Zak Malang
JF-Expert Member
- Dec 30, 2008
- 5,404
- 233
CHAMA cha Wananchi (CUF) kimeipongeza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU), kwa kuonyesha utendaji na uwepo wao hasa katika kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi kwa kuanzia kura za maoni zinazoendelea nchini na kuwakamata baadhi ya wagombea wakiwashawishi wachaguliwe kwa rushwa.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na Naibu Mkurugenzi wa Uenezi na Mahusiano wa CUF, Ashura Mustapha, ilieleza viongozi wengi wamekuwa wakijipatia nafasi mbalimbali za uongozi kwa njia isiyo halali, jambo linalosababisha utendaji wao kutokuwa makini kwa kuangalia masilahi yao zaidi na kutaka kurudisha viwango vya pesa walizotumia wakati wa mchakato wa kuchaguliwa.
"Kama TAKUKURU itafanya kazi hii kwa uadilifu na uaminifu wa hali ya juu, itakuwa msaidizi mkubwa kwa Watanzania wengi ambao wamekuwa wakishawishiwa kuuza haki zao za kimsingi za kuchagua viongozi wenye uchungu na wenye moyo wa kuleta maendeleo kwa wanaowachagua na kwa masilahi ya nchi," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Aidha, chama hicho kimeitaka TAKUKURU ili kuhakikisha haki inatendeka, ifanye kazi bila kubagua chama wala wagombea na ijikite zaidi katika kufanikisha uchaguzi ulio huru na wa haki, ili kila mgombea achaguliwe kutokana na utendaji wake, uwezo na sifa ya kuwa kiongozi bora.
Pamoja na hayo, chama hicho kimewaomba Watanzania wote watoe ushirikiano kwa kuwafichua hadharani wagombea wote wanaotaka uongozi kwa masilahi binafsi kwa kuwapa rushwa.
Chanzo: Tanzania Daima
My take:
Hivi kweli Takukuru wako serious katika harakati hizi za kukimbizana na makada wa CCM, au wanafanya usanii tu – kwa njia ya kutumwagia vumbi? Mwisho wa siku hatutaona chochote kitakachotokea – hakuna atakayeenda jela -- na kwa hili niko tayari kupigwa risasi.
Profesa wa CUF anawapongeza bure tu wasanii hawa. Kwanza haoni jinsi wanayofanya usanii kuhusu kukamatwa kwa wakwapuaji mabilioni katika Kagoda – au na hilo Profesa anawapongeza Takukuru?
Tusisahau kwamba Profesa alikuwa mmoja wa viongozi wa vyama (the other was Augustine Mrema) waliomponda Mengi alipowataja mafisadi papa.