Mujumba
JF-Expert Member
- Jan 20, 2011
- 853
- 306
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba
Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imeiagiza sekretariat yake kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba, kutokana na kauli anayodaiwa kuitoa kwamba chama hicho kinafadhiliwa na mataifa ya nje kufanya maandamano.
Msimamo huo ulitolewa jana na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Alikuwa akitoa taarifa kuhusu uamuzi wa kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho kilichofanyika juzi jijini Dar es Salaam.
Mbowe alisema hatua hiyo ilifikiwa baada ya CC kupokea na kujadili kwa umakini tathmini ya maandamano yaliyofanyika Kanda ya Ziwa, pamoja na matamko yaliyotolewa na viongozi wa serikali na Chama cha Mapinduzi (CCM).
"Viongozi hao ni pamoja na Rais Jakaya Kikwete, Mawaziri Bernard Membe, Stephen Wasira, Sophia Simba na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chiligati.
"Mambo mawili yanajitokeza katika kauli zao, kwamba maandamano ya Chadema yanahatarisha amani ya nchi kwa kuchochea wananchi kuitoa serikali iliyopo madarakani kwa njia ya maandamano," alisema.
Mbowe alisema Simba anadaiwa kusema kwamba, Chadema kinafadhiliwa na mataifa ya nje kufanya maandamano hayo.
Alisema kwa sababu hiyo, chama chake kitamwandikia barua waziri huyo kikitaka athibitishe nchi iliyotoa fedha kwa chama hicho, siku fedha hizo zilipotolewa na kiasi cha fedha hizo.
Alisema endapo Simba atashindwa kufanya hivyo, chama chake kitampeleka mahakamani ili iwe ni fundisho kwa wengine wasije wakaongea maneno ya kukichafua chama hicho bila sababu za msingi.
Katika hatua nyingine, Mbowe alisema kwamba Chadema wamemtaka Waziri wa Nishati ma Madini, William Ngeleja, kuwajibika kisiasa kwa kujiuzulu kwa kuwa amepoteza sifa za kushikilia nafasi aliyonayo kwa kushindwa kusimamia sekta ya umeme kwa ufanisi kutokana na tatizo hilo kuwa sugu nchini.
Kuhusu mabomu yaliyolipuka Gongolamboto, Mbowe alisema Chadema inaendelea kumhimiza Waziri wa Ulinzi, Dk. Hussein Mwinyi, awajibike kisiasa kwa kujiuzulu, kutokana na kushindwa kuchukua hatua thabiti katika kuhakikisha kuwa milipuko ya mabomu katika kambi za jeshi haijirudii.