Rutashubanyuma
JF-Expert Member
- Sep 24, 2010
- 219,470
- 911,172
Chuo Kikuu kipya kuiinua Tabora
Imeandikwa na Lucas Raphael, Tabora; Tarehe: 9th February 2011 @ 23:59
JANUARI 16 mwaka huu ni siku ya kukumbukwa katika mkoa wa Tabora, kutokana na mkoa huo kuandika historia mpya katika nyanja ya elimu nchini.
Siku hiyo mkoa huo ulipata chuo kikuu cha kwanza tangu Tanganyika ilipopata uhuru wake mwaka 1961.
Kwa muda mrefu mkoa wa Tabora haukuwa na vyuo vinavyotoa elimu ya juu nchini. Hali hiyo ilifanya mkoa huo ushindwe kupata ustawi mkubwa wa maendeleo, ikilinganishwa na mikoa mingine, ambayo ina vyuo vikuu.
Mkoa huo ulikuwa na vyuo vinavyotoa elimu ya kati tu, kama Chuo cha Ualimu Ndala wilayani
Nzega na Chuo cha Ualimu cha Tabora, vyuo hivyo vilianza kutoa huduma hiyo kwenye miaka ya 1960 na 1970.
Ukiondoa vyuo hivyo, vyuo vingine vilivyopo ni Chuo cha Utumishi wa Umma, Chuo cha Ardhi, Chuo cha Kilimo Tumbi, vyuo vya ufundi vya VETA na vituo vidogo vidogo vya utoaji wa elimu.
Taasisi hizo ndizo zilizokuwa zikifanya kazi ya kuwaelimisha wakazi wa Tabora katika fani tofauti. Kabla ya vyuo hivyo, Mkoa wa Tabora ulikuwa ukisifika kutokana na kuwa na shule mahiri za sekondari, ambazo zilichangia maendeleo ya taifa na kwa ushindani uliostahili.
Shule hizo ni Tabora Boys, Milambo, Tabora Girls na Kazima, ambazo kwa pamoja zimetoa wataalamu wengi zaidi nchini na viongozi wa serikali.
Hata hivyo, kukosekana kwa elimu ya chuo kikuu katika mkoa wa Tabora, kumeufanya mkoa huo uliosifika kielimu nchini, upoteze umaarufu wake wa miaka mingi na kujikuta ukiwa miongoni mwa mikoa isiyokuwa tena na sifa ya kufanya vizuri katika nyanja hiyo muhimu kwa maisha ya binadamu.
Chuo kikuu hicho kipya kilizinduliwa na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, alikuwa mgeni rasmi. Sherehe hizo za uzinduzi, zilifanyika katika uwanja wa Chipukizi mjini hapa. Katika hotuba yake, Sitta anasema hiyo ni hatua kubwa ya maendeleo katika mkoa wa Tabora, ambao umekuwa nyuma kwa muda mrefu na hivyo kuufanya usiwe miongoni mwa
mikoa yenye maendeleo makubwa kielimu nchini.
Anasema kuwepo kwa chuo hicho kikuu, kutainua uchumi na maendeleo ya mkoa. Anawataka wakazi wa mkoa huo, kuwa makini na kuwapa ushirikiano watumishi, wahadhiri na wanafunzi ili kuongeza sifa za mkoa huo katika elimu ya juu nchini.
Aliilaumu Bodi ya Mikopo Tanzania, kutokana na kushindwa kuweka mazingira mazuri ya utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini, huku akibainisha wazi
kuwa utendaji wa bodi hiyo, umejaa urasimu.
Anasema pamoja na urasimu, bodi hiyo imekuwa ikifanya kazi zake kwa chuki, upendeleo, dhuluma na kufanya mambo mengine ambayo hayakubaliki katika utoaji wa elimu ya juu nchini.
Anasema kuna haja ya kufanya mabadiliko makubwa katika bodi hiyo ili utendaji wake uwe na tija kwa Watanzania, wanaotafuta elimu ya juu nchini ili waweze kuja kulitumikia
taifa katika nyanja mbali mbali.
Anasema suala hilo atalifikisha serikalini, kwa ajili ya kutafutiwa ufumbuzi wa kina, ambao utaboresha utendaji katika bodi ya mikopo nchini, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa watoto wa Watanzania wananufaika zaidi na mikopo hiyo ya kielimu.
Akizungumza katika Ibada Maalumu ya Ufunguzi wa chuo hicho, Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Tabora, Paul Ruzoka, anasema chuo hicho kitaitwa Chuo Kikuu
Kishiriki cha Askofu Mihayo Tabora; au Archbishop Mihayo University College of Tabora ( AMUCTA).
Anasema kuwa elimu ni kitu muhimu kwa maisha ya binadamu; na kwamba Kanisa Katoliki litatoa huduma hiyo kwa Watanzania wote bila ubaguzi wa aina yoyote.
Askofu Ruzoka anasema ni wajibu wa kila mtu, kuhakikisha kuwa anapata elimu ili aweze, siyo tu kuishi vizuri, bali pia kuishi maisha ambayo yatamsaidia kumjua na kumthamini Mungu, ambaye ndiye aliyejalia vipawa vya kila namna kwa binadamu.
Anasema kwa kuwa Kanisa Katoliki, linatambua umuhimu wa jambo hilo, litaendelea kutumia fursa zilizopo ili kuendelea kuwasaidia wananchi, wapate fursa hiyo muhimu kwa maendeleo ya umma na kuondoa ubabaishaji katika utoaji wa huduma za kijamii miongoni mwa watanzania.
Askofu Mkuu anawahimiza waumini wa kanisa hilo na wale ambao si waumini, kukitumia vizuri chuo hich k ikuu kwa manufaa ya kijamii. Anasema lengo la kanisa ni kuhakikisha kwamba ustawi wa watu unakuwa bora zaidi kadri miaka inavyoongezeka.
Akizungumza baada ya uzinduzi wa Archbishop Mihayo University College of Tabora ( AMUCTA), ambacho kitakuwa chuo kikuu kishiriki cha Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine
(SAUT) cha jijini Mwanza, Makamu Mkuu wa chuo hicho nchini, Dk. Charles Kitima, anasema ni muhimu watoto wa Tanzania, wakinufaika na elimu ya juu.
Anasema katika siku za karibuni, kumeibuka mtindo wa baadhi ya viongozi wa serikali kuweka vikwazo kadhaa kwa wanafunzi wa vyuo vikuu binafsi, wakitaka wasipatiwe mikopo.
Anasema wanafunzi wengi wanaopewa mikopo hivi sasa ni wale wanaosoma vyuo na taasisi za serikali.
Anasema serikali haiwezi peke yake kuwasomesha wanafunzi wote waliomaliza elimu ya kidato cha sita na kufaulu mtihani, hivyo ni vyema ikashirikiana na vyuo vikuu vya binafsi,
vinavyowapatia vijana elimu hiyo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.
kuu wa AMUCTA, Dk. Thadeus Mkamwa, alisema chuo hicho kikuu kilianza rasmi Novemba 3 mwaka jana; na kwamba kimeanza kutoa mafunzo ya shahada ya kwanza ya Ualimu, kikiwa na wanachuo 886.
Alisema kutokana na mikakati ya chuo hicho kinatarajia kuanzisha pia shahada za masomo ya sayansi ya jamii, biashara na sheria ambayo yanatarajia kuleta mapinduzi mazito katika suala zima litakalosaidia maendeleo ya Taifa hili.
Alisema pamoja na kuanza fani hizo, alisema katika mipango ya muda mfupi chuo hicho kitaanza kutoa mafunzo ya elimu ya juu katika fani hizo kwa watu wa makundi maalum ambao
ni walemavu kama wasiosikia, wasiosema na wenye matatizo tofauti.
Anasema chuo hicho, kinatarajia kuwa na wanachuo wasiopungua 5,000 kitakapokamilika. Anasema kampasi ya chuo hicho, itajengwa katika eneo la Kazima, umbali wa kilomita nane kutoka mjini Tabora.
Kazi ya kulipa fidia kwa wananchi waliokuwa wakimiliki eneo hilo, inaendelea. Anawataka wakazi wa Tabora, kuwatambua na kuwathamini wanafunzi wa chuo hicho, hasa pale wanapotafuta makazi kwa ajili ya kusoma.
Anataka wasiwapandishie bei, kwa kudhani wana pesa za kutosha, hivyo kuwakwamisha kufikia malengo yao ya kielimu. Alisema hao ni watoto wa masikini kama wao, hivyo wanachopaswa kukifanya ni kuwasaidia; na si kuwakomoa.
Anasema kuwepo kwa wanachuo, kutakuza maendeleo na kuinua mji huo, kwa sababu mzunguko wa pesa utaongezeka.
Sherehe hizo za ufunguzi wa chuo hicho zimehudhuriwa na maelfu ya wakazi wa mji wa Tabora, viongozi wa chama Tawala na serikali, wabunge, maaskofu wa majimbo mbalimbali nchini na mapadri wanaoziwakilisha jumuiya mbalimbali katika jimbo Kuula Tabora.