Dowans yatua CHADEMA

Dowans yatua CHADEMA
• Wananchi wamtuma Mbowe akawashe moto bungeni

na Waandishi wetu


amka2.gif


WIMBI la wananchi kutokubaliana na uamuzi wa serikali kuilipa Kampuni ya kufua umeme ya Dowans (T) LTD limezidi kushika kasi baada ya wananchi wa Jimbo la Hai kumwagiza Mbunge wao, Freeman Mbowe, aende bungeni kuhakikisha fedha hizo hazilipwi.

Msimamo huo ulitangazwa jana kwenye Kijiji cha Nronga wakati mbunge huyo ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni alipokwenda kuwashukuru wananchi kwa kumchagua kuwa mbunge wao pamoja na kuchukua mawazo yao kwa ajili ya kuwasilisha bungeni.

Akiongea kwenye mkutano huo, Rowland Lema (77), alisema kwa sasa taifa linakabiliwa na tatizo kubwa la uhaba wa huduma ya nishati ya umeme, ambayo licha ya kuwa ghali, lakini haipatikani kwa uhakika na kwenye maeneo mengine hupatikana kwa mgawo.

Mzee huyo alisema jambo la kusikitisha ni kuona serikali inataka kutumia kiasi kikubwa cha fedha za wananchi kwa kampuni hiyo ambayo ilipewa jukumu la kuzalisha umeme na kushindwa.
"Kero ambayo tunataka uende ukaizungumzie bungeni na uisimamie kisawasawa ni hili la kupanda kwa gharama za umeme na kuna hiki kitu… sijui mtu anaitwa Dowans anataka serikali imlipe bilioni 96 …fedha hizi ni nyingi na Watanzania tuna hali ngumu. Tunataka uhakikishe fedha hizi halipwi, labda kutokana na uzee wangu huku kijijini sielewi lakini sioni sababu ya serikali kulipa fedha hizo," alisema Lema huku wananchi wenzake wakipiga makofi kuonyesha kumuunga mkono.

Akijibu hoja hiyo, Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) aliwaeleza wananchi hao kuwa atalishughulikia suala hilo kupitia Bunge kwani tayari walishaiambia serikali kutolifanyia mchezo suala hilo kutokana na ukweli kuwa linagusa masilahi ya wananchi wote wa Tanzania.

"Suala la umeme nimelisikia na huyo mdudu anayeitwa Dowans tumeshaambiwa serikali wasicheze naye na mtalisikia tukilishughulikia bungeni Dodoma na endapo serikali haitakuwa sikivu, basi mtalisikia nchi nzima," alisema Mbowe huku wananchi hao wakimshangilia.

Tayari CHADEMA ilishatangaza kuwa itafanya maandamano nchi nzima kupinga kuongezeka kwa gharama za umeme hapa nchini zilizopanda kuanzia mwezi Januari mwaka huu.
Aidha, wananchi hao walimweleza mbunge huyo kuwa kero nyingine inayowakabili ni uhaba wa masoko kwa ajili ya mazao yao, hasa mahindi, ambapo licha ya kutumia gharama kubwa katika kulima lakini wamekuwa wakipata mapato duni ambayo hayarudishi hata gharama za uzalishaji.

"Serikali inasema kuwa kilimo ni uti wa mgongo lakini haitilii maanani utekelezaji wa kauli hiyo. Tunalima mahindi lakini tukienda sokoni tunauza bei ndogo sana gunia shilingi 20,000 lakini kama wangeruhusu Wakenya kama walivyokuwa wakija walikuwa wakinunua gunia mpaka shilingi 45,000, tunaomba utusaidie hili," alisema Martin Mfuru.

Pia wananchi hao walisema kuna umuhimu kwa serikali kuanza kutoa ruzuku ya pembejeo kwa wafugaji, kwani wanakabiliwa na hali ngumu katika utunzaji na uzalishaji wa mazao yanayotokana na mifugo, hasa kutokana na ughali wa pembejeo hizo.

"Hapa tunategemea ufugaji kwa ajili ya kujiingizia kipato lakini tatizo hatuna mbegu nzuri na ng'ombe wetu wamepata kwashakoo kutokana na kula chakula ambacho hakitoshelezi na kutokana na uhaba wa malisho hata vyakula vya mifugo vinavyosindikwa tunavyonunua havina ubora," alisema Hellen Usiri.

Pia walimtaka mbunge huyo kuendelea kuhamasisha utaratibu wa wanafunzi kupatiwa maziwa shuleni ili kuwaongezea soko kama alivyoanzisha utaratibu huo mwaka 2001 akiwa mbunge wa jimbo hilo.

Walisema utaratibu huo ulisaidia kuboresha afya za watoto pamoja na kuwaongezea soko la maziwa yao.
Wakati huo huo Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, amesema suala zima linalohusu Dowans kulipwa fidia litaamuliwa na mahakama na kwamba hataki tena kulizungumzia zaidi suala hilo kwani anahofia kufungua mjadala mpya kutoka kwa wanasiasa nchini.

Kauli hiyo aliitoa jana wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari katika hafla ya uzinduzi wa mwongozo wa uendelezaji endelevu wa biofuel kimiminika nchini, iliyofanyika jijini Dar es Salaam na kusisitiza kauli yake aliyoitoa awali haijabadilika.
Alisema suala la hukumu dhidi ya Dowans ni la kisheria na kwa kuwa hivi sasa tayari limeshafika mahakamani ni vizuri ukaachiwa mhimili huo, kwani ndio wenye uwezo kisheria kuhusu hukumu ya Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Kibiashara (ICC).

"Sina maoni katika suala la Dowans, ila kauli niliyotoa awali inatosha na naogopa kufungua mjadala mpya kutoka kwa wanasiasa kwa kuwa suala hili lipo mahakamani na kuendelea kulisema ni kuingilia uhuru wa mahakama, kwa kweli inatosha turidhike na hayo," alisema Waziri Ngeleja.

Aidha, alisema umefika wakati kwa Watanzania kuunga mkono juhudi zinazofanywa na serikali katika kumaliza suala la mgawo wa umeme kwa kuibua miradi mbalimbali ambayo itasaidia kuleta ufanisi na kuondoa kero hiyo inayolikabili taifa.

Hata hivyo kauli hiyo ya Waziri Ngeleja ilipingwa vikali na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, ambapo alisema kuilipa Kampuni ya kufua umeme ya Dowans sh bilioni 94 ni makosa, kwani suala hilo nyeti lilihitaji kwanza kujadiliwa na kuamuliwa na baraza la mawaziri.
Sitta alisema Dowans ni Kampuni ya wajanja watatu waliocheza ujanja kwenye karatasi na serikali kuingia ‘mkenge' kulipa kitu ambacho alikielezea kuwa hakina sababu za msingi.

Waziri huyo alisema Kampuni ya Richmond iligunduliwa na Kamati ya Uchunguzi ya Bunge iliyoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe, kuwa haikuwa halali, lakini inasikitisha kuona na kusikia mbia wake Dowans amehalalishwa.

Akizungumzia mwongozo wa uendelezaji wa biofueli, Ngeleja alisema serikali inatambua manufaa yanayopatikana kutokana na uendelezaji huo, hususan ajira na kuongezeka kipato katika sekta ya viwanda na kilimo.
Alisema katika kuwezesha uendelezaji wa biofueli, sheria ya mafuta ya mwaka 2008, inatambua bidhaa zinazozalishwa na nishati hiyo hata kama zitachakachuliwa na wajanja kwa kutumia mafuta ya petroli.

"Mwongozo huu utasaidia kuinua kipato cha Watanzania hasa kwa kuunda vyama vya ushirika ambapo watanufaika na mpango huu kwa kuandaa mikataba mizuri iliyoandaliwa kisheria," alisema Ngeleja.

Alisema jambo la uzalishaji wa nishati mbadala Tanzania si nchi ya kwanza na hivi sasa dunia nzima inahamasisha uzalishaji huo katika kila mikutano mikubwa ya kimataifa.

Kwa upande wake, Kaimu Kamishna wa Nishati kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Mhandisi Hosea Mbise, alisema lengo la kuzindua mwongozo huo ni kutoa taarifa kwa umma ili watambue jinsi inavyotumika kwa mujibu wa sheria na kanuni. Alisema kuzalishwa kwa nishati ya biofueli kumezingatia sheria za uwekezaji ambao hautaliingiza taifa kwenye janga la njaa huku wawekezaji katika sekta hiyo wakitakiwa kuwekeza kwa kipindi cha miaka 25. "Tunaamini uzinduzi huu utasaidia kutoa taarifa kwa wananchi jinsi inavyotumika na kutambua matumizi yake kisheria kwa kuzingatia sheria ya uwekezaji nchini ambapo wawekezaji hupewa muda wa miaka 25," alisema Mhandisi Mbise.
 
Inasikitisha kuona wageni wanachezea utajiri wa nchi yetu wakati weneyewe tunakufa masikini!!!! Shime wananchi wote tusaidie kuwaamusha viongozi wote na kuwakumbusha kuwa TZ ni UHURU na wananchi wake ni binadamu wanaositahili kuheshimiwa na kuthaminiwa.:smile-big:

Thank you Hai people. Bado Moshi Mjini, Mwanza, Kigoma, Arusha, Shinyanga, Mbeya etc nao wanakuja. Dar es salaam bado wamelala tu?
 
Mafanikio ya kupinga DOWANS wasilipwe ni makubwa kama harakati hizi zinazofanywa na baadhi ya viongozi zingeungwa mkono na makundi yote.

Ila katika nchi ya Tanzania kuna ushabiki usiokuwa na tija wala sababu zozote za kushabikia. Watu wamekuwa wepesi kudanganywa na wao wakadanganyika.

Kwa mfano:
Akitokea kiongozi wa Chadema, CUF au chama kingine cha upinzani, utasikia mazezeta wa CCM wakisema; hayo ni ya chadema, Cuf na vinginevyo. Watu hawafikirii kuwa kama jambo lolote jema linapaswa kuunga mkono hata kama limetolewa/letwa na mtu mwenye itikadi tofauti na wewe.

Yatakayosikika kwa sasa ni yachadema, mara Sutta, mara Mwakyembe.

jamani tuwaunge mkono ili tufanikiwe kujikomboa.
 
Back
Top Bottom