X-PASTER
JF-Expert Member
- Feb 12, 2007
- 11,610
- 1,809
Dhuluma Haiondoki Bila Kubadili Mfumo
Topic hii ya leo suala itatazama suala zima la mfumo katika kutawala au kuongoza jamii. Kimsingi nchi inayoongozwa kidemokrasia haiongozwi kwa fikra za mtu mmoja bali huongozwa kwa kufuata na kuzingatia sera za chama tawala.
Kwa hiyo mfumo mzima wa uongozi kuanzia serikali kuu, serikali za mikoa hadi mitaa, mahakama na bunge kutenda shughuli zake kwa kuzingatia sera.
Tunapozungumzia mfumo kwa ufupi tunazungumzia serikali, mahakama na bunge. Serikali husimamia utekelezaji wa sera za chama tawala katika kila eneo la nchi. Bunge hutunga sheria, huwakilisha wananchi, hushauri serikali, hukosoa serikali, n.k. Mahakama husaidia kutafsiri sheria n.k. Kwa hiyo basi watawala (serikali), Mahakama na Bunge hufanya kazi pamoja kama mfumo wa utawala.
Dhana hii ya mfumo inaletwa ili kufuta dhana miongoni mwa wanajamii kuwa mafanikio au matatizo yanasababishwa na mtu na siyo mfumo.
Kimsingi ni kuwa mtu binafsi hawezi kuleta balaa au mafanikio katika nchi bila kupata ushirikiano wa mfumo wote kama ilivyooneshwa. Iwapo atatokea mtu au kiongozi ambaye utendaji wengi unapingana na mfumo anaoutumikia ni dhahiri kuwa mfumo huo utamwondoa katika nafasi yake.
Yeyote yule anayeonekana katika sehemu yake ya kazi hadi mwisho wa madaraka yake bila kuondolewa tafsiri yake ni kuwa anautumikia vyema mfumo uliopo.
Ni dhahiri basi kuwa endapo watu hawaridhiki na hali zao za maisha iwe katika elimu, huduma za jamii, n.k. lawama zao haziwezi kuelekezwa kwa mtu mmoja hata akiwa ni mkuu wa nchi. Mapungufu yatakuwa katika mfumo. Jambo kubwa la kuzingatia ni kuwa kila mfumo unayo tabia ya kujiendeleza yaani kutaka kuendelea kuwepo. Mbinu nyingi hutumika katika kuhalalisha kuendelea kuwepo mfumo fulani. Harakati hizi za mfumo kutaka endelea hazijali kama mfumo huo ni mzuri au mbaya machoni pa watu.
Wakati mwingine mfumo unapogundua kuwa haujafanya kazi yake vyema, wenyewe unaweza kutumia mbinu ya kumtoa mmoja wao kafara. Hatua hii inapofikiwa, mfumo tawala hufanya propaganda nyingi sana dhidi ya mwenzao ambaye hutakiwa aonekane machoni pa watu kuwa yeye ndiyo 'nuksi' na akiondoshwa mambo yote yatawanyookea wananchi. Katika harakati hizi mfumo tawala hutumia vyombo vya habari na hotuba za wakubwa.
Lengo la Topic hii ni kuwanasua wale wanaojiona kuwa wapo katika harakati za kidemokrasia zenye lengo la kuwapatia Watanzania wote fursa sawa wasije kuingia katika mtego huu. Pia ni kuwajulisha wanaharakati hao kuwa mabadiliko hayawezi kuja kwa kumwondoa mtu mmoja tu, bali kwa kuuong'oa mfumo wote na pahala pake kuchukuliwa na mfumo mwingine.
Wale wanaoamini kuwa wanabaguliwa kwa dini zao, kabila zao, mikoa yao au hali zao wasijidanganye kuwa dhuluma inafanywa na rais, mkuu wa mkoa au waziri la! Kama ipo dhuluma basi inafanywa na mfumo mzima na kama ipo haki nayo pia inatendwa na mfumo mzima.
Namalizia kwa kushauri kuwa harakati za mageuzi ya kidemokrasia ziendeshwe dhidi ya mfumo uliopo na ziache kabisa dhana pandikizi kuwa huyu fulani akiingia atakuleteeni haki, amani, upendo, utulivu, utajiri n.k. Mfumo unaolaumiwa kwa kushindwa kusimamia uadilifu usipewe kabisa fursa ya kupendekeza mtu au namna ya kutatua matatizo ya watu.