Dk. Slaa: Baraza la Mawaziri livunjwe

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,005
Dk. Slaa: Baraza la Mawaziri livunjwe
• Amshangaa Rais Kikwete kuendelea na ziara nje

na Waandishi wetu, Dodoma na Dar
Tanzania Daima



CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimelitaka Baraza lote la Mawaziri la Rais Jakaya Kikwete, kujiuzulu kwa madai kuwa limeshindwa kuona dharura ya tatizo la umeme nchini na kulitafutia ufumbuzi.
Pia chama hicho kimemtaka Rais Kikwete kujiuzulu nafasi yake kwa kudharau na kuendelea na ziara yake nchini Afrika ya Kusini wakati akijua fika kwamba Bunge limekwamisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, anakabiliwa na tuhuma za ufisadi.
Kauli hiyo nzito, imetolewa jana na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willbroad Slaa, wakati akitoa maoni yake baada ya juzi wabunge wote bila kujali itikadi zao, kukwamisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2011/2012.
Dk. Slaa alisema Rais Kikwete na mawaziri wake wanatakiwa kupima uzito wa tatizo lilipo na kuchukua hatua za kuwajibika wao wenyewe bila kuambiwa kwani wote wanahusika kuliingiza taifa katika hali hii ya giza totoro.
Dk. Slaa ambaye amepata kuwania urais katika uchaguzi mkuu uliopita kwa tiketi ya CHADEMA, alimshangaa Rais Kikwete kuendelea na ziara hiyo wakati uchumi wa Mtanzania mmojammoja na ule wa taifa ukiporomoka kutokana na tatizo la umeme linalolikabili na kulifedhehesha taifa kwa sasa.
Akitoa mfano wa Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron, Dk. Slaa alisema amekatiza ziara yake nchini Afrika ya Kusini kutokana na kashfa ya gazeti moja nchini humo kuingilia mawasiliano ya simu za siri za watu.
“Rais Kikwete anawezaje kuendelea na ziara wakati nchi iko kwenye matatizo makubwa ya umeme, lakini kibaya zaidi Bunge limekwamisha bajeti ya Wizara nyeti ya Nishati na Madini na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anakabiliwa na tuhuma nzito zinazopaswa kuamuliwa na Rais mwenyewe?” alihoji Dk. Slaa.
Kwa mujibu wa Dk. Slaa, tafsiri ya kukataliwa kwa bajeti ya wizara hiyo ni ishahara kwamba Waziri Ngeleja na watendaji wake, wameshindwa kazi na hawana uwezo wa kupanga mikakati na utekelezaji wake.
“Haiwezekani viongozi walewale wakarudishiwa bajeti ile na kuendelea kuaminika kwa Watanzania katika kuongoza wizara. Kama wameshindwa kuandaa mikakati ya wizara zao, basi wafukuzwe, waje wengine,” alisema Dk. Slaa.
Katibu mkuu huyo wa CHADEMA alijigamba kuwa kilichotokea Bungeni ni kielelezo cha kujibu hoja nzito ambazo zimekuwa zikitolewa na kambi ya upinzani kupitia bajeti zao mbadala, kuanzia ile ya Waziri Mkuu Kivuli (Freemani Mbowe), Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi (Zitto Kabwe) na sasa ya Waziri kivuli wa Nishati na Madini, (John Mnyika) ambazo zimeonyesha dhahiri kuwa kilichoandaliwa na wizara za serikali, hakiendani na bajeti yenyewe.
Kuhusu kashfa ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, David Jairo, Dk. Slaa alipendekeza kuwa Bunge liunde kamati maalum kuchunguza tuhuma zinazomkabili za kuandika barua katika taasisi na idara zilizo chini ya wizara hiyo, alizozitaka zichangie sh milioni 50 kila moja kwa ajili ya upitishaji wa bajeti hiyo.
Alisema kamati itakayoundwa, inapaswa kumchunguza Jairo, mawaziri wake na maofisa waandamizi katika wizara hiyo waliohusika kuandaa bajeti kuanzia hatua ya mwanzo hadi mwisho ili kupata mwenendo mzima wa namna bajeti hiyo ilivyoandaliwa.
“Kwa hili la Jairo, napata wasiwasi kuwa mchezo huu umekuwa ukifanywa na wabunge wa CCM kwa kushirikiana na mawaziri wao kupitisha bajeti mbalimbali za serikari, huu ni wizi wa mchana kwa Watanzania,” alisema Dk. Slaa. Dk. Slaa alilitaka baraza jipya litakaloundwa baada ya mawaziri wote kujiuzulu nafasi zao, kufumua upya bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini ili iwasilishwe upya bungeni na kuruhusu marekebisho kufanyika ili kulipatia suluhissho la kudumu tatizo la umeme.
Lema ambana Ngeleja, naibu wake

Wakati jijini Dar es Salaam, Dk. Slaa akitaka Baraza zima la Mawaziri livunjwe, ndani ya Bunge la Muungano, mkoani Dodoma, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (CHADEMA), amehoji kwa nini Jairo anayehusishwa na vitendo vya rushwa katika upitishwaji wa bajeti ya wizara hiyo ‘atolewe kafara’ peke yake wakati Waziri Ngeleja na naibu wake, Adam Malima, wakilifahamu suala hilo?
Alisema mawaziri hao, wanapaswa kuwajibishwa kwa kuwa si rahisi maamuzi hayo kuyatoa Katibu Mkuu pekee bila mawaziri hao kuhusika.
“Mheshimiwa Spika, jana wakati Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, anazungumzia ushauri wa wabunge kuhusu tatizo la umeme nchini kabla ya kuomba kusitishwa kwa mjadala wa bajeti hiyo, alisema Katibu Mkuu amejihusisha na vitendo vya rushwa.
“Naomba mwongozo wako Mheshimiwa Spika inawezekanaje Katibu Mkuu apitishe suala hilo bila waziri na naibu wake kujua? Je, anayepaswa kuwajibishwa ni Katibu Mkuu peke yake?” alihoji Lema. Hata hivyo, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alisema mjadala huo umekwishawekwa pembeni na kwamba Waziri Mkuu Mizengo Pinda anakwenda kulishughulikia suala hilo kiutawala.
Askofu Kakobe naye atema cheche

Askofu Mkuu wa Kanisa la Full Gossiple Bible Fellowship, Zacharia Kakobe, alisema kitendo cha Bunge kuikataa bajeti ya wizara hiyo, kimetokana na laani ya Mungu baada ya viongozi wa wizara hiyo kuamua kuvunja mabango ya kanisa lake, lililoko jijini Dar es Salaam.
Askofu Kakobe alisema Waziri Ngeleja na wenzake wanapaswa kutubu juu ya dhambi hiyo kwa kutumia mabavu kupitisha waya katika kanisa hilo kinyume na matakwa ya Mungu.
Alisema tabia ya baadhi ya watendaji wa wizara hiyo kudaiwa kutoa hongo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini si jambo la kushangaza kwani walifanya hivyo hata wakati wa kuundwa kwa tume iliyochunguza athari watakazopata waumini walio chini ya waya hizo.
“Mtakumbuka jinsi Askofu Kakobe alivyopambana katika suala la upitishaji wa waya na hata ile tume iliyoundwa ya chuo kikuu (BICO), aliituhumu waziwazi jinsi ilivyopindisha taarifa ile kutokana na rushwa ili wapitishe waya kanisani,” alisema.
“Katika ibada moja, Askofu Kakobe alisema wazi kuwa Mungu ndiye Mungu wa ‘mianga’ na ndiye aliyetoa vipaji kwa wanadamu vya kugundua umeme, hivyo kitendo cha wizara hiyo kujiona ipo juu zaidi ya Mungu, sasa tunaona matunda yake,” alisema.
Waumini wa kanisa hilo waliwahi kupiga kambi kanisani hapo na kupeana zamu kwa kupangiana makundi ya kuikabili TANESCO usiku na mchana isipitishe waya za umeme juu ya kanisa lao.
Aidha waliandaa na ujumbe mzito kwa ajili ya shirika hilo la umeme uliowekwa wazi katika fulana maalumu walizovaa zilizokuwa na maandishi ya maonyo na kejeli yasomekayo: “TANESCO muogopeni Mungu” (mbele) na “Baada ya Richmond mmegeukia kanisa” (nyuma). Hata hivyo hatua hiyo haikusaidia kwani TANESCO waliamua kupitisha nguzo katika eneo hilo ambapo hadi sasa haijafahamika iwapo kama umeme unapita katika njia hiyo.
Wananchi Dar wachachamaa

Wananchi mbalimbali jijini Dar es Salaam, wametoa maoni tofauti baada ya wabunge kukataa kupitisha bajeti ya ofisi ya Wizara ya Mishati na Madini.
John Paul, mkazi wa Temeke, alisema kitendo cha wabunge kuikataa bajeti hiyo ni kizuri na aliwataka wabunge kuendeleza ukali huo kwa wizara nyingine.
Pia alimtaka Waziri Ngeleja ajiuzulu nyazifa zake kutokana na wizara yake kutotimiza matakwa ya wananchi.
Magreth John wa Ilala, alisema bajeti nyingi za Tanzania ni za kuandaa na sio za utekelezaji kwani mawaziri wengi wameziandaa wakati wakijua hazitekelezeki.
“Tatizo la umeme limekuwa pigo kwa nchi yetu na mipango sahihi ya kulimaliza ilibidi ionekane kwenye bajeti lakini badala yake waziri ameweka fedha nyingi kwenye mipango isiyo na faida,” alisema Magreth. Wanaharakati wataka JK akatize safari

Wanaharakati wamemtaka Rais Kikwete akatize ziara yake nchini Afrika Kusini aje kukabiliana na tatizo hilo.
Mmoja wa wanaharakati hao, Deus Kibamba, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Maarifa kwa Wananchi, akichangia mada katika sakata hilo kwenye kipindi cha keki ya taifa kinachorushwa na kituo cha Mlimani, juzi, alisema anashangaa kumuona Rais akiendelea na ziara wakati huku nyumbani mambo sio shwari.
Kibamba alisema yote haya yanatokana na tabia ya viongozi waliyojijengea ya kutowajibika hivyo hata suala la kutopitishwa kwa bajeti wanaona ni jambo dogo.
Akitolea mfano, Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron, wa kukatiza ziara yake katika nchi za Afrika alizopanga kuzitembelea kutokana na mkuu wa jeshi la polisi nchini humo kujiuzulu.
Naye Rais wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Lawrence Mwantima, alisema hii ndiyo kazi hasa wananchi waliyowatuma wabunge na kuongeza kuwa huko nyuma walikuwa hawafanyi haya.
“Mimi binafsi sula hili limenifurahisha sana na ndio kazi tunayotaka wabunge watufanyie sio blaablaa na isiishie tu kwa Wizara ya Nishati na Madini hata bajeti nyingine zinazogusa maslahi ya wananchi zinatakiwa zifanywe hivi bila kujali mbunge ametoka chama gani,” alisema.
Naye mwandishi wa habari, Tumaini Makene, alisema muda wa wiki tatu uliotolewa kwa ajili ya kuangalia bajeti hiyo upya haitoshi ukizingatia kwamba bajeti huanza kuandaliwa kila inapoisha kupitishwa kwa bajeti ya mwaka husika.
Pia Makene alisema haingii akilini kwamba kutaletwa kitu kipya katika bajeti hiyo ya wiki tatu kwa kuwa watendaji wa kuipitia watakuwa walewale na kushauri kwamba ingeundwa timu maalumu ambayo itaangalia mambo ya msingi katika bajeti hiyo na kupeleka kitu kinachoeleweka bungeni.
Juzi Bunge lilikataa kupitisha bajeti hiyo kutokana na msimamo wa wabunge wa pamoja kati ya wale wa CCM na wa upinzani hasa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kukataa bajeti hiyo kwa maelezo kuwa haikuonyesha suluhisho la tatizo la umeme nchini.
Kutokana na wabunge wengi kuikataa bajeti hiyo, Waziri Mkuu Pinda aliliambia Bunge kuwa serikali itaondoa bajeti hiyo na kuifanyia marekebisho na kuiwasilisha upya wiki tatu zijazo.
Pia uamuzi huo wa Bunge umekuja baada ya mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo, kusoma bungeni barua ya katibu mkuu huyo iliyozitaka taasisi zote zilizo chini ya wizara hiyo sh milioni 50 kila moja kwa nia ‘kulainisha wadau’ katika kupitisha bajeti hiyo.

 
duh I hope hiyo ingekuwa kweli lakini hata Ngeleja tu ameshindwa kujiuzulu na kashfa ya Rushwa..., Mwinyi na Mambo ya Gongo la Mboto.., hiyo kabinet nzima?.... labda itokee richmond nyingine
 
DR. Slaa tunataka maandamano ya kuwashinikiza hawa magamba bila maandamno hawatawajibika, na safari hii yawe ya nchi nzima...
 
Nadhanihili sakata sio la baraza la mawaziri peke yake, litalihusu bunge zima.

Inakuwaje bunge linaendelea kudiscuss bajeti wakati wanajua fika kuwa kutokuungwa mkono kwa bajeti ya wizara moja kunaonyesha mapungushu katika mtiriiriko mzima wa maandalizi ya bajeti? Nani anaimani na bajeti zilizopitishwa hadi sasa? Je hazikupitishwa kwa rushwa? Na je hesabu za ujumla za wizara ya fedha zimathirika vipi?

Nadhani hii issue ni pana kuliko tunavyoichukulia. Uzembe wa wizara ya ngeleja umedhihirisha pia uzembe, kukosa umakini au rushwa kwenye wizara ya fedha na kamati za bunge (wawakilishi wa wabunge na wananchi kwa ujumla).
 
DR. Slaa tunataka maandamano ya kuwashinikiza hawa magamba bila maandamno hawatawajibika, na safari hii yawe ya nchi nzima...

mkuu yakitangazwa na wewe uhudhurie ili tuwe wengi askari wa magamba wapige risasi hadi ziwaishie.
 
Uwajibikaji si utamaduni wetu ndomana waziri anajibu kwa jeuri kuwa sijiuzuru kwani tatizo la umeme ni la kitaifa.so far hakuna kitu.
 
Tumempigia kelele Ngeleja muda mrefu sana kwamba ni dhaifu kuongoza wizara hii nyeti, hakuna aliyesikia. Juzi kiongozi wa kambi ya upinzani ameeleza vizuri sana bungeni kwamba si kila mbunge ana sifa za kuwa waziri wa nishati. bado wameweka pamba masikioni. Haya ni matokeo tu. Huitaji elimu yoyote kubaini kwamba ngeleja ni bonge la kilaza. Hebu cheki sekta anazo simamia zote kavurunda. Umeme, Madini na Mafuta bei inazidi kupaa. Ningekua Ngeleja nisingesubiri watu wapige kelele, ningeachia ngazi kwa kuwa najua pia kwamba watanzania ni wepesi wa kupongeza na kusahau, wataanza kunimwagia sifa kwa ushujaa kama wanavyofanyiwa Rostam, Lowassa, Jairo.
 
hii ni laana ya MUNGU kwa wizara hii na hasa ngeleja aliyejifanya ana weza kumfanyia usanii mtumishi wa Mungu askofu kakobe.
 
Kwa wenye uelewa juu ya kanuni na shera za bunge, watusaidie kuelewa "Nini kinatakiwa kufanyika ikiwa Bunge limekataa kupitisha bajeti ya Wizara fulani?", na sio kujifanyia tu mambo kienyeji kwa "kwenda kuifumua na kuipanga upya kwa muda wa wiki tatu". Hii ni kusema kuwa bajeti iliyopangwa kwa miaka 5 na kutofaa, inataka kutiwa viraka kwa wiki 3 ili ifae.
Nchi hii bana........!
 
Hata mimi sielewi kinachojadiliwa baada ya kuikataa bajeti ya wizara moja. Kutaka bajeti ya wizara fulani ibadilishwe sana ni kuathiri bajeti ya wizara zote. Fedha za kuongezea Nishati na madini (ili igharimie umeme wa uhakika) zitatoka wapi kama sio kukatwa kwenye hizo wizara nyingine?

Au ndio pendekezo la kodi mpya na kutembeza bakuli?
 
Nasema hivi.....kama Slaa analazimisha Ngeleja ajiuzulu kutokana na Rushwa ya Jairo basi na yeye ajiuzulu kwa kuzungukwa na madiwani Arusha
 
Dk. Slaa: Baraza la Mawaziri livunjwe
• Amshangaa Rais Kikwete kuendelea na ziara nje
na Waandishi wetu, Dodoma na Dar
Tanzania Daima
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimelitaka Baraza lote la Mawaziri la Rais Jakaya Kikwete, kujiuzulu kwa madai kuwa limeshindwa kuona dharura ya tatizo la umeme nchini na kulitafutia ufumbuzi.

Pia chama hicho kimemtaka Rais Kikwete kujiuzulu nafasi yake kwa kudharau na kuendelea na ziara yake nchini Afrika ya Kusini wakati akijua fika kwamba Bunge limekwamisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, anakabiliwa na tuhuma za ufisadi.


Haya ndio majibu ya mkuu wa kaya

Pasco said:
...Rais Jakaya Kikwete, ameuzungumzia mgao wa umeme unaendelea sasa nchini kote, amesisitiza "tatizo ni ukame".

Rais Kikwete alikuwa akizungumza kwenye mahojiano maalum na BBC akiwa nchini Afrika Kusini yaliyorushwa jioni hii na BBC Swahili.

Rais amesisitiza, kwa vile mitambo yetu mingi inategemea nguvu za maji, hivyo tatizo la umeme limesababishwa na ukame.

Mwandishi akahoji kuwa tangu 2006 mgawo ulipoanza, bado tuu mlikuwa mkitegemea mvua?.

Rais alijibu kuwa baada ya 2006 hatua mbalimbali zimechukuliwa kuzalisha umeme kwa njia za gesi, makaa ya mawe hata umeme wa nguvu za upepo, lakini miradi hii yote inahitaji muda muafaka wa kuagiza mashine, akasisitiza ununuzi ewa mitambo unachukua muda, "huwezi kununua mitambo ya umeme hivi hivi tuu kama unavyoingia dukani kununua koti lako, mitambo huagizwa kwa kupeleka order kiwandani utengenezewe. hata hii mitambo inayoingizwa nchini hivi sasa, iliaagizwa toka mwaka jana.

Rias Kikwete amewataka wanasiasa wasibeze juhudi za serikali kuwaletea umeme wa uhakika Watanzania
.

Pia Rais Kikwete, ameuhakikishia tena ulimwengu kupitia BBC kuwa serikali yake ni sikivu, kama kuna watyu wenye hoja za msingi kuhusu utatuzi wa tatizo la umeme, wasiishie tuu kulalamika, bali waje na hoja za jinsi ya kutatua tatizo hili na serikali yake itazipokea hoja hizo na kuzifanyia kazi.
 
Back
Top Bottom