Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,319
- 33,125
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimekishutumu Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwa kimeanza mkakati wa kununua shahada za kupigia kura za vijana wanaoonekana kushabikia vyama vya upinzani katika mikoa yote nchini.
Mkurugenzi wa Sheria na Haki za Binadamu wa chama hicho, Tundu Lissu, alisema jana kuwa viongozi na makada wa chama hicho kuanzia ngazi za mashina na matawi wamekuwa wakikusanya taarifa za wananchi waliojiandikisha karika daftari la kudumu la wapiga kura.
Alidai kuwa katika kutekeleza mkakati huo, makada hao wa CCM wanashirikiana na maofisa watendaji wa kata na vijiji ambao katika uchaguzi mkuu watakuwa wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi.
Alisema Chadema imepata ushahidi unaoonyesha kuwa sensa ya wapiga kura inayofanywa na CCM ni maandalizi ya kuharibu uchaguzi wa mwaka huu kwa kutoa rushwa kwa wapiga kura wenye mwelekeo wa kuviunga mkono vyama vya upinzani.
Lissu alisema Jumamosi iliyopita, wanachama wa Chadema wa kijiji cha Nkhoiree, kata ya Ihanja Jimbo jipya la Singida Magharibi kulimkamata kada mmoja wa CCM akiwa katika zoezi la kuchukua taarifa za wapiga kura.
Alisema katika purukushani za kumkamata, kada huyo alifanikiwa kukimbia na kutoroka, lakini wanachama na wafuasi wa Chadema walifanikiwa kukamata nyaraka alizokuwa nazo.
Alisema nyaraka alizokamatwa nazo ni muhtasari wa kikao cha CCM kata ya Ihanja ambayo inawataja pia Mwenyekiti wa kata na Katibu wa kata hiyo ya Ihanja.
Lissu alisema ajenda namba 5 ya muhtasari huo inahusu maazimio ya Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Taifa inayoelekeza makatibu wote wa matawi yote ya CCM wafanye sensa ya wapiga kura wote wa vyama vya upinzani kujua wako wangapi hasa vijana wa rika la kati ili kupata idadi yao Tanzania nzima.
Hata hivyo, Mkurugenzi wa Kitengo cha Propaganda cha CCM, Tambwe Hizza, alipoulizwa alisema hizo ni taarifa za uongo kwani CCM inachofanya ni kuhakiki wanachama wake na si kuhangaika na wapinzani.
Alisema zoezi hilo ni la kawaida na limekuwa likifanyika miaka mingi iliyopita hivyo hakuna kitu kipya.
Alisema wanachofanya sasa ni kuhakikisha kila mwanachama wa chama hicho amejiandikisha katika daftari la wapiga kura.
Tunahakikisha kila mwanachama wetu anajiandikisha katika daftari la wapiga kura ili siku ya uchaguzi apige kura na ambaye hatafanya hivyo hataruhusiwa kupiga kura za maoni ndani ya chama, alisema Tambwe.
CHANZO: NIPASHE