CUF imeonyesha mfano wa kudhibiti matumizi ya serikali

Averos

JF-Expert Member
Aug 6, 2010
993
695
Kuna taarifa kuwa Chama Cha Wananchi (CUF), kimewazuia mawaziri wake wanaounda Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar kutumia magari ya serikali kwa ajili ya shughuli za kisiasa za chama hicho kwa madhumuni ya kufuata misingi ya utawala bora.
Uamuzi huo umetangazwa na Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Ismail Jussa Ladhu, na kufafanua kuwa umeshachukuliwa na chama baada ya kubainika kuwa baadhi ya mawaziri wake kutumia magari ya serikali katika shughuli mbalimbali za chama hicho ikiwemo mikutano ya hadhara.
Ladhu alisema kuwa matumizi ya magari ya serikali katika shughuli za chama ni kwenda kinyume na misingi ya utawala bora.
Kufuatia maamuzi hayo, tayari mawaziri wote wa CUF wameshataarifiwa na kutakiwa watumie magari yao binafsi katika shughuli za kichama, na kwa wale wasiokuwa na magari watafute utaratibu mwingine utakaowawezesha kufika katika shughuli za kichama.
Kiongozi pekee wa serikali kutoka CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais, ndiye aliyeruhusiwa kutumia gari la serikali kwa shughuli za kichama kutokana na nafasi yake ambayo inazingatia itifaki.
Chama hicho kimesema kuwa kimechukua hatua hiyo kutekeleza kwa vitendo msimamo wake wa siku nyingi kabla ya kuingizwa serikalini kuhusu kupinga matumizi makubwa ya serikali.
Chama hicho kimefanya uamuzi mzuri ambao bila shaka wananchi wengi watakubaliana nao kwa kuwa licha ya kufuata misingi ya utawala bora, pia unalenga kuwapunguzia mzigo walipakodi.
Moja ya mambo ambayo yanasababisha matumizi makubwa ya serikali ni magari kwa maana ya uendeshaji wake kama mafuta na gharama za matengenezo.
Uamuzi uliochukuliwa na chama hicho sio vibaya kama wengine wataufuata kwa nia njema ya kupunguza matumizi ya serikali ili fedha zitakazookolewa zitumike kwa matumizi megine hususan kuboresha huduma za jamii kwa wananchi.
Ni jambo lililowazi kuwa mawaziri wote wana magari binafsi hivyo, hawanabudi kuyatumia kwa ajili ya shughuli za kichama.
Inaeleweka kwamba vyama vyote vinavyounda Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar vinapata ruzuku ya serikali kila mwezi hivyo hakuna sababu zozote kwa mawaziri wanaotokana na vyama hivyo kutumia magari ya serikali kwa shughuli za vyama hivyo.
Kama mawaziri hao wana nyadhifa za kichama, basi vyama vyao vinawajibika kuwagharimia, zikiwemo gharama za usafiri.
Na kwa upande wa serikali ya Muungano, ni wakati mwafaka sasa kuwekwa utaratibu wa kuwabana mawaziri kutumia mgari ya serikali katika shughuli za kichama.
Hivi sasa serikali inasema kuwa inachukua hatua kadhaa za kubana matumizi yake ili fedha zitakazookolewa zielekezwe katika kuboresha huduma za jamii.
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, hivi karibuni aliyataja maeneo ambayo serikali inajitahidi kuyabana ili kuokoa fedha zaidi ni ununuzi wa magari; masomo ya nje kwa watumishi; posho, semina, warsha, makongamano na mikutano pamoja na ununuzi wa samani.
Itakuwa vizuri kama kubana ununuzi wa magari ya kifahari kutakwenda sambamba na kubana matumizi ya magari hayo.
Wako mawaziri wengi wa Jamhuri ya Muungano ambao pia ni viongozi katika chama na wamekuwa wakiyatumia magari ya serikali kwa shughuli za chama.
Kwa kufanya hivyo, tutaokoa fedha nyingi ambazo zinaweza kuelekezwa katika kuboresha huduma za elimu, afya, maji na barabara.
Kwa kuanza na hatua ya kubana matumizi ya magari ya mawaziri yasitumike kwa shughuli za chama, utakuwa ni mwanzo mzuri katika jitihada za kubana matumizi ya fedha za wananchi walipakodi.




CHANZO: NIPASHE
 
Mambo mengi bara wanaiga zanzibar,hasa mfumo wa kisiasa wanasoma zanzibar. kwani wanafahamu zanzibar ni kitua cha siasa.
 
Mwanzo mzuri!..Lakini hawakujua kuwa mambo ya serikali hayachangamani na ya kichama hadi wakawa wanaenda nayo? Kweli wapinzani bado kazi wanayo!
 
Utekelezaji utatekelezeka,lazima watanganyika tuwafundishe siasa na uwongozi...
 
Wazo zuri, lakini tatizo liko kwenye kutofautisha majukumu ya kiserikali na kichama... lakini tusubiri tuone!!
 
Back
Top Bottom