norbit
JF-Expert Member
- Jul 30, 2007
- 835
- 699
- Wateule wa Rais wathibitishwe na Bunge
- Baraza lisiwe na mawaziri zaidi ya 15
- Vyama viungane siku 21 kabla kampeni kwisha
- Rais aunde tume huru kwa ushauri wa wadau
Chama cha Wananchi (CUF), kimeweka hadharani mambo yaliyomo kwenye rasimu ya mapendekezo yake ya Katiba mpya; mojawapo likiwa ni Tangazo la kuwapo Jamhuri ya Shirikisho la Tanzania, ambayo itaundwa na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Jambo lingine lililomo kwenye rasimu hiyo, linahusu uwepo wa Serikali ya Tanganyika na Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo ya Shirikisho na kwamba, kiongozi mkuu wa serikali hizo, ataitwa "Gavana" na kila gavana, atachaguliwa kwa mujibu wa Katiba ya nchi anayotoka (yaani Tanganyika au Zanzibar).
Kwenye rasimu hiyo, pia kuna katazo la kumshtaki rais anapokuwa madarakani na iwapo atakuwa nje ya madaraka anaweza kushtakiwa kwa makosa maalum.
Pia vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu kwamba, vitaweza kuungana kuunda chama kimoja kwa ajili kushiriki uchaguzi siku 21 kabla ya tarehe iliyotangazwa na tume ya uchaguzi kwa ajili ya uzinduzi wa kampeni bila vyama hivyo kupoteza usajili wao.
Rasimu hiyo iitwayo: "Dhana ya rasimu sifuri ya mapendekezo ya wadau kuhusu Katiba mpya ya Jamhuri ya Shirikisho la Tanzania" au "Rasimu ya mapendekezo ya Katiba ya Tanzania, ina sura 16, Ibara 131 na nyongeza tatu na iko katika kurasa 88.
Iliwekwa hadharani na Naibu Katibu Mkuu wa CUF Tanzania Bara, Julius Mtatiro, alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana.
Alisema rasimu hiyo ilianza kuandaliwa mwaka 2006 na wadau waliotokana na jopo lililoundwa na chama hicho lililowashirikisha watu zaidi ya 400 wa kada mbalimbali.
Alisema hadi kufikia Julai, mwaka huu, walitumia Sh. milioni 138 kuandaa rasimu hiyo na kwamba, katika kuiandaa, walipata msaada wa Katiba zaidi ya 30 za nchi za barani Afrika, Amerika na Ulaya kwa kuchukua sampuli zake.
Jambo lingine muhimu lililomo kwenye rasimu hiyo, ni uwapo wa tume huru ya uchaguzi ya shirikisho, ambayo wajumbe wake watateuliwa na Rais baada ya kupendekezwa kwake kutokana na mamlaka za wadau wanaohusika, ambapo mjumbe mmoja atatoka katika chama cha siasa chenye wabunge wa kuchaguliwa walau kutoka upande mmoja wa Shirikisho.
Wajumbe wengine watatoka mashirika na taasisi zisizo za kiserikali zinazoshughulikia uongozi wa jamii, taasisi za kidini, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, watu wenye ulemavu, wanawake, vijana na wazee.
Pia mwenyekiti na makamu mwenyekiti wa tume, watachaguliwa na wajumbe wa tume husika kutoka miongoni mwao.
Jambo lingine linahusu uwepo wa mabaraza mawili ya wawakilishi, moja la Tanganyika na lingine la Zanzibar, ambayo yatakuwa na mamlaka ya kutunga sheria kuhusu mambo yasiyo ya Shirikisho, kujadili, kusimamia na kudhibiti shughuli za Serikali za Tanganyika na Zanzibar.
Kuhusu mgombea binafsi, rasimu hiyo inatamka kwamba, kila mwananchi aliyetimiza umri wa miaka 18 anayo haki ya kupiga au kupigiwa kura katika uchaguzi unaofanywa Tanzania na wananchi.
Hata hivyo, inatamka kwamba, uchaguzi hautarudiwa iwapo mbunge aliyechaguliwa jimboni atafariki dunia, badala yake chama anachotoka, kitateua mwanachama wake mwingine mwenye sifa kurithi kiti hicho na kwamba, uchaguzi utahitajika kama atakayekufa atakuwa ni mbunge aliyegombea binafsi.
Rasimu hiyo pia inatamka kwamba, kutakuwa na wizara 15 na rais hataunda wizara mpya nyingine isipokuwa kwa ushauri wa Bunge.
Pia Waziri Mkuu, waziri, naibu waziri, balozi, Gavana wa Benki Kuu (BoT), Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), makamishna wa mamlaka zilizoundwa kwa mujibu wa sheria na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama, itakuwa ni wajibu wa Bunge kuidhinisha uteuzi wao utakaofanywa na Rais.
Vilevile inatamka kwamba, kutakuwa na Mkutano Mkuu wa Katiba, ambao wajumbe wake watachaguliwa na sekta mbalimbali za umma wa Watanzania kwa wawakilishi 10 kutoka kila chama cha siasa kilichosajiliwa na madhehebu makuu ya Wakaristo na Waislamu.
Wawakilishi wengine 10 watakuwa wa mashirika yasiyo ya kiserikali ya raia wa Tanzania, vyama vya wafanyakazi, vyama vya wakulima, vyama vya wanafunzi wa vyuo vikuu, vijana, wanawake, vyama vya waajiri, vyama vya wasiojiweza, vyama vya wafanyabiashara, Spika na wabunge wa shirikisho, Rais, Makamu wa Rais na Baraza la Mawaziri wa Shirikisho.
Wengine ni majaji wa Mahakama Kuu ya Shirikisho, Tanganyika, Zanzibar na Mahakama ya Zanzibar, Gavana wa Tanganyika, Zanzibar na Mabaraza ya Mawaziri wa Tanganyika na Zanzibar, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Tanganyika na Zanzibar, wajumbe 10 wanaowakilisha wasanii na wajumbe 10 wanaowakilisha vyama vya michezo. Mkutano huo wa Katiba utakuwa na mamlaka ya kutunga Katiba.
Jambo lingine ni Mahakama Kuu ya Shirikisho, ambayo itakuwa "Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Shirikisho la Tanzania" itakuwa na mamlaka yasiyokuwa na mipaka ya kusikiliza mashauri ya jinai, daawa na upatanishi kwenye mambo ya Shirikisho, kutoa hukumu na amri zenye nguvu kisheria kuzidi mahakama nyinginezo zilizoko chini yake.
Pia haitakuwa na mipaka ya kutafsiri Katiba ya Shirikisho na sheria za nchi na kufanya kila jambo linalohusu utoaji wa haki kwa mujibu wa mila za kisheria zinazotumika Tanzania, ambazo hufanywa na mahakama kuu na kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi pamoja na taratibu zake.
Vilevile, Rais wa Mahakama ya Rufani, ambaye atatajwa kama "Rais wa Mahakama" na kutakuwa na uhuru wa mawazo, majadiliano, ambao hautahojiwa na chombo chochote katika Jamhuri ya Shirikisho la Tanzania.
Jambo lilingine linahusu Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, ambayo itakuwa na mamlaka ya kuchunguza tabia na mwenendo wa kiongozi yeyote wa umma.
Rasimu hiyo pia inatoa haki ya uraia kwa watu wote waliokuwa raia wa Tanganyika na Zanzibar kabla ya Aprili 26, 1964, waliozaliwa baada ya tarehe hiyo na wazazi wawili wa Kitanzania au mzazi mmoja wa Kitanzania na wenye uraia wan chi nyingine na wale watakaotaka kuasili.
Akizungumzia kauli ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema ya kukataa kuandikwa Katiba mpya, Mtatiro alisema: "Mwanasheria Mkuu hawezi kusema ukweli kwa sababu ananufaika na Katiba iliyopo."