Elections 2010 Dr Bilal akosa watu wa kuwahutubia Dodoma!

Malafyale

JF-Expert Member
Aug 11, 2008
13,813
11,126
Bilal(6).jpg






Mgombea Mweza CCM, Dk. Mohammed Gharib Bilal



Fukuto la kura za maoni lingali linachemka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kiasi cha kuathiri mahudhurio ya wanachama kwenye mkutano wa kampeni wa Mgombea Mweza, Dk. Mohammed Gharib Bilal, hali iliyolazimu kusafirisha watu kwa magari baada ya uwanja kuwa mtupu.

CCM ilalazimika kuwasafirisha wanachama wake kwa malori ili washiriki mkutano wa kampeni wa mgombea mwenza katika kata ya Dodoma- Makuru mkoani Dodoma jana.
NIPASHE ilishuhudia watu waliovaa sare zinazotumiwa na CCM zikiwa na rangi ya kijani, njano na alama ya jembe na nyundo, wakiwa wamebebwa kwenye malori na kushushwa katika uwanja wa mikutano uliopo kwenye kata hiyo.

Miongoni mwa watu waliokuwa kwenye malori hayo ni wasanii wa vikundi mbalimbali vya burudani.

Mkutano huo ulipomalizika, malori yaliyotumika awali, yaliwabeba wasikilizaji wa mkutano huo na kuwarejesha kwenye maeneo tofauti yaliyosemekana kuwa karibu na makazi yao.

Kata hiyo inasadikiwa kuwa ngome ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) hasa baada ya mgombea udiwani aliyeshinda katika kura za maoni katani humo, Ally Biringi, kuihama CCM na kujiunga na chama hicho cha upinzani.

Kuhama kwa Biringi kwenda Chadema kulitokana na Halmashauri Kuu ya CCM mkoani Dodoma, kutorudisha jina la Biringi, ambaye alishinda kwa kura za maoni 196.
Nec badala yake ilirudisha jina la mshindi wa pili katika kinyanganyiro hicho, Zuwena Aweda, aliyepata kura 72.

Kutokana na hali hiyo ya upinzani katika kata ya Dodoma-Makuru, wagombea wote walichukua muda katika hotuba zao kuwasihi wananchi kutomchagua Biringi kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, mwaka huu.

Akizungumza katika mkutano huo, Dk. Bilal alisema wapo wanachama wanaoingia CCM kwa ajili ya kutafuta vyeo, na wanapovikosa wanahamia upinzani. “Cheo ni dhamana, wengi wanaingia katika chama kwa ajili ya kutafuta vyeo, hatuna uhakika kule wanakokwenda wakikosa wanafanyaje,” alisema Dk. Bilal.

Dk. Bilal aliwataka wananchi waliohudhuria katika mkutano huo, kumwambia (Biringi), ajiandae kwenda katika chama kingine mara baada ya kushindwa kwenye Uchaguzi Mkuu.
Pia Dk. Bilal alisema kuwa ujenzi wa uwanja wa ndege mpya wa mjini Dodoma, utaanza kushughulikiwa katika kipindi hiki cha miaka mitano ijayo.

Alisema dhamira ya serikali ya kuhamia Dodoma iko palepale, na kuwataka wananchi kumchagua Rais Kikwete, wabunge na madiwani wanaotokana na CCM.

Kwa upande wake, mgombea ubunge wa Dodoma Mjini kupitia chama hicho, David Mallole, alisema endapo atachaguliwa, atayashughulikia matatizo ya ardhi yanayowakabili wakazi wa Njendegwa.

Alisema kwa nafasi hiyo ya ubunge atakuwa mjumbe wa bodi ya wakurugenzi wa Mamlaka ya Ustawishaji ya Mji wa Dodoma (CDA) na hivyo kumpa fursa ya kutatua matatizo hayo.
Pia aliahidi kuyashughulikia matatizo ya maji, umeme na zahanati yanayoikabili kata hiyo ili wananchi waweze kuishi kwa amani.

Mallole aliwataka wakazi wa kata hiyo wasiziamini ahadi za Biringi hasa kuhusu ujenzi wa zahanati katika aeneo hilo.

“Mimi nimekuwa Naibu Meya hapa mjini, sijawahi kusikia akitoa hoja ya ujenzi wa zahanati kwa kipindi chote nilichokuwa pale, leo hii anasema atahakikisha kuwa zahanati inajengwa huo ni uongo mtupu,” alisema.

Habari hii imeandikwa na Sharon Sauwa Dodoma na Godfrey Mushi, Iringa.
 
Back
Top Bottom