BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,792
- 287,994
Chadema yalipua mawaziri wawili
2009-03-27 11:13:27
Na Richard Makore
2009-03-27 11:13:27
Na Richard Makore
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimewalipua mawaziri wawili na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) na kuwataka wajiuzulu kutokana na kushindwa kusimamia kazi zao ipasavyo.
Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa alipozungumza na waandishi wa habari.
Alimtaka Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrence Masha ajiuzulu kutokana na kushindwa kuzuia mapigano ya koo yanayoendelea wilayani Tarime, mkoa wa Mara na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, kwa kushindwa kuzuia nchi kuingia gizani kutokana na mgawo wa umeme ulioanza juzi jijini Dar es Salaam.
Aidha, Dk. Slaa alisema mapigano hayo yanafadhiliwa na wanasiasa wilayani Tarime ili ionekane kwamba Chadema ambacho kinaongoza Halmashauri ya Wilaya imeshindwa kufanya kazi.
Aliongeza kuwa Waziri Masha anatakiwa kujiuzulu katika nafasi hiyo kwa kuwa wananchi wengi wanapoteza maisha huku akiangalia bila kuchukua hatua yoyote kuzuia.
``Huyu Masha anatakiwa kujiuzulu kwani ameshindwa kuzuia mapigano, ila nchi hii viongozi wake hawana utamaduni wa kuachia ngazi, anapokosea na hili huenda lisifanyike,`` alisema.
Kuhusu suala la mitambo ya kufua umeme ya kampuni ya Dowans Tanzania Ltd, Dk. Slaa ameitaka serikali kutaifisha mitambo hiyo na sio kuanza kujadili namna ya kuinunua.
Dk. Slaa alisema Kamati Teule ya Bunge iliyokuwa chini ya uenyekiti wa Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, ambayo ilichunguza suala la Richmond ilisema mitambo hiyo iliingizwa nchini kwa njia za rushwa hivyo haiwezekani serikali ifikirie kuinunua mitambo isiyopatikana kwa njia za halali.
Alisema suala la kununua ama kutonunua mitambo hiyo halitakiwi kuzungumzwa kwa kuwa haikuingizwa nchini kwa njia halali, hivyo kujadili suala hilo ni kupoteza muda.
Aidha, alimtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Dk. Idris Rashid, pamoja na Waziri Ngeleja kujiuzulu kutokana na nchi kukumbwa na giza.
Kuanzia jana Tanesco ilitangaza kuanza kwa mgawo wa umeme sehemu mbalimbali hapa nchini.
Kuhusu mgawo wa umeme, Dk. Slaa alisema Kamati ya Dk. Mwakyembe iliyochunguza Richmond mwaka 2007 ilitoa mapendekezo kwa shirika hilo kuchukua tahadhari ili nchi isiingie katika mgawo wa umeme.
Alidai kuwa Dk. Rashid hawezi kuisaidia Tanesco kwa kuwa ni mmoja kati ya watu waliochota fedha akiwa Gavana wa Benki Kuu Tanzania (BoT) kupitia ununuzi wa rada.
Alisema ununuzi wa rada haukuwa na maslahi kwa taifa na kwamba Dk. Rashid ndiye aliyekazania suala hilo, lakini lengo lake lilikuwa kutaka apate fedha.
Alimtaka Waziri Ngeleja kueleza matumizi ya mitambo ya Songas iliyopo Ubungo kwa kushindwa kutatua tatizo la umeme mpaka nchi kuingia katika giza.
Katika hatua nyingine, Dk. Slaa aliungana na Dk. Mwakyembe na kuwaita mafisadi watu wanaompinga kuhusu ununuzi wa Dowans.
Alisema msimamo wa Dk. Mwakyembe kwamba mitambo ya Dowans haifai kununuliwa ni sahihi na yeye anaunga mkono suala hilo.
Kuhusu Naibu Katibu Mkuu wake, Zitto Kabwe, kutofautiana naye katika suala la ununuzi wa mitambo hiyo, Dk. Slaa alisema hawezi kutoa maoni.
Alisema Zitto anaongoza Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma na kwamba ripoti yake ataijua itakapofikishwa bungeni na hapo ataweza kujua kwa nini msaidizi wake anakazania serikali inunue mitambo hiyo.
Aliongeza kuwa msimamo wa Zitto kutaka serikali inunue mitambo hiyo na yeye kupinga hakujazua migogoro kama ilivyoripotiwa na vyombo vya habari.
Lakini kwa upande mwingine, Dk. Slaa alisema anakerwa na tabia ya Mbunge wa Igunga CCM, Rostam Aziz, kwa kumchezea rafu, Dk. Mwakyembe katika mradi wa umeme wa upepo anaotarajia kuanzisha mkoani Singida.
Alisema kampuni ya kizalendo ya Dk. Mwakyembe ilikuwa inatarajia kuzalisha umeme katika kijiji cha Kisesida mkoani Singida, lakini Rostam akaingilia kati na kuvuruga mpango huo ili kazi hiyo aifanye yeye.
Katika hatua nyingine, chama hicho kimewavua uanachama wanachama wake 15 kwa kosa la kueneza propaganda zilizolenga kuibua migogoro na kukigawa chama hicho.
Uamuzi wa kuwavua uanachama ulitangazwa jana jijini Dar es Salaam na Dk. Slaa na kueleza kuwa uamuzi huo ulifikiwa baada ya kuunda kamati ya kuchunguza tuhuma hizo dhidi ya Mbowe na kubainika kuwa zote zilikuwa za uongo.
Wanachama hao walimtuhumu Mbowe kwa kutafuna fedha za chama, kushiriki kumuua marehemu Chacha Wangwe kutumia chama kwa itikadi za ukabila, kudhoofisha vita dhidi ya ufisadi na kushindwa kufanya ziara mikoani.
Aliongeza kuwa kamati ya kuchunguza madai hayo ya wanachama iliongozwa na Mwenyekiti mstaafu wa Chadema, Bob Makani.
Dk. Slaa alisema wanachama wote walipoitwa na kamati hiyo ili kutoa ushahidi walikataa na kwamba matokeo ya uchunguzi yanaonyesha kwamba wanachama hao walikuwa wanatumiwa na watu kukivuruga chama.
Katika uchunguzi huo kamati ilibaini watu saba kuwa wanatoka chama fulani cha siasa akiwemo mmoja ambaye ni mfanyakazi wa Mbunge mmoja jijini Dar es Salaam.
Alimtaja mfanyakazi huyo kuwa jina tunalisitiri, jambo ambalo linaonyesha kuwa migogoro iliyokuwa ikisemwa ilipandikizwa na watu wasiokitakia mema chama hicho.
Alisema wanachama hao kwa kutumiwa na wapinzani wao kisiasa walizusha tuhuma ambazo hazikuwa na ukweli wowote dhidi ya mwenyekiti wake, Freeman Mbowe.
Dk. Slaa alisema mmoja wa wanachama waliofukuzwa ni Kaimu Mwenyekiti wa chama hicho wa Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, Martin Mng`ong`o.
Alisema wanachama hao walikuwa wanatumiwa na watu wasiokitakia mema chama hicho na kwamba hivi sasa wamewasafisha ili kukiwezesha chama kusonga mbele.
Aliongeza kuwa walipata taarifa za kuwepo mipango ya kukivuruga chama hicho na hapo ndipo walipoanza kuweka mitego ya kuwafuatilia wanachama hao.
``Sisi tunapata taarifa nyingi kutoka sehemu mbalimbali hivyo ilikuwa rahisi kuwakamata mamluki hao wa kisiasa,`` alisema.
Dk. Slaa alisema mwanachama yeyote anayetumiwa na watu kukivuruga chama chake watamshughulikia kwa kuwa wana mtandao mkubwa wa kuwabaini.
SOURCE: Nipashe