CHADEMA INAFAA KUKOMAA KISIASA
KAULI kuwa kumalizika kwa uchaguzi ni mwanzo wa maandalizi ya uchaguzi ujao, ingawa si mpya, lakini hivi karibuni imetumika sana katika vyombo vya habari na majukwaa ya kisiasa tena ikipewa maana tofauti na iliyokuwapo hapo awali.
Kauli hiyo ambayo mara kwa mara imekuwa ikitumiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) hasa baada ya uchaguzi wao wa ndani ya chama, sasa inatumiwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuhalalisha maandamano na tunaona huenda ndio sababu ya kubadilishwa maana yake.
Katika maana ya awali, CCM waliitumia kauli hiyo kuponyesha makovu ya baada ya uchaguzi kwa kuwataka walioshindwa kushikana mikono, kupendana na kushirikiana kukiimarisha chama chao ili kishinde Uchaguzi Mkuu na kuongoza Dola.
Lakini maana ya sasa ya Chadema iliyojitokeza kwa vitendo ni kuhamasisha hisia za kutengana, kuharibu mshikamano na kuzuia Serikali isipate fursa ya kutekeleza majukumu yake ya kuiletea nchi yetu maendeleo.
Mifano iko dhahiri, kilichotokea mkoani Arusha na hata yaliyofanyika kwa mfululizo katika Kanda ya Ziwa ambako wabunge wa chama hicho, licha ya kuwa na majukumu katika majimbo yao, walifuatana na viongozi wenzao kusambaza propaganda kuwa Serikali haifanyi kitu chochote.
Tunaona kuwa zilikuwa propaganda zenye nia mbaya kwa kuwa pamoja na kuwa walitumia usafiri wa anga na barabarani, wakapata huduma zote muhimu, hawakusikika wakisifia kazi ya Serikali katika kuboresha mazingira ya upatikanaji wa bidhaa na huduma au uboreshaji wa miundombinu kama viwanja vya ndege, ukiwemo wa Mwanza walioutumia.
Hawakusikika, wakisifia na kuhamasisha wananchi kushirikiana na Serikali katika kuboresha miundombinu mingine kama ya barabara walizozitumia; zaidi ya kusema maneno yasiyopendeza kuhusu Serikali kuanzia mwanzo mpaka mwisho kuonesha hakuna jema linalofanyika.
Hatua hiyo ya Chadema, tumeiona kuwa ni ya uchanga inayoonesha kutokukomaa kisiasa, kwani baadhi ya mambo waliyokuwa wakihamasisha katika jamii, yanatokana na mabadiliko ya siasa na uchumi wa kimataifa au ya hali ya hewa ambayo hakuna Serikali yenye uwezo wa kuyadhibiti.
Kwa mfano, wanapigia kelele kupanda kwa gharama za maisha ambazo katika uchumi wa Tanzania, husababishwa zaidi na hali ya upatikanaji wa chakula na bei ya mafuta katika soko la kimataifa.
Pamoja na Chadema kufahamu hilo, hatukusikia wakiwaelimisha wananchi kuwa hata mgogoro wa Libya unaoongeza bei ya mafuta na mabadiliko ya hali ya hewa yaliyosababisha ukame, si Tanzania, Serikali wala Rais Jakaya Kikwete wanaohusika.
Lakini juzi, tuliwasikia wabunge wawili wa Chadema, Tundu Lissu wa Singida Mashariki na wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, wakitoa kauli za kuisaidia Serikali na kuisifu jambo lililoonesha wanakaribia kukua kisiasa.
Lissu akiwa jimboni kwake, sio katika Operesheni Sangara, alihamasisha uongozi wa vijiji katika jimbo hilo kufanya tathmini ya haraka ya hali ya upungufu wa chakula katika maeneo yao na kupeleka taarifa mapema wilayani.
Kwa kauli zao za Operesheni Sangara, Lissu alitarajiwa aseme njaa imesababishwa na Serikali iliyopo madarakani, lakini alitoa kauli ya kiutuuzima, kama kiongozi kusaidia Serikali ipate taarifa mapema ili izuie njaa na huo ndio ukomavu tunaoona umeanza kujitokeza.
Naye Mbilinyi akiwa jimboni kwake, alisikika akiipongeza Serikali kwa kujenga Uwanja wa Ndege wa Songwe, akisema ameridhishwa na hatua za ujenzi zinazoendelea baada ya kuutembelea na kuwataka wananchi wajipange kunufaika nao ifikapo Agosti mwaka huu ndege zitakapoanza kutua katika uwanja huo.
Kauli kama hiyo inapingana na kauli nyingine walizosikika wakisema kuwa kazi yao si kuisifu Serikali na kwa hili, tunawapongeza wabunge hao kwa kuanza hatua zinazoonesha wanaelekea kukua kisiasa.
Tunawashauri Chadema, kutafakari changamoto za kiuchumi, kisiasa na kijamii na kuanza kuhamasisha wananchi namna ya kushirikiana na Serikali yao kukabiliana nazo.
Tunatarajia ukomavu huo ukifikia penyewe, tutaisikia Chadema ikiimba Kilimo Kwanza, kuhamasisha wananchi waongeze uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara, si tu ili wajipatie kipato, lakini pia wasaidie kupungua kasi ya kupanda kwa gharama za maisha.
Tunatarajia Chadema ihamasishe vijana shuleni, kujikita zaidi katika masomo ya sayansi, ili Tanzania ijayo iwe na wanasayansi wa kutosha watakaosaidia kupaisha ndege yake ya kiuchumi na kijamii na sio kukimbia nchi yao baada ya kupotea kwa amani.
GAZETI LA HABARI LEO
KAULI kuwa kumalizika kwa uchaguzi ni mwanzo wa maandalizi ya uchaguzi ujao, ingawa si mpya, lakini hivi karibuni imetumika sana katika vyombo vya habari na majukwaa ya kisiasa tena ikipewa maana tofauti na iliyokuwapo hapo awali.
Kauli hiyo ambayo mara kwa mara imekuwa ikitumiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) hasa baada ya uchaguzi wao wa ndani ya chama, sasa inatumiwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuhalalisha maandamano na tunaona huenda ndio sababu ya kubadilishwa maana yake.
Katika maana ya awali, CCM waliitumia kauli hiyo kuponyesha makovu ya baada ya uchaguzi kwa kuwataka walioshindwa kushikana mikono, kupendana na kushirikiana kukiimarisha chama chao ili kishinde Uchaguzi Mkuu na kuongoza Dola.
Lakini maana ya sasa ya Chadema iliyojitokeza kwa vitendo ni kuhamasisha hisia za kutengana, kuharibu mshikamano na kuzuia Serikali isipate fursa ya kutekeleza majukumu yake ya kuiletea nchi yetu maendeleo.
Mifano iko dhahiri, kilichotokea mkoani Arusha na hata yaliyofanyika kwa mfululizo katika Kanda ya Ziwa ambako wabunge wa chama hicho, licha ya kuwa na majukumu katika majimbo yao, walifuatana na viongozi wenzao kusambaza propaganda kuwa Serikali haifanyi kitu chochote.
Tunaona kuwa zilikuwa propaganda zenye nia mbaya kwa kuwa pamoja na kuwa walitumia usafiri wa anga na barabarani, wakapata huduma zote muhimu, hawakusikika wakisifia kazi ya Serikali katika kuboresha mazingira ya upatikanaji wa bidhaa na huduma au uboreshaji wa miundombinu kama viwanja vya ndege, ukiwemo wa Mwanza walioutumia.
Hawakusikika, wakisifia na kuhamasisha wananchi kushirikiana na Serikali katika kuboresha miundombinu mingine kama ya barabara walizozitumia; zaidi ya kusema maneno yasiyopendeza kuhusu Serikali kuanzia mwanzo mpaka mwisho kuonesha hakuna jema linalofanyika.
Hatua hiyo ya Chadema, tumeiona kuwa ni ya uchanga inayoonesha kutokukomaa kisiasa, kwani baadhi ya mambo waliyokuwa wakihamasisha katika jamii, yanatokana na mabadiliko ya siasa na uchumi wa kimataifa au ya hali ya hewa ambayo hakuna Serikali yenye uwezo wa kuyadhibiti.
Kwa mfano, wanapigia kelele kupanda kwa gharama za maisha ambazo katika uchumi wa Tanzania, husababishwa zaidi na hali ya upatikanaji wa chakula na bei ya mafuta katika soko la kimataifa.
Pamoja na Chadema kufahamu hilo, hatukusikia wakiwaelimisha wananchi kuwa hata mgogoro wa Libya unaoongeza bei ya mafuta na mabadiliko ya hali ya hewa yaliyosababisha ukame, si Tanzania, Serikali wala Rais Jakaya Kikwete wanaohusika.
Lakini juzi, tuliwasikia wabunge wawili wa Chadema, Tundu Lissu wa Singida Mashariki na wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, wakitoa kauli za kuisaidia Serikali na kuisifu jambo lililoonesha wanakaribia kukua kisiasa.
Lissu akiwa jimboni kwake, sio katika Operesheni Sangara, alihamasisha uongozi wa vijiji katika jimbo hilo kufanya tathmini ya haraka ya hali ya upungufu wa chakula katika maeneo yao na kupeleka taarifa mapema wilayani.
Kwa kauli zao za Operesheni Sangara, Lissu alitarajiwa aseme njaa imesababishwa na Serikali iliyopo madarakani, lakini alitoa kauli ya kiutuuzima, kama kiongozi kusaidia Serikali ipate taarifa mapema ili izuie njaa na huo ndio ukomavu tunaoona umeanza kujitokeza.
Naye Mbilinyi akiwa jimboni kwake, alisikika akiipongeza Serikali kwa kujenga Uwanja wa Ndege wa Songwe, akisema ameridhishwa na hatua za ujenzi zinazoendelea baada ya kuutembelea na kuwataka wananchi wajipange kunufaika nao ifikapo Agosti mwaka huu ndege zitakapoanza kutua katika uwanja huo.
Kauli kama hiyo inapingana na kauli nyingine walizosikika wakisema kuwa kazi yao si kuisifu Serikali na kwa hili, tunawapongeza wabunge hao kwa kuanza hatua zinazoonesha wanaelekea kukua kisiasa.
Tunawashauri Chadema, kutafakari changamoto za kiuchumi, kisiasa na kijamii na kuanza kuhamasisha wananchi namna ya kushirikiana na Serikali yao kukabiliana nazo.
Tunatarajia ukomavu huo ukifikia penyewe, tutaisikia Chadema ikiimba Kilimo Kwanza, kuhamasisha wananchi waongeze uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara, si tu ili wajipatie kipato, lakini pia wasaidie kupungua kasi ya kupanda kwa gharama za maisha.
Tunatarajia Chadema ihamasishe vijana shuleni, kujikita zaidi katika masomo ya sayansi, ili Tanzania ijayo iwe na wanasayansi wa kutosha watakaosaidia kupaisha ndege yake ya kiuchumi na kijamii na sio kukimbia nchi yao baada ya kupotea kwa amani.
GAZETI LA HABARI LEO