishi Iringa kwa miaka saba sasa. Nikiri, kuwa sijapata kushuhudia maandamano makubwa ya wafuasi wa chama cha siasa kama yale ya CHADEMA Alhamisi iliyopita. Sijapata pia kushuhudia mkutano mkubwa wa chama cha siasa kama ule wa CHADEMA pale viwanja vya Mlandege" Na ukazidi kunena: "Na si tuliona, pale Mlandege, kulikuwa na akina mama watu wazima pia. Katika Tanzania hii, ukiona mikutano ya Chama cha siasa inaanza kuhudhuriwa na akina mama watu wazima, basi, hicho si chama cha kukibeza."

Hizi tafakuri zako tunduizi zimenigusa kwani ni sawasawa na zangu tangu niliposhuhudia mkuatano wa kwanza wa kampeni ya kwanza Dar es Saalaam ya kunadi Dr. Slaa kama ngombea wa Urais kwa tiketi ya Chadema viwanja vya Jangwani mwaka jana.Nakushukuru sana Ndugu Mjengwa kwa kutumegea busara yako kwa kuongozwa na imani ya TANU uliyonukuu ya "Nitasema kweli daima, fitina kwangu mwiko". Asante Ndugu Mjengwa . Labda tembelea Njombe na Songea upate kujua mikutano na maandamano ya Chadema huko yalikuwaje na utujulishe kwa Kiswahili chako chenye lafudhi ya karafuu na alwa!!. Tusaidiane kuendelea kuwasidia Watanzania wazidi kutambua ukweli unaozidi kupiga hodi yeyote apende hasipende ambao ni kutaka kuongozwa na chama mbadala ya CCM....

Wenzetu Zanzibar walau wamefanikiwa kulazimisha kuwepo serikali yenye kuongozwa na CCM nusu na chama mbadala yake cha CUF nusu...Kujivua gamba kwa ukweli ni kwa wana-CCM wenyewe kusaidiana na Watanzania wengine kuondoa ukilitimba wa serikali ya Muungano kuongozwa na CCM pekee kulikodumu kwa miaka 50 sasa. Ndio maana mzee mmoja wa kijiji cha jirani na Chuo Kikuu cha Mzumbe Mororgoro alitamka kwenye Kongamano la Katiba lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Mzumbe Ijumaa iliyopita kuwa yeye ndiyo kwanza alikuawa ameiona Katiba ya sasa ya Jamhuri ya Muungano lakini kwa vitendo vya serikali ya sasa basi Katiba hiyo lazima haifai na ilikuwa muafaka ije mpya mbadala yake. Ndiyo maana unawanukuu watu wakikwambia " Ah, CCM tumeichoka bwana!” Kwanini? Namwuliza jamaa wa mtaani; ” Tumeichoka tu, basi!” Na kuna wanaosema mitaani; ” CCM ni Chama Cha Mafisadi!”" Hayo ndiyo maoni ninayokumbana nayo mimi pia kila siku kote nchi nzima nilikobahatika kupita hivi karibu: Dar es Salaam, Arusha, Kilimanjaro, Morogoro, Mwanza, na Kagera. Asante sana Ndugu Mjengwa kwa maoni yako ya kina. Elimu kweli haina mwisho.
Mwl. Lwaitama




Date: Mon, 23 May 2011 00:10:18 +0300
Subject: [wanabidii] Ujio wa CHADEMA Iringa: Tafsiri Yangu
From: mjengwamaggid@gmail.com
To: wanabidii@googlegroups.com


icon1.png
Ujio wa CHADEMA Iringa: Tafsiri Yangu


Ndugu zangu,


CCM inayumba, kusema kingine ni kuwadanganya CCM, haitawasaidia.
Ndio, jahazi linapopoteza mwelekeo kinachofuatia ni kuyumba na hatimaye kuzama. CCM kama chama, kiko hatarini kuzama. Kuna ishara zinazoonekana.

Nimeishi Iringa kwa miaka saba sasa. Nikiri, kuwa sijapata kushuhudia maandamano makubwa ya wafuasi wa chama cha siasa kama yale ya CHADEMA Alhamisi iliyopita. Sijapata pia kushuhudia mkutano mkubwa wa chama cha siasa kama ule wa CHADEMA pale viwanja vya Mlandege.

Na kuna Wana- CCM wenye kubeza; ” Ah, wale vijana wa CHADEMA ni wavuta bangi tu!” Ananiambia Mwana-CCM hapa Iringa. Nikamjibu; ” Kama vijana wale wa CHADEMA kwa mamia wameweza kujipanga vile wakaudhuria maandamano kwa amani na hata kukaa mkutanoni wakiwasikiliza viongozi wao, basi, bangi ya siku hizi inawatia watu akili kuliko kuwalewesha!”


Na si tuliona, pale Mlandege, kulikuwa na akina mama watu wazima pia. Katika Tanzania hii, ukiona mikutano ya Chama cha siasa inaanza kuhudhuriwa na akina mama watu wazima, basi, hicho si chama cha kukibeza.


Ndio, kwa CCM, CHADEMA sio wa kubezwa. Wahenga walinena; mdharau kipele hushtukia ana jipu. Unapoona wananchi wanaandama kwa miguu kwa kilomita 5 hilo si jambo la kubeza. Unapoona wananchi wanatoka Tanangozi, Ilula na kwengineko kwenda Iringa kumsikiliza Dr Slaa na wenzake, hilo si jambo la kubeza hata kidogo. Hapo kuna jambo.

Na kwa CCM, si busara kukimbilia kuwaparamia CHADEMA bali kuyafanyia kazi mengi ambayo CHADEMA wametumia majukwaa kuishtaki CCM na Serikali yake kwa Wananchi. Na katika hili, kuna Watanzania wanaiona CHADEMA kama wingu nene la mvua lililotanda angani kwenye nchi yenye ukame. Hata kama wingu litapotea bila mvua kunyesha, lakini bado , kwao ndio matumaini waliyo nayo, kwa sasa.

CCM haina jingine, bali kufanya kazi ya ziada kulinusuru jahazi lake lisije kuzama. Na Iringa ilikuwa moja ya ngome za CCM kisiasa, si hivi leo ninavyoandika. Kuna mawimbi makubwa wanayokwenda nayo CHADEMA kwa sasa, na kama fasheni, wengi wanaelekea kuyafuata mawimbi hayo. Na hata ukimwuliza mtu kwanini? Anakujibu; ” Chama ni CHADEMA tu!”.

Wenye kujibu hivyo hawajui ni kwanini hasa wanayafuata mawimbi hayo. Lakini wanajua walichokiacha nyuma yao, ni CCM. Kuna wanaosema wazi; ” Ah, CCM tumeichoka bwana!” Kwanini? Namwuliza jamaa wa mtaani; ” Tumeichoka tu, basi!” Na kuna wanaosema mitaani; ” CCM ni Chama Cha Mafisadi!”

Na hilo la mwisho ndio haswa ’ msalaba’ mzito waliojibebesha CCM, au labda wamebebeshwa. CCM ina lazima, sio tu ya kuutua msalaba huo, bali kuuchimbia shimo na kuuzika. Kwa namna gani? Si kwa kujivua gamba kama Chama, bali kuongoza juhudi za taifa zima kujivua gamba. Ndani yake kuna KATIBA MPYA, Miiko ya Uongozi, Kuheshimu Haki za Kibinadamu na mengineyo.

Maana, bila Taifa kujivua gamba, inaweza kesho ikaondoka CCM na wakaja CHADEMA. Kisha tukabaki tukisema; ” Alaa, tulistaajabia ya Mussa, tumeyaona ya Firauni!”

Na katika yote haya, CCM isije ikasahau dhamana yake kwa taifa. Ndio, CCM ni chama tawala. Ni chama kilichobeba dhamana kubwa ya uongozi wa nchi. Ni ukweli huo unaofanya yanayotokea ndani ya CCM yatuhusu sote hata tusio wafuasi wa itikadi za vyama.

Na historia ni mwalimu mzuri. Aliyekuwa kada wa CCM na Katibu Mkuu wa chama hicho marehemu Horrace Kolimba ndiye aliyeanza kuusema ukweli juu ya mwelekeo wa CCM. Ni zaidi ya miaka 20 iliyopita. Kolimba aliusema ukweli wake na akausimamia.

Alitamka hadharani, kuwa CCM imepoteza dira. Hata wakati huo, uongozi wa CCM uliikana kauli ya Kolimba. Kolimba alikuwa na ujasiri wa kuisimamia kauli yake hadi kufa kwake. Atakumbukwa daima kwa kauli na msimamo ule aliouonyesha.

Miaka mingi imepita tangu Kolimba atamke kauli ile. Tumeanza kusikia sauti nyingi zaidi zikitamka mambo yenye kufanana na yale aliyoyasema Kolimba. Alianza Marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Ikafika mahali Mwalimu hakuishia tu kuzungumza juu ya yanayotokea ndani ya chama chake. Mwalimu aliandika kitabu ili kuacha kumbukumbu ya kudumu juu ya alichotaka kusema.

Hata baada ya Mwalimu tumeanza kuwasikia makada wengine wa CCM wenye kutamka hadharani yale yenye kufanana na ya Kolimba na Mwalimu. Ni leo tu, tumesoma kauli ya Mzee Ibrahim Kaduma, kuwa CCM imepoteza mwelekeo.

Kwamba wana- CCM wenyewe wameanza kujihoji ni jambo la heri kwa chama hicho tawala. Wenye kuhoji yanayotokea ndani ya CCM wanafanya hivyo kwa mapenzi mema na chama chao, hata kama wanajiweka katika hatari ya kupigwa mihuri ya “upinzani’ na kuhatarisha kutengwa kutoka kwenye kundi kuu.

Tunapozungumzia dhana ya kuimarisha demokrasia ya ndani ya vyama ( Intra-party democracy) si jambo la busara hata kidogo kujaribu kuzuia sauti zenye kuhoji, kudadisi na hata kupinga na kushutumu. Si busara hata kama wenye kuhoji na kudadisi ni kumi tu kati ya wanachama milioni moja.

Hata katika familia ya watoto wa tumbo moja wote hawawezi kuwa na fikra na mitazamo yenye kufanana. Kuzizima sauti hizo kunasaidia tu kuongeza manung’uniko na minong’ono ya chini chini. Zinachangia kuongezeka kwa harakati za chini kwa chini.

Manung’uniko, minong’ono na makundi yanaimarika pale ambapo wenye fikra na mitazamo tofauti wanapobanwa sana ndani ya chama na hata kufikia kukosa majukwaa ya kusemea. Ni pale watu hao wanapojisikia hofu ya kuchapwa bakora za chama na hata kutengwa kutoka kwenye kundi kuu. Hofu hiyo hupelekea nidhamu ya woga na watu kutoaminiana. Hupalilia zaidi hulka za kinafiki.


Wanachohitaji CCM kwa sasa ni kurudi kwenye misingi yao iliyopelekea kuundwa kwa Chama mama TANU na Afro-Shiraz na baadaye kuzaliwa kwa CCM. CCM irejee kwenye misingi yake ya miiko na maadili ya uongozi. Na irejee kwenye ahadi za mwanachama wa chama hicho kwa chama chake. Moja ya ahadi muhimu za mwana TANU na baadaye Mwana – CCM ni hii ifuatayo; ” Nitasema kweli daima, fitina kwangu mwiko”.

Nakumbuka, Tambwe Hizza, aliyeingia CCM akitokea CUF alipata kutamka hadharani, kuwa walipokuwa upinzani kazi yao ilikuwa ni kutunga uongo. Alichomaanisha Tambwe Hizza ni kuwa kama alikuwa ni mmoja wa watunga uongo kwenye kambi ya upinzani, basi, kuondoka kwake kutoka upinzani na kujiunga na CCM kulikuwa ni jambo la heri kwa aliowaacha huko kwenye upinzani. Bila shaka waliobaki huko walifurahia kwa kuondokewa na mtu mwongo.

Imefika wakati kwa Wana-CCM kuacha hofu ya kuambizana ukweli. Tulio nje tunakiona chama kinachoyumba. Rushwa na ufisadi ndani ya chama zinakiyumbisha chama. Ndani ya CCM kuna wanaoliona hilo pia. Baadhi yao kwa unafiki watamwambia nahodha; “Kanyaga mafuta baba!” Huku wakijua kinakoelekea chombo siko.

Na kila jahazi huwa na panya wake. Wenye kumsisitiza nahodha akanyage mafuta mara nyingi huwa na tabia za panya wa jahazini. Jahazi likianza kuzama, panya wake huwa wa kwanza kurukia majini na kukiacha chombo kikizama.

Inahusu umuhimu wa kusema yaliyo ya kweli. Na kuna aina tatu za wasema kweli. Kuna anayeusema ukweli na kujificha. Huyu anaweza kuwa na sababu za msingi za kutaka kuusema ukweli na kujificha. Ndiyo huyu atakayekwambia ukweli juu ya jambo fulani kisha kukutamkia; ”Tafadhali jina langu lihifadhi”.

Aina ya pili ya msema ukweli ni yule anayeusema ukweli na kisha kuukimbia. Atausema ukweli, akibanwa sana na wenzake, basi, ghafla ataukanusha ukweli aliousema hadharani. Atauruka ukweli wake mwenyewe. Atayakanusha maneno yake hata kama yamerikodiwa kwenye kaseti na kila mmoja akayasikia. Atang’aka, atakikimbia kivuli chake. Hii inatokana na woga unaozaa unafiki.

Lakini mwisho, kuna huyu anayeusema ukweli na kisha kuusimamia kwa lolote lile. Inyeshe mvua liwake jua. Ni watu wa aina ya akina Kolimba. Jamii yetu ilihitaji kuwa na watu wengi zaidi wenye kulikaribia kundi hili la tatu la wasema ukweli. Na siku zote , ukweli ni mzigo mzito, haupaswi kubebwa. Ukweli husambazwa.

Maggid,
Iringa, Jumapili, Mei 22,2011
 
Hao ndio lile sikio la kufa, huwaga halisikii dawa, kili kizuri utakachowaambia ccm akieleweki kwao. Muulize Idi Azam atakwambia.:A S 103:
 
Maggid, Unasomeka vizuri na hongera kwa makala hii. Kwa mara ya kwanza nimeona umesema yaliyo ya kweli, hongera sana.

Siku zote ulikuwa unaibeza CDM, lakini tunashukuru sana maan ukweli umeuona na mungu akusaidie uzidi kuwaelimisha watanzania wajue ili mabadiliko ya kimaendeleo yawepo.

Wana CCM watakubeza sana, lakini umenena yaliyo ya kweli na daima Ukweli huwa haubadiliki na kuwa uongo.

Hongera Maggid.
 
Kipi ambacho umekipenda maana nimesona hapo sijaona chochote kikubwa.
Una matatizo ya kuelewa ndiyo maana huelewi au umeamua kuchagua kutoelewa. hapo kuna mambo mengi ya kujifunza, kwanza CCM inaanguka, Chadema inazidi kujichimbia mizizi miongoni mwa wanajami, nk. Kwa sisi wapenda mabadiliko hilo ni jambo la kupendeza! au ulitakaje?
 
Hapa ccm inatakiwa kujisafisha na kujivua magamba kwa uadilifu, kwa kukimbia, bila kutazamana usoni. Kujitetea bila serious commitment for positive change nibure. Tukumbuke kwamba no body is infallible in the party. Let us not make gods and goddesses in the party. Remember there is only one living God. The rest of us will die n decay. No one and no is infallible.
 
hongeara sana Maggid kwa thread yako..maana ukweli mara zote upo pale pale kuwa
CDM ni chama peekee cha kumkomboa mTZ , tunamsubilia mzee Mapunda wa Tazama
naye abadilike...maana kwa sisi wenye uelewa tunashindwa kuelewa makala zake ktk jamii
 
Mimi tangu nimjue, nilikuwa nafikiri Dr Lwaitama ni mwanachama wa CCM ila ni mkosoaji pia wa CCM, lakini kwa maandishi haya nimejua kumbe haikuwa hivyo.
 
Majid kaandika vizuri,na hii article kama ccm wameisoma ilikuwa iwasaidie sana .
Nijuavyo mimi kama sumu ubora wake ni kuua basi kwa vile
Ccm wenyewe ndio gamba na sumu bado ipo ,article hii ni ya kuimaliza.
 
Safi sana, nimeipenda hii cause hapo awali kuna watu walibeza hiki chama.But kihalisia ni chama ambacho ukiangalia mtiririko wa uongozi wake ni tofauti sana na vyama vingine.Kuna vyama vinaongozwa na watu kana kwamba ni PAPA, hawataki changamoto za kubadilisha viongozi kwa kutumia Demokrasia.Yale yote yaliyokuwa yanasemwa na CCM wakati wa uchaguzi yameonekana kuwa ni propapaganda na hivyo watu wameamua kwa uwazi kabisa kuwaunga mkono CHADEMA ndio maana makundi ya watu wengi yanajitokeza kwenye mikutano yao.Mwisho wa siku ni kwamba CCM itaangukia pua ipende isipende, kwa sababu watu wameamua kufanya mabadiliko ya Kisiasa ambayo yataambatana na mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji Serikali tofauti kabisa na wa sasa.VIVA CHADEMA.
 
Back
Top Bottom