John Nditi, Morogoro
Daily News; Friday,December 26, 2008 @00:02
Daily News; Friday,December 26, 2008 @00:02
Umoja wa Makanisa ya Kikristo Tanzania (CCT), umeonyesha hofu ya kile kinachoonekana kuwapo kwa mgawanyiko wa viongozi ndani Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa usipothibitiwa kwa haraka, unaweza kuathiri uhai wa taifa kisiasa na kiuchumi.
Hivyo kutokana na mwonekano huo, Umoja huo unaishauri serikali inayoundwa kutokana na chama hicho kuchukua hatua ya kudhibiti makundi hayo kwani yanaweza kuleta hali mbaya ya kuvurugika kwa amani.
Kauli hiyo ilitolewa na Askofu Jacob Ole Mameo wa Dayosisi ya Morogoro ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) jana wakati akihubiri kwenye ibada ya Sikukuu ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo ambayo Kitaifa ilifanyika mkoani hapa.
Askofu Mameo alisema Umoja huo umeanza kuona mgawanyiko tangu wakati wa utawala wa awamu ya tatu pale wananchi walipoanza kuwazomea baadhi ya viongozi wa chama hicho mbele ya viongozi wa kitaifa bila ya kujua hatima yake.
Kwa mujibu wa Askofu huyo, jambo hilo limeendelea na kanisa limeona zipo athari ya kuwapo kwa mgawanyiko hasa kwa wananchi nao wamepoteza imani na viongozi wa serikali yao tangu ngazi ya chini hadi juu.
Umoja huo pia umeitahadharisha serikali kwa baadhi ya viongozi waliopewa dhama ya kushughulikia maslahi ya wengine, jambo ambalo linaendelea kufanya wananchi wapoteze imani kwa serikali yao.
Akitolea mfano wa uwajibikaji wa viongozi wakati wa hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, Askofu huyo alisema ili kuendelea kunahitajika watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora katika kupambana na maadui wakubwa watatu; ujinga, umasikini na ardhi, lakini bado tatizo la uongozi bora limekuwa kikwazo na hivyo wananchi kupoteza imani na serikali yao.
Aidha, Umoja huo pia uliitahadharisha serikali kuwa makini na baadhi ya watu wanaochezea imani za kidini kiasi cha kuhatarisha taifa kuingia katika migogoro inayoweza kuchafua sifa, utulivu na mshikamano uliozoeleka kwa muda mrefu.
Pia alitaka serikali kuzichunguza baadhi ya dini zinazoanzishwa kwa wingi kuwa miongoni mwao zinawahubiria wananchi injili inayowajengea watu imani ya watu kupata utajiri na wanaposhindwa wanaamua kujiunga na dini za mashetani.
Alisema matokeo yake ni watu hao kuanza kuwawinda watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), kwa watu hao kugeuka na kujikita katika masuala ya ushirikina. Alisema hali hiyo imefikia kuleta imani ya kuua mtu ili kujipatia mali, hivyo aliiomba serikali isifanye mzaha na jambo hilo, bali ilichukulie hatua kali kwa wahusika wote.
Naye mgeni rasmi, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Diodorus Kamala, akiwasilisha salamu za serikali, alisema madhehebu ya dini yamesaidia taifa hususan katika huduma za jamii ikiwamo elimu, afya, maji utunzaji wa mazingira na kuziomba taasisi hizo ziendelee kutoa mchango huo. Alizihakikishia taasisi hizo za dini kuwa serikali imeanza kuchukua hatua na wale wanaojihusisha na maovu, watakaobainika watachukuliwa hatua kali kulingana na sheria za nchi.